Ukoloni mkongwe unakua kwa kasi nchini,huku ukishabikiwa kwa nguvu kwa mgongo wa sekta binafsi

mwakajilae

Member
Mar 11, 2011
58
46
Baada ya Uhuru wengi tutakumbuka kwama Mwl Nyerere alisema Tanganyika haikuwa na matabaka.Ni dhahiri kwamba alikuwa akizungumzia hali ya Wazawa,kwasababu wageni[Wazungu,Wahindi, na Waarabu] walikuwa matabaka ya juu wakati wa ukoloni na mpaka miaka ya mwanzoni ya Tanzania Huru.Hawa ndiyo waliounda sekta binafsi au sekta ya Soko,wakimiliki biashara kubwa za rejareja na Jumla.
Tofauti hii ya wageni na wazawa ilianza kupunguzwa nguvu mwaka 1964 Serikali ilipotengua mfumo wa kibaguzi ulioitwa "Tripartite system" ambao ulitoa huduma za ubora tofauti kwa Wazungu,Wahindi,Waafrika[wazawa].Ubaguzi huo ulionekana wazi katika huduma za elimu na afya,kadharika katika makazi na Mishahara,suala mbalo kwasasa linazidi kushangiliwa na baadhi ya wasomi pamoja na baadhi ya wanasiasa wa sasa pasipo kujua kwanini tulidai uhuru kama Taifa huru.
Sera ya "Africanization" Ilisaidia kuondoa ubaguzi wa ajira serikalini kati ya wageni na wazawa.
Ujamaa ulipowasili kupitia Azimio la Arusha[1967 na kuendelea],Sekta binafsi kwa ujumla wake ilidhoofu kutokana na Sera ya utaifishaji wa makampuni makubwa na ya kati.
Mahusiano ya Sekta binafsi na Utawala wa nchi katika Sera ilionekana kabisa kwamba Sekta binafsi ilitakiwa ishughulikie vitu vidogovidogo kwa sababu nguzo kuu za uchumi zilishikwa na kuendeshwa na Mashirika ya umma yaliyosimamiwa na Serikali.Lakini kilichojili ni kwamba wafanyabiashara wakubwa,wengi wao wakiwa wa-kiasia,walishirikiana na mameneja wa mashirika ya ummah katika kuendesha kile kile kilichoitwa Uchumi mbadala[second Economy].Baadhi ya viongozi nao walificha uwekezaji wao katika huu uchumi mbadala na kuyatafuna mashirika ya umma kwa kuchukua bidhaa kwa upendeleo au hata bila malipo.Uthibiti ulishindikana kwasababu nani angemthibiti nani?Viongozi wote waliimba wimbo wa ujamaa,lakini ni wachache walikuwa wajamaa halisi.
Hatua zilianza kuchukuliwa miaka ya 1980,uchumi mbadala ulikuwa karibu robo nzima ya uchumi wa nchi,ambapo mwaka 1983 vita dhidi ya wale wahujumu uchumi [makapteni wa uchumi mbadala]vita kali iliendeshwa na serikali,Sokoine akiongoza mapambano,ilitungwa sheria kali na kuundwa Tribunal au mahakama ya kushughulikia wahujumu uchumi.,matokeo yake ikawa ni kudidimia kwa sekta binafsi nchini kwa kutiwa hofu, baadhi yao wailiteketeza bidhaa na mitaji yao.
Licha ya vita ya wahujumu uchumi ambayo ilichelewa sana kuja,tunaweza kusema sekta binafsi ilifanya kazi mafichoni ikishirikiana na baadhi ya viongozi na watumishi wa Serikali wasiowaadilifu na kufanikiwa kuyadhoofisha mashirika ya ummah kwa kiasi kikubwa na kuwafanya wananchi na wahisani wadai kwamba uchumi wa kijamaa umefeli japo ndilo lillikuwa lengo lao kuu,hivyo hauwezi kuwaletea wananchi maendeleo.Na ndiyo maana sera ya Kiliberali au soko huria zilipokelewa na wananchi wengi kama mkombozi kumbe bado halijawa mkombozi kwasababu halijawa huria kwa waliowengi,limekuwa soko la wauzaji na siyo walaji.
Mwinyi aliingiza Falsafa ya Ruksa,tokeo la kisiasa la sera hii ilikuwa ukuaji wa ushabiki wa utawala wa Mwinyi kutoka kwa kada hii ya chini ya sekta binafs na baadhi ya viongozi namna ya kufaidiana.Viongozi wa serikali waliipa kada hii sehemu za kufanyia biashara zao na kuwalinda walipo ingiliwa na polisi,nayo kada hii ikawapa viongozi hao Sapoti ya Fedha za kampeni za Uchaguzi pamoja na kuwapigia debe na kuwapa kura zao.
Tokea hapo Vijana wakitaka kuchukua eneo kwa ajili ya biashara zao wanaweka kwanza jiwe lililo andikwa "shina la wakereketwa wa CCM"Ili kulindwa na chama tawala katika biashara zao.
Utawala wa Mwinyi uliwaweka wafanyabiashara wakubwa na wa kati karibu sana na utawala wake na pia karibu sana na Chama Tawala[CCM] Suala lililoendelezwa na Mkapa.Wafanyabiashara walitoka walimo kuwa mafichoni kipindi cha Mwalimu Nyerere na kuanza kutamba hadharani.
Baadhi yao walianza kuchukuliwa na CCM kama washauri rasmi na wasio rasmi kwa serikali na chama.,hasa kwaajiri ya sapoti kubwa ya kipesa kwa chama na wagombea wake katika chaguzi.Matumizi makubwa ya fedha katika chaguzi zetu yalianza katika ushirikiano huu wa serikali pamoja na sekta binafsi.
Ushirikiano huu wa KUFAIDIANA uliwezesha wafanyabiashara kushinikiza sera walizozitaka na chama tawala kikapata fedha kubwa ya kuendeshea chaguzi na shughuli za chama.
Kwasababu utakumbuka kwamba wakati wa mfumo wa chama kimoja[CCM]fedha za shughuli za chama na uchaguzi zilitoka moja kwa moja hazina kuu.Baada ya kuanzisha mfumo wa Vyama vingi ilibidi CCM ibuni vyanzo vipya kikiwepo hiki cha ushirikiano huu wa KUBADILISHANA FEDHA NA SERA.
Njia nyingine ikiwa ni kushinikiza sera kupitia wabunge wa chama tawala kwa kuwapa fedha za uchaguzi,pia wafanyabiashara wenyewe kuingia bungeni kwa kutumia uwezo wao wa kifedha au wafanyabiashara wakubwa kutoa msaada kwa mgombea urais kwa sharti la kupata uwaziri,hasa wizara zinazoendana vizuri na biashara zao.
Mwisho,Sekta binafsi hapa nchini ni Changa na dhaifu.Hii inatokana na historia yake na kukosekana kwa sera madhubuti ya kuijenga.Tuliingia na kuimba sekta binafsi ndiyo injini ya ukuaji uchumi.Lakini Sekta hiyo iko wapi?haionekani kama ukiondoa wawekezaji wa nje na wafanyabiashara wanje.Wazawa ni wachache sana na hawawezi ushindani wa wawekezaji wa nje pasipo mkakati wa makusudi wa serikali katika kuwasaidia.
 
Back
Top Bottom