BARD AI
JF-Expert Member
- Jul 24, 2018
- 3,416
- 8,200
Wakati safari ya Watanzania kwenda kupata Katiba mpya ikiendelea, Balozi Willibrod Slaa ameukosoa mchakato huo, akisema kinachofanyika ni kiinimacho na hakina uhalali kisheria.
Hoja ya mwanasiasa huyo aliyewahi kuwa katibu mkuu wa CHADEMA, inajengwa kwenye msingi kwamba “Katiba haipaswi kutungwa kwa maagizo ya Rais bali ni wananchi wenyewe”.
Kauli ya Dk Slaa inakuja baada ya Rais Samia Suluhu Hassan Mei 6, mwaka huu kukutana na viongozi na watendaji kadhaa wa Serikali kujadili mchakato huo, kisha kumwagiza Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi kuitisha Baraza la Vyama vya Siasa kuanza mchakato huo.
Tayari Baraza hilo limefanya kikao cha awali Mei 26 na kwa mujibu wa mwenyekiti wa Baraza hilo, Juma Khatibu, mkutano wa pili utakaohusisha wadau mbalimbali utafanyika Agosti mwaka huu.
Njia hiyo ya Rais Samia kutoa maagizo hayo kwa msajili wa vyama vya siasa, ndiyo inayokosolewa na Dk Slaa akisema: “Huo si misingi wa mchakato wa Katiba mpya na msajili hana mamlaka ya kufanya hivyo”.
Akizungumza katika mahojiano maalumu na Mwananchi nyumbani kwake jijini Dar es Salaam juzi, Dk Slaa aliieleza hatua hiyo kama kiinimacho.
“Hiki ni kiinimacho na hakikubaliki kwa sababu uamuzi kuhusu Katiba na mabadiliko yake yanapaswa kuwa ya Watanzania na si kauli ya Rais au mtu mmoja,” alisema.
Aliifananisha Katiba na mkataba wa ajira, akifafanua kuwa unapaswa kuandaliwa na mwajiri ambaye ni wananchi kwenda kwa muajiriwa ambaye ni Rais na si kinyume chake.
"Sheria zinasainiwa na Rais, kwenye Katiba kuna sehemu ya saini ya Rais? Lakini hiki kiinimacho eti Rais anaagiza msajili aitishe Baraza la vyama, hakikubaliki," alisema.
Kinachopaswa kufanyika kwa mujibu wa Dk Slaa, ni kutungwa kwa sheria ya mabadiliko ya Katiba itakayoeleza mchakato mzima utakavyokwenda.
Anasema hatua hiyo inatakiwa ifuatiwe na mkutano wa wananchi wote kupitia vyombo vyao, wapendekeze utaratibu wa kuuendea mchakato na kueleza kile wanachohitaji ndani yake.
“Mimi siamini kwamba hawajui mchakato unavyopaswa kuwa, siamini kwamba hawajui nchi inaongozwa kwa sheria na wameapa kwenye viapo vyao,” alisema.
Mwanasiasa huyo aliyeziaga siasa za ndani ya vyama, alieleza kushangazwa na mchakato wa Katiba mpya kukabidhiwa kwa vyama ambavyo havijawahi kushinda katika uchaguzi hata wa Serikali a Mitaa.
"Hawana mtaa hata mmoja unawapa kazi ya kutengeneza Katiba, ndiyo hivihivi kwenye uchaguzi wa mwaka 2020 vyama karibu 14 vilijitokeza kudai eti uchaguzi ulikuwa huru na haki," alieleza.
Dk Slaa alisema hata eneo la utangulizi kwenye Katiba linasema, “sisi wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tumeamua rasmi na kwa dhati kujenga katika nchi yetu jamii inayozingatia misingi ya uhuru, haki, udugu na amani.”
Akifafanua hilo alisema: “Katiba ni ya wananchi, tunapaswa kufuata taratibu. Rais atoe waraka na muswada upelekwe bungeni ili tujue sasa mchakato unakwendaje na si kusubiri matamko tu”.
Mchakato wa awali wa Katiba mpya ulioanzishwa mwaka 2012 katika awamu ya nne ulifuata hatua anazozitaja Dk Slaa, ingawa ulikwama mwaka 2014 baada Bunge Maalumu kupitisha Katiba Pendekezwa.
Aprili 25 mwaka huu, Waziri wa Katiba na Sheria, Dk Damas Ndumbaro aliwasilisha bajeti ya wizara yake kwa mwaka 2023/24, ikiwa na vipaumbele mbalimbali, vikiongozwa na mchakato wa Katiba.
Pia aliahidi maboresho ya sheria za uchaguzi wa Serikali za Mitaa mwaka 2024 na uchaguzi mkuu 2025.
Kwa nini Katiba Mpya
Dk Slaa, aliyewahi kuwa Balozi wa Tanzania nchini Sweden, alisema hoja ya Katiba mpya inaibuka kwa kuwa iliyopo ina mrengo wa siasa za chama kimoja.
Alisema Katiba ya sasa ilitungwa na watu 20, wakiwemo Thabit Kombo (mwenyekiti), Pius Msekwa aliyekuwa katibu na wengine 18 ambao walianza kwa kuandaa katiba ya CCM.
“Walipomaliza ya CCM wakaambiwa sasa tunataka mtutengenezee ya Serikali, ukitaka kujua kwa nini tunahitaji Katiba mpya lazima ujiulize ile ya CCM tangu 1977 imebadilishwa mara ngapi?" alisema.
Alihoji kwa nini katiba ya CCM imebadilishwa mara kadhaa lakini ya Taifa isibadilishwe.
Jambo lingine linaloibua haja ya Katiba mpya alisema ni hatua ya mkuu wa nchi kuwa na mamlaka makubwa mithili ya mfalme.
"Leo Rais hapa ni kila kitu, Tanzania Rais ni Mungu, kama mfalme wakati hata nchi zenye mamlaka ya malkia zimeshaacha, lakini sisi tumerudi huko," alisema.
Kinachohitajika kwa mujibu wa Dk Slaa, ni Katiba itakayowapatia wananchi mamlaka yao.
Alichojibu Msajili
Alipoulizwa kuhusu wajibu waliopewa, Jaji Mutungi alisema msajili wa vyama ni katibu wa Baraza la Vyama vya Siasa na wajibu wake ni kuwezesha vikao vya Baraza hilo.
“Ndugu mwandishi, nimeona concern (dukuduku) yako, si vyema kupotosha kama wengi wanavyojaribu kuupotosha umma.
"Kikosi kazi ni matokeo ya mkutano wa wadau wa siasa ambao uliandaliwa na Baraza la Vyama vya Siasa, baraza lina haki ya kupokea mrejesho kuhusu mapendezo ya kikosi kazi," alisema.
"Kwa kuwa sote tunatambua kwamba suala la Katiba ni la wananchi wote, ndiyo maana kwa agizo la Rais sasa baraza linaandaa mkutano wa wadau ili kuona namna bora ya kuanza utekelezaji wa mchakato," alisema.
Jaji Mutungi alisisitiza kuwahakupewa jukumu la kutunga Katiba na wala si kazi anayoifanya.
Anachokifanya, alisema ni uwezeshaji wa kuelekea mchakato wa utungwaji wa Katiba mpya na ukifika wakati huo, wenye mamlaka ya kufanya hivyo watapewa kutekeleza.
“Itafika hatua wenyewe wanaopaswa kutunga au kuandaa Katiba mpya wataachiwa hiyo kazi waifanye, mimi nafanya uwezeshaji kuelekea mchakato huo, situngi Katiba wala sijapewa jukumu hilo," alisema.
Kwa sababu hizo hizo, alisema ndiyo maana amewaambia hata wanasiasa wasibweteke, wakiamini kwamba wao ndio pekee wenye mamlaka ya kuandaa Katiba mpya, bali ni jukumu la wananchi wote.
Jaji Mutungi, aliyepo Uturuki kwa matibabu, alisema alipaswa kupumzishwa, lakini amelazimika kulijibu hilo ili ieleweke vema," alieleza.
Waziri wa Katiba na Sheria hakupatikana kuzungumzia hatua zitakazofuatwa katika mchakato huo na zitakuwa lini baada ya simu kuita bila majibu.
CCM kukagua miradi
Katika hatua nyingine, Dk Slaa vilevile alieleza kushangazwa na hatua ya Chama cha Mapinduzi (CCM) kukagua miradi na hata kutoa maagizo kwa mamlaka za Serikali.
Alisema hiyo ni kazi ya vyombo vya Serikali na si ya CCM, akisisitiza ikihitaji kufanya hivyo inapaswa kuandika kwa mamlaka husika ya Serikali.
"Juzi nimeona Katibu Mkuu wa CCM (Daniel Chongolo) anaagiza kuchongwa barabara na kesho yake trekta limekwenda, hivi bajeti inatoka wapi," alisema.
Alisema CCM haina bajeti ya kutekeleza miradi ya Serikali, inapata wapi mamlaka ya kuagiza na utekelezaji ufanyike.
Mambo hayo, alieleza ndiyo yanayofanya nchi iongozwe kiholela.
Alipotafutwa kuzungumzia hilo, Katibu Mkuu wa CCM, Daniel Chongolo simu yake iliita bila majibu. Hali ilikuwa hivyo hivyo hata kwa Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi, Sophia Mjema.
Azungumzia CHADEMA
Alipoulizwa maswali yahusuyo Chadema, Dk Slaa alisema hapendelei kuikosoa kwa kile kinachoaminiwa na wengi kuwa akifanya hivyo ni kwa sababu ana hasira nayo.
Alisema hana mpango kurejea katika chama hicho kwa kuwa aliapa kutofanya siasa ndani ya vyama vya siasa.
"Nikishasema mwanasiasa makini akitoa kiapo huwa habadiliki, mimi niliapa najitoa kwenye siasa ya vyama na nikarudia, lakini ninapoona nchi yangu inaenda vibaya nitaendelea kupiga kelele, nitaongea kama raia," alisema.
Makali nje ya Serikali
Dk Slaa alisema si kweli kama inavyodhaniwa na wengi kwamba alikuwa haikosoi Serikali alipokuwa balozi na sasa anafanya hivyo baada ya kuwa nje.
“Nilikuwa balozi na nilikuwa na nafasi ya kuhojiana na Rais moja kwa moja, asikilize asisikilize shauri yake lakini mimi ushauri umefika.
“Sasa natoka hadharani kufanya nini wakati nina nafasi ya kumwambia Rais moja kwa moja, ndiyo maana hata mawaziri huwasikiki wakiongea,” alisema.
MWANANCHI