Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,318
- 33,125
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi), Celina Kombani.
Ofisi ya Waziri Mkuu, imemhamisha Mkurugenzi Mtendaji wa Manispaa ya Shinyanga, Jane Mutagurwa, aliyesimamishwa kazi kwa amri ya Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Mutagurwa amehamishimiwa katika halmashauri ya wilaya ya Kiteto mkoani Manyara atakapoendelea kuwa katika wadhifa huo.
Uhamisho huo umetangazwa siku chache baada ya baraza hilo, kumsimamisha Mutagurwa kutokana na tuhuma za matumizi mabaya ya madaraka.
Taarifa zilizoifikia Nipashe zilieleza kuwa, Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa( Tamisemi) iliyo chini ya ofisi ya Waziri Mkuu, ilitoa uhamisho huo unaojulikana kuwa wa kawaida.
Alipoulizwa na gazeti hili kwa njia ya simu kuhusu taarifa hiyo, Mutagurwa, alikiri kupokea uhamisho huo na kwamba ulitolewa tangu Ijumaa iliyopita.
Mara baada ya madiwani hao kumsimamisha Mkurugenzi huyo, zilisikika tetesi kuwa tayari, alikuwa ameshapata uhamisho kwenda katika kituo chake kipya cha kazi.
Akizungumzia kuhusu tuhuma zilizotolewa na madiwani dhidi yake, Mutagurwa, alizikanusha na kusema madiwani hao hawakufanya uchunguzi kuhusiana na kadhia hiyo.
"Hivi sasa tunapozungumza niko wilayani Kiteto, kwani ofisi ya DED wa manispaa ya Shinyanga nimeshakabidhi tangu Ijumaa iliyopita, kwa sasa nipo katika ofisi mpya hapa wilayani Kiteto," alisema.
Hata hivyo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi), Celina Kombani, alisema utaratibu uliotumika kufikia uamuzi wa madiwani hao, ni kinyume cha uendeshaji wa halmashauri hapa nchini.
Kombani, alisema utaratibu unaotakiwa kufanywa na madiwani ni kuandika malalamiko yao kwa Mkuu wa mkoa mwenye mamlaka ya kuyawasilisha Tamisemi na hatimaye kufikishwa kwa Waziri MKuu mwenye mamlaka ya kuwajibisha.
Pia, Kombani alithibitisha kuhusu uhamisho wa Mutagurwa na kwamba ulifikiwa kabla ya madiwani hao kumtimua.
Nipo jimboni lakini taarifa nilizozipata ni kwamba Mkurugenzi huyo amepata uhamisho wa kawaida kwenda halmashauri ya wilaya ya Kiteto.. alisema.
Naye Meya wa Manispaa ya Shinyanga, Hassan Mwendapole, alisema uchunguzi wa kina utafanywa kuhusu tuhuma zinazomkabili Mutagurwa na kwamba ushahidi ukithibitika kisheria, atafikishwa mahakamani.
Mwendapole aliyezungumza kwa njia ya simu kutoka Dodoma, alisema halmashauri ya manispaa ya Shinyanga inatambua kwamba tuhuma zinazomkabili Mutagurwa, hazitofautiani na wahalifu wengine wanaovunja sheria.
Hata hivyo, alisema kinachomkabili Mutagurwa ni tuhuma, hivyo si vizuri kumhukumu kwa vile hajapatikana na hatia.
CHANZO: NIPASHE