Hivi Samuel Sitta huwa ana kumbukumbu na anachokiongea?

Mkodoleaji

JF-Expert Member
Apr 27, 2008
458
138
Sitta: Elimu na Afya bure inawezekana Send to a friend
Saturday, 01 September 2012 09:03

Edwin Mjwahuzi, Kagera
WAZIRI wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta amesema Serikali kutoa huduma ya Elimu na Afya bure inawezekana ikiwa tu mianya ya rushwa na ufisadi itadhibitiwa ipasavyo na wananchi wataweza kunufaika na rasilimali zilizopo nchini.

Sitta alisema ni lazima turudi kwenye misingi ya uadilifu, kujali wanyonge, kukataa rushwa na kukataa ufisadi wa aina yoyote ndipo tutaweza kukusanya na kuinua uchumi wa kutosha na kulipana mishahara mizuri, kumlipa pensheni mzee na kutoa huduma hizo bure.

Aliyasema hayo alipokaribishwa katika mkutano wa akinamama wajane kutoka wilayani Karagwe na Kyelwa mkoani Kagera na kuwashirikisha wazee wa Wilaya hizo uliofanyika katika ukumbi uliopo katika ofisi za CCM wilayani Karagwe.

Sitta alisema itakuwa ndoto za kupata huduma hizo bure kama nchi haitafanikiwa kuziba mianya yote ya rushwa na wananchi wataendelea kupiga kelele wakitaka kupatiwa huduma hizo bila ya mafanikio.

“Ningependa kuwaambia wananchi, najua karibu wote tunataka utoaji wa huduma ya afya, elimu ya kuanzi msingi mpaka elimu ya juu kuwa bure, ndugu zangu katika hali ambayo hata huduma ya afya ya kawaida haipatikani ni mtihani mkubwa kwa kutoa elimu ya bure,” alisema.

Aliongeza, “Hatuwezi kuwa na nchi ina kila kitu, tunayo makaa ya mawe, maziwa, mito, bahari, madini, gesi, mbuga za wanyama, Mlima Kilimanjaro na tuna hekta za kilimo zaidi ya milioni 88, tunataka Watanzania muamke na muache kushabikia rushwa ndogo ndogo tuingie katika utamaduni unaotuwezesha kujenga heshima ya nchi yetu kwa kujali uongozi ulionyooka na wenye uhadilifu.”

Sitta alisema wananchi wasiwe na ndoto ya maisha bora kwa kila mtanzania ikiwa rushwa na ufisadi utaendelea kutawala na kufumbiwa macho.

"Ndugu zangu hatuwezi kupata maisha bora kama kiwango cha rushwa, ufisadi na dhuluma kikiwa hivi hivi tunavyokiona hivi sasa, kwa sababu Serikali ilileta utoaji pembejeo kwa kutumia vocha sasa tutaendelea vipi kama vocha zenyewe zinachakachuliwa?" alihoji.

“Iwapo tutadhibiti mianya ya ufisadi na rushwa, nchi yetu itainuka na kuweza kuwasaidia wazee wetu, wajane, watoto yatima kwa kuwapatia huduma nyingi nzuri, ilimpadi tu ufisadi unatakiwa kupigwa vita kuanzia chini huku,” alisema Sitta.

Sitta pia aliwaomba wajane hao na wazee kupita kila mahali na kuwashaui wananchi wao wakiwemo na wana CCM kuwa makini wa watu wanaojitokeza kuwania nafasi mbalimbali za kisiasa na kiserikali wasije wakafanya makosa kuwaweka watu wenye nia mbaya na nchi hii kwa kujali matumbo yao na familia zao.

“Sasa hivi hata kule bungeni mnaona baadhi ya mawaziri, anatokea mtu amekuwa waziri ndani ya miaka 2 au chini ya hapo unasikia kanunua nyumba Mikocheni ya mabilioni, haiwezekani na wala haingii akilini hakuwa waziri wa wananchi huyu ameingia kuchuma tu,” alisema.

Waziri Sitta amemaliza juzi ziara ya kiserikali ya siku tano mkoani humo alipokuwa akiangalia miradi mbalimbali inayohusiana na muingiliano wa uchumi na kijamii kwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).

Source: Mwananchi 2/9/2012

Jaji Mfalila: Chagueni upinzani ASEMA MGOMBEA ATAYETOA ELIMU, AFYA BURE NDIYE ANAFAA KUWA RAIS Send to a friend
Tuesday, 21 September 2010 20:29

jajimfalila.jpg
JAJI mstaafu wa Mahakama ya Rufaa nchini, Lameck Mfalila​
Patricia Kimelemeta
JAJI mstaafu wa Mahakama ya Rufaa nchini, Lameck Mfalila, amewataka Watanzania kuchagua mgombea aliyethubutu kusema; "atasomesha wanafunzi na kutoa huduma ya afya bure." Akitetea msimamo huo, Jaji Mfalila alisema:"Huyu ni shujaa, sio ghilba bali amethubutu kusema anaweza kufanya mabadiliko hayo, mchagueni."

Katika mkutano wa wanaharakati kuhusiana na Uchaguzi Mkuu jijini Dar es Salaam jana, Jaji Mfalila alitoa sifa kwa mgombea mmojawapo wa urais kutoka kambi ya upinzani ambaye ameweka wazi kwamba akiingia Ikulu, elimu na afya zitatolewa bure.

“Kuna mgombea mmoja kutoka kwenye vyama vya upinzani, naona anaitia changamoto serikali, yeye alithubutu kusema ikiwa atachaguliwa kuingia Ikulu, atasomesha wanafunzi na kutoa huduma ya afya bure, huyu ni shujaa, sio ghilba bali amethubutu kusema anaweza kufanya mabadiliko hayo, mchagueni,” alisisitiza.

Kwa mujibu wa Jaji Mfalila, ikiwa wananchi watafanya mabadiliko hayo wataweza kupata kiongozi bora atayesimamia mali asili za nchi yake vizuri.

Ingawa hakumtaja mgombea huyo, lakini wagombea urais kwa tiketi ya Chadema, Dk Willibrod Slaa na wa CUF, Prof Ibrahim Lipumba ndiyo ambao wamekuwa wakitoa ahadi hiyo ya kutoa elimu na afya bure kama wakishinda uchaguzi.

Kwa upande wa Dk Slaa, amekuwa akisema iwapo Chadema itapewa ridhaa ya kuongoza nchi, fedha zilizoporwa kifisadi zitarejeshwa na kuwa mwanzo wa kutoa elimu na afya bure kwa wananchi.

Ahadi yake hiyo ilimsababishia Dk Slaa kuingia katika mgogoro na Spika wa Bunge aliyemaliza muda wake, Samuel Sitta, aliyepinga sera ya wapinzani ya kutoa elimu bure akisema kuwa haiwezekani.

Naye Prof Lipumba mara kadhaa amenukuliwa akisema kama akichaguliwa kuwa rais katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu, Serikali yake itaondoa gharama za elimu katika ngazi zote.
Lipumba alitoa kauli hiyo hivi karibuni wakati akijinadi katika mikutano tofauti ya kampeni iliyofanyika mkoani Lindi na Mtwara.

Lipumba alisema CUF imeazimia kuweka suala la elimu ya bure katika vipaumbele vyake, kwa vile sekta hiyo ni mkombozi wa umaskini uliokithiri kwa wananchi wengi.

Katika mkutano huo wa jana, Jaji Mfalila alisema Tanzania ina kampuni kubwa ambazo zinafanya shughuli za kuzalisha madini yakiwamo ya dhahabu na almasi, jambo ambalo lingeweza kuingiza kiasi kikubwa cha fedha, lakini kutokana na ujanja uliopo makampuni hayo yanalipa kiasi kidogo cha kodi huku yakiwanufaisha wachache.

Jaji Mfalila ambaye alitumia zaidi ya saa moja kuitafakari serikali, ilipotoka, ilipo sasa na inapokwenda, alisema kuwa rasilimali zilizopo zinatumika kiujanja ujanja jambo ambalo limesababisha nchi kutegemea misaada kutoka kwa wahisani na nchi marafiki.

Alisema kutokana na hali hiyo, wananchi wanapaswa kufanya mabadiliko ya kumchagua kiongozi atakayeweza kuleta maendeleo kwenye taifa lake, hasa katika nafasi ya rais ambayo ndio injini ya maendeleo.

“Tanzania bila ya misaada inawezekana, tuna rasilimali za kutosha ambazo zikitumika vizuri zinaweza kuleta mabadiliko ya kimaendeleo. Wananchi wanapaswa kufanya mabadiliko ya kumchagua kiongozi anayeweza kuthubutu kuleta maendeleo hayo, chagueni upinzani kwa ajili ya maendeleo,” alisema Jaji Mfalila.

Jaji Mfalila alisema nchi nyingi duniani zilizopiga hatua kimaendeleo zilitumia rasilimali zake vizuri bila ya kuingiza ujanja ujanja.

Akizungumzia kilimo, Jaji Mfalila alisema kwamba inashangaza kilimo cha Tanzania mpaka sasa kinategemea mvua za misimu na pale ambapo mvua hizo hazinyeshi, viongozi wanaitana Ikulu kutafuta nchi ya kuomba msaada wa chakula wakati ardhi yenye rutuba ipo.

“Hii ni aibu ya kutosha kuona tunaomba msaada wa chakula wakati tuna ardhi bora kwa ajili ya shughuli za kilimo, lakini bado tunasubiri mvua ya miezi mitatu ambapo isiponyesha viongozi wanaitana Ikulu kwa ajili ya kutafuta nchi ya kuomba msaada wa chakula, kweli tunahitaji mabadiliko," alisema.

Akizungumzia enzi za uongozi wa Mwalimu Julius Nyerere, Jaji Mfalila alisema wanafunzi wa chuo kikuu waliweza kupatiwa mahitaji yote muhimu ili wasome kwa umakini zaidi, lakini siku hizi fedha za matibabu, chakula na kulipia gharama za ada zimekuwa tatizo kwao.
“Nasikia tu wanafunzi wamegoma kwa ajili ya kukosa fedha za ada, chakula na matibabu wakati enzi zetu tulikuwa tunakabidhiwa hundi ya malipo kabla ya kufika shuleni,”alisema.

Naye Profesa Chris Peter Maina, wa Shule ya Sheria ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Kituo cha Huduma ya Sheria Zanzibar, aliunga mkono kauli iliyotolewa na Jaji Mfalila akisisitiza kuwa elimu yaweza kutolewa bure.

“Nimesoma bure kuanzia darasa la kwanza hadi nilipopata shahada yangu ya uzamili. Sharti kuu lililokuwapo ni kwamba nilihitajika kujaza fomu kuazimia kuwa nitalitumikia taifa langu baada ya kuhitimu masomo yangu,” alisema Profesa huyo.Aliongeza: “Kama nisingepata elimu ya bure, leo hii ningelikuwa nachunga ng'ombe kijijini kwetu.”

Profesa Maina alisema tatizo kubwa linaloikabili Tanzania ni kwamba viongozi wamevigeuza vipaumbele juu chini kwa kuwapa wakaguzi wa elimu wanaotumia magari ya Sh 150milioni yaliyo na viyoyozi kazi ya kukagua madarasa yasiyo na madawati na yenye wanafunzi wanaoketi chini.

“Sielewi ni kwanini mpaka leo miaka 50 baada ya uhuru wanafunzi wa Tanzania bado wanaketi chini kwenye madarasa yao?” alishangaa Profesa huyo wa sheria.

Source: Mwananchi 21/9/2010.

MY Take
Hivi huyu jamaa 2010 alikuwa anawabishia nini akina Dr Slaa waliposema kuwa wanaweza kutoa elimu bure?



 
Back
Top Bottom