Kaimu Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Bara, Amani Golugwa, amesema chama hicho kilifanya mashauriano ya kina na makundi mbalimbali ya kijamii kabla ya kuanza kampeni za mikutano ya hadhara ya viongozi wake wakuu, na matokeo yake yameonesha uungwaji mkono mkubwa wa madai ya mageuzi ya mfumo wa uchaguzi nchini.
Akizungumza katika mahojiano maalum na Wilberforce Ngoto kupitia kipindi cha Maswali na Majibu kinachorushwa na Jambo TV, Golugwa amesema chama kilitumia zaidi ya siku 35 kukutana na wadau mbalimbali nchini kote.
Ameongeza kuwa baada ya mazungumzo hayo, CHADEMA ilianza mikutano ya hadhara ambayo kwa ushahidi alioutaja kama wa kisayansi, ilionesha wananchi wengi wanaunga mkono wito wa chama hicho wa “No Reforms, No Election” (Hakuna Mageuzi, Hakuna Uchaguzi).
“Mikutano ya hadhara ilitupa ushahidi jinsi ambavyo watu wanaunga mkono hitaji hili la nchi, kwamba nchi hii inahitaji reforms kwenye mifumo ya uchaguzi. Na majibu ya mikutano yalitupa uthibitisho zaidi kwamba madai haya sio ya kisiasa pekee, bali ni hitaji la kitaifa,” amesisitiza Golugwa.