Tuache mzaha, tuangamize mazalia ya mbu kisayansi

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,357
33,200
KATUNI%28278%29.jpg

Maoni ya katuni


Kumekuwa na kauli tete kwamba mbu wameongezeka sana katika eneo la Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, na ongezeko hilo linadaiwa kuchangiwa na utafiti uliokuwa unafanywa katika bonde la Jangwani. Uvumi huo ambao ulikanushwa vikali na waliokuwa wakiendesha utafiti huo, kwa kutoa sababu za kisayansi kwamba hawawezi kuwa chimbuko la ongezeko la mbu hao, bado watu wasiotaka kusumbua vichwa vyao wameendelea kung’ang’ana kwamba mbu hao wameongezeka kwa sababu ya utafiti huo.

Wakati jamii ikiendelea kung’ang’ana na uvumi huo, kuna habari kwamba lile wimbi la kuongezeka kwa mbu sasa limebisha hodi maeneo ya Magomeni. Watu wanadai kwamba mbu hawa wameongezeka sana na sababu zinazosukumwa juu ya ongezeko hilo ni utafiti uliokuwa unafanywa katika bonde la Jangwani ambako vilijengwa vibanda kadhaa, lakini baada ya utafiti kukamilika vibanda vile vilibomolewa.

Tumekuwa tukifuatilia uvumi huu kwa muda lakini sasa imetubidi kuweka sawa baadhi ya mambo kwa ajili ya kusaidia jamii ijitambue na kuondokana na fikra dhaifu na ambazo hazina nguvu yoyote ya kisayansi katika kuzungumzia mambo mazito ya kitaalam.
Kwanza tungependa kusema kwamba jamii inafahamu vilivyo mbu wanaongezeka vipi.

Tangu elimu ya msingi watoto wetu wanafundishwa kuwa mbu huzaliana sehemu yoyote ambayo maji yametuama; penye majani marefu na hali ya majimaji ambayo huweka mazingira ya kutagwa kwa mayai ya mbu na kisha kuanguliwa.
Ndiyo maana fomula namba moja ya kupambana na mbu ni kuharibu mazalia yake; yaani kila maji yanapotuama, kwa maana ya madimbwi, maji yaliyosimama kama kwenye makopo, vifuu na vipande vya vyungu ni lazima viharibiwe na kuhakikisha kuwa hakuna maji.

Katika makaro ya maji machafu majumbani ni lazima juhudi zifanywe kumwaga dawa ili kuteketeza mayai ambayo yatakuwa yametagwa yakisubiri kuanguliwa
Juhudi hizi ni lazima ziendeale na usafi wa mazingira endelevu, si mara moja, ila ni kazi ya kudumu ambayo itafanya maisha ya mbu kuwa magumu kuzaliana na hivyo kuteketea

kabisa katika mazingira wanamoishi watu.
Kwa muda mrefu tumekuwa tukihoji mbinu za taifa hili za kupambana na malaria kwa kugawa vyandarua vya bure, tena kwa wanawake wajawazito na watoto wenye umri wa miaka mitano. Tumekuwa tukihoji harakati hizi kwa sababu hakika haziwezi kuwa endelevu, lakini muhimu zaidi hazilengi kwenye kiini cha matatizo ya malaria nchini, ugonjwa unoongoza kwa kuua zaidi ya magonjwa mengine yote ukiwamo Ukimwi.

Mbinu hizi hata kama zinamfanya mtu kulala kwa amani usiku kwa kuwa anakuwa ameondokewa na kero ya mbu, bado mbu wanaendelea kuzaliana na kushamiri sawa sawa katika mazingira yetu. Inawezekana chandarua kikatoboka na mbu akazama ndani na kuendeleza uharibifu wake, lakini pia wapo wale wanaofanya kazi hadi usiku wa manane,

kama walinzi, wanaoingia shifti za usiku kama vile wauguzi na madaktari, wote hawa hawawezi kutembea na chandarua.
Lakini wapo pia wanafunzi wanaoamka usiku wa manane kwa ajili ya kujisomea nao pia hawawezi kuwa ndani ya vyandarua wakati wakisoma na kufanya mijadala mbalimbali ya masomo miongoni mwao shuleni na vyuoni.
Ni kwa maana hiyo suala zima la kupambana dhidi ya malaria linapaswa litazamwe

kisayansi, kwa kuendesha kampeni kabambe ya kuteketeza mazalia ya mbu. Hii ni gharama ambayo taifa haliwezi kuikwepa sana kama ikitazamwa sawia na gharama ya kutibu wagonjwa wa malaria na maisha ya watu wetu wanaopoteza maisha kila kukicha kwa ugonjwa huo unaoambukizwa na mbu.
Tukumbuke katika miji mingi ya nchi yetu, Dar es Salaam ikiwamo, tumeamua kuishi na

uchafu, mazingira ni machafu, uchafu hauzolewi, mitaro ya maji taka imevunjikavunjia au kuziba na maeneo mengi hakuna mitaro kabisa.
Vijito na mabonde katika mazingira tunayoishi ndiyo yamegeuzwa sehemu ya kutiririshia maji machafu ya vyooni, kwa ujumla hali ya mazingira yetu ni ya kutisha kila mji wa nchi hii. Hali hii haibagui bonde la Jangwani, ambako maji yametuama kwa muda mrefu, hakuna

juhudi yoyote ya kunyunyuzia dawa ya kuua mbu na kuvuruga mazalia yake, matokeo yake tunaishi kwa uvumi kama huu kwamba ongezeko la mbu Muhimbili na Magomeni ni utafiti uliofanywa Jangwani na si kushindwa kwetu kuharibu mazalia ya mbu. Ndiyo maana tunasema inatubidi kubadilika na kutenda mambo kisayansi kwa kuachana na uvumi kwa kuwa hautatufaa kitu.



CHANZO: NIPASHE
 
Back
Top Bottom