Sitta aelezea siri ya ubabe wake bungeni..

Pdidy

JF-Expert Member
Nov 22, 2007
50,956
22,148
SPIKA wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, Samuel Sitta, ametoa siri ya ujasiri alionao katika kukabiliana na vita dhidi ya ufisadi awapo kwenye kiti chake bungeni.
Sitta, alitoa kauli hiyo hivi karibuni mjini Tabora wakati wa hafla ya kutimiza miaka 20 tangu kuanzishwa kwa Kanisa Kuu la Anglikana la Mtakatifu Stephano, na harambee ya uanzishwaji wa sekondari itakayokuwa chini ya kanisa hilo.
Spika huyo aliongozana na mkewe, Margaret, aliyemwakilisha Waziri Mkuu, Mizengo Pinda. Katika harambee hiyo alisema mara nyingi anapigiwa simu na watu mbalimbali hususan wakazi wa Jimbo lake la Urambo Mashariki, wakieleza kushangazwa na ujasiri wake katika vita dhidi ya ufisadi, bila kujua anakoupata ujasiri huo.
“Leo nataka niwape siri ya ujasiri wangu, nawaambia vijana msisome Biblia kama hadithi. Nakumbuka baba yangu miaka ya nyuma, aliniambia ni vema nikawa na mistari ya Biblia ninayoiamini…niitumie kila siku katika maisha yangu, hasa ninapokuwa kwenye wakati mgumu.
“Tangu wakati huo hadi sasa kuna mistari ya Biblia ninayoitumia kila siku kabla ya kuingia katika kuongoza vikao vya Bunge na ndiyo inayonipa ujasiri huu nilionao.
“Mistari hiyo inatoka katika Agano la Kale, Ayoub sura ya 19, mstari wa 25; bila shaka wote mnafahamu jinsi Ayoub alivyoteseka na hakuna binadamu anayeweza kumfikia mateso yake.
“Ayoub 19 mstari wa 25 unasema: ‘Najua ya kuwa mtetezi wangu yu hai na najua ya kuwa atasimama juu yangu.’ Mistari hii ndiyo inayonipa ujasiri wa kukabiliana na mambo yote hayo mnayoyasikia,” alisema Sitta na kushangiliwa na waumini waliofurika kuhudhuria hafla hiyo.
Alisema, kuwa bungeni ni mzigo mzito kutokana na matatizo yanayowakabili wananchi ambao mara nyingi husubiri maamuzi ya wabunge, hivyo anapopata nafasi ya kuingia kanisani ili kumuomba Mungu, kwake ni faraja na baraka.
“Kule bungeni jamani ni mizigo mitupu, mara mfikirie mafisadi yasiyokamatwa, mara mhangaike na matatizo ya kina mama na watoto, hivyo unapopata nafasi ya kuingia kwenye Kanisa kama hili la Mtakatifu Stephano ni baraka tupu,” alisema Sitta.
Hata hivyo, Spika huyo alisema kuwa wakati mwingine inakatisha taama unapokimbilia kanisani kama sehemu ya kutuliza matatizo, unakutana na mambo ya ajabu yanayofanywa na baadhi ya viongozi wa dini.
Naye Askofu Mkuu wa Kanisa la Anglikana nchini, Askofu Valentino Mokiwa, alitahadharisha kuwa kama uchaguzi mkuu unaokuja unakuwa na dalili za kumwaga damu kama ilivyotokea katika uchaguzi mdogo wa Biharamulo, Busanda na Tarime, ni bora uchaguzi huo usifanyike.
Alisema, viongozi wasipokuwa makini na mwenendo wa sasa wa siasa nchini, damu inaweza kumwagika kutokana na uroho wa madaraka wa viongozi wachache.
“Tumeshuhudia Biharamulo, kiongozi wa chama kimoja amekatwa katwa kwa mapanga, unajiuliza hivi tatizo ni nini? Inawezakana vipi harakati za kumpata kiongozi lazima damu imwagike? Watanzania tusikubali hali hiyo na nasema viongozi wataka madaraka kwa kumwaga damu, kamwe wasichaguliwe,” alisema.
Askofu huyo alieleza kukerwa kwake na matumizi ya rushwa, wizi wa kura kwenye uchaguzi, na kuwataka wabunge kuendelea kuwa na ujasiri wa kukabiliana na vita dhidi ya ufisadi nchini.
Pia alitahadharisha wawekezaji wanaoingia nchini kuchuma mali zetu, lakini licha ya kutuacha tungali maskini, husababisha maafa yanayotokana na sumu wanazozalisha kwenye maeneo wanayowekeza.
“Angalia hali ya kule North Mara, watu wameathirika na athari zile kwao ni za milele, lazima tufike mahala tuwe na umakini na wawekezaji wa aina hiyo,” alisema.
Kwa upande wake, Margaret Sitta, ambaye alikuwa mgeni rasmi akimwakilisha waziri Mkuu, Mizengo Pinda, alisema kuwa serikali iko tayari kushirikiana na taasisi za kidini katika kutoa huduma za kijamii kwa Watanzania.

juu
 
YEP kila jema ni la Mungu mwenyezi. Bila shaka hivyo ndivyo Mungu alivyo Mkuu. Ila mabaya yose ni ya yule mpumbaf shetani lucifer
 
Back
Top Bottom