Wachawi, Mandondocha Na Misukule ya Kisiasa (Falsafa Binafsi)

X-PASTER

JF-Expert Member
Feb 12, 2007
11,610
1,810
Wachawi Mandondocha Na Misukule ya Kisiasa

Wengi wanaweza kukishangaa kichwa cha habari hapo juu, kiukweli ninachotaka kukizungumzia ni hao hao Mandondocha na Misukule wa Kisiasa.

Wengi wetu tunaelewa nini maana ya Wachawi, ndondocha na Misukule, kwa faida ya wachache wasio elewa maana ya hizo sifa hapo juu, nitawadokezea kabla ya kuingia kwenye mada.

Wachawi ni watu wanaotumia nguvu za giza kwa ajili ya kuwasumbua na kuumiza watu wengine kimazingara, kwa ajili ya kujilinda au kwa ajili ya kujifurahisha kwa kuwatesa watu wengine kwa kuwachukua msukule au kuwafanya kuwa ndondocha au kuwafanya wengine waugue au wafe na huii ni kwa faida zao binafsi.

Ndondocha ni watu waliotoroshwa na kudhaniwa kuwa wamepotea, kiasi ya ndugu, jamaa na marafiki kufikia kusema kuwa labda wanaweza kuwa wamefariki dunia, lakini kumbe wamechukuliwa na wachawi kisha wakarogwa na kubadilishwa akili zao na kuwa kama watumwa na wakajikuta wanafanya mambo ya ajabu na haswa yale ambayo mchawi wao anataka wayafanye.

Msukule kwa upande mwingine ni watu ambao wanaaminiwa kuwa wamekufa lakini kumbe wamechukuliwa kwa madawa ya kichawi ili kumtumikia mganga, mchawi, au mwanamazingara Fulani, japokuwa ndugu, jamaa na marafiki wanaweza kushuhudia mazishi yao.

Basi hali hii ya kuwa Wachawi, Ndondocha au Misukule ndio hali ambayo imewakumba wanasiasa na washabiki wa siasa wa vyama vya siasa vilivyoko hapa Tanzania.

Unaweza kushangaa mtu mzima na msomi wa kiwango cha PhD, lakini jinsi anavyochangia mijadala ya kisiasa hana tofauti na wale ambao hawakubahatika kufikia kiwango cha elimu aliyokuwa nayo yeye. Kinachowekwa mbele hivi sasa ni ubinafsi, umimi, usisi au wao wakiongozwa na tamaa mbaya za kimaisha.

Sababu kubwa ni kwamba wengi wao hawana tena ule uzalendo wa kutetea nchi na wananchi, wengi hivi sasa wanajali maslahi ya muda mfupi na faida za papo kwa papo. Hali hii imetokana na watu kukata tamaa ya maisha na kuamua kubangaiza bangaizatu ili siku ipite na yeye au wao wapate mradi wao/wake wa siku ile.

Ndio watu kama hawa mimi siwaiti wabangaizaji tu, bali kama si Wachawi basi ni Mandondocha au Misukule ya kisiasa, ambao hawajui wanacho kitetea, wala wanacho kipinga, yaani wapo wapo tu, hawana tofauti na hao misukule na mandondocha ya kichawi. Mladi wao wamepata mlo wao wa mashudu/pumba za mahindi (Nasikia ndio chakula cha
misukule na Ndondocha), basi hawana fikra endelevu tena.

Wakati mwingine huwa nahisi hivi vyama vya siasa vimekuwa kama vilinge vya wachawi, hao wanasiasa wenyewe ndio magwiji wa uchawi wenyewe na raiya wanao washabikia ndio misukule na mandondocha wao, kwa sababu mambo mengi yanayo changiwa na hao washabiki wa vyama vya siasa, hakika yanatia kichefu chefu, na utafikiri kuwa viongozi wao hawaoni la wanaona sana, ila wanayafurahia hayo ya kugombana kwa misukule na mandondocha ndio kunakowapa ulaji wachawi (wanasiasa). Na ndio utaona kuwa hawakemei chochote kile kinacho fanywa na misukule yao.

Tatizo kubwa la hawa mandondocha na misukule ya kisiasa wanafikiria kuwa na imani ya dini tofauti au kushabikia chama tofauti ni uadui. Awa demokrasia yao ni demokrasia ya kindondocha, demokrasia ya visasi na kukomoana. Kwao mwananchi akijiunga na chama kingine, tofauti na kile anacho kishabikia yeye, au kuwa na imani ya dini tofauti na ile anayo iamini yeye, basi mtu huyo hustahili hata kunyimwa haki zake za msingi za kibinadamu na zile za kiraia.

Baadhi (ya mandondocha hao) hudhani kuwa ni halali hata kutumia lugha za matusi, kejeli na kashfa za uongo kum’bughudhi na hata kuzulia mtu na familia yake mambo ambayo yanaweza kumpelekea kumuangamiza. Kwa wale mandondocha walio na madaraka, japo ya umeneja kama si ukurugenzi limekuwa ni jambo la kawaida sana kuwanyima ajira na njia yoyote ya kujitafutia riziki kwa wale wote wenye kuonekana kuwa hawapo pamoja kwenye siasa na imani za kidini.

Imefikia mahala ambapo hata kwa biashara ya genge la kuuza vitunguu na nyanya, inakuwa ni muhali mtu kuwa nalo. Ndio maana imekuwa kawaida ya wachawi wengi kuwaalika baadhi ya viongozi wa kidini ili wapate uhalali wa kufanyiwa kampeni uko kwenye majumba yao ya ibada.

Mtu yeyote ambaye ajahathiriwa na urozi wa wachawi wa kisiasa na anayeitakia mema nchi hii hawezi kutumia lugha ya udini na kuwagawa watu kama vile kuanza kuwaita wengineo wao, na wengine sisi ndani ya nchi moja, iwe kwa siri au dhahiri. Hii ni kwa sababu kitu kiitwacho jamuhuri ya Muungano ya Tanzania, ni muungano wan chi mbili, na nchi hzi zimekusanya wa watu wa makundi mbalimbali, yaani kutoka kabila mbalimbali, dini mbalimbali, na rangi mbalimbali, na hali tofauti za kiuchumi na maendeleo. Kwa ajili hiyo lugha za kusema wao Waislamu, na sisi Wakrsito au wao chama chao, sisi chama chetu, hizo ni lugha chafu za kukemea, kwa kuwa zinamong'onyoa umoja wa kitaifa na kuchochea mgawanyiko ambao hauna msingi.

Binadamu uliye kamilika lazima uwe na tofauti kubwa sana na msukule au ndondocha, tena kwa viwango vikubwa sana. kila mtu ana fursa nzuri ya kuyaelekeza kwa busara mawazo yake katika maisha. Lakini basi hakuna kitu kilicho muhimu kwa mtu na kwa wakati huohuo kikawa kigumu zaidi kama kuidhibiti hisia na matamanio ya nafsi yake. Basi tunashauriwa kwamba yale tunayo yataka kuwa yasizidi kupita kiasi na kuondoa busara zetu, kiasi ya kwamba tukawacha kushirikisha akili zetu katika kuyaendea yale tunayo yataka yawe.

Tanzania ni nchi ya amani, wanachi wake wengi ni wenye kuamini imani tofauti tofauti na wameishi kwa miaka mingi kwa maelewano makubwa kabla ya hata mkoloni wa kwanza kukanyaga ardhi hii. Tanzania ni nchi katika nchi chache duniani iliyoweka msingi madhubuti wa kuishi pamoja watu wa dini na makabila mbalimbali katika hali ya kukubali kutokubaliana.

Kwanini tunashindwa kuondoa ubinafsi, kwanini tunashindwa kutumia bongo zetu, tukawavuta wale tunaowatenga na kuwaona kuwa ni maadui zetu, kwanini tunashindwa kuwavuta kwa maneno mazuri na yenye hikma! Mara nyingi naona washabiki wengi wa kisiasa upenda kutumia maneno ya kebehi na yenye kuudhi, katika kujibu hoja. Hali hii sidhani kama inaweza kumvuta mtu yeyote mwenye akili zake timamu, labda tu na yeye ni miongoni mwa ndondocha au msukule au naye anajitahidi kutaka kuwa mchawi. Yaani kila mchangiaji aishi kutoa mipasho kama vile tupo kwenye taarabu za rusha roho. Inaudhi sana, tena sana tu.

Binadamu ukijipenda sana, kunakupelekea kuwa na kiburi na kujiona wewe ni bora kuliko wengine. na hali hii ni sawa na kujenga ukuta badala ya kujenga daraja la kutuunganisha na wale tunao waona kuwa si bora kama sisi. Na hali hii tukiiachia kuendela basi huwa ni muhali kupatikana mafanikio ya maisha kwa sababu kama hakuna nidhamu katika majadiliano basi hakuta kuwa na muwafaka, na siku zote tutakuwa kama kuku wa kienyeji kwenye banda, kwa maana hakuna masikilizano...!

Binadamu tumeumbwa ili tushirikiane kwa pamoja ili kufikia malengo na mustakabari wa maisha yetu... Kwa sababu kila binadamu anapenda kusikilizwa na wengine. Kila mtu anapenda kuishi kwa masikilizano na wengine na anachukia asiposikilizwa. Lakini ikitokea mtu kuwa na roho mbaya, yenye chuki zisizo na sababu, basi moyo wake ukosa utulivu na ukosa amani kwenye nafsi yake, kiasi ya kwamba uwachukia hata wale wanao mpenda na kumwelekeza kwenye mafanikio yake mwenyewe.

Amani, upendo, masikilizano na ushirikiano na watu wengine, ndio msingi muhimu wa maisha ya katika jamii yoyote ile. Sharti la kwanza kabisa la kuwepo upendano na masikilizano ni kuheshimu hisia na haki za watu unaofanya nao majadiliano. Jambo hili ndilo linaloimarisha na kudumisha uhusiano kati ya kila mtu.

Watu wasiokuwa na sifa kama hii husababisha kuvunjika masikilizano kati yao na kila mtu katika jamii, huregeza nguzo ya urafiki na upendo, na wala hawawezi kuhifadhi uhusiano wao na watu wengine katika hali inayokubalika.

Tabia ambayo ni mbaya kabisa na yenye kuondoa mafungamano ya kirafiki na umoja katika jamii ni kutosikilizana, kubezana, kutukanana kukebeihana, haya mambo uleta ugomvi. Mara nyingi mtu mgomvi uonekana mbele ya jamii kama hana sababu, lakini sababu kubwa kabisa ni yeye mwenyewe na nafsi yake kwa kuruhusu roho chafu kumtawala na kujiona kuwa yeye ni bora na mwenye kutaka kusikilizwa peke yake, kumpelekea kujenga kiburi ambacho uharibu na kuathiri hisia zake na kuuchafua moyo wake na kupoteza nishati inayotunza mwili wake, na kusababisha mtu huyu kuzeeka upesi na wakati mwingine kupata matatizo ya kiafya.

Lakini pia kuna ulazima wa sisi wenyewe tuelewe kwamba ubinafsi wetu uliopitiliza kiasi ndio sababu ya kutopendana kwetu. Kwani mmea wa ugomvi na chuki ukua kwa kumimiwa maji na kupaliliwa na mbolea ya ubinafsi.

Kuwa na vyama vingi isiwe ndio sababu ya kuvunja umoja wa kitaifa, Watanzania wasitegemee kujenga utaifa huo huku baadhi ya viongozi (wachawi) kwenye vyama vya kisiasa, vikiongozwa na chama tawala wakikaa kila kukicha kukashifiana, kukejeliana na kutukanana na baadhi ya viongozi na wananchama wa vyama vya upinzani na chama tawala.

Umefikia muda sasa Watanzania tujifunze kwa wenzetu, kama vile Afrika ya kusini, jinsi viongozi wa chama tawala wanavyoweza kufanya kazi na wale wa upinzani kwa mslahi ya taifa. Mfano mzuri na wa karibu ni ule alio uonyesha Mzee Nelson Mandela wa Afrika ya Kusini ambapo aliweza kushirikiana na vyama vingine kuijenga nchi yao ya Afrika ya kusini. Kwanini Wachawi wa Kitanzania wanashindwa, kiasi ya kuwapelekea ndondocha na misukule kuchukuwa majukwaa yao!?

Imefikia mahali sasa hakuna tofauti tena, kati ya mchawi na ndondocha, wote wamekuwa hali moja, tofauti tu mmoja mchawi mwanasiasa na mwingine ni ndondocha shabiki wa siasa. Wakati mwingine huwa nahisi hata hao wachawi wetu nao wamerogwa na mchawi mkuu, sijui Konikoni au Gagula, maana hata hatujijui kabisa. Uko tunako elekea nahisi kabisa tunaelekea kwenye maangamizi.

Hali kama hii ikiendelea uzalendo lazima ufe, na anayeua uzalendo katika nchi hii ni ni hao wachawi wachache wa kisiasa wakishirikisha ndondocha na misukule yao. Nasema na litakumbuwa ili neno, siku kule vijijini nako kukipatikana mandondocha na misukule kama iliyoko mijini basi kutapelekea hata hao wachache waliobakia kutokuwa na uzalendo tena, na uzalendo ukisha kufa kabisa na isiwepo japo chembe ndogo tu kwa watu wachache, hapo ndipo nchi inapofanana na zile simulizi za kwenye vitabu vya dini, nchi za Sodoma na Gomora ambapo walihitajika wenye haki watano tu ili nchi isiangamizwe lakini wakakosekana.

Tujikwamue kifikra, tutoke kwenye makucha ya hawa wachawi walio turoga na kutuusababishia kuwa kama Mandondocha na Misukule ya kisiasa.


__
Matamanio Yetu (Falsafa Binafsi)

Mabishano Haya Kwa Faida Ya Nani!?

Kutojijua Mwenyewe (Falsafa Binafsi)
 
Tamaa zimejaa kila anaepata nafasi anataka kuiba haraka,badala ya kusaidia jamii.
Kitu kingine,kwa sababu watu wengi si waaminifu, hivyo mwaminifu anakata tamaa.
 
Elimu yako katika jukwa hili inani kosha sana.Vitu unavyovizungumza ndivyo vilivyo katika jamii zetu.(HUYU X-PASTER NI NANI?)
 
Maneno mazuri lakini tuliofika wenye kuelewa lugha yako ni wachache sana tena sana.Ila Mungu ufanya kazi in a mysterious way majibu ya Wachawi hao[Wanasiasa] na Mandondocha wao [Wapenzi na Wanachama wao] yako njiani kwani sie tusio na vyama vya kisiasa tupo pembeni na yetu macho,na Mungu anatuonyesha kila njia wanayopita.

Wanasiasa wa sasa wamejaa unafiki, uchoyo, husda, vijcho, ulevi, ulaghai, uongo, uchonganishi, uzushi, wizi, utapeli, ubabaishaji, uzandiki, ufilauni, tamaa na mengineyo yote yanayohusu vinyongo na uhalibifu kwenye jamii.Wanasiasa wamekuwa lango la unyanganyi na dhuluma dhidi ya haki na ustawi wa Wananchi na Taifa letu kwa ujumla.Wanasiasa wamekuwa ndio waandaaji na wapangaji wa dhuluma na utapeli wa mambo yote muhimu juu ya umma na si tena kuwa watetezi wa wanajamii na Taifa letu.

Sifa bora ya wanasiasa na wapenzi wao wa sasa ili mtu awe mzalendo wa kweli wa Nchi ni kuwa mjuzi wa kusema au kufitinisha wengine kuwa nani anawasema vibaya watawala wa nchi hii.Kibaya wameingia kwenye vyombo muhimu vya utetezi wa haki halisi ya ubinadamu wa mtu na wameweka makazi huko wanahujumu kufikia kutishia haki za watu za kuishi kwa kuwachongea na kuweka mazingira wanyimwe kazi za kuwapatia riziki duniani kama wanadamu,hivyo kuwafanya waishi vibaya na wapendwa wao,chini ya udhalimu huo.

Hakika kwa matendo kama hayo ni kumkufuru Mungu, na kutaka kuchukua nafasi ya uumbaji wake.Lakini yote hayo yana mwisho ukiniuliza mimi hakika tumekaribia mwisho wa mateso,kwa wanaojua crimax ya Miungu watu ndani ya mfumo ilikuwa shida sana kwa miaka saba nyuma yake kwenye utawala wa mzee wa ukapa.Ukweli hapa ndio kiwango cha juu cha Umungu mtu ulisimama na kwa sasa ni kama JK amechangia sana kuua Umungu mtu huo ndio maana wenye akili zao walimtunukia shahada ya Udaktari wa sheria wakijua nini anachokifanya.

Leo hii tunajadiliana hadharani lakini hakuna kipindi kibaya cha uadui na majungu ya chama na serkali kushika hatamu huku viongozi wakuu wakitenda maozo ya kutisha huku wananchi wakipolwa maliasili yao lakini kukiwa hakuna mwanya wa taarifa ya maozo yao wezi wa mali hiyoo ya umma kuanikwa hadhalani na ilipotokea aliyesababisha kuanikwa hayo maovu au udhalimu huo atakiona cha mtemakuni na pengine kuishi pabaya.

Tujiulize kulikoni mbona mataifa ya wenzetu baadhi ya viongozi wao wanapata heshima kubwa za kuthamini michango yao kama ile ya Ibrahim Mo, na juzi juzi Yoweri Kaguta Museveni nae kapata heshima hiiyo ya kimataifa iweje viongozi wetu ambao ndani ya Nchi yetu walijitanabaisha kusimamia mambo ya wageni kuliko wazawa lakini bado dunia haiwatambui je wanajua nini kuhusu viongozi wetu.

Hakika kwa kuwa Mungu yupo natuamani viongozi wengi sana wataaibika kwa mujibu wa matendo yao ya dhuluma kwa umma, waswahili wanasema mwisho wa uovu ni aibu.Viongozi wetu wengi wametenda maovu mengi na wakasahau kumwogopa Mungu na mafundisho ya muasisi wa Taifa letu Mwalimu Julius K Nyerere.Lakini hatimae ya yote wataulipia uovu huo kwa kuwa wazungu wanasema what goes around comes around,haya si manano yangu bali ni kanuni za wanadunia walizojiwekea na zinafanya kazi.
 
Wachawi Mandondocha Na Misukule ya Kisiasa

[Ndondocha ni watu waliotoroshwa na kudhaniwa kuwa wamepotea, kiasi ya ndugu, jamaa na marafiki kufikia kusema kuwa labda wanaweza kuwa wamefariki dunia, lakini kumbe wamechukuliwa na wachawi kisha wakarogwa na kubadilishwa akili zao na kuwa kama watumwa na wakajikuta wanafanya mambo ya ajabu na haswa yale ambayo mchawi wao anataka wayafanye.

Msukule kwa upande mwingine ni watu ambao wanaaminiwa kuwa wamekufa lakini kumbe wamechukuliwa kwa madawa ya kichawi ili kumtumikia mganga, mchawi, au mwanamazingara Fulani, japokuwa ndugu, jamaa na marafiki wanaweza kushuhudia mazishi yao.

vyote sio sawa kimaana hivi?
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom