Hoja ya kukataa Rais kuratibu uundwaji wa katiba mpya inastahili kuungwa mkono

Ntemi Kazwile

JF-Expert Member
May 14, 2010
2,182
307
Tume ya kukusanya maoni inashangiliwa​



M. M. Mwanakijiji

KATI ya vitu ambavyo Rais Jakaya Kikwete hakuvifanya kwenye salamu zake za mwaka mpya ni kuwaahidi Watanzania Katiba mpya ifikapo 2015.
Alichotuahidi ni kuwa kwanza amekubali hoja ya upinzani ya kuwa Tanzania inahitaji Katiba mpya na pili alikubali hoja ya Dk. Willbrod Slaa kuwa mchakato wa kuelekea Katiba mpya ungeanza ndani ya siku 100 za kwanza za Dk. Slaa.
Katika kuliahidi taifa kuwa hoja ya katiba mpya ina nguvu Rais Kikwete alijipa madaraka yeye mwenyewe ya kuamua namna ya kuelekea katiba hiyo mpya na kutotoa nafasi kwa michango ya mtu mwingine yeyote ile.
Amefanya hivyo kwa kutumia wadhifa wake kama Rais kinyume na kiapo chake cha kulinda, kuitetea na kuihifadhi Katiba iliyopo.
Kukubaliwa kwa hoja ya katiba mpya na Rais Kikwete watu wengi wamekupokea kwa shangwe huku baadhi ya vyombo vya habari rafiki na vya propaganda mamboleo vikitutaka tuamini kuwa "serikali inasikiliza .
Hawa leo wameamka na kupata mwanga na sasa wanakumbatia kwa shangwe hoja ya Katiba mpya. Lakini wote hawa hawataki kuangalia alichoahidi Rais Kikwete hasa ni nini na kwa nini kilivyo sasa kinachostahili pongezi ni yeye hatimaye kuona mwanga na si kitu kingine.
Nimesema Rais hakuahidi Katiba mpya ifikapo 2015; uchaguzi wa mwaka jana uliopita ulionyesha ni kina nani wanataka Katiba hii mpya. Vyama karibu vyote vya upinzani vikiongozwa na CUF na CHADEMA vilisimama waziwazi na kusema kuwa kutakuwepo Katiba mpya ifikapo uchaguzi mkuu ujao.
CCM haikuahidi hata mara moja au hata kuashiria kwa mbali kuwa inatambua haja ya katiba mpya. Ukweli huu unatufanya sisi wengine tuhoji kama kilichoahidiwa na Rais Kikwete ndicho wapinzani walikuwa wanakitaka na ndicho kiu cha Watanzania?!
Rais Kikwete ameunda tume ya kukusanya maoni tu. Hili ndilo Rais Kikwete alilisema. Rais hakuunda tume ya kusimamia uundwaji wa katiba mpya; Rais Kikwete hakuunda tume ya kuweka utaratibu wa kufikia katiba mpya, na kwa jinsi alivyoisema tume hiyo ni wazi kuwa lengo lake kuu ni kukusanya maoni tu yanayohusu katiba hiyo na baada ya kukusanya akatuambia kuwa hiyo tume "itatoa mapendekezo yake kwa vyombo stahiki.
Sasa wanaoshangilia hii tume ya "katiba mpya sijui walimsikiliza Rais au wanafikiria walimsikia akisema ameunda tume ya Katiba Mpya? Hakuna mahali popote katika salamu zake zile za mwaka mpya ambapo Rais aliunda tume ya kusimamia uundwaji wa Katiba mpya. Hakuna.
Lakini zaidi vile vile Rais hakuonesha kulipa swala hili uzito unaostahili wani ni suala ambalo litabadili kabisa sura ya taifa letu kwani laweza kutupeleka kwenye kuuvunja Muungano wetu ulivyo sasa. Sikuelewa kwanini jambo hili zito namna hii liliwekwa kama kipengele cha salamu za mwaka mpya. Kulikuwa na haraka gani?
Yeye mwenyewe alituambia alifikia uamuzi huo baada ya kushauriana na wenzake serikalini; tunajua kuwa Chama cha Mapinduzi hakikufanya uamuzi huo - na kama ni serikali yawezekana hata Mwanasheria Mkuu hakuwa ameshirikishwa na kama siyo yeye tu hata Waziri wa Sheria na Katiba. Kwa ufupi huu ulikuwa ni uamuzi wake peke yake ushahidi wote unaelekeza kuwa hivyo ndivyo ilivyo - niko tayari kusahihishwa.
Sasa jambo zito kama hili ni kweli limezungukwa kwa heshima inayostahili? Kulikuwa na ubaya gani kabla ya kuamua kuunda hiyo tume Rais Kikwete angekaa na uongozi wa upinzani kwanza pamoja na uongozi wa CCM kuweza kuifanya iwe ni ajenda ya taifa na kukubaliana ni namna gani twende kuandika Katiba hiyo mpya?
Maana ilivyo sasa Rais Kikwete ndiye ataunda hiyo tume, atachugua yeye wajumbe wake, na watu hao wataendeshwa kwa misingi ya kumridhisha Rais (mteule wao). Ni hili hili lilitufanya sisi wengine tupinge ile tume ya Madini aliyoiunda kufuatia sakata la Buzwagi na wote tunajua iliishia wapi pamoja na ripoti yake.
Lakini hilo niliache kwa muda kwani nimeliandika sehemu nyingine vizuri zaidi. Ninachotaka kukumbushia kuwa kwa serikali yetu kukubali tuzungumzie Katiba mpya ijue kuwa "yote yanazungumzika . Maana yake ni kuwa mjadala wa Katiba mpya hauwezi kuamuliwa nini kisizungumzike kwani unatuhusu sisi wananchi na watawala wetu na uzao wetu wa baadaye.
Hivyo, hakuna jambo la mwiko ambalo litakatazwa kuzungumzika na katika mtindo huu wa tume ya maoni nina wasiwasi mkubwa kutakuwa na kuburuzana kutakakoudhi watu wengi.
Nina uhakika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lichukue nafasi yake katika hili. Binafsi ningependa Rais Kikwete abadili uamuzi wake wa kuunda tume ya maoni na badala yake alipeleke jambo hilo bungeni ili kwanza kabisa itungwe sheria ya kusimamia mchakato wa Katiba mpya pamoja na kuweka muda wa kukamilisha hatua mbalimbali.
Kwa sababu, hadi hivi sasa nina hofu kuwa kwa kuamuru kuanza kupitia Katiba ya sasa na kuahidi Katiba mpya - Rais Kikwete yuko kwenye hatari ya kuvunja Katiba aliyoapa kuilinda. Kwanza, kwa sababu hakuna sheria iliyompa madaraka ya kuvunja katiba ya sasa hata kwa nia nzuri kiasi gani na pili, hakuna chombo ambacho kina nguvu za kisheria kufanya hicho alichoamuru kufanya. Hii tume ya maoni hadi hivi sasa ni kinyume na sheria kwani ina lengo la kuanza kuvunja Katiba iliyopo!
Hivyo, baada ya kukubaliwa kwa hoja ya Katiba mpya kilichotakiwa kufuatia siyo kuundwa kwa tume ya maoni na mtu mmoja asiye na madaraka ya kisheria kufanya hivyo bali kupeleka mswada kupitia mwanasheria mkuu wa kuweka utaratibu wa mchakato wa Katiba mpya na nguvu za kisheria za kufanya hivyo. Hivyo, Bunge likichukua nafasi yake mjadala utafanyika na mawazo ya pande zote mbili yataingizwa na hatimaye chombo chenye nguvu za kisheria siyo kukusanya maoni tu bali kuweka utaratibu wa:
Lini maoni yawe yamekusanywa, lini mapendekezo yawe yameanishwa, lini Baraza la Katiba Mpya liwe limeundwa, lini Kura ya Maoni ya Katiba Mpya ipigwe, lini Katiba hiyo iwe iwe na nguvu.
Bila ya kuweka utaratibu wa namna hiyo wa kisheria, sote tunajikuta tumeingizwa kwenye garimoshi la Rais Kikwete na kuanza kupelekwa anakotaka yeye kama watu wasio na fikra huru. Naam, ni vizuri kumpongeza kwa kukubali hoja ya Katiba mpya lakini ni jukumu letu kupinga tume hii aliyoiunda ambayo kama nilivyodokeza haina nguvu zozote za kisheria kufanya inachotakiwa kufanya bila kushirikisha Bunge.
Ni matumaini yangu mojawapo ya majukumu ya kwanza ya Bunge linalokuja ni kuunda sheria itakayosimamia mchakato huu na ni mpaka hapo Bunge (ambalo ndilo wawakilishi halali wa wananchi wa Tanzania) watakapopotisha sheria hiyo na Rais Kikwete kuiridhia ndipo tume iliyoundwa itakuwa na nguvu na madaraka ya kufanya kazi inayotakiwa kufanya.
Kwani hivi sasa wakianza kazi ya kuelekea kuivunja Katiba iliyopo kwa nia yao "nzuri watakuwa wanashiriki katika vitendo vya uvunjaji wa sheria na wasipoangalia hata yule aliyewapa madaraka hayo atajikuta anastahili kuondolewa kwa taratibu za kibunge (impeachment) kwa kutumia madaraka yake vibaya.
Rais wa Tanzania hawezi kuamka siku moja ati kwa nia njema akaanza kubadili Katiba au kujiwekea utaratibu wa Katiba Mpya kwa sababu "amewasikiliza wananchi . Maana kama kweli hii serikali inasikiliza wananchi kuna mambo mengine tungejaribu kuwauliza kama waliyasikia au ndio waliziba masikio.
Maana kama kweli ingekuwa inasikiliza hivi kweli tungekuwa hapa tulipo kwenye suala la Dowans? Kama kweli wanasikiliza tungefikia tulipofikia kwenye Meremeta? Au huku kusikia kunachagua ni kipi kinaujiko?
Heri ya mwaka mpya!!

Source:http://www.freemedia.co.tz/daima/habari.php?id=22576
.........................................................

Binafsi naunga mkono kuwepo kwa katiba mpya, lakini pia napinga kwa nguvu zote madaraka ya rais kuchagua nani asimamie hili zoezi nyeti, pia ningependa zoezi hili liendeshwe kisheria zaidi na siyo kimasilahi zaidi kama ambavyo wanasiasa wanataka kufanya
 
Naunga mkono na kumpongeza Rais Kikwete kukubali hoja ya kuwa na katiba mpya Tanzania. Namshukuru kwasababu, kwa mamlaka ya kupita kipimo aliyopewa na Katiba ya sasa ya Tanzania angeweza kupuuzia matakwa ya WaTanzania na kutulazimisha kutumia njia dumavu ama zenye maafa kuipata katiba mpya. Hata hivyo ninapinga pendekezo la Rais kutumia mamlaka na Katiba iliyopo kuamua mchakato na wahusika wa utengenezaji wa Katiba hiyo mpya. Kwa maoni yangu, katiba inayokataliwa ama kudaiwa imepitwa na wakati haiwezi kutoa mfumo endelevu na unaokubalika wa kuibadilisha. Busara na ujasiri wa Rais kukubali kuwa na katiba kwa Tanzania itumike kuanzisha mchakato wa jinsi gani tutengeneze katiba mpya. Nasema ni ujasiri kwasababu amekwenda kinyume na utashi na matakwa ya Chama Chake na labda wafuasi wake serikalini na kulifanya lile litakalomlindia heshima yake sasa na hata baadae.
 
Back
Top Bottom