Elections 2010 JK akiri wizara zinanuka rushwa; Awaagiza watendaji waiokomeshe ili CCM ishinde 2015

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797




*Awaagiza watendaji waiokomeshe ili CCM ishinde 2015
*Asisitiza nidhamu ya matumizi ya fedha za walipakodi
*Makamu wa Rais: Ufisadi ulipunguza ushindi wa CCM


Na Pendo Mtibuche, Dodoma

RAIS Jakaya Kikwete amekiri kuwa vitendo vya rushwa vimekithiri katika wizara na idara za serikali na
hivyo kuwaagiza mawaziri, manaibu wao na watendaji wengine wakuu kuisafisha ili Chama Chama Mapinduzi kipewe ridhaa ya kuendelea kuongoza mwaka 2015.

Alibainisha kuwa vitendo vya rushwa hivi sasa vinatendeka ndani ya wizara na idara mbalimbali za serikali hivyo hatua za haraka za kukabiliana na tatizo hilo ni mawaziri, manaibu wao, makatibu wakuu na manaibu wao kujisafisha ili waweze kufanana na mabango yaliyopo katika ofisi zao.

Alisema kuwa ili serikali iliyopo madarakani iweze kuendelea baada ya uchaguzi wake wa 2015 ni lazima viongozi hao waanze kuweka maandalizi mazuri ya uchaguzi unaokuja kwa kujisafisha na rushwa na kujali maslahi ya wananchi wanaowaongoza.

Rais Kikwete aliyasema hayo jana wakati akifunga semina elekezi kwa viongozi na watendaji wakuu wa serikali ambayo ilifanyika kwa muda wa siku saba mjini Dodoma ambapo rais alisema kuwa semina hiyo imekuwa na mafanikio makubwa ukilinganisha na iliyofanyika Ngurudoto Mkoani Arusha katika kipindi chake cha kwanza.

Rais alisema kuwa katika utekelezaji wa shughuli mbalimbali kwa viongozi hao wa serikali lazima waweke mbele nidhamu ya matumizi ya fedha za umma, hivyo suala la viongozi kutosimamia vita dhidi ya rushwa kikamilifu katika idara zao ni tatizo.

Alisema kuwa rushwa inayotendekea hivi sasa inatendeka chini ya wizara na idara za chini ambazo viongozi hao wanazifanyia kazi, hivyo lazima viongozi hao wachukue hatua katika kukabilia na vita dhidi ya rushwa.

“Hakuna mtu mwingine anayeweza kupigana na tatizo hilo. Wakati natembelea wizara mbalimbali nilikuwa nakutana na mabango makubwa mbele ya wizara nyingi ambayo yana ujumbe wa unaosema hapa si mahala pa rushwa, ninachowaomba mabango hayo yafanane na mwenendo na tabia halisi ya maneno yaliyopo katika mabango hayo,” alisema.

Alisema kuwa mabango hayo ya rushwa yafanane na tabia na muundo wa wizara husika na afisa anayefanya kazi katika ofisi hiyo lazima aendane na upigaji vita rushwa kwani hakutakuwa na maana kama mabango hayo yataendelea kuwepo kwenye wizara lakini utekelezaji ukawa haupo, hicho kitakuwa ni kiini macho na kichekesho kwa wananchi.

“Piganeni muonekane mnapigana na tatizo hilo na mkifanya hivyo mtakuwa mmefanya kazi kubwa ya kuondoakana na kero hii ya rushwa katika nchi, hivyo lazima mfanye kazi kwa kufuata katiba, utawala wa sheria na taratibu zilizowekwa,” alisema.

Alisema kuwa kila waziri, naibu waziri, katibu mkuu na naibu katibu mkuu anapotoka katika mkutano huo ahakikishe kuwa anaenda kutekeleza suala hilo kwa umakini mkubwa kwani kuondoa rushwa ndani ya maofisi kutawezesha kuwepo kwa utendaji unaojali maslahi ya wananchi.

Alisema kuwa lazima nidhamu ya fedha za umma iwepo kwani wananchi wanapenda kuona ukusanyaji wa mapato unaimarika na kuongeza uwezo wa serikali katika kuongeza mapato ya wananchi.

Rais alisema kuwa wananchi wanatarajia baada ya semina hiyo kumalizika wataona mabadiliko ndani ya serikali kwa viongozi kufanya kazi karibu na nao na kutatua kero zao ili kuwaletea maendeleo.

Alisema kuwa ni lazima viongozi hao wafanye kazi kwa umakini mkubwa wawe wabunifu na wenye kuona mbali zaidi juu ya changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi ikiwa ni pamoja na kuwataka viongozi hao kupanga mipango yao kwa umakini katika sekta za uzalishaji na uchumi katika serikali.

Alirudia kuwakumbusha viongozi hao kutoka katika maofisi yao na kwenda vijijini kwa wananchi waliko ili kuwasikiliza kero zao na kuwatatulia kuliko kuendekeza kukaa maofisini huku wananchi wakilalamikia huduma.

Alisema viongozi hao ndiyo wenye majibu ya wananchi, hivyo viongozi hao wanapaswa kwenda mikoani wilayani na hata vijijini kwa ajili ya kujionea wao wenyewe kero za wananchi na kuzipatia majibu na kuyatolea taarifa.

Alisema kuwa lazima viongozi hao wajenge tabia ya kutoa taarifa kwenye vyombo vya habari juu ya mambo mbalimbali wanayoyatekeleza na wasiwaache waandishi watafute habari wao wenyewe wakati wao wapo na mamlaka ya kutoa habari wanayo.

Alisema kuwa ili Chama cha Mapinduzi kiweze kushinda uchaguzi 2015 ni lazima viongozi hao wawajibike kikamilifu kwa kutoa taarifa sahihi za mambo mbalimbali ynayotekelezwa na serikali na hayo ndiyo yatakayokuwa maandalizi mazuri kwa chama hicho katika uchaguzi ujao.

Wakati huo huo, Mwajuma Juma anaripoti kuwa Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi amesema kuwa CCM ilipata ushindi mdogo katika uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka jana, kutokana na kushamiri kwa
vitendo vitendo vya ufisadi, vilivyofanywa na baadhi ya viongozi katika kura za maoni.

Balozi Seif alitoa kauli hiyo Kisiwani Pemba wakati akizungumza na viongozi wa chama hicho kufuatia ziara yake ya siku mbili kisiwani humo.

Alisema kuwa katika kura ya maoni ya kuchagua viongozi watakaogombania nyadhifa katika majimbo kulifanyika vitendo vya ufisadi na rushwa na kupelekea wanachama wao wengi kupoteza imani kwa wagombea hao ambao walipita bila ya kuwa na ridhaa zao.

“Tabia ya baadhi ya viongozi kujishirikisha na vitendo vya ufisadi kwa mali za umma kumesababisha wananchi kupoteza imani na chama ndio maana CCM imeamua kujivua gamba kwa kuwatimuwa viongozi wasiokuwa waadilifu,” alisema Balozi Seif.

Alisema kuwa kutokana na hali hiyo chama hicho sasa kimeamua kujipanga upya katika safu zake za uongozi upya, kwa kuzingatia kaulimbiu ya kujivua gamba.

“Lengo kubwa ni kudhibiti njia zote zinazopelekea ushawishi wa rushwa, hasa wakati wa kutafuta viongozi ili waweze kupatikana viongozi waadilifu na wenye kuzingatia misingi ya utawala bora,” alisema Balozi Seif na kuwataka viongozi kuwa makini wakati wa uchaguzi kwa kuwachagua viongozi bora na si bora kiongozi.

Aidha Balozi Seif ambae pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa alisema kuwa CCM haitomvumilia kiongozi yeyote ambaye atabainika ushindi wake umepatikana kwa ushawishi wa rushwa, kwa vile vitendo hivyo vinakwenda kinyume na maadili ya katiba ya chama hicho.

Katika uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka jana CCM ilipoteza viti vitatu katika ngome yake kisiwani Unguja likiwemo jimbo la Magogoni, Mtoni na Nungwi.
 
Tumechoshwa na maagizo ya huyo mzee, hana jipya badala ya kuwaza kupunguza ukali wa maisha anawzia uchaguzi wa 2015. Huo uchaguzi atakichagua nani ccm kwa hali ilivyo kwa sasa hata kwa nini ccm haiwezi kuongoza nchi hii tena, hata awamu hii sijui kama itamaliza.
 
The only power of our government has is the power to crack down on criminals. Well, when there aren't enough criminals, one makes them. One declares so many things to be a crime that it becomes impossible for men to live without breaking laws but still our government let them go... Fisadi's Mmmm...
 
Ama kweli dunia hakuishi maajabu, kwa gharika yote hii ya ufisdi kila mahali hadi ikulu bado tu mtu Kikwete anaota kushinda kiti zaidi hata cha udiwani wa kule kata Magogoni kulikojengwa ikulu?????????????

Mmmmmmmmmmmmmmmmmm, makuwaaaa!!!!!!!!!!!!!!!!!!!
 
Ili hayo anayosema yawezwe kufuatwa, inabidi viongozi, hasa yule aliye wa juu kabisa aonnyeshe mfano. Kama ukiwa baba kwenye nyumba huwezi kukanya wanao waache ulevi kama wewe ni chapombe.
 
Back
Top Bottom