Tutafakari Watanzania

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,789
288,015
Kaa chonjo, kina Karl Peters wa zama hizi waja!

Johnson Mbwambo Julai 9, 2008
Raia Mwema~Muungwana ni Vitendo

WIKI iliyopita nilijadili kuhusu ahadi ya kutengeneza ajira mpya milioni moja iliyotolewa na CCM wakati wa kumnadi mgombea urais wake (Jakaya Kikwete) kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2005.

Nilisema kwamba Rais Kikwete tayari ameshamaliza nusu ya kipindi chake cha miaka mitano cha urais, na bado hajaweza kutengeneza ajira mpya japo 300,000 tu. Isitoshe, baadhi ya ajira zilizokuwepo zimepotea kwa sababu ya kuendelea kubinafsishwa kwa mashirika ya umma kama vile TRC (sasa TRL). Hiyo ni kwa sababu kazi ya kwanza kubwa inayofanywa na wamiliki wapya ni kupunguza wafanyakazi.

Nilieleza athari za nchi yetu kugeuzwa soko la bidhaa za nje hata zile ambazo zamani zilikuwa zinatengenezwa na viwanda vyetu hapa nchini. Zama za utawala wa Mwalimu Nyerere, nchi yetu ilikuwa imepiga hatua kubwa katika sekta ya viwanda.

Tulikuwa tumeweza kujenga viwanda vya kuzalisha bidhaa nyingi ambazo hapo awali zilikuwa zikiagizwa kutoka nje (Import Substitution Industrialization). Viwanda vya Urafiki, Mwatex, Mutex, UFI, Tanga Cement, Mgogolo (karatasi), viwanda vya mazao ya mkonge na kahawa, Tanzania Fertilizer (TFC) na Minjingu n.k, ni ushahidi tosha wa hatua tuliyokuwa tumefikia katika sekta ya viwanda.

Kwa hakika, kuanzia mwaka 1971 Tanzania ilikuwa imeanza kuandaa mpango wa ujenzi wa viwanda vikubwa vya kuzalisha nyenzo za uzalishaji (heavy industries).

Si siri kwamba kama tusingesambaratishwa na sera za uchumi za mabeberu wa dunia zinazoshinikizwa kwa nchi masikini duniani (uchumi wa soko huria, ubinafsishaji, utandawazi na vikorombwezo vyake), leo hii tungekuwa mbali kiviwanda; na vijana wetu wasingekosa ajira kwa kiwango tunachokiona hivi sasa.

Nilihitimisha tafakuri yangu kwa kusema kwamba ni vigumu kuwapatia ajira wahitimu wa vyuo vyetu vikuu zaidi ya 13 nchini, kama serikali hii ya CCM itaendelea kupuuza ujenzi wa viwanda nchini; vikiwemo vile vinavyohusiana na sekta ya kilimo.

Leo, napenda kuuendeleza mjadala huo kwa lengo la kutoa tahadhari juu ya ujio katika nchi yetu (na kwingineko Afrika ) wa kina Karl Peters wa zama hizi wanaosaka ardhi kwa ajili ya manufaa yao Ughaibuni.

Huko nyuma nilishatahadharisha katika safu hii kuhusu kumiminika katika nchi masikini duniani (ikiwemo Tanzania) kwa mashirika na makampuni makubwa ya kibeberu, kwa lengo la kusaka ardhi kwa ajili ya kilimo kipya cha mazao ya nishati (Biofuel au Agrofuel).

Tayari kampuni moja ya kibeberu ya Uingereza inayoitwa Sun Biofuels plc, kupitia tawi lake la hapa nchini – Sun Biofuels Tanzania Limited, imeshafanikiwa kupata hekta 8,200 katika wilaya ya Kisarawe, kwa ajili ya kilimo cha jatropha (mibono) . Eneo hilo ni la vijiji 11 vyenye idadi ya watu 11,000.

27.jpg

KARL Peters

Kama ilivyokuwa kwa kina Karl Peters wa miaka ile ya 1884 na kuendelea ambao walijenga urafiki na machifu wetu na kuwalaghai wawagawie ardhi; huku wakiwapa ‘vizawadi' vya shanga na vioo, makampuni haya ya kibeberu nayo yanawaingia watawala wetu kwa "gea" ya kutengeneza ajira.

Kwa mfano katika suala hilo la Kisarawe, ukiachilia mbali kiwango kidogo cha fidia ambacho vijiji vimelipwa/vitalipwa ( Sh. milioni 800 tu kwa hekta 8,200 – sawa na dola 77 tu kwa hekta moja), vijiji hivyo vimeahidiwa kwamba ajira 1,500 zitatengenezwa kwa ajili yao.

Lakini suala hapa si malipo madogo ya fidia, ambayo tayari baadhi ya vijiji vimeanza kuyalalamikia, na wala si ajira hizo ambazo hakuna mwenye uhakika kama kweli zitatolewa kwa idadi hiyo kwa kuwa si sehemu ya mkataba (makubaliano). Suala hapa ni vijiji hivyo 11 vyenye wakazi 11,000 kupoteza ardhi yao kwa kampuni hiyo ya Uingereza.

Nimetoa mfano mmoja tu wa Kisarawe, lakini ukweli ni kwamba sehemu kubwa ya ardhi ya Tanzania itachukuliwa na makampuni hayo ya kibeberu kwa ajili ya kilimo hicho kipya cha mazao ya Biofuel.

Naamini hivyokwa sababu nchi yetu, hivi sasa, inanadiwa huko nje kwamba ina hekta zaidi ya milioni 88 za akiba zinazofaa kwa kilimo cha mazao ya Biofuel; tena katika mnada huo wanazii kuisifu ardhi yetu kwa kusema ; "none of which is virgin forest or environmentally sensitive" (rejea ripoti The Agrofuel Industry in Tanzania:A Critical Enquiry into Challenges and Opportunities) .

Nimetoa mfano wa kampuni hiyo moja ya Uingereza ya Sun Biofuel plc, lakini ukweli ni kwamba zipo nyingine kadhaa za kigeni zinazoendelea kujadiliana na vijiji kadhaa hapa nchini kupata ardhi kwa ajili ya kilimo hicho zikiwemo za Finland na Afrika Kusini.

Na kama nilivyoeleza mwanzo; wakati kina Karl Peter wa zama zile walikuja na shanga na vioo, hawa wa sasa wanawajia watawala wetu na msamiati wa uwekezaji mabilioni, misaada ya kiuchumi na hasa hasa ahadi za kutengeneza ajira mpya.

Labda swali la kujiuliza ni hili: Ni kwa nini mabepari wa dunia – Marekani, Uingereza, Finland n.k na hata wenzetu katika kundi la Nchi Zinazoendelea kama vile China, wanazihamasisha, hivi sasa, kampuni zao kuja Afrika kukamata ardhi kwa ajili ya kilimo?

Kwa upande wa kilimo cha mazao ya Biofuels jibu ni rahisi – wametishwa na kuzidi kupaa kwa bei ya mafuta katika soko la dunia, na hivyo wameamua kuhamia kwenye nishati ya mimea. Lakini kwa kuwa kwao hawana maeneo makubwa na mazuri kwa kilimo hicho, wanaitamani Afrika kwa kuwa ardhi inapatikana kirahisi (kifisadi) na kwa gharama za chini mno!

Isitoshe, nguvukazi katika Afrika ni ya gharama za chini mno, na hivyo faida itakayopatikana kwa kuendesha mashamba hayo Afrika ni kubwa kuliko ambavyo ingekuwa kwa kuendesha kilimo hicho kwao (hadithi ile ile ya kwa nini wakoloni walikuja Afrika!).

Lakini sababu ya pili na kubwa ni kwamba raslimali zao (yakiwemo mafuta ya ardhini) zinakauka kwa kasi kwa sababu ya matumizi makubwa; na ili kuzifanya ‘zipumue', ni lazima kuhamia Afrika!

Si siri kwamba wachotaji wa kufuja, wazalishaji kwa ubadhirifu na watumiaji kwa ulafi wa maliasili za dunia yetu hii, ni nchi tajiri zikiongozwa na Marekani.

Hebu fikiria; mtumiaji mmoja wa nishati katika Marekani hutumia nishati nyingi mara 20 kuliko mtumiaji aliyeko India, au China na mara 60 hadi 70 kuliko mtumiaji wa nishati wa Bangladesh au Tanzania.

Inaaminika kwamba kiasi cha mafuta ya petroli yanayotumiwa nchini Tanzania kwa mwaka mzima yanaweza kukidhi mahitaji ya Japan kwa saa 48 tu!

Kama ndivyo hivyo, haishangazi basi kwa nini matajiri hao wa dunia wanamaliza haraka maliasili zao na sasa wanatujia Afrika kwa staili ile ile ya kina Karl Peters kuturubuni ili watumie za kwetu.

Katika suala hili la kusaka ardhi ya kilimo barani Afrika, safari hii Waarabu nao wamo; yaani wameaua kufuata nyayo za Wazungu. Katika ukurasa wa 18 wa gazeti hili tumechapisha makala ya gazeti la The Guardian la Uingereza inayoeleza jinsi nchi za Kiarabu zinavyohaha kutafuta ardhi Afrika kwa ajili ya kujilimia chakula.

Nchi hizo za Kiarabu zimeamua kufanya hivyo baada ya maeneo yao madogo ya kilimo kukaukiwa na maji. Ripoti zinasema kwamba Rais Omar el- Bashir wa Sudan tayari ameshaipa bure Abu Dhabi eneo la hekta 31,000 kwa ajili ya kujilimia chakula ambacho kitauzwa katika nchi zinazounda Muungano wa Falme za Kiarabu.

Inaaminika kwamba Sudan imetoa eneo hilo bure kwavile eti inaona itanufaika na ‘teknolojia' kutoka Abu Dhabi, na pia inatarajia mahusiano yake na nchi hiyo ya Kiarabu yataimarishwa kwa ‘ofa' hiyo.

Kwa mtazamo wangu, Abu Dhabi imefanikiwa kuingiza kichwa cha ngamia kwenye hema, na haitashangaza ikiingiza kiwiliwili chote kwenye hema miaka ya karibuni - hila zile zile za kina Karl Peters!

Ripoti ya utafiti - "The Agrofuel Industry in Tanzania: A Critical Enquiry into Challenges and Opportunities", inayataja maeneo ya Tanzania yanayowindwa na makampuni hayo ya kigeni kwa ajili ya kilimo cha mazao ya Biofuel kuwa ni Arusha, Biharamulo, Rukwa, Shinyanga, Ruvuma, Tanga, Tabora, Lindi, Mtwara na mkoa wa Pwani.

Sehemu kubwa ya ardhi inayotafutwa katika maeneo hayo ni ya vijiji. Hofu yangu ni kwamba wanavijiji wetu wanaweza kuwakaribisha ngamia waingize vichwa kwenye mahema yao ili kujikinga na mvua; lakini mwisho wa yote ngamia wataingiza pia viwiliwili vyao, na mwisho wanavijiji watajikuta wametoswa nje kwenye mvua!

Kwa ufupi, ujumbe wangu ni wa kuwatahadharisha watawala wetu kwamba wanapaswa kuwa makini na wimbi hili la sasa la matajiri wa dunia kusaka ardhi za kilimo Afrika.

Watajitia wanatupenda na wanataka kutusaidia, lakini ukweli ni kwamba wanataka kuturejesha katika zama zile ambapo waliligeuza bara la Afrika kuwa eneo la kuzalisha malighafi zao kwa ajili ya viwanda vyao Ulaya, Marekani na sasa Asia (Japan na China).

Na kama ilivyokuwa zama zile za Karl Peters wanatughilibu na ‘vijizawadi' vya kututengenezea ajira na ahadi nyingine ambazo zinaweza kuwa hewa.

Tuamke, tugome kwa kudai mikataba inayolinda uhuru wetu, mikataba ambayo, mwisho wa yote, haitatufanya tupokonywe ardhi yetu na kujikuta tumebakia tu na vijiajira vya ukibarua kwenye mashamba yao. Kina Chifu Mangungu wa zama zile hawakuwa wamesoma; angalau sisi tumekwenda shule.

Tusikubali kupakwa mafuta kwa mgongo wa chupa na mabeberu wa dunia; eti sera zetu za kufufua uchumi ni nzuri, eti tunaongoza kwa demokrasia, eti hakuna ufisadi mkubwa nchini, eti tuna viongozi waadilifu n.k; kumbe sifa zote hizo ni janja - wanamezea mate ardhi yetu!

Tafakari.

Email: mbwambojohnson@yahoo.com
 
Back
Top Bottom