Kikwete na migomo yake

AMARIDONG

JF-Expert Member
Jun 24, 2010
2,502
180
MARA nyingi tumekuwa tukishuhudia baadhi ya wafanyakazi wa kampuni au viwanda wakiingia katika migomo na migogoro kutokana na madai ya kutaka kuboreshewa haki zao mishahara ikiwemo.
Migomo hiyo hutokea katika taasisi za serikali na zisizokuwa za serikali kwa kuwahusisha waajiri na waajiriwa.
Wafanyakazi wengi wamekuwa wakiamini kwamba njia ya mgomo inaweza kusaidia kusikilizwa kilio na menejimenti kukaa chini na kuangalia njia mbadala kuwaboreshea maslahi yao.
Hali hiyo ndiyo iliyotokea hivi karibuni katika kiwanda cha kutengeneza mablanketi (Blanket Textile) kilichoko Chang’ombe Dar es Salaam ambapo wafanyakazi wake wameingia katika mgomo na mwajiri wao kutokana na madai mbalimbali.
Wafanyakazi hao wako katika mgomo takriban wiki sasa hawajaingia kiwandani kwa ajili ya kufanya uzalishaji wakimshinikiza mwajiri kuwaboreshea kiwango cha mshahara pamoja na marupurupu mengine.
Matukio ya aina hiyo huwa yanaambatana na migomo, maandamano na zaidi uharibifu wa mali za taasisi husika.
Lakini vurugu za migomo zinazotokea katika sehemu za kazi huwa zinasababisha machafuko ikiwa ni pamoja na wengine kupoteza maisha ama kupata vilema vya kudumu.
Hata hivyo mara baada ya kumalizika kwa mgomo husika, waajiri huwa wanajichukulia sheria zao kwa kuwafukuza baadhi ya wafanyakazi ambao kwa namna moja ama nyingine walionekana kuwa ni vinara wa mgomo huo hata kama walikuwa sahihi kudai maslahi yao.
Katika makala hii Tanzania Daima iliyofika kiwandani hapo na kufanya mazungumzo na Kaimu Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi (TUICO) Ramadhan Khalfan ambaye anasema wako katika mgomo kuushinikiza uongozi kuwaongezea kipato chao lakini hadi sasa hawajui hatma yao kutokana na menejimenti hiyo kukaa kimya.
Zaidi ya wafanyakazi 85 wa kiwandani hapo wako katika mgomo wa kuitaka menejimenti kukaa nao na kufanya mazungumzo ili waweze kuboreshewa maslahi yao kwa kuwa wanataabika na kudai kuwa maisha ni magumu.
Khalfan anasema takriban mwaka wa tisa sasa wanalipwa ujira mdogo wa sh 80,000 ambapo wanashindwa kujitosheleza katika matumizi yao na hata kuiangalia familia na kusomesha watoto wao.
Aidha anasema ingawa wanalalamikia mshahara wa sh 80,000 kwa mwezi kutowatosha lakini pesa hizo hizo wanakatwa na kupelekwa katika Mfuko wa Pensheni (PPF).
“Mshahara huo ni mdogo lakini pia katika kiasi hicho hicho tunakatwa kiasi cha sh 4000 kwa ajili ya kupelekewa PPF…cha kushangazwa fedha hizo hazijapelekwa huku tukiwa tumekatwa kwa miaka tisa sasa,” anasema Khalfan.
Anasema hata uzalishaji katika kiwanda umeshuka kutokana na kuwa hapo awali kilikuwa na mashine nane lakini hadi sasa zimebakia mashine mbili, huku kukiwa hakuna malighafi zozote za kuzalisha bidhaa kiwandani hapo.
Aidha Khalfan anadai wamekuwa wakipeleka malalamiko mara kadhaa kwa mwekezaji wa kiwanda hicho lakini wanapata majibu ya kukatisha tamaa.
Wafanyakazi hao wameitaka serikali kuingilia kati ili waweze kulipwa haki zao kwa kuwa wapo kiwandani hapo tangu mwaka 1998.
Mwekezaji wa kiwanda hicho ambaye ni mzalendo alipotafutwa ili azungumzie malalamiko hayo kutoka kwa wafanyakazi lakini haikufanikiwa kumpata.
Tanzania Daima ilipotaka kuingia katika ofisi za kiwanda hicho kwa ajili ya kuzungumza na mkurugenzi haikuruhusiwa lakini ilifanikiwa kupata namba ya simu ya meneja mwajiri.
Meneja Mwajiri Kassim Shabani anasema yeye kazi yake ni kuajiri wafanyakazi wanaofanya kazi katika kiwanda hicho cha blanketi na si kuzungumza na vyombo vya habari.
“Mimi sio mzungumzaji wa kiwanda hiki… mimi kazi yangu kuajiri na si vinginevyo hivyo naomba umtafute mzungumzaji alitolee ufafanuzi,” anasema Shabani.
Mwanajiri huyo anasema kama nitakuwa na shida na kumpata mzungumzaji niwasiliane na aliyenipa namba yake ya simu ndio kwani atakuwa pia na namba ya mmiliki wa kiwanda hicho. Kutokana na hali hiyo serikali inatakiwa kuwa macho na wawekezaji wa ndani na nje ya nchi ili kuweza kuleta maendeleo kwa pande mbili yaani mwajiri na mwajiriwa.
 
Vyama vya wafanyakazi vipo tu, disorganized, ndo maana migomo yote hazijatoa tangible results!
 
Back
Top Bottom