Allien
JF-Expert Member
- Jul 6, 2008
- 5,546
- 1,861
Ufisadi wa kutisha taasisi za umma
Ufisadi wa kutisha taasisi za umma
na Salehe Mohamed na Rachel Chizoza, Dodoma
JINAMIZI la ufisadi linaendelea kuitafuna serikali na taasisi zake baada ya ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kubainisha kuwapo kwa ukiukwaji mkubwa wa matumizi ya fedha za umma.
Katika eneo moja, ofisi ya CAG imebaini kwamba, zaidi ya sh bilioni 29 zilizokatwa kutoka katika michango ya wafanyakazi kwenye mishahara yao zinazopaswa kuwasilishwa katika mifuko ya hifadhi ya jamii, hazikupelekwa kama sheria inavyoagiza.
Taasisi zilizokutwa na kashfa ya kutowasilisha michango ya wafanyakazi wake kwenye mifuko hiyo ya hifadhi za jamii ni STAMICO, Bodi ya Biashara ya Nje (BET), Shirika la Posta Tanzania (TPC) na Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).
Matatizo hayo yalibainishwa jana mjini hapa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Ludovick Utouh wakati akizungumza na waandishi wa habari baada ya kuwasilisha bungeni ripoti tatu za ukaguzi kwa mwaka 2007/2008.
Utouh alisema, kutokana na matatizo hayo, serikali imejikuta ikitumia fedha nyingi kwa ajili ya kulipa adhabu kwa wakala husika pindi wastaafu wanapoanza kudai fedha zao za viinua mgongo na pensheni.
Mbali ya hiyo, CAG alisema ofisi yake imebaini ufisadi mwingine wa hatari katika Hifadhi ya Taifa (TANAPA), ambako yalifanyika malipo ya awali yanayofikia kiasi cha bilioni 1.9 bila ya kuwa na dhamana na kabla ya kupokea vifaa kutoka kwa wazabuni mbalimbali, jambo ambalo ni kinyume cha Sheria ya Manunuzi ya Umma.
Alisema ugunduzi uliofanywa na ofisi yake umeweza kuinusuru serikali kupata hasara ya zaidi ya sh milioni 532 ambazo wangelipwa wastaafu kama pensheni.
Aidha, Utouh alisema ukaguzi huo walioufanya umewaokoa wastaafu kulipwa pungufu ya fedha walizostahili kwa zaidi ya sh milioni 416.
Utouh alisema mapungufu hayo yalisababishwa na Mhasibu Mkuu wa Serikali kimakosa jambo ambalo lingesababisha hasara kwa serikali na malalamiko kwa wastaafu.
Hii ingekuwa hasara kubwa kwa serikali, lakini pia ingeleta malalmiko kwa wastaafu ambao wangepunjwa mafao yao, kama ukaguzi usingebaini mapungufu hayo, alisema.
Utouh alisema, kama ilivyo katika maeneo hayo, Bodi ya Tumbaku nayo haikuzingatia Sheria ya Ununuzi ya Umma kutokana na hatua yake ya kununua bidhaa na huduma nyingine zenye thamani ya zaidi ya sh milioni 200 pasipo kuwa na taarifa sahihi katika hesabu zake.
Mashirika yetu ya umma yamekuwa na tatizo kubwa la kufuata sheria ya manunuzi ya umma, hivyo kusababisha hasara kwa shirika au taasisi husika, alisema Utouh.
Aidha, ripoti hiyo ilibainisha kwamba, Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limepata hasara ya zaidi ya sh bilioni mbili kwa sababu ya kutopata tozo kutokana na ukiukwaji wa mkataba baina yake na Kampuni ya Dowans Holdings.
Aliyataja madudu mengine ya ukiukwaji wa taratibu kuwa ni ule wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) ambayo iliingia mkataba na TICTS Mei 2000 ambao ulikuwa unaipa kibali cha kufanya kazi kwa muda wa miaka 10 ambapo mkataba huo umeongezwa na kufikia miaka 25 kabla ya kuisha kwa mkataba wa awali.
Utouh alisema mbali na eneo hilo la Mamlaka ya Bandari, pia alifanya ukaguzi maalum katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT) na kubaini kuwepo kwa jumla ya sh bilioni 133 zilizolipwa kutoka kwenye akaunti ya malipo ya madeni ya nje (EPA).
Alisema kwa mujibu wa ukaguzi huo, amebaini kuwa kati ya fedha hizo, jumla ya sh bilioni 90 zimebainishwa kulipwa kinyume cha utaratibu kutoka kwenye akaunti hiyo ambapo sh bilioni 42 kati ya hizo bado zinahitaji kufanyiwa uchunguzi zaidi.
Alisema ukaguzi alioufanya katika maeneo mbalimbali, umebaini kuwepo kwa ukiukwaji mkubwa wa Sheria na Kanuni za Ununuzi za Umma hali iliyosabaisha kuwepo kwa upotevu wa fedha katika baadhi ya maeneo.
Alisema kwa mujibu wa ukaguzi wake alioufanya katika Mamlaka ya Bandari, ameona kuwepo kwa kasoro nyingi katika kusainiwa kwa mkataba huo ambako hakukuzingatia taratibu za Sheria ya Ununuzi ya Umma ya mwaka 2004.
Aidha, alisema wamebaini mapungufu ya zaidi sh bilioni 25 katika manunuzi yasiozingatia taratibu yaliyofanywa na serikali, idara na wizara zake.
Katika hatua nyingine, Utouh alisema, kuna mashirika 158 anayopaswa kuyakagua, lakini ripoti aliyowasilisha bungeni inahusu jumla ya mashirika 91 tu ambapo 67 hayakuweza kukaguliwa kutokana na kutoandaa ripoti zao za hesabu.
Alisema kati ya mashirika hayo 91 yaliyokaguliwa, 80 kati yake yalipata hati zinazoridhisha, 10 yalipata hati za shaka ambapo ni shirika moja tu lililopata hati chafu.
Alibainisha matatizo mengine makubwa yanayoyakabili mashirika ya umma kuwa ni kudai madeni makubwa wateja wake ambapo Shirika la Taifa la Bima (NIC) linawadai wapangaji wake zaidi ya sh milioni 933.
Aidha, udhaifu mwingine ulibainishwa kuwepo katika Mamlaka ya Mapato (TRA), ikizitoza kimakosa kodi ya ongezeko la thamani (VAT) TSN na Shirika la Posta zaidi ya sh milioni 375 na hivyo kutakiwa kuwarejeshea fedha zao.
Shirika la NSSF lenyewe likikabiliwa na kutolipwa kwa madeni yake yanayofikia zaidi ya sh bilioni nne kutoka kwa wadaiwa wakubwa saba, huku Benki ya Posta ikidai zaidi ya sh milioni 196.
Pamoja na matatizo hayo, ripoti hiyo inaonyesha kuboresha kwa utendaji na matumizi ya fedha kwa Serikali Kuu pamoja na zile za mitaa tofauti na ripoti ya mwaka 2005/2006.
Ripoti ya mwaka huu ya serikali za mitaa imefanya vizuri ambapo halmashauri 79 zimepata hati zinazoridhisha tofauti na mwaka uliopita ambapo ni halmashauri 53 zilizopata hati hizo.
Alisema mwaka jana halmashauri zilizopata hati zisizoridhisha zilikuwa ni nne wakati mwaka huu hakuna halmashauri iliyopata hati zisizoridhisha.
Mwaka huu halmashauri nyingi zimefanya vizuri kuliko miaka iliyopita, labda kutokana na tishio la kuzifuta halmashauri zitakazopata hati chafu lililotolewa na Rais Kikwete na kutotoa ruzuku kwa halmashauri hizo, alisema Utouh.
Aidha, alisema ili kuwaridhisha wahisani wameanzisha utaratibu wa kukagua miradi inayotolewa na wafadhili pamoja na ofisi 30 za ubalozi zilizopo hapa nchini.