WAKATI wingu la utata wa hesabu sahihi za mapato katika mechi ya watani wa jadi, Simba na Yanga, iliyopigwa Jumatano iliyopita likitanda, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), limesisitiza sh 390,568,000 ilizotangaza ni sahihi.TFF ilitangaza kuwa, fedha hizo zinatokana na mauzo ya tiketi kwa watazamaji 50,455 walioingia kushuhudia pambano hilo, kwa viingilio vya sh 5,000, sh 7,000, sh 10,000, 15,000, sh 20,000 na sh 30,000.Hata hivyo, hesabu hiyo ya watazamaji iliyotangazwa na TFF inapingana na ile iliyooneshwa na kituo cha SuperSport kilichoonesha watu 58,000 waliingia uwanjani kushuhudia pambano hilo la mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu bara.Kutokana na hali hiyo, wadadisi wa mambo, pamoja na klabu ya Yanga, wamehoji uhalali wa mapato hayo na idadi ya watu walioingia uwanjani siku hiyo na ufanyike uchunguzi wa kina kuhusu suala hilo.Akizungungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Katibu Mkuu wa Yanga, Lawrence Mwalusako, alisema kwamba hali hiyo inatia shaka, kwani hata takwimu za idadi ya watazamaji zilizotolewa na TFF ni tofauti na ile ya SuperSport.Alisema kwa mahesabu ya haraka haraka, hata mashabiki waliohudhuria mechi hiyo wangelipa sh 15,000 kila mmoja, zingepatikana zaidi ya sh milioni 600, hivyo hata klabu husika zilistahili kupata zaidi ya sh 93,345,549.15 walizogawiwa kila moja.Mwalusako aliongeza kwamba, wanashindwa kuelewa hali hiyo inatokana na nini na kuiomba TFF kufanya uchunguzi wa haraka ili kujua tatizo linatoka wapi, lakini kinyume na hapo hali itazidi kuwa mbaya.Katibu huyo aliongeza kuwa, wanatarajia kuwasiliana na viongozi wenzao wa Simba ili kujadili hali hiyo kabla ya kutoa tamko la pamoja.Kwa ypande wake, Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah alisema kuwa, idadi waliyoitangaza ni ya watazamaji walionunua tiketi pekee.