JK na CCM ni "Dr. No" wakati Dr. Slaa na Chadema ni "Dr. Yes"

Rutashubanyuma

JF-Expert Member
Sep 24, 2010
219,470
911,173
Hali hii kweli inashangaza kabisa. Ungelitegema JK na CCM kwa kile wanachokiita ni wazoefu wa utawala wangelikuwa mstari wa mbele kusema "YOTE YANAWEZEKANA" lakini wao sasa wamekuwa mstari wa mbele kudai "YOTE HAYAWEZEKANI." Hili linashtua sana kwa Chama kinachodai ni mbunifu wa njozi ya "MAISHA BORA KWA KILA MTANZANIA" sasa kukiri hadharani kumbe hakina program ya kutuletea neema hizo.

Dr. Slaa na Chadema kwenye Ilani yao ya uchaguzi wamesema elimu bure hadi kidato cha sita inawezekana lakini Jk na CCM wanasema hizo ni njozi...........Sasa CCM inafikiri "MAISHA BORA KWA KILA MTANZANIA" yatatoka wapi kama elimu haitakuwa bure?

Dr. Slaa na Chadema wanasema afya bure inawezekana lakini JK na CCM yake wanasema hapana........Sasa CCM inafikiri "MAISHA BORA KWA KILA MTANZANIA" yatatoka wapi kama afya haitakuwa bure?

Dr. Slaa na Chadema wanasema vifaa vya ujenzi kuondolewa kodi ili kumpunguzia mwananchi gharama za ujenzi na hivyo kuongeza kasi ya ujenzi wa makazi ya raia na kuachana na nyumba za tembe lakini JK na CCM wanasema haiwezekani hata kidogo na wanakuja na vihunzi vya EAC....Sasa CCM inafikiri "MAISHA BORA KWA KILA MTANZANIA" yatatoka wapi kama vifaa vya ujenzi vitaendelea kuwa ghali?

Dr. Slaa na Chadema wanasema ya kuwa pesa za kutoa huduma hizi zote zitatoka katika kufuta misamaha ya kodi kwa wawekezaji wakubwa ambao wanatumia mianya ya kifisadi kutochangia maendeleo ya nchi hii. Mifano wanayotoa ni pamoja na misamaha ya kodi ya zaidi ya Tshs 700 bilioni kwa wachimba madini wakubwa...CCM na haswa JK wanasema hilo hapana tutafukuza wawekezaji na hivyo kuthibitisha ya kuwa CCM ni "Dr. No" na Wenzao ni "Dr. Yes"

Dr. Slaa na Chadema mwishowe wasema "TANZANIA BILA CCM YAWEZEKANA" lakini JK na CCM wang'aka haiwezekani....Sasa CCM inafikiri "MAISHA BORA KWA KILA MTANZANIA" yatatoka wapi kama JK na CCM yake ambayo ni "Dr. No" wataendelea kukwamisha maendeleo?

Tathmini hii kwa uwazi kabisa imethibitisha ya kuwa JK na CCM yake ni akina "Dr. No" wakati Dr. Slaa ni "Dr. Yes" katika kutuleta njozi ya "MAISHA BORA KWA KILA MTANZANIA"
 
Back
Top Bottom