Tanzania hoi kwa utawala bora

Luteni

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
2,274
302
headline_bullet.jpg
Utendaji wa Takukuru bado
headline_bullet.jpg
Serikali inakalia mihimili mingine
headline_bullet.jpg
Chaguzi zadaiwa kujaa mizengwe

Ripoti ya utafiti uliofanywa na Mpango wa Hiari wa Nchi za Umoja wa Afrika kwa Vigezo vya Utawala Bora (APRM) Tanzania imebainisha kuwa Tanzania bado inakabiliwa na changamoto kubwa katika demokrasia na utawala bora.
Aidha, ripoti hiyo imesema ufanisi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) katika kushughulikia tatizo la rushwa nchini hauridhishi kabisa.
Changamoto nyingine imetajwa kuwa ni kushindikana kuendesha chaguzi zilizo huru na haki hasa upande wa Zanzibar, jambo ambalo limekuwa ni tatizo kubwa linalokwamisha maendeleo ya demokrasia na utawala bora.
Utafiti huo ulijielekeza zaidi katika masuala mbalimbali, ikiwamo Tanzania kuridhia mikataba ya kikanda na ya kimataifa, Muungano, uhalali wa Muungano, hatua zilizochukuliwa kushughulikia matatizo ya Muungano, migogoro baina ya vyama vya siasa na kushindwa kutekelezwa kwa makubaliano baina ya vyama vya siasa Zanzibar, migogoro ya ndani ya vyama na ushirikiano (Muungano) wa vyama vya siasa.
Mambo mengine yaliyojitokeza ni suala la mgombea binafsi, fursa ya kupata haki kwa wote, mfumo mbadala wa kutatua kesi, demokrasia na utawala sheria, changamoto kubwa, migogoro ya utawala, utatuzi wa migogoro baina ya mihimili mitatu ya dola na kupambana na rushwa.
Ripoti hiyo ilisomwa na Mhadhiri Mwandamizi katika Idara ya Sayansi ya Siasa na Utawala ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk Mohammed Bakari, katika semina ya kitaifa ya kuhakiki ripoti hiyo, iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.
Dk. Bakari alisema maoni ya jumla ya raia katika utafiti huo ni kwamba, kiwango cha rushwa kwa watumishi wa umma ni cha juu sana, huku ufanisi wa Takukuru ukiwa hauridhishi kabisa.
“Takukuru inalaumiwa kwamba inajihusisha zaidi na kesi ndogo na kukwepa kesi kubwa za vigogo,” alisema Dk. Bakari.
Dk. Bakari alisema mwaka 2003-2007, malalamiko yaliyofikishwa Takukuru, ni 22,184, huku yaliyofikishwa mahakamani yakiwa ni 74 tu, katika kipindi hicho zaidi ya kesi 5,000 zimefunguliwa jalada, lakini hazijafikishwa mahakamani. Alisema baadhi ya matatizo na changamoto zilizopo, ni pamoja na kuiweka Takukuru chini ya Ofisi ya Rais na kuilazimisha taasisi hiyo ipate idhini ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) katika kufungua kesi kubwa za rushwa.
Pia, kuzuia vyombo vya habari na asasi za kiraia kuripoti kesi, ambazo ziko chini ya uchunguzi wa Takukuru na kwamba licha ya kukiukwa kwa maadili ya viongozi, Tume ya Maadili haijaonyesha uwajibikaji wa kiongozi yeyote wa umma kwa kukiuka maadili.
Alisema mbali na mafanikio yaliyopatikana katika baadhi ya maeneo ya demokrasia na utawala bora, bado kuna matatizo makubwa yanayoikabili nchi, hususan yale yanayohusiana na ushindani wa kisiasa.
Dk. Bakari alisema kushindikana kuendesha chaguzi zilizo huru na haki, hasa kwa upande wa Zanzibar, limekuwa ni tatizo kubwa linalokwamisha maendeleo ya demokrasia na utawala bora.
Alisema karibu miaka 18 tangu kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi, bado hakuna makubaliano ya msingi ya kikatiba, sheria na asasi zinazosimamia ushindani wa kisiasa nchini. Katika ripoti hiyo, APRM Tanzania ilipendekeza kuwapo na chombo maalum cha kutatua migogoro baina ya mihimili mitatu ya dola nchini kutokana na hali iliyopo hivi sasa nchini ya mhimili mmoja kutoheshimu maamuzi ya mwingine.
Kati ya migogoro inayoikabili hivi sasa mihimili hiyo ya dola; yaani Bunge, Serikali na Mahakama, ni pamoja na ule unaohusisha uamuzi wa Mahakama Kuu ya Tanzania wa kuruhusu kuwapo kwa mgombea binafsi katika uchaguzi wa kisiasa nchini, ambao umeshindwa kuheshimiwa na serikali.
Dk. Bakari alisema licha ya uamuzi wa Mahakama Kuu ya Tanzania kuruhusu mgombea binafsi katika kesi namba 10 ya mwaka 2005 iliyofunguliwa na Mwenyekiti wa Chama cha Democratic (DP), Mchungaji Christopher Mtikila, hadi sasa serikali haijachukua hatua zozote za utekelezaji wa hukumu hiyo. Hata hivyo, alisema raia wa Tanzania wakati wa utafiti, walikuwa wanaliangalia Bunge vizuri kutokana na uhuru wake, huku asilimia 88 ya raia wa kawaida wakisema Bunge lina uhuru wa kufanya maamuzi, wakati asilimia 70.7 walisema bila wasiwasi, asilimia 17.3 walisema inategemea na asilimia 12 walisema Bunge halina uhuru kabisa.
Alisema kwa upande wa wataalamu, asilimia 89.2 walisema Bunge ni huru, wakati waliosema uhuru kiasi wakiwa ni asilimia 38.2, uhuru mkubwa asilimia 51 na uhuru kidogo asilimia 10.8.
Dk. Bakari alisema katika utafiti huo, asilimia 71.9 ya raia walisema chaguzi zinazofanywa zinakuwa huru na haki wakati asilimia 18.6 walisema haziwi huru na haki na asilimia 10.3 walisema hawajui.
Alisema tangu kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1992, Tanzania imepiga hatua kwa kiwango fulani katika nyanja hiyo na kumekuwapo na mabadiliko ya katiba, sheria na asasi kwa ajili ya kujenga demokrasia na utawala bora.
Dk. Bakari alisema uhuru, hasa kwa asasi zisizokuwa za kiserikali, uhuru wa kujieleza na ule wa habari, umeongezeka, ingawa hadi sasa serikali haijapitisha sheria mahsusi ya uhuru wa habari. Alisema utafiti huo umebaini kuwa uhuru wa vyombo vya habari, umeongezeka sana na jambo hilo linathibitishwa na namna kesi kubwa za rushwa zinazowahusisha viongozi wa ngazi za juu zinavyoripotiwa.
Pia, umebaini serikali iliyoko madarakani (kuanzia mwaka 2005 mpaka sasa), inaonekana kuwa na uvumilivu mkubwa wa uhuru wa habari ukilinganisha na serikali zilizotangulia na viwango vya kuheshimu haki za binadamu na utawala wa sheria vimeongezeka.
Kuhusu matatizo, Dk. Bakari alisema kesi za haki za binadamu zinashughulikiwa na Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufaa, lakini utaratibu huo huwa mgumu na ghali kwa raia wa kawaida.
Alisema Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, ambayo imeanza vizuri kazi, inakabiliwa na changamoto za kiutendaji, hasa nyenzo na wafanyakazi wenye ujuzi wa kutoa hudumu kwa upana zaidi, uelewa mdogo wa raia, ambapo wachache tu ndio wanaweza kufuatilia kesi za haki za binadamu na kudai haki zao kwenye vyombo husika.
Alisema tatizo hilo linaongezeka kutokana na uhaba wa watendaji pamoja na mazingira yasiyoridhisha ya kazi. Hata hivyo, alisema Mpango wa Marekebisho ya Sekta ya Sheria unajaribu kutatua tatizo hilo.
Alisema pia ada za mahakama na kuweka mawakili ni tatizo kubwa kwa maskini kuweza kupata haki. Hata hivyo, alisema serikali imeanzisha utaratibu wa vyombo mbadala vya kutoa haki, ambavyo huduma zake hazina malipo tangu mwaka 2000, kama vile Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Mahakama ya Ardhi na Mahakama ya Kazi.
Dk. Bakari alisema mgawanyo baina ya Serikali na Bunge, una utata na upungufu na kwamba mawaziri wote na manaibu wao kuwa wabunge kunakwamisha uwajibikaji wa Baraza la Mawaziri kwa Bunge.
“Rais ambaye ni mtendaji pia ni sehemu ya Bunge. Katika serikali zote mbili (ya Muungano na ya Zanzibar) serikali imekuwa ndio inatawala au kudhibiti mihimili mingine ya dola,” alisema.
Alisema Katiba ya Tanzania na ile ya Zanzibar, zinatoa haki za msingi. Hata hivyo, baadhi ya sheria bado haziwiani na mikataba ya kimataifa.
Awali, akifungua semina hiyo, Mkuu wa Idara ya Afrika wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Balozi Francis Malambugi, aliyemwakilisha Waziri wa Wizara hiyo, Bernard Membe, alimnukuu Rais Jakaya Kikwete kwamba, Tanzania imeamua kujiunga na mchakato wa APRM, si tu kwa utayari wake wa kujitathmini kwa vigezo vinavyokubalika vya utawala bora, bali pia kuwa tayari kuiendesha serikali na mfumo mzima wa uongozi kwa kuzingatia sheria, hekima, busara na weledi, kwa faida kama taifa na bara la Afrika kwa jumla.
 
Tuko hoi tukifananisha na nchi gani? mimi ninadhani tuache nadharia na tufanye comparative analysis.
Binafsi naamini kuwa tuna kazi kubwa lakini hatuko hoi na inachotakiwa na kuongeza spidi ili tufike mahala tuseme 'kazi imefanyika'
 
Tuko hoi tukifananisha na nchi gani? mimi ninadhani tuache nadharia na tufanye comparative analysis.
Binafsi naamini kuwa tuna kazi kubwa lakini hatuko hoi na inachotakiwa na kuongeza spidi ili tufike mahala tuseme 'kazi imefanyika'
Sioni haja ya kujifariji kwa kujiringanisha Nchi nyingine! Ukweli ni kwamba tuko hoi! Fisadi wanaiibia nchi, bado wanatamba mabarabarani! Ufisadi wa dhahili kabisa kama Richmond serikali inashidwa hata kuwawajibisha waliohusika bado unatafuta kujilinganisha na wengine? Hebu tuambie mazuri yaliyofanywa na serikali! Absolutely nothing?
Kibaya zaidi ni kwamba hata wale wachache wenye mapenzi mema na nchi yetu wanapojaribu kuyakabiri na kuyaanika madudu watu wanafanya huko serikalini wananyamazishwa kwa gharama yeyote! Serikali inaangalia!
 
Back
Top Bottom