Hoja ya mgombea binafsi iliporwa, sasa imerudishwa!

Kiganyi

JF-Expert Member
Apr 30, 2012
1,242
765
Wednesday, 30 May 2012 09:08 0digg

0000000001christopher%20mtikila.jpg

Na Mwandishi Wetu
BAADA ya Mahakama ya Rufani ya Tanzania kutoa hukumu yake ya Juni 16, 2010, kuhusu suala la mgombea binafsi na hatimaye kufuta kabisa ndoto ya Watanzania kupata haki hiyo, sasa matumaini yameanza tena kuonekana.
Hukumu hiyo ilitolewa na jopo la majaji saba akiwemo Jaji Mkuu mstaafu Agustino Ramadhan, Eusebio Munuo, Januari Msofe, Benard Luanda, Mbarouk Mbarouk, Nathalia Kimaro na Sauda Mjasiri ambao walidai kuwa mahaka haina mamlaka ya kutengua ibara ya Katiba.
Moto wa kuwepo kwa mgombea binafsi katika chaguzi za kisiasa ulianzishwa na Mchungaji Christopher Mtikila alipofungua kesi ya kikatiba katika Mahakama Kuu, Kanda ya Dodoma mwaka 1993 akiiomba iruhusu kuwepo kwa mgombea binafsi.

Katika hukumu iliyotolewa Oktoba 24, 1994 na Jaji Kahwa Rugakingira, Mchungaji Mtikila aliibuka mshindi.

Hata hivyo, Serikali ilikata rufaa Mahakama ya Rufani, lakini wakati rufaa hiyo ikisubiri usikilizwaji na uamuzi, Serikali ilipeleka muswada bungeni na kufanya marekebisho ya kikatiba na kuweka ibara inayotamka kuwa kila mgombea ni lazima awe amependekezwa na chama cha siasa.

Februari 17, 2005, Mchungaji Mtikila alifungua kesi nyingine Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam akipinga marekebisho hayo ya Katiba ya mwaka 1994. Katika kesi hiyo alikuwa akiiomba Mahakama hiyo pamoja na mambo mengine, iamuru kuwepo kwa mgombe binafsi.

Katika hukumu iliyotolewa Mei 5,2006, Mchungaji Mtikila aliibuka mshindi kwa mara nyingine baada ya Mahakama Kuu kukubaliana na hoja na maombi yake na kuwepo kwa mgombea binafsi.

Hukumu hiyo ilitolewa na na jopo la Majaji watatu wa Mahakama Kuu wakiongozwa na aliyekuwa Jaji Kiongozi, Amir Manento, Salum Massati na Thomas Mihayo.

Serikali ilikata tena rufaa katika Mahakama ya Rufani, ikipinga uamuzi huo wa Mahakama Kuu, iliyosikilizwa na Jopo la Majaji Saba wa Mahakama ya Rufani Aprili 8, 2010 na hatimaye kushinda.

Baada ya kuona hivyo, Mchungaji Mtikila pamoja na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu walifungua kesi nyingine katika mahakama ya Afrika wakiendelea kudai haki hiyo. Kesi hiyo inatarajiwa kusikilizwa Juni 15 na 16 mwaka huu jijini Arusha.

Hata hivyo Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM iliyoketi hivi karibuni imebariki suala la kuwepo kwa mgombea binafsi.
Hoja ya mgombea binafsi imekuwa ikipingwa na chama hicho kwa muda mrefu kwa hofu kuwa ingeweza kukiumiza pindi wanachama wake wanaposhindwa kura za maoni, kwani wangeweza kusimama binafsi na kushinda.
Mbali na mgombea binafsi Nec ya CCM pia imeruhusu kuwepo kwa mjadala wa kuhoji mahakamani matokeo ya uchaguzi wa Rais, uwezekano wa kuwa na serikali tatu, kupunguza madaraka ya Rais, kuwa na Tume huru ya uchaguzi, kuwa na mgombea huru na kujadili kero za Muungano.

Akizungumza katika kipindi cha Jenerali on Monday hivi karibuni Katibu wa itikadi na uenezi CCM Nape nnauye amesema kuwa chama hicho hakijawahi kuhofu hoja hiyo,

“Mimi nakumbuka tuliwahi kujadili wakati kesi iko mahakamani, hatukutoa tamko kwa sababu kesi ilikuwa mahakamani. Tena tunapaswa kupongezwa hatukuingia mihimili ya dola kufanya kazi zakw” anasema Nape na kuongeza kuwa kama mgombea binafsi ataruhusiwa basi watakaoathirika ni vyama vya upinzani.
“Leo kama kuna watu watapata hasara kwa kuwa na mgombea binafsi basi ni vyama vya ushindani siyo CCM. Leo tunao wabunge waliokuwa CCM wakaona kuwa hawakutendewa haki wakajiondoa na kwenda upinzani.
Kama kungekuwa na mgombea binafsi wasingekuwa kule. Hasara hii ni kwa wapinzani kwasababu wamezoea kusubiri, hata ukiangalia uteuzi wao…..”
Naye January Makamba aliyekuwepo katika mjadala huo anasema Serikali ilipokata rufaa kuhusu hoja hiyo, haikwenda kupinga mgombea binafsi bali ilikwenda kupinga utaratibu wa kubadilisha Katiba,
“Sisi hatupingi mgombea binafsi, wajibu wetu ni kutetea Katiba na wenye wajibu wa kubadilisha Katiba ni Bunge, ndiyo maana mahakama ikasema kama tunataka kubadilisha Katiba twende Bungeni….”anasema Makamba.
Hata hivyo kwa upande wake msemaji wa Chadema John Mnyika amekanusha kuwa hoja hiyo itakuja kuathiri vyama vya upianzani akisema kuwa, chama hicho kimekuwa kikiitetea tangu kilipoanzishwa.
“Tangu Chadema imeanzishwa ilikuwa ikitetea hoja ya mgombea binafsi. CCM ndiyo walikuwa wakipinga. Ni kejeli kuona leo wanasema eti itaathiri wapinzani. Kama ingekuwa hivyo basi wangeikubali tangu mwazo ili tuathirike basi.”anasema Mnyika.
Anatoa mifano akisema kuwa hata Tume ya Jaji Francis Nyalali iliyoundwa mwaka 1992 kwaajili ya kuwauliza wananchi kama wanautaka mfumo wa vyama vingi ilitoa pendekezo la kuwa na mgombea binafsi lakini CCM ikapinga.
“Tena Mwalimu Nyerere naye aliunga mkono hoja jiyo, lakini CCM iliweka vikao vya kupinga ikihofia kuwa wanachama wake watakimbia.”anaongeza.
Anaendelea kusema kuwa Serikali ya CCM iliendelea kupinga hata kesi mahakamani kiasi cha mahakama kulifanya suala hilo kuwa la kisiasa.
“Hii ni ishara ya nguvu ya umma siyo vyama, kwani vyama vya siasa vina wanachama kwa asilimia 20 tu. Uamuzi wa huu wa CCM ni mkakati wa kuwapata wananchi wanaounga mkono hoja hiyo. Ni mwaka jana tu Serikali yake ilipinga mahakamani, leo wanakubali” amesema Mnyika.

Mnyika amejigamba kwamba hata ikitokeakada yoyote wa Chadema akijitoa leo na kwenda kuwa mgombea binafsi hata fikia nguvu yake kimtandao.
“Ni kweli mtu akijitoa leo tutakuwa tumempoteza, lakini ajue kwamba hatakuwa na wanachama isipokuwa watu wachache watakaomuunga mkono. Kuna faida za kugombea katika chama, kwanza unakuwa na mtandao, mtaji wa sera, wanachama na oganaizesheni. CCM kina mtandao lakini watu wanakihama na wao ndiyo wanaoathirika” anasema Mnyika.
Kwa upande wake mwasisi na mpambanaji wa hoja hiyo Mchungaji Christopher Mtikila anasema kitendo cha CCM kurejea hoja hiyo ni danganya toto na kwamba wataendelea kushikilia msimamo wa kesi waliyofungua hadi haki ipatikane.
“Hao CCM ni danganya toto tu, sisi tumeshafungua kesi na tutasimamia hapo. Ndiyo mambo yao hao, hata wakati ule si ndiyo walioleta ‘white paper’ halafu mwisho wake wakageuka?” anahoji Mtikila.
Amekosoa pia mchakato wa Katiba akisema ni mchezo huo huo.
“Hata hayo mabadiliko ya Katiba ni uongo tu. Wewe uliona wapi mabadiliko ya Katiba yakisimamiwa na Rais? Rais ni sehemu ya Katiba, wenye Katiba ni wananchi. Lakini hata asilimia 20 ya wananchi hawaijui hata hiyo Katiba na wala serikali haiwawezeshi kuijua.
“Tumeteseka mno kuwafumbua macho Watanzania lakini serikali inaendelea kuwapumbaza kwa mwenge wa uhuru.” anasema Mtikila na kuongeza,
“Wewe unawakataza watu wasijadili muungano wakati kiini cha Katiba ni kujadili muungano.”
Naye mwanasheria wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) Wakili Harold Sungusia anasema CCM kimekumbuka shuka wakati tayari kumeshakucha.
“Unajua wakati ule tulipokuwa tukidai haki hiyo, wanasiasa wengi hawakutuelewa. Walichofikiria ni kukimbiwa tu na wanachama bila hata kujali haki ya binadamu. Sasa CCM ndiyo wameona umuhimu wake, huku ni kukumbuka shuka wakati kumeshakucha.”anasema Sungusia.
Sungusia amekishauri CCM kufanya marekebisho ya Katiba hata sasa kama kweli kina nia njema ya kutaka haki ya mgombea binafsi.
“Kama kweli wanataka mgombea binafsi, basi waipeleke Bungeni. CCM wana wabunge wengi na wana Serikali, basi wapeleke muswada na waiunge mkono hata sasa. Kwanini wasubiri mchakato wa Katiba?” anahoji Sungusia.

SOSI; Mwananchi!
 
Ni kweli iliporwa kutokana na mazingira ya wakati ule, kumbuka ndio wakati makundi yalikuwa yamepamba moto ndani ya nyinyi EM, anyway kwa sasa yamekufa makundi kwa kuzalisha vikundi vidogo vidogo na wakati umefika wa wao kuwa chama cha upinzani 2015
 
Big up Mtikila na sungusia(haki za binadamu) kwa movement yenu mtiti hadi ICC kwa okampo(ingawa anastaafu)
 
Back
Top Bottom