Mama Amon
JF-Expert Member
- Mar 30, 2018
- 2,021
- 2,478
Yesu wa Nazareth
WANAZUONI wengi duniani, bado wanaumiza vichwa kuhusu tarehe sahihi aliyozaliwa Yesu Kristo, ambaye ni Nabii wa Wakristo.
Miaka nenda rudi, vitabu vingi vimeandikwa na makundi ya wanazuoni wa dini na historia kuanzia Mashariki ya Kati, Amerika, Ulaya, Afrika na bado hadi leo, maandishi mapya yanaendelea kuchapishwa juu ya kuzaliwa kwa Yetu Mnazareti.
Mjadala huo upo na hakika hautakoma kwani wanaoandika wanapingana kwa hesabu na historia. Wameshindwa kupata tarehe hasa aliyozaliwa Yesu ambaye pia huitwa Masihi.
Miaka 2000 iliyopita, mtawala wa tano wa Wayahudi, Pontio Pilato alimuuliza Yesu wa Nazareti swali lifuatalo: “Ukweli ni kitu gani?”
Aliuizwa swali hili wakati anakaribia kupewa hukumu ya kuwambwa msalabani baada ya kukamatwa akituhumiwa kujiita “Mfalme wa Wayahudi.”
Yesu hakujibu swali hili. Na hadi leo, kambi kadhaa za wanazuoni zinazidi kuvutana kuhusu jawabu sahihi kwa swali hili. Mfano mzuri wa mvutano huo unajitokeza katika mjadala kuhusu “siku ya kuzaliwa kwa Yesu wa Nazareti.”
Mpaka leo, kuna siku tatu tofauti zinazotajwa kama siku za kuzaliwa kwa Yesu. Kuna Desemba 25, Januari 6 na Januari 7. Ufafanuzi wa utata huu unafuata.
Tuanze na Desemba 25. Haya ni mawazo ya Mtakatifu Hippolytus wa Roma. Kwa mujibu wa utafiti wa Profesa Andrew McGowan wa Chuo Kiukuu cha Melbourne, mwaka 204BK, Hippolytus aliandika kwamba, “Tarehe ya kuzaliwa Yesu, Bethlehem, ni Desemba 25.”
Hippolytus alianzia kwenye tukio la Malaika Gabriel kumtokea Zakaria hekaluni na kumwambia kwamba mkewe Elizabeth angepata mimba na kumzaa Yohane.
Zakaria alikuwa kwenye ibada ya malipizi ya dhambi. Kwa mujibu wa kalenda ya Kiebrania ibada hiyo ilifanyika tarehe Julai 10 kila mwaka wa Kiyahudi.
Ulinganisho wa kalenda ya kale ya Wayahudi na kalenda ya kisasa unaonyesha kuwa siku hiyo ni sawa na Septemba 24 ya siku hizi. Hii maana yake ni kwamba Elizabeth alianza ujauzito wa Yohane Septemba 24.
Kwa mujibu wa uchambuzi wa Hippolytus, miezi sita baadaye malaika Gabriel alimtokea Bikira Maria na kumwambia atapata mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu. Hivyo, ujauzito wa Yohane ulioanza Septemba 24 uliutangulia ujauzito wa Yesu kwa miezi sita.
Hii maana yake ni kwamba, mimba ya Yesu ilianza Machi 25 na akazaliwa miezi tisa baadaye, yaani Desemba 25, anahitimisha Hippolytus.
Lakini, bado wapo Wakristo waliopinga tafsiri ya Hippolytus. Walihoji uhalali wa hesabu zake, wakitaka awaonyeshe hiyo miezi tisa ilikuwa na jumla ya siku ngapi.
Hawa wenye kupinga Krismas ya Desemba 25, huadhimisha Krismas ya Januari 7. Ni wafuasi wa Mfamle Julius Kaizari wa dola ya Kirumi. Sababu za upinzani wao zinafuata.
Katika mwaka 46KK Julius Kaizari aliunda kalenda iliyotokana na imani kwamba mzunguko wa dunia unachukua siku siku 365 tu. Lakini, baadaye wanasayansi waligundua kuwa mzunguko wa dunia huchukua siku 365 na robo.
Robo nne zinaunda mwaka mmoja. Hii maana yake ni kwamba, kila baada ya miaka mitatu, yaani katika mwaka wa nne, mzunguko wa dunia huchukua siku 366.
Miaka mitatu huitwa miaka mifupi, na mwaka wa nne kuitwa mwaka mrefu. Mwaka mrefu hugawanyika kwa namba “nne.”
Kwa mujibu wa “Kalenda ya Julius” mwaka wenye siku 365 una miezi 12; ambapo miezi minne ina siku 30, kila mmoja; miezi saba ina siku 31, kila mmoja; na mwezi Februari una siku 28.
Hesabu hizi hazihusishi siku 365 pekee kati ya siku 365 na “robo” za mzunguko wa dunia. Hivyo, kila baada ya miaka minne, “Kalenda ya Julius” ikawa inapoteza siku moja kamili.
Kwa ajili ya kuondoa dosari hii, katika kila mwaka mrefu, Julius aliamua kuongeza siku moja kwenye mwezi wa Februari, ili uwe na siku 29, na hivyo kukamilisha siku 366 za mwaka mrefu.
Kalenda hii ina miezi minne ya siku 30, miezi saba ya siku 31, mwezi Februari wa siku 28 katika mwaka mfupi, na mwezi Februari wenye siku 29 katika mwaka mrefu. Huitwa “Kalenda ya Julius”.
Baadaye wanasayansi waligundua tena kuwa mzunguko wa dunia hauchukui siku “365.25” pekee, bali huchukua siku “365.24218967.” Hapa kuna tofauti ya siku “0.00781033,” sawa na dakika “11.2468752.” Yaani, kimakosa, “Kalenda ya Julius” ilikuwa imeongeza dakika “11.2468752” katika mwaka mzima.
Kanisa Katoliki lilianza kutumia kalenda ya Liturijia inayofuata mantiki ya “Kalenda ya Julius” mwaka 325. Lakini, mwaka 1582 Papa Gregory wa 13 aligundua makosa hayo yaliyo kwenye “Kalenda ya Julius.”
Hivyo, Papa akakosoa dosari husika kwa kuunda kalenda mpya, ikaitwa “Kalenda ya Gregory”. Baadhi ya Wakristo waliikataa mantiki iliyoongoza utengenezwaji wa “Kalenda ya Gregory” na kuendelea kutumia “Kalenda ya Julius.”
Hivyo, tangu mwaka 325 hadi leo imepita miaka 1697. Kwa kuzingatia tofauti ya siku “0.00781033” tulizoona hapo awali, hesabu ya kuzidisha inaonyesha kwamba “Kalenda ya Gregory” inaitangulia “Kalenda ya Julius” kwa siku “13.25413001.” Huu ni wastani wa siku 13 na robo.
Hivyo, wakati Wakristo wanaofuata “Kalenda ya Gregory” wanaposherehekea Krismas ya Desemba 25, wale wanaofuata “Kalenda ya Julius” watasubiri hadi Januari 7, yaani siku 13 baadaye.
Lakini pia, kuna Wakristo wanapinga Krismas ya Desemba 25 na kukataa Krismas ya Januari 7, wao wanaadhimisha Krismas ya Januari 6.
Kitabu cha “New Advent Encyclopedia,” kinasema hawa wanaoamini Yesu alizaliwa Januari 6 ni wafuasi wa Clement wa Alexandria, nchini Misri.
Clement alionyesha kwenye kitabu chake kiitwacho “Stromata,” kwamba Yesu alizaliwa “Januari 6.” Baadhi ya Wakristo walikubaliana na Clement hadi leo.
Kutokana na mkanganyiko huo wa siku aliyozaliwa Yesu Mnazareti, ndiyo maana yapo maeneo duniani yanaadhimisha kuzaliwa kwake Desemba 25, wengine Januari 6 na wapo wanaofanya kumbukizi Januari 7.
Mchungaji wa Kanisa la Mfalme Yesu lililoko Mwanjelwa, Mbeya, Ibarhim Kalembo akizungumza na Pambazuko kuhusu tarehe hasa ya kuzaliwa Yesu Kristo, alisema ni kweli kuna tofauti kulingana na maeneo husika, lakini uhakika kabisa hauelezwi kinagaubaga na Biblia yenyewe.
Amesema katika vitabu vingi vya vya Injili, ambavyo vikisomwa kwa pamoja, kuna utata wa siku ya kuzaliwa Yesu Kristo, kwani haitamkwi wala kuelezwa kwa uwazi.
“Hata wewe ni Mkristo, umewahi kusoma ama kuelezwa mahali kwamba Desemba 25 ndiyo hasa alizaliwa Mwana wa Mungu (Yesu), hakuna, lakini watu waliamua iwe hiyo Desemba 25 kwa wengi, pamoja na kwamba wapo wanaopinga tarehe hiyo,” ameongeza mchungaji huyo ambaye amesema ana shahada ya uzamili katika teolojia.
Anaeleza kuwa mvutano wa siku ya kuzaliwa Yesu huenda usifike mwisho na labda unaweza kutatuliwa na Yeye mwenyewe siku atakaporejea na endapo atatoa nafasi ya kuulizwa maswali.
“Hili swali limetushinda, limewashinda hata wakongwe wa historia ya maisha ya Yesu, wakiwamo Wayahudi wenyewe, huenda siku nzuri ya kupata jibu na tutakapomuona Mwenyewe,” ameongeza.
Chanzo: Gazeti laPambazuko, Toleo la Jumatatu, Desemba 26, 2022-Januari 1, 2023, ukurasa wa 10-12.