Kuteua watendaji kwa kufuata u-CCM wao tunavunja Katiba

sulphadoxine

JF-Expert Member
Nov 1, 2010
2,257
645
TANZANIA tuliingia kwenye demokrasia ya mfumo wa vyama vingi vya siasa mwaka 1992 baada ya kupitishwa sheria Na. 4 ya mwaka 1992 ambayo pia ilifuta ibara ya 10 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliyokuwa inatoa mamlaka kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kusimamia Serikali (nafasi na mamlaka ya Chama, Sheria ya 1984 ibara ya 6).

Baada ya Tanzania kuingia kwenye mfumo wa demokrasia ya vyama vingi na mamlaka ya chama kufutwa, bado baadhi ya viongozi wa ngazi za juu serikalini wanaendelea kufuata mfumo huo na kwa kuwa wengi ni washauri wa Rais kuna uwezekano mkubwa ushauri wanaompatia Rais ukawa na upungufu mkubwa.

Hata hivyo nashukuru, Rais Jakaya Mrisho Kikwete aliona tatizo hilo na katika hotuba yake alipokuwa anafungua Bunge mwaka 2005 aligusia suala hilo na kutamka, “Ni kweli nchi yetu sasa ni ya demokrasia ya vyama vingi vya siasa, lakini ni wazi bado utamaduni wa mfumo huu wa siasa ni mchanga na kwa ujumla haujaimarika vya kutosha. Serikali ya Awamu ya Nne itajitahidi kutimiza wajibu wake katika kujenga na kuimarisha utamaduni wa mfumo wa vyama vingi.”

Ibara ya 9 ya Katiba yetu inaelezea kwa kina malengo ya Katiba na kusisitiza utekelezaji wa misingi ya Ujamaa na Kujitegemea pale inapotamka, “Kwa hiyo, mamlaka ya nchi na vyombo vyake vyote vinawajibika kuelekeza sera na shughuli zote katika lengo la kuhakikisha kwamba, 9 (h) aina zote za dhulma, vitisho, ubaguzi, rushwa, uonevu au upendeleo zinaondolewa nchini”.

Ni jambo lisilofichika kwamba serikali zote zilizoingia madarakani baada ya kuanzishwa kwa demokrasia ya vyama vingi vya siasa ziliendelea na uteuzi wa watu kushika nafasi za madaraka kwa kuzingatia sheria ya mwaka 1984 Na. 15: ambayo ilianzishwa wakati wa mfumo wa chama kimoja.

Hatua hiyo inafanya mamlaka za uteuzi kuendelea na mtazamo potofu wa chama kushika hatamu hivyo kulazimu kuwateua wanachama wa CCM pekee kushika nafasi nyeti, jambo ambalo ni kuwabagua wananchi kwenye ajira kinyume na katiba yetu, na hasa ikizingatiwa kwamba hii ni ya vyama vingi na wakati huo huo asilimia kubwa ya Watanzania si wanachama wa makundi haya yanayoitwa vyama.

Serikali kuendelea na mtazamo wa kufanya uteuzi wa watu kwenye nafasi za uongozi ndani ya serikali na taasisi za umma kama wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya na wakurugenzi wa mashirika ya Umma kwa kuzingatia maoni ya kisiasa ya mtu ni ukiukwaji mkubwa wa Katiba yetu.

Serikali zote zilizopita zilikataa kwa makusudi kabisa kuwashirikisha watu ambao sio wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwenye nafasi za uongozi wa Serikali na Utumishi wa Umma kwa madai kwamba ni wapinzani.

Neno upinzani lilitumika visivyo na bado hadi leo hii kuna baadhi ya viongozi wa serikali wanaendelea na dhana potofu kuwabagua wananchi kwa misingi ya maoni yao ya kisiasa kinyume na Katiba yetu ibara ya 13(i) inayosema, “Watu wote ni sawa mbele ya sheria na wanayo haki bila ubaguzi wowote, kulindwa na kupata haki sawa mbele ya sheria”.

Kama mtu ambaye ni mwanachama wa Chadema, CUF, UDP, TLP au NCCR-Mageuzi inaonekana dhahiri kwamba haruhusiwi kufanya kazi za aina fulani za serikali na umma. Huo “usawa na bila ubaguzi wowote” uko wapi? Na je, serikali kuendelea kuwateua watu kushika nafasi za madaraka ambao ni wanachama wa CCM pekee sio ubaguzi?

Ibara ya 13(40) ya Katiba yetu inakataza ubaguzi wa aina yoyote na inatamka, “Ni marufuku kwa mtu yeyote kubaguliwa na mtu au mamlaka yoyote inayotekeleza madaraka yake chini ya sheria.

“Neno kubagua maana yake ni kutimiza haja, haki au mahitaji mengineyo kwa watu mbali mbali kwa kuzingatia utaifa wao, kabila, watu wanakotoka, maoni yao ya kisiasa, rangi, dini, jinsia au hali yao ya maisha”.

Katiba inampa Rais mamlaka ya kuanzisha na kuwateua watu kushika nafasi za madaraka (angalia Katiba yetu sura ya 2 ibara ya 33-61) ibara ya 61(2) inampa Rais mamlaka ya kuteua wakuu wa mikoa katika Tanzania Bara. (2) baada ya kushauriana na Waziri Mkuu.

Lakini kwa zaidi ya miaka 20 iliyopita tangu tuingie kwenye demokrasia ya vyama vingi vya siasa (1992- 2010) wakuu wote wa Mikoa na Wilaya walioteuliwa na wanaoendelea kuteuliwa wote ni makada wa CCM huku walio katima vyama vingine wakibaguliwa kwa misingi ya siasa kinyume na Katiba.

Kwa nini, miaka 20 baada ya nchi kuingia kwenye mfumo wa vyama vingi vya siasa Serikali inaendelea kuwabagua wananchi kwenye ajira za serikali na taasisi za umma, hasa hizi za kuteuliwa na Rais kama Wakuu wa Mkoa, Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi na wajumbe wa Bodi za Taasisi za Umma, pamoja na mabalozi wa nchi za nje zifanywe kisiasa ambapo ni ukiukwaji wa Katiba?

Ibara ya 37 inampa Rais uhuru wa kuteua mtu yeyote kushika nafasi yoyote lakini pia ibara hii inazungumzia Rais asifanye uteuzi kwa ubaguzi. Angalia ibara 37(10), “Mbali na kuzingatia masharti yaliyomo katika katiba hii na sheria za Jamhuri ya Muungano katika utendaji wa kazi na shughuli zake, Rais atakuwa huru na hatalazimika kufuata ushauri atakaopewa na mtu yeyote isipokuwa tu pale anapotakiwa na Katiba hii au sheria nyingine yoyote”.

Rais anatakiwa na Katiba kutobagua mtu kwa misingi ya maoni yake ya kisiasa anapofanya uteuzi (Katiba ibara 13(4) (5). Serikali inatakiwa itoe maelezo kwa nini hadi leo miaka 20 tangu kuanzishwa kwa demokrasia ya vyama vingi na kufutwa kwa mamlaka ya chama kimoja (ibara ya 10 ya katiba) bado serikali inaendelea na utekelezaji wa shughuli zake kwa kuzingatia mfumo wa chama kimoja cha siasa hivyo kuwanyima kazi wananchi wenye sifa ambao sio wanachama wa CCM?

Baadhi ya wagombea wa vyama vingine walioshindwa Ubunge mwaka 1995, 2000 na 2005 walipoamua au walipolazimika kurejea CCM waliteuliwa kuwa Wakuu wa Wilaya na wengine kupata nafasi za Ubunge wa kuteuliwa na Rais.

Kumteua mtu baada ya kujiunga na CCM ni sawa na kumlazimisha mtu kewamba ili apate ajira serikalini ama kwenye sekta yoyote ya umma, ni lazima awe mwanachama wa CCM kinyume na katiba. Katiba yetu, ibara ya 20(4) inasema, “Itakuwa ni marufuku kwa mtu yeyote kulazimishwa kujiunga na chama chochote au shirika lolote au chama chochote cha kisiasa, kukataliwa kusajiliwa kwa sababu tu ya itikadi au falsafa ya chama hicho”.

Kama serikali inaona mtu anafaa kwenye nafasi fulani kwa nini asipewe? Kwani hawezi kufanya kazi hiyo akiwa kwenye chama chake? Kurudi au kujiunga na CCM kunamuongezea sifa zipi? Kama ubaguzi wa namna hiyo ukiendelea dhana ya upendo na mshikamano inayohubiriwa na Rais Kikwete itakuwa ni ndoto.

Ninaandika haya nikijua tunajiandaa na kuandika Katiba mpya na bila shaka tutajitahidi kuzingatia hali hii. Lakini, kwa vile Rais anaendelea na uteuzi, nimeandika hapa kumkumbusha kwamba uteuzi wake mwingi wa nafasi zinazofanana na ajira unavunja katiba kwa sababu unapendelea

Tukumbuke kwamba vyama vingi lakini taifa ni moja.
 
Back
Top Bottom