Mzee Mwanakijiji
Platinum Member
- Mar 10, 2006
- 33,476
- 39,995
Mojawapo ya ukosoaji mkubwa wa wakati wa Nyerere ni kuwa "watu walikufa na njaa" na kuwa tulilazimika "kula yanga" na kupanga mistari kusubiri mgao - the infamous "duka la kaya". Ukiwasikiliza wanaozungumzia hayo ni watu ambao wanaamini kabisa kuwa Tanzania sasa hivi kuna neema ya chakula na hakuna watu wanaohangaika na njaa na ambao bila msaada wa serikali watakufa njaa. Na kama wengine wanakumbuka miaka michache tu iliyopita (wakati wa Kikwete huu huu) kuna watu huko Pwani walikuwa wakiishi kwa kula mizizi, na sehemu nyingine kwa kula matunda pori - Yaani hata siyo Yanga!!
Tuangalie mifano michache:
Februari 11 - Zanzibar - 7000 wakabiliwa na upungufu wa chakula:
7OOO WAKABILIWA NA UPUNGUFU WA CHAKULA MICHEWENI
Balozi Seif azitaka Kilimo, Fedha kutafuta ufumbuzi haraka
Na Mwantanga Ame, Pemba
TATIZO la uhaba wa chakula limejitokeza tena katika wilaya ya Michweni na kusababisha wananchi zaidi ya 7,000 wa maeneo hayo kukumbwa na upungufu mkubwa wa chakula cha mazao.
Hali hiyo imejitokeza kwa muda wa miezi mitano sasa baada ya eneo kubwa la mashamba ya wakulima kutokuwa na uzalishaji wa chakula cha aina yoyote.
Juni 2011 - Ngorongoro uhaba wa Chakula
TARAFA za Ngorongoro, Sale na Loliondo zilizopo wilayani Ngorongoro mkoani Arusha zinakabiliwa na baa la njaa. Mpaka sasa taarifa zinaonesha kuwa Tarafa ya Ngorongoro inahitaji zaidi ya tani 1500 za mahindi, tarafa ya Sale na Loliondo zinahitaji zaidi ya tani 1000 .
Kutokana na kilio hicho cha msaada wa chakula, kamati maalumu imelazimika kuundwa ili kukutana na Rais Jakaya Kikwete kumueleza juu ya tatizo hilo. Mkutano huo uliofanyika jana juu ya majadiliano ya upatikanaji wa uhakika wa chakula uliwashirikisha wadau wa maendeleo na jamii inayoishi ndani ya hifadhi ya Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA).
Akizungumza katika mkutano huo Mbunge wa Jimbo hilo, Saning'o Ole Telele alisema, tatizo la chakula wilayani humo kwa ujumla limesababishwa na ukame mkubwa. "Wananchi wanahitaji chakula kwa sasa kitakacho watosheleza hadi Januari 2012,"alisema Telele.
Mei 2011 - Serikali yasababisha upungufu mkubwa wa chakula mikoa ya Kaskazini
MIKOA ya Kanda ya Kaskazini na Kati inakabiliwa na upungufu mkubwa wa chakula kutokana na Serikali kutotoa vibali vya kununua chakula kwa kampuni mbalimbali.
Mwenyekiti wa Bodi ya Mazao Mchanganyiko, Kanda ya Kaskazini, Philemoni Mollel alisema licha ya maombi kuwasilishwa Februari mwaka huu kutaka kununua vyakula kutoka kwenye maghala ya Serikali yaliyoko Arusha, Serikali haijatoa vibali.
Mollel alisema kutokana na urasimu huo, kampuni husika zimekosa mahindi ambayo walikuwa wakiyanunua kutoka kwenye maghala ya Hifadhi ya Chakula ya Taifa (SGR) na kusaga unga kwa ajili ya kuuza.
Watoto 43,000 wanakufa kila Mwaka TZ kwa Utapiamlo (Malnutrition) 2010
Utapiamlo
Je, Tanzania inaweza kupuuzia vifo 43,000 vya watoto
na upotevu wa Sh bilioni 700 kila mwaka?
Bagamoyo wapewa msaada wa chakula kukabiliana na njaa
Serikali imetoa jumla ya tani 372.4 za chakula kwa wilaya ya Bagamoyo ili kuweza kukabiliana na tatizo la Njaa
Na Anna Nkinda – Maelezo, Bagamoyo - 05/10/2009
Serikali imetoa jumla ya tani 372.4 za chakula kwa wilaya ya Bagamoyo ili kuweza kukabiliana na tatizo la njaa linaloikabili wilaya hiyo.
Hayo yamesemwa jana na Mkuu wa wilaya hiyo Magessa Mulongo wakati akieleza hali ya chakula kwa mke wa Rais Mama Salma Kikwete wakati wa ziara yake ya kikazi ya siku moja katika wilaya hiyo .
Mulongo alifafanua kuwa tani 186.2 ziligawiwa bure kwa wananchi na tani 186.2 zilitolewa kwa utaratibu wa kuuza ambapo kilo moja iliuzwa Tshs.50.
"Vijiji 64 kutoka katika kata 16 zenye jumla ya watu 132,703 wameombewa msaada wa chakula kupitia TASAF kwa mradi wake wa uhakika wa chakula (FOOD Security)", alisema.
Simanjiro wahitaji tani 3000 za chakula- Mei 2011
Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro, Khalid Mandia, ameiomba serikali kupeleka zaidi ya tani 3,000 za chakula ili kukabiliana na uhaba mkubwa wa chakula ulioikumba wilaya hiyo.Alisema wilaya hiyo ilipata tani 600 za nafaka wiki iliyopita lakini bado hazikithi haja ya wakazi wa wilaya hiyo ambao wengi wao ni wafugaji.
Alisema tani hizo zilipelekwa maeneo yanayokabiliwa na upungufu mkubwa wa chakula, lakini kwa maeneo yenye nafuu kidogo hayakupelekewa. Akizungumza upungufu huo, diwani wa Kata ya Langai, Jackson Sipitek, alisema hali si shwari kutokana na mahindi yaliyolimwa kukauka kwa jua.
Watu 80,000 Longido wahitaji msaada wa chakula - Januari 2010
Zaidi ya watu 80,000 wa Wilaya ya Longido, mkoani Arusha, wanahitaji msaada wa haraka wa chakula ili kukabiliana na njaa iliyosababishwa na ukosefu wa mvua kwa miaka miwili mfululizo.
Wilaya hiyo inahitaji takriban tani 5,770 za chakula kwa wananchi wasiokuwa na chakula.
Hayo yalisemwa jana wakati wa ziara ya siku mbili na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi), Aggrey Mwanri.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mkuu wa Wilaya ya Longido, James ole Millya, zaidi ya tani 6,145 za chakula, ndizo zilizofikishwa na serikali katika wilaya hiyo ambazo zimegawiwa katika kaya tofauti.
Mkuu huyo wa Wilaya alisema hali ya chakula ni mbaya hasa maeneo ya vijijini na kwamba imesababisha mahudhurio katika shule za msingi kushuka kwa wastani wa asilimia 45 kulingana na utafiti uliofanywa na Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) katika vijiji mbalimbali vya wilaya hiyo.
Lissu - Singida wakabiliwa na Njaa Machi 2011
Wito huo umetolewa jana na mbunge wa jimbo hilo mhe Tundu Lisu kwenye sherehe
ya kuwashukuru wananchi wa tarafa ya Mungaa kwa kumchagua kuwashika wadhifa huo
katika uchaguzi mkuu ulipita.Mhe Lisu amesema kuwa wakati wananchi katika jimbo wanakabiliwa na upungufu
mkubwa wa chakula, taarifa zilizopo serikali zinaonesha kuwa kwa mkoa wa Singida
ni wilaya ya Manyoni pekee ndio yenye uhaba wa chakula na inatakiwa kupelekewa
msaada.
Kutokana na hali hiyo mbunge huyo amezitaka Serikali za Vijiji katika jimbo lake
kufanya tathimini haraka kwa kila kaya ili kujua hali halisi ya upungufu wa
chakula na kupeleka taarifa wilayani kwa ajili ya kuchukua hatua za kuomba
chakula serikali mapema.
Watu 372,000 Arusha wakabiliwa na njaa - 2009
ZAIDI ya watu 372,980 katika vijiji mbalimbali vya mkoa wa Arusha wanakabiliwa na tatizo kubwa la chakula.
Hali mbaya ya hewa iliyosababisha kukosekana kwa mvua za vuli na masika imetajwa kama ndiyo sababu kubwa ya wananchi hao kukabiliwa na uhaba wa chakula.
Kutokana na hali hii mkoa wa Arusha unahitaji zaidi ya tani 13, 431 za nafaka kwa ajili ya kuwasaidia waathirika hao.
Mkuu wa mkoa wa Arusha Isdori Shirima alisema idadi ya watu wanaokabiliwa na upungufu wa chakula mkoani humo ni kubwa ukilinganisha na miaka mingine ya nyuma.
Dewji asaidia wenye upungufu wa chakula Singida Mjini - Aprili 2011
MBUNGE wa Jimbo la Singida Mjini (CCM), Mohammed Dewji ametoa msaada wa chakula
wa zaidi ya tani 100 wenye thamani ya Sh milioni 40 kwa wananchi wanaokabiliwa na upungufu wa chakula katika jimbo hilo.
Dewji alitoa msaada huo wakati wa ziara ya kukabidhi chakula hicho Jumanne kwenye kata za Mtamaa, Mwankoko, Mandewa na Uhamaka ambako alitoa magunia kadhaa ya mahindi.
Mbunge huyo alisema kuwa amefikia uamuzi huo, baada ya kupewa taarifa na madiwani wa
kata hizo kuwa maeneo hayo yanakabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula.
Mpwapwa watu waishi kwa kula mbogamboga na matunda pori, njaa kali - Januari 2010
HOFU kubwa imetanda kwa ndugu, jamaa na majirani wa wananchi wanaokabiliwa na njaa kali katika baadhi ya maeneo wilayani Mpwapwa, mkoani Dodoma.
Hofu hiyo inatokana na kuweko kwa hali mbaya ya upungufu wa chakula, hali inayosababisha baadhi ya familia kuishi kwa kula mbogamboga na matunda ya porini.
Uchunguzi uliofanywa na Tanzania Daima katika baadhi ya maeneo ya wilaya ya Mpwapwa umebaini kuwepo kwa njaa kali hali ambayo kama itaendelea upo uwezekano wa wananchi kupoteza maisha kutokana na kukosa chakula.
Maeneo mbalimbali yaliyofanyiwa uchunguzi yamebainika kuwa na upungufu mkubwa wa chakula huku hali mbaya zaidi ikiwa katika tarafa za Kibakwe na Mima katika kijiji cha Berege.
Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi, wananchi wa kijiji cha Kibakwe pamoja na viongozi wao walisema hali ni mbaya na baadhi ya watu tayari wameelemewa na kuvimba miguu kutokana na kukosa chakula kwa muda mrefu.
Watu wapoteza matumaini Isimani Iringa, Njaa!! Mei 2011
NI balaa hili kwani unapofika katika vijiji mbalimbali vya tarafa ya Isimani wilaya ya Iringa unapokewa na nyuso za watu waliopoteza matumaini na vilio vyao karibu wote ni maombi ya msaada wa chakula kutoka serikalini.
Ukijikumbusha historia ya maisha katika maeneo hayo hasa wakati kama huu wa mwaka , haikuwa rahisi kuwasikia wananchi wa huko wakilia njaa.
Hii ni kutokana na ukweli kwamba, huu ndio msimu wa mavuno ya mahindi. Lakini, sasa kilio cha njaa kwa wananchi wengi wa wilaya ya Iringa kimekuwa kawaida! Karibu kila nyumba unayobisha hodi kilio chao kikuu, ni njaa.
Kwa asili, wananchi wa maeneo hayo ni wakarimu, lakini kwa kipindi hiki ukarimu huo haupo tena kwa sababu kila wakisikia hodi, lazima wapatwe na mawazo jinsi gani wataweza kumhudumia mgeni, kutokana uhaba wa chakula uliopo.
My Take and Questions:
a. Yawezekana wale wanaolalamikia kula Yanga au dona wakati wa Mwalimu na kupewa mafuta yale ya misaada kutoka kwa USAID hawajui kinachoendelea nchini, au hawataki kujua. Yawezekana tuliokula Yanga hali haikuwa mbaya kama ilivyo baadhi ya sehemu nchini kwa miaka kadhaa sasa. Yanga oyee!!
b. Tatizo la njaa ni mojawapo ya matatizo mengine ambayo yanawasumbua Watanzania kama ilivyo nishati lakini ni tatizo ambalo linadhalilisha utu wa mwanadamu kuliko tatizo jingine lolote lile, hata magonjwa hayadhalilishi utu wa mwanadamu kama kufa njaa. Kwanini tatizo hili haliangaliwi kwa ukaribu na uzito wake unaostahili? Kwanini bado kuna watanzania ambao wanahangaikia mlo wa siku moja tu?
c. Walioshiba yawezekana kweli hawamjui mwenye njaa, mifano mingi ambayo nimeitoa hapa (mingine hata sijaigusa) ingetosha kabisa kutuambia kuwa Tanzania kuna tatizo la njaa, lakini ni wangapi wanaokula na kusaza huko Dar, nyama choma kila jioni, n.k wanajua kinachoendelea sehemu nyingine ya nchi? Je wabunge wetu (niliangalia zile sherehe ambazo Waziri Mkuu aliandaa nyumbani kwake Dodoma na zile za wapinzani katika kupongezana) wanajua kuna tatizo kubwa sana la njaa nchini?
d. Kama hali ilikuwa mbaya wakati wa Mwalimu na watu wanatukumbushia hivyo, hivi hawa wa leo ambao nimewadokeza ukiwaambia utawala wa Kikwete watu walikuwa wanashiba na kusaza watakuelewa? Wananchi wa Mpwapwa kwa mfano ambao hata unga wa yanga hawakupata na kujikuta wanakula matunda mwitu wanaweza kusema kuwa "hali ilikuwa nzuri" wakati wao?
Ninachoweza kuona ni kuwa yawezekana pasipo kuangalia jambo kubwa zaidi ambalo lingehitaji kumalizwa "once and for all" ni hiki kitu tunachokiita "usalama wa chakula". Je, Tanzania inaweza kweli kufikia "usalama wa chakula", itakuwaje kama hatuwezi kufikia?
e. Je mikataba ya hivi karibuni ya kugawa maeneo makubwa ya ardhi nchini kwa ajili ya kilimo cha makampuni makubwa na kutumia GMF (Genetically Modified food) vitatuleta kwenye usalama wa chakula? Mikataba ambayo baadhi ya makampuni yatazalisha chakula nchini kwa AJILI YA nchi zao, yatatusaidia sisi vipi? Je, tukija kujisikia kuwa tunaexport chakula na nafaka zaidi wakati watu wetu wanakufa njaa tutashangaa?
Lakini swali la msingi ambalo nalipendekeza kwenu ni KWANINI BADO TUNA TATIZO LA UPUNGUFU WA CHAKULA NCHINI, KITU AMBACHO NYERERE ALIONEKANA AMESHINDWA NA KUBEZWA NA KUBEBESHWA LAWAMA? Kwanini mtazamo huo wa upungufu wa chakula wakati wa Mwalimu hauonekani wakati huu? au hadi kitokee nini?