WIZARA YA MALIASILI NA UTALII: Hoteli 60 zapaisha utalii wa Tanzania

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797

Imeandikwa na Shadrack Sagati; Tarehe: 30th November 2011 @ 14:56

KATI ya wizara ambazo Tanzania inajivunia ni Wizara ya Maliasili na Utalii. Hii ni kwa sababu ni moja ya wizara ambazo zinachangia pato kubwa kutokana na kukua kwa sekta ya utalii nchini.

Machapisho mbalimbali yanayohusu sekta ya utalii, yanaeleza kuwa historia ya uhifadhi wa maliasili na utalii inaanzia kabla ya Wakoloni kuingia Tanganyika ambapo kila jamii ilijivunia umiliki wa maliasili ikiwemo misitu, nyuki, ardhi na mazingira ambavyo vilikuwa na umuhimu katika imani zao.

Inaelezwa kuwa Tawala za makabila ya Tanganyika chini ya uongozi wa kimila zilihifadhi maliasili kwa kuzingatia umuhimu wake kama chanzo kikuu cha mvua, rutuba, maji, urekebishaji wa hali ya nchi, mbao na vifaa vya ujenzi na madini kwa ajili ya utengenezaji wa zana.

Hivyo, maliasili kabla ya ukoloni ilikuwa ni chanzo cha maisha na utawala na mwanzo wa uhifadhi kwa kuzingatia mila na desturi. Msingi wa utalii wa kisasa kwa Tanzania ulianza kujengwa kabla ya ujio wa wakoloni. Katika kipindi hicho misafara ya kibiashara na watumwa, vita vya makabila na migogoro kati ya makabila mbalimbali ilikithiri.

Kwa wakati huo Afrika ilitambulika kwa wazungu kama Bara lenye giza ambalo halikufaa kwa mapumziko. Kwa wakati huo Afrika ilitambulika kwa wazungu kama Bara lenye giza ambalo halikufaa kwa mapumziko.

Lakini machapisho hayo yanaeleza kuwa kufikia karne ya 19, watu wengi walimiminika Afrika Mashariki hasa Tanganyika kwa misukumo mbalimbali ya uvumbuzi na kueneza dini. Wanasayansi na wafanyabiashara nao pia walikuja kutafuta fursa mbalimbali zilizokuwa zinapatikana Tanganyika.

Licha ya uvumbuzi uliofanywa na wageni walioitembelea Tanganyika, kulikuwepo na uharibifu mkubwa wa malihai na maliasili uliofanywa na wafanyabiashara waliokuwa wakitafuta meno ya ndovu, nyama, ngozi, vipusa na nguzo za mikoko.

Biashara ya meno ya ndovu ilikuwa maarufu katika Afrika ya Mashariki kwa zaidi ya miaka 2000 ikianzia zama za kati ambapo kulikuwa na mtandao wa wawindaji wa kiafrika, waendesha meli, wafanya biashara wa kati wa kiarabu na wachuuzi wa kiasia waliosambaza meno ya ndovu katika Bara la Asia na baadaye katika masoko ya Ulaya.

Hali hii ilisababisha uharibifu mkubwa na viongozi wa kikabila hawakuwa na utaratibu maalumu wa ulinzi wa maliasili hizo. Kumbukumbu zinaonesha kuwa kabla ya Vita Kuu, Tanganyika ilikuwa koloni lililopendwa na Wajerumani (1892 - 1918), kati ya makoloni ya Afrika kutokana na maliasili na malikale zake.

Aidha, maliasili na malikale hizo zilivunwa na kuhamishwa kwa ajili ya maendeleo ya nchi za kikoloni. Katika kipindi hicho Wajerumani waliweka sheria ya kwanza ya Uhifadhi na Matumizi ya Misitu na Wanyamapori.

Tangu wakati huo hadi leo hii kuna mambo mengi yamefanyika katika wizara hiyo ikiwemo mabadiliko ya sera mbalimbali pamoja na kuongezeka kwa vivutio vya utalii vinavyojumuisha hifadhi za wanyama, mambo ya kale na fukwe za bahari.

Kuongezeka kwa idadi ya mikusanyo ya Malikale Vituo vya malikale vimeongezeka kutoka vitatu mpaka 16 na kutangaza maeneo 88 kama urithi wa Taifa. Mashamba ya miti aliongezeka kutoka 14 mpaka 16 na misitu ya asili kutoka 597 mpaka 802.

Pia Makumbusho za Taifa ziliongezeka kutoka moja mpaka sita; Mapori ya Akiba kutoka tisa mpaka 28, mapori tengefu hayakuwepo sasa yapo 44 na Hifadhi za Taifa zimeongezeka kutoka tatu mpaka 15.

Machapisho hayo yanaeleza kuwa vituo vya kumbukumbu Wizara hiyo imejenga Vituo vya Kumbukumbu na Taarifa katika vituo vya mambo ya kale vya Michoro ya Miambani Kolo, Kondoa; Makumbusho ya Kumbukizi ya Dk. Livingstone Ujiji, Kigoma; Caravan Serai, Bagamoyo; na Isimila, Iringa na nyumba za watumishi tatu katika vituo vya Olduvai na Laetoli, Arusha.

Wakati Tanganyika inapata uhuru Desemba 9, 1961 Wizara ilikuwa inahifadhi jumla ya mikusanyo 10,151 ya fani za Akiolojia, Mila, Historia, Baolojia na Nyaraka mbalimbali.

Baada ya uhuru kutokana na tafiti zilizofanywa na watafiti wazawa na wageni wa kutoka nje ya nchi na kurejeshwa kwa mikusanyo ya Tanzania ambayo ilikuwa imehifadhiwa nje ya nchi, Wizara hadi Juni, 2011 imefanikiwa kuhifadhi nchini urithi wa malikale unaohamishika wenye jumla ya mikusanyo 337,361.

Kuingiza maeneo katika Orodha ya Urithi wa dunia Tangu uhuru, maeneo sita ya uhifadhi yaliwezeshwa kuingizwa katika urithi wa dunia ambao ni ngazi ya juu kabisa ya uhifadhi.

Maeneo hayo ni Magofu ya Kilwa Kisiwani na Songo Mnara; Michoro ya Miambani, Kondoa Dodoma; Eneo la urithi mchanganyiko la Hifadhi ya Ngorongoro; Pori la Akiba Selous, Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro na Hifadhi ya Serengeti.

Maeneo hayo sasa yanatambuliwa kimataifa, hivyo kuwezesha kubadilisha uzoefu na utalaam katika usimamizi na uendeshaji wake. Wizara hiyo imebainisha Njia ya Kati ya Biashara ya Watumwa na Vipusa yenye urefu wa kilomita 1,200 kutoka Ujiji, Kigoma mpaka Bagamoyo.

Usimamizi shirikishi wa Maliasili, malikale na utalii

Wizara imefanikiwa kuanzisha jumuiya 33 za uhifadhi wa wanyamapori; vijiji 2,328 sawa na asilimia 22 ya vijiji vyote nchini chini ya mpango shirikishi wa kuhifadhi misitu, vinashiriki kusimamia hekta 38 4,122,500 ambazo ni sawa na asilimia 12 ya misitu yote.

Pia, kuna vikundi viwili vya uhifadhi na uendelezaji wa malikale; na vijiji 34 vya mfano wa utalii wa utamaduni vimeanzishwa. Vilevile, Wizara imeanzisha klabu 1,687 za Malihai katika
shule za msingi na sekondari.

Lengo la kuanzisha klabu hizi ni kujenga uelewa na umuhimu wa uhifadhi kwa jamii. Kupanua wigo wa mazao ya utalii Mwaka 1961 wakati nchi inapata uhuru, watalii wa ndani na nje walivutika sana na utalii wa wanyamapori na kupanda mlima.

Hivyo, mwelekeo wa utalii ulielekezwa zaidi katika mikoa ya Kaskazini katika hifadhi za Serengeti, Ngorongoro, Manyara, Tarangire na kupanda mlima Kilimanjaro na mlima Meru.

Juhudi za Wizara katika kuboresha maeneo ya malikale, kuhimiza na kuhamasisha utalii wa kihistoria, utamaduni, fukwe, mandhari na mikutano kumefanya idadi ya watalii wanaozuru
nchini iongezeke.

Idadi ya Watalii wanaoingia nchini Idadi ya watalii waliotembelea maeneo ya mambo ya kale imeongezeka. Kuanzia mwaka 2005 hadi 2010 idadi ya wageni waliotembelea maeneo ya malikale iliongezeka kutoka 42,649 na kufikia 103,777.

Idadi ya watalii walioingia nchini iliongezeka kutoka 8,947 mwaka 1960 mpaka 782,699 mwaka 2010. Pia mapato kutokana na watalii hao yaliongezeka kutoka Dola za Marekani milioni 13.39 mwaka 1970 kufikia milioni 1,159.82 mwaka 2010.

Biashara ya Utalii
Machapisho hayo yanaeleza kuwa Kampuni zinazofanya biashara ya Utalii nchini ziliongezeka kutoka nne mwaka 1962 kufikia 546 mwaka 2010. Aidha, idadi ya vyumba katika nyumba za malazi iliongezeka kutoka 4,000 mwaka 1970 kufikia 15,000 mwaka 2010.

Mafunzo ya Utalii
Wizara imeboresha mafunzo kwa kuongeza kampasi zinazotoa mafunzo ya Hoteli na Utalii kutoka Kituo cha mafunzo ya Utalii cha Halmark Hotels mwaka 1969 na kufikia Kampasi tatu za Temeke, Arusha na Dar es Salaam mwaka 2011 chini ya Wakala wa Chuo cha Taifa cha Utalii.

Kampasi ya Dar es Salaam inayojengwa Mtaa wa Shaaban Robert jijini ikikamilika itadahili wanafunzi 500 kwa mwaka katika ngazi na fani mbalimbali.

Kupanga hoteli katika Daraja
Katika kuboresha huduma kwa watalii na kuhakikisha viwango vya ubora vinazingatiwa, Wizara kwa mara ya kwanza ilifanikiwa kufanya zoezi la kupanga hoteli katika daraja katika mikoa ya Dar es Salaam na Pwani mwaka 2010.

Jumla ya Hoteli 66 zilipatiwa daraja za ubora wa nyota. Wizara pia ilifanikiwa kuhakiki hoteli katika mikoa 12 ya Dar es Salaam, Arusha, Manyara, Pwani,Tanga, Kilimanjaro, Mwanza, Mara, Iringa, Morogoro, Mbeya na Dodoma.

Nyaraka hizo zinaeleza kuwa Mwaka 1978, Wizara ilianzisha mfuko wa kuhifadhi wanyamapori (TWPF) ambao unasaidia kugharimia shughuli za kulinda wanyamapori, utafiti na mafunzo, kutoa elimu kwa umma na kukarabati Miundombinu.

Katika kukabiliana na uwindaji na biashara haramu za nyara za Serikali, Wizara iliunda Kikosi Dhidi Ujangili (KDU) kilichokuwa na kanda nne za Tabora, Mwanza, Arusha na Dar es Salaam. Idadi hii imeongezeka hadi kufikia kanda nane mwaka 2011.

Ulinzi wa kizazi cha Faru Weusi Wizara imefanikiwa kulinda na kudhibiti ujangili wa kizazi cha faru weusi katika mazingira yao ya asili kutoka idadi ya faru watano mwaka 1995 hadi faru 33 mwaka 2010.

Maendeleo ya Jamii katika Bonde la Ngorongoro
Kwa miaka 50 iliyopita kumekuwa na maendeleo makubwa ya jamii katika Hifadhi ya Ngorongoro.

Katika hali ya kushirikisha wananchi kutekeleza jukumu hili la kisheria, Mamlaka ya Hifadhi inashirikiana kwa karibu na Baraza la Wafugaji ambalo ni chombo kilichoundwa kisheria kwa lengo la kuangalia na kushughulikia mahitaji halisi ya wafugaji wenyeji ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro.

Kwa sasa Baraza hupewa bajeti ya Sh bilioni 1.25 kwa mwaka kugharimia huduma za jamii ambazo husimamiwa moja kwa moja na Baraza. Baadhi ya kazi zilizofanyika ni kusomesha wanafunzi 704 ambao ni watoto wa wafugaji katika ngazi mbalimbali, ununuzi wa chakula (mahindi), ujenzi wa majengo ya shule za msingi na gharama za kuendesha zahanati.

Idadi ya shule za msingi imeongezeka kutoka sita mwaka 1980 hadi 34 mwaka 2011 na shule za sekondari hazikuwepo kabisa lakini sasa zipo mbili. Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro imeweza kuwa na eneo maalum la kuwahamishia wenyeji wanaotaka kulima, kwa hiyo kuwezesha eneo kutokuwa na msongamano na kutolimwa tena.

Hadi sasa, Kaya 140 zenye watu 553 zimehamia Jema Oldonyo Sambu, Wilayani Ngorongoro ambako wanaruhusiwa kuendesha shughuli za kilimo.


 
eti idadi ya vyumba katika nyumba za malazi iliongezeka kutoka 4,000 mwaka 1970 kufikia 15,000 mwaka 2010.... yani miaka yote hio mmeongeza vyumba 11,000? then mnajisifia?
 
Yameongelewa mengi lakini uzembe katika swala zima la uhifadhi wa mazingira ya national parks na conserved areas haliongelewi.Ujenzi holela wa mahoteli kwenye mapitio ya wanyama pamoja na ujenzi wa barabara ya lami hifadhini hauongelei.Je ujenzi wa kiwanda cha madini ya phosphate lake natron penye mazalia makubwa ya flamingo licha ya kelele za wanaharakati kupinga ujenzi huo hakikusikilizwa.Miaka 50 sisi tumekuta icho,je miaka 50 ijayo na uzembe wetu wa uhifadhi tutawacha nn?
 
Good narative but it seems like a report staff anamwandikia bosi wake kuliko ripoti ya public consumption
 
vipi kuhusu kusafirisha wanyama kwenda qatar na uae? Mbona hiyo 'ripoti' yako haijaongelea the other side of the coin? 'criticisims za wizara ya maliasili na utalii'
 
Back
Top Bottom