Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,351
- 33,188
Na Mwandishi Wetu
Wakati jamii ya muziki wa Kizazi Kipya na mashabiki wao wakiwa bado katika maombolezo ya msiba wa Julieth D. Mrina Pendo (24), kubwa zito limeibuka kuhusu anayetajwa kuwa ni mchumba wake, Hamad Ally Madee, Amani limekusanya vielelezo...
Baadhi ya waombolezaji kwenye msiba huo uliokuwa umepigwa kambi Kimara, jijini Dar ni wanamuziki wa Kizazi Kipya, akiwemo Joseph Haule Profeja J, Tundaman, Khadija Shaban Keisha, Kasim Maganga Kasim na ma-andagraundi wengine kibao.
Ulipofika muda wa kusomwa kwa wasifu wa marehemu Pendo, kwamba ni nani, alizaliwa wapi, mwaka gani na amefanya nini hadi kifo kinamkuta ndipo lilipoibuka jambo zito ambalo liliwaacha midomo wazi baadhi ya kampani ya Madee.
Wasifu huo ulimalizika bila kutajwa kuwa, marehemu alikuwa amechumbiwa na Hamad Ally Madee jambo ambalo lilizua maswali lakini hakukuwa na mwenye jibu.
Amani liliongea na baadhi ya wasanii waliohoji kulikoni kwenye vyombo vya habari kuandikwa wawili hao ni wachumba lakini asitajwe kwenye wasifu wa marehemu?
Mimi nilijua nakuja kwenye msiba wa mchumba wa Madee, sasa mbona kwenye wasifu hawajasema kama marehemu mpaka kifo chake alikuwa ameshachumbiwa? Alihoji msanii mmoja wa Bongo Fleva, jina tunalo.
Mwingine alisema kuwa, anavyojua yeye, wasifu wa marehemu unaacha kumtaja mtu kama alikuwa mpenzi tu, lakini kuanzia mchumba mpaka mume au mke hutajwa, alisema.
Aidha, habari nyingine zinadai kuwa, licha ya Madee kutotajwa kwenye msiba huo kama mchumba wa marehemu, mama yake mzazi mama Hamadi naye alikuwepo msibani hapo kama binadamu kwa sababu shughuli ya msiba ni ya kibinadamu zaidi na haihitaji mwaliko kama ilivyo kwenye sherehe za ndoa harusi.
Habari zaidi chini ya zulia zinadai kuwa, baadhi ya ndugu wa marehemu wanamtambua Madee kama mchumba mtarajiwa, lakini hakuwahi kujitambulisha rasmi kwa barua na posa katika familia hiyo ndiyo maana hakupata festiprioriti katika wasifu wa marehemu.
Hata hivyo, bado tano inatolewa kwa msanii huyo kutoka skwadi ya TiP Top Connection, Manzese jijini Dar ikisemekana kuwa, ndiye aliyefanikisha kuusafirisha mwili wa marehemu Pendo kutoka Hospitali ya Mkoa wa Pwani, Tumbi, Kibaha kwenda Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Jijini Dar es Salaam.
Marehemu Pendo alifariki dunia Machi, 13, 2010 katika ajali iliyoshirikisha basi la Shabiby na lori iliyotokea Kibaha, mkoani Pwani. Katika ajali hiyo, ni Pendo tu aliyepoteza maisha.