Wapinzani waibua ulaji wa mamilioni kwa posho Nishati na Madini

Pdidy

JF-Expert Member
Nov 22, 2007
50,956
22,150
Wapinzani waibua ulaji wa mamilioni kwa posho Nishati na Madini Send to a friend
Friday, 15 July 2011 20:28
0diggsdigg

Fidelis Butahe, Hussein Issa
WAKATI Kambi rasmi ya Upinzani Bungeni ikiiponda bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini kwa kusema imejaa fedha za kulipana posho, badala ya kutekeleza miradi maendeleo wakati nchi iko kwenye giza, Kamati ya wabunge wa CCM imeshindwa kuafikiana kuhusu namna ya kuiokoa bajeti hiyo.

Habari ambazo Mwananchi ilizinasa kutoka mjini Dodoma kutoka kikao hicho cha wabunge wa chama tawala waliokutana juzi usiku, zimeeleza jana kuwa hawakufikia msimamo wa pamoja wa jinsi ya kuiokoa bajeti hiyo inapopitishwa Jumatatu.Awali, jana, upinzani ulidai kuwa mabilioni ya fedha yametumika kwa shughuli kama za anasa badala ya kuelekezwa kwenye miradi ya kuzalisha umeme na kuwaondoa gizani Watanzania.

Katika hotuba mbadala ya kambi hiyo iliyosomwa jana na John Mnyika, ambaye ni Mbunge wa Ubungo (Chadema) imeitaka Serikali kueleza bayana hatua ambazo imechukua kufuatia ripoti ya tume mbalimbali ambazo ziliundwa kwa nyakati tofauti na kutumia fedha nyingi za walipa kodi ambazo mapendekezo yake bado hayajatekelezwa.

Akisoma hotuba hiyo bungeni jana, msemaji wa upinzani , John Mnyika, alisema kati ya Sh 402.4 bilioni zilizotengwa kwa wizara hiyo, matumizi ni Sh 76,953,934,000 huku maendeleo yakitengewa Sh 325,448,137,000.

Aliongeza, “Vitabu vya Bajeti ya Serikali iliyopitishwa vinathibitisha ukweli mchungu kwamba jumla ya fedha zilizotengwa kwa ajili ya nishati na madini ni Sh 539.3 bilioni ambazo hazitoshi kuwaondoa Watanzania gizani.”

Alifafanua kwamba, fedha nyingine kidogo za maendeleo ambazo ni Sh 126.6 bilioni zipo kwenye fungu la miradi ya MCC kwa kutegemea wahisani.

“Bajeti hii haijaichukulia kwa uzito unaostahili sekta za nishati na madini hususani umeme, hali ambayo inaibua maswali iwapo serikali ina dhamira ya dhati ya kukabiliana na changamoto za msingi zinazolikabili taifa,”alisema Mnyika.

Alisema wamebaini kwamba bajeti hiyo ni ya mgawo mkubwa wa posho na ufujaji. Kwa mfano, “Idara ya Kitengo cha Mawasiliano katika kulipana posho zitatumika Sh 405.62 milioni sawa na asilimia 63 ya fedha yote iliyotengwa ambazo ni Sh 641.99 milioni kwa idara hii, idara ya fedha na uhasibu itatumia Sh 598.49 milioni sawa na asilimia 42 ya fedha yote iliyotengwa," alisema .

Aliongeza kuwa ili kulipa posho mkoani Mwanza pekee, zitatumika Sh 389.68 milioni sawa na asilimia 40 ya fedha yote iliyotengwa na kuongeza kuwa kuna posho ya kuwanunulia mavazi wafanyakzi wanaosafiri nje ya nchi, sherehe na maonyesho, chakula na vinywaji, huduma za wageni pamoja na posho za kukaimu nafasi.

“Kwa jumla wizara inakadiriwa kutumia Sh. Bilioni 7.9 kulipana posho na matumizi mengine ya kawaida ya anasa,”alisema Mnyika.

Aliongeza:, “Jumla hii ni nje ya posho za msingi kama za uhamisho, mafunzo, nyumba, maji na umeme. Serikali ifanye marekebisho kwenye bajeti ili fedha hizi zipunguzwe ziweze kuongezwa kwenye kuongeza ujenzi wa miundombinu wa Chuo Cha Madini hapa Dodoma,” alisema.

“Usalama na amani katika taifa letu kwa sasa siyo migomo wala maandamano bali ni migogoro inayoendelea ya kirasilimali, maeneo mbalimbali ya nchi ambayo ni bomu litakalolipuka iwapo kasi ya ukuaji wa uchumi wenye kutoa fursa kwa wengi haitaongezwa,”alisema.

Mnyika pia, aliitaka Serikali itoe kauli juu ya Kampuni ya Uchimbaji madini ya New Almasi Ltd ambayo imechimba madini kwa miaka 35 bila kuwa na leseni, kiasi cha almasi iliyochimbwa kwa kipindi chote na zilizokoenda fedha zilizotokana na mauzo ya almasi hiyo.

Kamati ya Wabunge CCM
Mwananchi imebaini kuwa wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wameshindwa kuweka msimamo wa pamoja wa kuokoa bajeti hiyo isitupiwe lawama za hadharani.

Habari za uhakika zinaeleza kuwa wabunge hao walishindwa kuafikiana katika mpango huo juzi usiku, walipokutana kama kamati kwenye ukumbi wa Pius Msekwa, ingawa kimsingi waliafikiana tatizo la umeme lililopo kwa sasa

Taarifa zilizolifikia gazeti hili mjini hapa zilieleza kuwa mkutano huo ulikuwa mahususi kuwaeleza wabunge unyeti wa bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini na kwamba waliokusudia kuikamia ili isipite wasifanye hivyo kwa kuwa tatizo la umeme nchini linajulikana na ni la taifa na hapaswi kutupiwa mtu lawama.

"Kilichoonekana ni kwamba tatizo la umeme linawapa wengi hasira na bila kuliweka sawa, wengi watalipuka. Lakini, ni vyema wakajua suala hili kwa undani ili wakitamka jambo bungeni wajue wanafanya nini," kilieleza chanzo chetu.

Ilidaiwa kuwa wabunge hao walielezwa kuwa tatizo linatokana na Tanzania kutegemea umeme wa maji kwa asilimia 55 na wala hakuna mtu aliyefanya makusudi wala uzembe bali ni matokeo ya uwekezaji uliofanywa na Serikali kwa nia njema kama zilivyofanya nchi nyingi duniani.

Wakaelezwa wabunge hao kuwa tatizo la uzalishaji mdogo linatokana na m mabadiliko ya tabia nchi katika miaka ya karibuni na kwamba si Tanzania tu wanaathirika bali hata nchi nyingine duniani.

Pamoja na ushauri huo baadhi ya wabunge inaelezwa kuwa hawakuafiki kwa kile walichoeleza ni ahadi nyingi zilizotolewa na wizara kwa muda mrefu pasipokutekelezwa.

Hata hivyo, wabunge hao walieleza kwamba umefika wakati kwa viongozi wabababishaji ndani ya CCM kuachia madaraka kwa sababu lolote baya linalofanywa na Serikali, linapunguza imani ya wananchi kwa chama chao.

Lakini, walikubaliana kimsingi kuwa tatizo la umeme la mara kwa mara ni suala ambalo hata angekuwepo mtu wa namna gani kwenye nafasi ya uwaziri, asingeweza kulitatua.

Ikaonekana kuwa tatizo la uhaba wa maji kwenye mabwawa kuwa ni jambo ambalo halikutarajiwa na hata katika miaka ya nyuma haijawahi kutoke kiwango cha maji kupungua kiasi hicho.

Inasemekana wabunge wengi walikuwa na munkari wa hali ya juu ya kutema cheche, inaelezwa kuwa walitakiwa kuwa waangalifu na kauli zao wasije wakawa wanaibebesha lawama Serikali kwa mambo ambayo yako nje ya uwezo wake.

Maoni ya Kamati ya Makamba
Kwa upande wake, Kamati ya Nishati na Madini imeitaka Serikali kutoa maelezo kwamba ilikuwaje Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) linunue mtambo mkubwa wa Symbion bila kupanga kuwepo kwa gesi ya kuundesha ikizingatiwa kwamba mtambo huu umeagizwa zaidi ya miezi 18 iliyopita.
Mwenyekiti wa kamati hiyo, January Makamba alisema jana kuwa kamati yake ilijulishwa kwamba mitambo ya kusafisha gesi na bomba la kusafirishia gesi hiyo imefikia ukomo wa juu, na hata mtambo wa Symbion uliopo sasa, hauzalishi umeme kwa uwezo wake wa megawati 112 kutokana na kutokuwapo kwa gesi ya kutosha.

Alisema kuwa mbali na tatizo hilo, hata juhudi za sasa za kuongeza uwezo wa kusafisha gesi, haziwezi kukidhi mahitaji haya mapya hadi upanuzi wa miundombinu ya gesi utakapokamilika miezi 18 ijayo.
“Kamati inapendekeza Serikali iuhakikishie umma kwamba mtambo huu utapata gesi mara utakapofungwa Desemba na hautakuwa 'tembo mweupe (white elephant),”alisema Makamba.
Aliongeza kwamba, kamati yake ilibaini kuwa gesi asili, ikitumika vizuri kama inavyopaswa, inayo fursa ya kubadilisha sura ya uzalishaji wa umeme, maendeleo ya viwanda na uchumi wa nchi inawezekana.

Alisema kamati yake ilipata shaka kwamba nchi hainufaiki ipasavyo kutokana na kuwapo kwa gesi nchini, kwa maana ya unafuu wa bei, uharaka wa upatikanaji wa gesi na kujenga uwezo kwa Watanzania katika uwekezaji na utaalamu katika masuala ya gesi.

Alisema licha ya kwamba gesi ni maliasili muhimu kwa uchumi na usalama wa nchi, lakini imebainika kwamba biashara na utaratibu mzima wa uchimbaji, usafishaji, usambazaji na uuzaji nchini vimegubikwa na utata mkubwa wa kimkataba usio na maslahi kwa taifa na ukiritimba.

Alisema kamati haijaridhishwa na ushiriki, ufanisi na uadilifu wa Kampuni ya Pan African Energy Tanzania katika mchakato wa uendelezaji gesi nchini.
Kufuatia utata huo uliopo, kamati hiyo imeeleza kuwa itaunda kamati yake ndogo ili kufuuatilia na kuongeza kwamba ushauri wa kamati kwa serikali kupitia Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC), sasa ichukue uongozi madhubuti katika suala zima la gesi na si kukaa pembeni na kusubiri mapato.

Aliitaka Serikali ichukue hatua za haraka za kuondoa ukiritimba uliopo katika biashara ya usafirishaji na usambazaji wa gesi nchini kwa kushinikiza kampuni za Songas na Pan-African Energy ziruhusu wachimbaji na watumiaji wengine wa gesi watumie miundombinu ya kusafisha na kusafirisha gesi.

Aliongeza kuwa fedha zote zitokanazo na mapato ya uzalishaji wa petroli ambazo Pan African Energy wameipunja TPDC zikabidhiwe kwa shirika hilo la umma.
Alisisitiza kuwa katika hatua ya kuvutia wawekezaji, Serikali ihakikishe inaondoa vikwazo vya urasimu visivyo vya lazima hususani katika upatikanaji wa leseni.

Aliitaka Serikali kuipa EWURA (Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji) uwezo na mamlaka zaidi ya kudhibiti bei ya mafuta, na hatua kali zichukuliwe kwa wale wataokuwa wanauza mafuta kwa bei ya juu ya bei elekezi.

Alisema kwa kuwa Serikali inapoteza kodi ya kati ya Sh25 bilioni hadi Sh33 bilini kwa mwezi kutokana na tatizo la uchakachuaji mafuta, haina budi kuingilia kati suala hilo na kuhakikisha bei hizo zinadhibitiwa.

Sekta ya Madini
Kamati hiyo imeeleza kutoridhishwa na kiasi cha Sh1,189,630,000 zilizotengwa kwa ajili ya wachimbaji wa dogo nchini kwani ni ndogo mno ikilinganishwa na mahitaji yaliyopo.
Iliongeza kuwa wachimbaji wadogo watengewe fedha za kutosha ambazo zitawawezesha kununua vifaa ambavyo ndiyo nyenzo muhimu katika biashara yao na kushauri jitihada kubwa zaidi zifanyike kuwasaidia wachimbaji wadogo kuwawezesha kuendesha shughuli zao kwa tija, katika mazingira ya usalama zaidi na waweze kunufaika na jasho lao.

Kuhusu Shirika la Madini la Taifa (Stamico), Makamba alisema kamati imeipongeza Serikali kwa kuliweka chini ya uangalizi wake. Hata hivyo, alisema kamati inataka shirika hilo likabidhiwe fedha zilizopatikana kutokana na kuuzwa kwa nyumba zake nne na mali zake nyingine ili zitumike katika kutekeleza kazi zake za maendeleo
 
Back
Top Bottom