Suley2019
JF-Expert Member
- Oct 7, 2019
- 1,815
- 4,565
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Masanja Kadogosa amesema Treni ya Reli ya Kisasa (SGR) imetumia umeme wa Sh336,000 katika safari ya abiria ya majaribio kutoka jijini Dar es Salaam mpaka Morogoro na kurudi leo Februari 26, 2024.
“Miundombinu ya treni ya umeme ni gharama kubwa ukilinganisha na ile ya inayotumia mafuta lakini kwenye gharama za uendeshaji wa treni ya mafuta ni mara tatu ukilinganisha na treni ya umeme,” amesema Kadogosa alipokuwa akifanya mahojiano na Wasafi FM.
Akizungumzia kuhusu nauli za abiria zitakazotumika, Kadogosa amesema shirika hilo limewasilisha mapendekezo yake kwa Latra yenye jukumu la kutangaza nauli hizo.
Ameongeza kuwa, upatikaaji wa mizigo mingi utachangia kupungua kwa nauli kwenye treni ya abiria na kufanya watu wengi wawe na uwezo wa kumudu bei za kupanda treni hiyo.
“Tunatarajia kupata fedha zaidi kwenye mizigo na ndio maana unaona tunajenga reli kwenda Msongati sababu kuna machimbo ya Nikel, tunakwenda kwa sababu tutapata mzigo kutoa kule na kupeleka bandarini. Upatikanaji wa mzigo ndio utatufanya tusiwe na bei kwenye treni ya abiria,” amesema.
Treni ya umeme ya abiria imefanya safari ya kwanza ya majaribio hii kutoka Dar es Salaam kwenda Morogoro huku ikitumia takribani saa nne kwenda na kurudi.