Sitta arusha kombora kuhusu mfumo wa elimu nchini

TANMO

JF-Expert Member
Apr 12, 2008
11,514
11,277
WAZIRI wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta (pichani) amesema hasara ambazo taifa limepata kutokana na mikataba mibovu ni matokeo ya kasoro zilizopo katika mfumo wa utoaji wa elimu nchini.Sitta alisema hayo juzi usiku kwenye Sherehe za Maadhimisho ya miaka 10 ya Shirika la HakiElimu zilizofanyika jijini Dar es Salaam.

Alisema kasoro hizo zimesababisha mfumo huo wa elimu nchini kuzalisha watendaji mafisadi, wasiokuwa na maadili katika utendaji.

Sitta alisema sekta ya elimu ni kama imepewa kisogo, kiasi kwamba hakuna uwiano wa kiutendaji wa watu wanaohitimu mafunzo mbalimbali ikilinganishwa na vyeti vyao vinavyoonyesha kwamba walifanya vizuri darasani.

"Tumeshuhudia miaka 10 iliyopita, serikali imeingia hasara kutokana na baadhi ya viongozi kukosa uadilifu, wakaliingizia hasara taifa kwa kusaini mikataba feki," alisema Sitta na kuongeza:"... Hayo yote ni kwa sababu ya kuipa kisogo sekta ya elimu.

Hii inatoa viongozi wasiojiamini na wanaokosa maadili."
Hii ni mara ya pili kwa Sitta kuikosoa serikali ambayo yeye ni mmoja wa mawaziri wake.

Moja ya mambo ambayo Sitta amewahi kuipingana na serikali ni malipo ya fidia kwa Kampuni ya kufua umeme ya Dowans Tanzania Ltd.Sitta ambaye ni Mbunge wa Urambo Mashariki (CCM), alitaka serikali isiilipe fidia ya Sh94 bilioni kwa kampuni hiyo akieleza kuwa kufanya hivyo ni sawa na kuhujumu uchumi wa nchi.

Katika hotuba yake juzi, Sitta alisema serikali inawajibika kuhakikisha inawekeza katika sekta ya elimu ili kuwaandaa viongozi wenye nidhamu na maadili."Tunataka viongozi wajiamini wakiwa kazini na waweze kutetea maslahi ya nchi, vinginevyo nchi itaendelea kuzalisha viongozi wajanja wajanja na wahuni tu," alisema.

Waziri Sitta alitaka Shirika la HakiElimu kuendelea kusema ukweli na kufichua mambo yanayodidimiza elimu kwa maslahi ya watu wachache wenye nia mbaya.Alisema kwa bahati nzuri kwa sasa yupo serikalini na kuahidi kuwa balozi wa HakiElimu na kuwatetea pale watakapobezwa na kutishwa na baadhi ya watu wenye nia mbaya wanapoeleza ukweli.

“Napenda kuwaambia kwamba nitakuwa balozi wenu na kuwaunga mkono na nitaendelea kuwa pamoja na nyie hadi tuhakikishe tunaleta maendeleo katika sekta ya elimu mchango wenu ni mkubwa sana,”alisema Sitta.

Serikali ya Awamu ya Tatu ilitishia kuifungia HakiElimu na kuionya kuacha kutumia matangazo yake katika vyombo vya habari, kueneza chuki miongoni mwa watoto na vijana nchini. Matangazo ya HakiElimu ambayo yaliiudhi serikali ni pamoja na lile serikali kueleza kuwa uchumi unapanda wakati hali ya wananchi bado duni. Jingine ni lile lililoonyesha matatizo sugu ya walimu wanaofanyia kazi maeneo ya vijijini.

Tangazo hilo lilimuonyesha mwalimu akitumia siku mbili kufuata mshahara mjini. Akitumia baskeli lakini anapofika benki anakuta mshahara bado haujaingizwa.

Waziri Sitta ambaye alikuwa Spika katika Bunge la Tisa, alisema kila mtu anatambua mchango na umuhimu wa HakiElimu tangu kuanzishwa kwake mwaka 2001, hivyo hakuna haja ya shirika hilo kuogopa kusema ukweli katika harakati za kuboresha elimu nchini.

“Ukweli ni kwamba katika nchi zilizoridhia makubaliano ya Dira ya Elimu ya mwaka 2015 na katika Jumuiya ya Afrika Mashariki tuna nchi tano, lakini Tanzania ni ya mwisho kielimu. Hali hii inatishia uhai wa nchi,” alisema Sitta.Alisema kuwa elimu bora inaweza kumbadili mtu kitabia na kiuchumi na hivyo kumfanya ajiamini.

Hata hivyo, Waziri Sitta alisema tofauti na ukweli huo, sasa umaskini hasa kwa watu wa hali ya chini nchini, unazidi kuongezeka huku baadhi ya viongozi wasiokuwa na maadili wakiendelea kulipeleka taifa kusikokuwa na mwelekeo.

Waziri Sitta alifafanua kuwa mtu hapimwi kwa ufaulu wa mitihani na shahada alizonazo, bali anapimwa kutokana na utendaji wake na maadili mema kazini na kuwa mstari wa mbele katika kulinda maslahi ya taifa.“Kiongozi hapimwi kwa shahada, vyeti wala kiwango cha ufaulu wa mitihani yake, maana Tanzania ina viongozi wengi wenye shahada na vyeti kibao, lakini wanayofanya viongozi hao wenye shahada, wote tunayajua,” alisema.

Awali, akizungumza katika hafla hiyo, Mwenyekiti wa Bodi ya HakiElimu Joaquine De-Mello alisema hadi wanapoadhimisha miaka hiyo kumi tangu kuanzishwa kwa shirika hilo, Hakielimu imepitia changamoto nyingi ikiwamo vitisho wanapojaribu kueleza ukweli.

“Tumepitia milima na mabonde maana siku zote mtu anayeeleza ukweli anaonekana ni mchochezi, lakini baadhi ya watu wametambua mchango wa HakiElimu na baadhi yao hadi sasa hawatambui mchango wetu katika harakati za kuleta maendeleo ya elimu nchini,” alisema De-Mello.

Alizitaja changamoto nyingine inazoikabili HakiElimu kuwa ni upatikanaji wa taarifa katika taasisi zinazosimamiwa na serikali.Alisema baadhi ya watendaji katika taasisi hizo, hawataki kueleza ukweli wakidhani HakiElimu inataka kupotosha jamii.

"Sisi lengo letu siyo kupotosha, tunataka kuielimisha jamii na kuleta mabadiliko katika sekta ya elimu na wanafunzi kupata elimu yenye manufaa na kumwezesha kujiajiri na kuajiriwa," alisema.

De-Mello alitaja kikwazo kingine cha maendeleo ya elimu nchini kuwa ni baadhi ya viongozi kutaka kuchanganya elimu na siasa…"Hii ni hatari katika maendeleo ya elimu ambayo ndiyo mhimili wa kila jambo duniani."

(Chanzo:Gazeti Mwananchi)
 
ana matatizo ya akili huyu, anamaanisha kuwa mzee wa vijisent kasoma udsm???
 
Chenge, amesoma USA(Harvard),Karamagi kasoma Russia,Mkono amesoma UK...Mfumo wetu wa elimu ni mbovu lakini sikubaliani na Sitta kama ndio umesababisha viongozi wetu kusaini mikataba mibovu.Tatizo ni uafrika-tamaa na ubinafsi.
 
Chenge, amesoma USA(Harvard),Karamagi kasoma Russia,Mkono amesoma UK...Mfumo wetu wa elimu ni mbovu lakini sikubaliani na Sitta kama ndio umesababisha viongozi wetu kusaini mikataba mibovu.Tatizo ni uafrika-tamaa na ubinafsi.

Nakubaliana na Sitta,Tatizo letu ni kutofanya maamuzi sahihi,Hapa sizungumzi kuhusu mafisadi kwa uchache wao kama ulivyo wataja na elimu zao na waliko zipata.Hapa nazungumzia watanzania tulio wengi ambao elimu zetu tumepata hapa petu Tanzania kiukweli zinawalakini, kwani tumewaacha mafisadi wachache kuiongoza nchi kwa mabavu bila kuchukua hatua za msingi kama maandamano yakupinga ufisadi na kuwataka wahusika wa achie ngazi.Bali wasomi tunashadadia huo ufisadi je hapa Tz kuna elimu gani? Upuuzi mtupu tena upuuzi mtupu msomi gani hana logic na reasoning.Nchi hii wajinga waliopitia chuo kikuu na hawajui lolote ni wengi.NAIPENDA TANZANIA LAKINI WASOMI WAKO NI WENDAWAZIMU HAWAKUTAKII MEMA KATIKA USO WA DUNIA HII.MALI ASILI KIBAO LAKINI NCHI MATONYA KUWAPI WASOMI MWEEE?!!
 
Sitta kachanganyikiwa
Mkuu, mimi nadhani wewe na wapinzani wa sitta ndio mmechanganyikiwa. Huyu mzee anasema ukweli ambao kila anayehusika lazima amchukie maana wanaanikwa hadharani. Maana yako ni kwamba hata HakiElimu wamechanganyikiwa? Maana anachosema sitta ndicho wasemacho HakiElimu. Labda hujaishi na walimu kijijini unajua ya daladala tu. Wamechanganyikiwa wakisema kuna watoto wa shule wanamaliza darasa la saba hawajui kusoma wala kuandika isipokuwa majina yao kikushotokushoto? Unasemaje walimu wanapoamua kukusanya shilingi mia kutoka kwa kila mwanafunzi kwa visingizio mbalimbali na kugawana ili kujipunguzia makali lakini serikali inaona na haisemi kitu? Unaonaje wewe walimu wanapowekeza zaidi kwenye tuition kuliko kufundisha madarasani kama ilivyokuwa enzi za Mwalimu?

Niambie walimu wanapowatumia wanafunzi kulima mashamba ya walimu ili walimu hao wasife njaa maana mshahara hautabiriki utakuja lini, si useme tu hujui uhalisia kwa kuwa wewe watoto wako unawasomesha kwenye shule za binafsi ambazo mwananchi wa Ng'wagitolyo hana uwezo? Hivi hujasikia kwamba mikataba mingi wanasheria wanapelekwa kwenye ma-Air conditioner na matai yao wakiandaliwa bahasha zilizovimba baada ya makubaliano yao pale wanaposema "wanachambua mkataba" na kuishia kumezwa na bahasha badala ya maslahi ya nchi?

Sitaki kusema mengi utafiti mwenyewe kama kweli unataka kusema ukweli. Wewe ndio sawa na wale wanaosema kila mtanzania ana maisha bora, asemaye kinyume chako unasema amechanganyikiwa. Mficha nanihii hazai. Hatuwezi kusogea mbele kwa heshima kama hatutaki kuyaita mavi tuliyokanyaga kwa jina halisi tukayaita matope ati kwa kuogopa kuitwa tumechanganyikiwa. Itatugharimu sana huko tuendako maana ni jumuiya ya Afrika mashariki sasa na wenzetu watutawala tutabaki watumishi wa maofisini na majumbani mwao tu. Inakuwaje, umeshajua kwamba Karamagi amefanya biashara zaidi kuanzia urusi "akisoma" kuliko kusoma shule, na imekaa kwenye damu kiasi kwamba hata anapopewa wadhifa aniona shilingi zidi kuelekea kwake kuliko maendeleo anayotazamiwa kuliletea taifa? Kina chenge na mkono waone hivyo hivyo kama hutaki kujua maisha yao ya shuleni huko walikokuwa na ilivyowaathiri leo. Bora Mkono anagawa kwa wananchi wa kawaida mapato apatayo kama shukran kwa waliomwezesha kuwa hapo alipo, vijisenti je? Kuua na kujisifu kwamba ni bingwa Afrika ndio maendeleo ya Taifa? Leo angekuwapo Mwalimu angechanganyikiwa zaidi kuona waliotumia resources za nchi wanafanya wanachofanya mchana kweupe.

SITTA HAJACHANGANYIKIWA!!!
 
Back
Top Bottom