BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,789
- 288,015
Kuwakamatwa wamiliki wa Tashrif kuwe somo kwa wengine
Gloria Tesha
Daily News; Wednesday,January 14, 2009 @20:00
Gloria Tesha
Daily News; Wednesday,January 14, 2009 @20:00
Ajali za barabarani hapa nchini si jambo jipya au geni masikioni mwako msomaji, bila shaka umesikia matukio hayo katika maeneo unakoishi au hata katika mikoa mbalimbali.
Matukio ya ajali yamekuwa yakisababisha vifo vya watu wengi hasa nikikumbuka ile iliyotokea majuzi tu, katika Kijiji cha Hale, wilayani Korogwe, Tanga na kuhusisha basi la kampuni ya Tashrif linalofanya safari zake kati ya Dar es Salaam na Tanga. Katika ajali hiyo watu 28 walikufa na wengine 22 walijeruhiwa.
Ajali hiyo ni miongoni mwa ajali nyingi mbaya kuwahi kutokea nchini ikijumlishwa pia ile iliyotokea takriban wiki mbili zilizopita katika eneo la Uchira, Kilimanjaro na kusababisha vifo vya watu 11, ndugu wa familia moja. Ajali nyingine mbaya kutokea mkoani Tanga ni iliyohusisha basi la No Challenge iliyotokea mwaka 1998 na kusababisha vifo vya abiria karibu 70.
Si lengo langu kueleza historia ya ajali zilizowahi kutokea kipindi cha nyuma au hata hivi karibuni, bali ni kukupa taswira ya namna ndugu, jamaa na marafiki zetu walivyopoteza maisha, viungo na kupata ulemavu wa maisha kutokana na ajali hizo ambazo nyingi zinaweza kuepukika.
Kikubwa zaidi ni hatua iliyochukuliwa na polisi wa mkoa huo ya kuwakamata wamiliki wa kampuni inayoendesha mabasi hayo. Sifurahii kukamatwa kwao, kwa kuwa anayejua kuwa wana kosa au hawana ni vyombo vya dola (mahakama) lakini kwa mujibu wa Kamanda wa Tanga, Simon Sirro katika mahojiano na gazeti hili katika habari iliyoandikwa jana, inasemekana kuwa wamiliki hao wanadaiwa kuruhusu gari kufanya safari ya kubeba abiria huku wakijua kuwa ni bovu.
Madai mengine ni kushindwa kutunza kumbukumbu za dereva wao aliyetoroka mara baada ya ajali kutokea Januari 10 mwaka huu, hivyo polisi kushindwa kujua kama alikuwa ni dereva kweli ama la.
Madai hayo kama ni kweli yanadhihirisha wazi kuwa kuna udhaifu mkubwa kwa wamiliki wa mabasi kutokuwa na muda wa kufuatilia hali ya magari yao badala yake wamekuwa wakifurahia kukusanya fedha zitokanazo na mapato bila kuhoji uzima wa magari yao.
Inakuwaje mmiliki wa kampuni ya magari ya kubeba abiria (mabasi) kama huyu wa Tashrif anakosa kuwa na kumbukumbu za dereva wake? Sitaki kuamini suala hilo pengine mpaka baada ya uchunguzi wa polisi ukamilike, lakini pia ni madai ambayo yamebainika baada ya kuhojiwa na polisi.
Eti mmiliki wa gari hana hata nakala ya leseni ya dereva wake! Hata hana maelezo binafsi yanayomhusu dereva huyo. Hii inadhihirisha wazi kuwa baadhi ya wamikili huajiri madereva wa uchochoroni, wasiokuwa na sifa wala vigezo bila shaka kwa kuwa labda ni mjomba au shangazi.
Hali hii isipodhibitiwa, itatumaliza. Pamoja na Mkuu wa Polisi nchini, Inspekta Jenerali, Said Mwema jana kupitia gazeti hili kukiri kuwa bado kuna udhaifu wa kuhimili ajali za barabarani kwa polisi nchini kutokana na kukosa umahiri katika kazi, pia tukubali kuwa wamiliki, madereva na hata abiria wamekuwa wakichangia kutokea kwa ajali kama tunavyoshuhudia kwa ajali hii ya Tanga.
Mara nyingi tumesikia na kushuhudia abiria wakimlazimisha dereva kufanya jambo la hatari, mfano; kumlazimisha dereva aongeze mwendo au kumpita mwenzake, ushabiki huu umesababisha maisha ya wengi kupotea.
Ndiyo maana nasema wamiliki kama hawa wanapaswa kuwa mfano kwa wengine, si kwamba nawahukumu kwa tukio hilo la ajali lakini iwe njia mojawapo kuwapa angalizo wamiliki wenye tabia ya kupuuza ubovu wa magari yao au kuhifadhi kumbukumbu ya madereva.