Sheikh yahya ametumwa na nani?

Malisa Godlisten

JF-Expert Member
Jan 20, 2010
201
1,534

SHEIKH YAHYA AMETUMWA NA NANI?
KAMA kuna watu walioibua mijadala mizito kutokana na kutoa “hoja mufilisi” katika kipindi cha mwaka jana miongoni mwao ni Sheikh Yahya Hussein aliyetabiri ”Kifo cha ghafla” cha mtu atakayepingana na Jakaya Kikwete kwenye kinyanganyiro cha Urais ndani ya Chama cha Mapinduzi.

Mwingine aliyefunga mwaka kwa mawazo mgando ni Mwenyekiti wa TLP Augustine Mrema aliyedai kuwa wote waliokaa katika Kongamano lililoandaliwa na Taasisi ya Mwl. Nyerere kujadili na kukosoa Serikali ya Kikwete ni wachochezi na yawezekana wakahesabiwa kama wahaini. Anadai yeye “enzi za uhai wake” aliwahi kufichua maovu mengi kwenye Serikali ya Mkapa lakini hakuwahi kutaja majina ya wahusika; maana eti angefanya hivyo angekuwa mchochezi.

Mrema alizungumza mengi akimuunga mkono Katibu Mkuu wa CCM (Mropokaji) Yusuph Makamba kuwa wote waliokaa katika Taasisi ya Mwl. Nyerere kuanzia Mwenyekiti wake Joseph Butiku hadi Maprofesa kama Baregu Mwesiga kuwa wote ni wehu. Lakini lengo langu si kujadili “Fikra kurupushi” za Mrema maana kwa hakika Mrema wa leo si yule wa miaka ya 90, alipokuwa akitetemesha taifa kwa nguvu ya hoja.

Mrema wa sasa amepoteza mvuto, amechuja, amepauka kisiasa, amechoka mwili na roho. Ni ombaomba anayetamani kujishibisha kwa makombo yadondokayo kwenye meza za watawala ndio maana anawanyenyekea. Hivyo kwa leo tujadili “mambo ya maana kidogo” japo hili la Mrema nalo linahitaji mjadala.

Leo nataka kujadili kauli ya yule mtaalamu wa nyota na anga za mbali Mnajimu Sheikh Yahaya Hussein kuwa atakayeshindana na Rais Kikwete kutafuta ridhaa ya CCM ili kugombea urais 2010 “atakufa ghafla” inastahili kujadiliwa kwa kina na katika mjadala utakaotoa nafasi kwa watu wa rika tofauti na Imani mbalimbali kutoa maoni yao.

Najua wapo wengi waliokwishatoa maoni yao; kutokana na kauli hii kuibua mjadala mpana; nani naomba kutumia fursa hii kueleza yangu machache. Sheikh Yahya anasema mpinzani wa Kikwete (ndani ya CCM) atakufa ghafla. Kufa ghafla kunaweza kutafsiriwa kama kufa bila taarifa, bila kuugua au kufa bila kujiandaa (kama kifo kina maandalizi).

Kwa kuwa Sheikh Yahya hakueleza kuhusu wakati hasa mtu huyo mwenye kutaka urais kwa tiketi ya CCM “atakapokufa ghafla” basi ni dhahiri kuwa vifo vya ghafla vingeweza kuanza mara tu baada ya tangazo lake.

Kwa maana hiyo Tangazo hilo la Sheikh Yahya laweza kutafsiriwa kuwa ni “Parapanda”
Hivyo tutegemee “vifo vingi vya ghafla” mara baada ya Parapanda hiyo iliyolia tarehe 23/Desemba/2009 pale Magomeni – Mwembechai nyumbani kwa Sheikh Yahya Mwenyewe. Kwa hiyo tukishuhudia mtu yeyote ndani ya CCM “amekufa ghafla” tangu wakati “Parapanda” ilipolia basi tujue huyo alikuwa na mpango wa kumpinga Kikwete 2010.

Ikiwa hivyo ndivyo alivyomaanisha Shekh Yahya basi kifo cha Waziri Mkuu Mstaafu Rashid Mfaume Kawawa “Simba wa Vita” kina utata maana nacho kilikuwa cha “ghafla”

Akiongea na vyombo vya habari kuhusu kifo cha Kawawa tarehe 31/12/2009 saa 5:00 asubuhi pale Ikulu Dar –es – Salaam, Rais Kikwete alisema Mzee Kawawa hakuwa mgonjwa sana



kwani alienda Muhimbili mwenyewe kupima malaria baada ya kutojisikia vizuri hali yake jioni ya tarehe 30.

Taarifa zinasema alipopima hakuwa na malaria na alipokuwa akitoka akahisi kuishiwa nguvu (hivi ina maana kuwa nguvu iliyokuwa inaishia ni ile aliyokuja nayo – kwa hiyo alikuja na nguvu).

Hatimaye akarudishwa wodini na baada ya vipimo akakutwa na matatizo kwenye Figo na Moyo na hali iliendelea kuwa mbaya hadi umauti ulipomfika asubuhi ya tarehe 31. (Mungu amlaze mahali pema peponi).

Lakini matukio haya yote tangu mzee Kawawa amefika Muhimbili hadi umauti unamkuta yametokea ndani ya Saa 24, yaani Jumatano ya tarehe 30 hadi asubuhi ya tarehe 31/12/2009. Kwa maana hiyo kifo cha Kawawa kilikuwa cha ghafla. Na ikumbukwe wakati kifo cha Kawawa kinatokea, tayari Mnajimu Yahya alishapuliza “Parapanda” yake.

Je Mzee Kawawa nae alikuwa na mpango wa kuchuana na Jakaya Kikwete kuomba ridhaa ya CCM kwenye uchaguzi Mkuu 2010?
Swali hili anapaswa aulizwe Sheikh Yahya labda anaweza kujibu kwa uyakinifu.

Sheikh Yahya Hussein ni Mnajimu na mganga wa siku nyingi. Amekuwa akitabiri mambo kadha wa kadha lakini akijiegemeza zaidi katika Siasa, hali inayoibua maswali kwa wenye kufikiri. Kwanini amekuwa akivuma sana kipindi cha uchaguzi Mkuu unapokaribia?

Je unajimu upo katika Siasa tu? Mbona hatusikii akitabiri mambo ya kijamii, Kiuchumi na masuala mengine ya utamaduni? Kwanini utabiri wa nyota uwe katika siasa tu? Yawezekana Sheikh Yahya alikuwa “nia njema” ya kutaka kumwokoa mpinzani wa Kikwete na janga la Kifo cha ghafla.

Lakini kama nia yake ni kuokoa, kwanini hakuwatabiria wale watu wa Mamba-Miamba kule Same Mashariki kuwa wahame maeneo yao kabla hawajafunikwa na maporomoko ya udongo yaliyotokana na mvua za El – Nino? Kwa kufanya hivyo angewaokoa ndugu zetu Wapare na “Vifo vya ghafla” vilivyowakuta.

Au kama kweli ana nia njema kwanini hakutabiri mafuriko ya Kilosa na kupiga “parapanda” ili watu wahame kabla maafa hayajawafika. Au nia njema anayo kwa wana- CCM tu? Ndio maana anataka kuwaokoa na “vifo vya ghafla” lakini hana muda wa kuwatabiria Wananchi hasa katika majanga makubwa kama El – nino, maana vifo “vya ghafla” vya Wananchi haviumi kama vifo vya ghafla vya Wana –CCM.

Lakini wengine wanahoji kama kweli utabiri wa Sheikh Yahya ni wa “ukweli na uhakika”, kwanini hakumtabiria rafiki yake kipenzi Sheikh Suleiman Gorogosi kuwa asisafiri siku ile alipopata ajali hatua chache kutoka uwanja wa ndege wa Lindi muda mfupi baada ya kuwasili kutoka Dar –es – Salaam. Kwa kuwa walikuwa marafiki walioshibana si ajabu kuwa Sheikh Gorogosi alimuaga rafikiye Yahya kuwa anakwenda Lindi.
Lakini Yahya hakutaka kusoma nyota zinasemaji; kama zimelala, zimeamka, au zinapiga mswaki, ili kumtahadharisha Gorogosi na Safari yake. Yamkini angefanya hivyo mauti yasingemfika Gorogosi maana angeahirisha safari.
Lakini Sheikh Yahya ni mshabiki wa Siasa wa muda mrefu na si ajabu kuwa ni mwanachama wa CCM. Je hii ndio kazi ya wanaCCM?

Lakini CCM inadaiwa ni Chama cha Mapinduzi. Na kazi ya Wanamapinduzi ni “Kupindua”. Ndio maana Sheikh Yahya anaanza kupindua uhuru wa kuchagua; kupindua haki ya mtu ya kumchagua amtakaye. Kwa kifupi kupindua mfumo wa Demokrasia nchini. Huyo ndiye Sheikh Yahya Hussein. Mnajimu, mtaalamu wa elimu ya nyota na Mwanamapinduzi aliyetumia Sayansi yake ya anga kupindua akili za Watanzania.

Watu wengi walijitokeza kumpinga na kumkosoa Sheikh Yahya waziwazi. Miongoni mwao ni Askofu Mkuu wa Kanisa la Full Gospel Bible Fellowship Mch. Zacharia Kakobe aliyesema kuwa rais wa nchi hii hapatikani kwa ushirikina.

Tukichagua rais Mshirikina, kwa hofu ya ushirikina basi tutegemee maendeleo nayo yaje kishirikina. Tusimlaumu mtu barabara zitakapokuwa hazijengwi maana rais alichaguliwa kwa elimu ya Nyota, hivyo mwongozo wake utategemea nyota, na sisi wananchi tutaona nyotanyota, maana maendeleo yetu yatategemea nyota ziseme.

Wapo wachache waliojitokeza kumpinga Askofu Kakobe na kudai kwamba Sheikh Yahya alitoa maoni yake kwa mujibu wa katiba na hivyo maoni yake yanapaswa yaheshimiwe. Watu hao (wenye kuamini katika nyota) Kama wanatambua Sheikh Yahya ametoa maoni na wanataka yaheshimiwe mbona wao hawataki kuheshimu maoni ya Askofu Kakobe?

Wamesahau kuwa hata Kakobe alikuwa anatoa maoni yake kwa mujibu wa Katiba na maoni yake nayo yanapaswa yaheshimiwe. Lakini walio wavivu wa kufikiri wakafika mbali zaidi kutaka kuibua hoja ya udini, eti Kakobe alimpinga Yahya kwa kuwa yeye ni Askofu wa Kikristo na Yahya ni Ustadhi wa Kiislamu.

Labda niwasaidie hao wenye ufinyu wa mawazo kuwa kinachopingwa ni HOJA na si MTOA HOJA. Lazima tujifunze kusikiliza hoja kwa makini na kuzijibu kwa kuzikubali au kuzikataa bila kujali uhusiano wetu na mtoa hoja. Sheikh Yahya Hussein mnajimu anayeheshimiwa Afrika Mashariki na Kati anataka kutumia fursa hiyo kudumaza demokrasia nchini. Unajimu wa aina hii haufai.

Lakini Sheikh Yahya ni mtabiri wa siku nyingi na maarufu, si hapa nchini tu bali katika ukanda wote wa Afrika Mashariki na kati. Na katika kazi yake si ajabu wanasiasa wengi wemewahi kuwa wateja wake.

Kwa kuwa ni mnajimu nguli na wa siku nyingi vilevile unajimu wake umekuwa ukizingatiwa na wengi. Labda kwa kulitambua hilo wapo watu wameanza kumtumia Kisiasa, kuupotosha na kuutisha umma, kwa maslahi yao binafsi.

Je sheikh Yahya ametumwa na nani? TAFAKARI.
Tafadhali naomba maoni yako mara umalizapo kusoma.
Tutafutane:
god.malisa@gmail.com
0712-025958

 
Kawawa hakufa ghafla kwani watanzania wote tulikuwa tunafahamu ni mgonjwa kwa miaka mingi tuu,au wewe mwenzetu hukai Tanzania?
 
hii hoja ya huyo bwana mkubwa (Yahaya) ina mambo mengi ambayo yamejificha,,
kabla sijaanza kuchambua nijuavyo mimi ningeomba tuanzie na respond ya kutoka ikulu (Salva), kwamba hayo ni mawazo yake kwa hiyo yaheshimiwe,
sasa hapa kuna tatizo kubwa sana Tanzania, mtu anapokuwa na cheo na anapotoa comments, suggestion au hoja yoyote huwa hawana hulka ya kutuweka wazi kwamba hizo kauli ni zao kama watu personal au ni kauli za taasisi walizopo mfano (Kikwete na Ikulu, Zitto na Chadema, Salva na Ikulu, Makamba na CCM, Simba na Wizara yake ya UWT nk),

sasa nikirudi kwenye hiyo hoja panakuwa pana utata kidogo na hizo hoja za Salva kwamba aliyoyaongea ni misimamo ya ikulu au ni yake yeye kama Salva, whatever the case swali ni kwa nini Salva ndio awe wa kwanza Kucomment positively hizo kauli za Sheikh Yahaya?

Swali lingine ni kuwa kila mgombea atakayepingana na JK hata kama hana umaarufu (Yaani sio tishio say G. Malisa) naye atakufa?

Swali lingine huyo mpinzani wa JK atakyekufa ghafla ni lazima awe wa CCM au hata wa Upinzani?

kwa majibu mepesi na kwa nimjuavyo huyo mzee (Yahaya), kwa miaka Mingi sana Tangu Nyerere ni kuwa yupo kwenye system, kama inavyojulikana hao watu wa UWT wako wa kila fani na yeye anawakilisha hiyo sehemu yake,

ukweli ulishaonekana kwamba JK yupo kwenye wakati mgumu sana kurudi madarakani kwa njia ambazo wanazitumiaga, upinzani wake ulikuwa ni mkubwa sana, na kama mapenzi yake angependa amalizie hicho kipindi chake cha pili, lakini kutokana na huo ugmu katika kila eneo njia moja ambayo ndio silaha kuu aliyonayo ni kwenda kwa Bwana Otham pale UWT kupanga mikakati,.Kwa Sheikh Yahaya kutamka hayo maneno hata kama EL au RA walikuwa na nia ya kushindana na JK kupitia CCM (NEC) Hawawezi tena kupitia hiyo njia kwani msg imeshawafikia na wanaifahamu hiyo msg kuliko raia yoyote wa kawaida ambaye hayo mambo yakitokea tutakuwa ni watu wa kwanza kumsifia Sheikh Yahaya kwa utabiri unaokuwa kweli

kwa kifupi hiyo ni msg ya kweli kutoka jengo jeupe kwa wapinzani wa kweli (EL at el) wa JK

na hapo ndio kuna tatizo kubwa sana kwenye hii taasisi yetu ya UWT, bado inafatilia nani kasema nini na nani anampinga nani, bado ipo kwenye misingi ile ya ujamaa na bado haiko huru kutetea maslahi ya TAifa kwa manufaa ya taifa zima, bali ipo hapo kwa maslahi ya mtu mmoja mmoja,

ni kitu cha ajabu kabisa mikataba mibovu kama ya EPA, MADINI, RICHMOND and DOWANS ambayo inagusa kabisa usalama wa taifa, hawa jamaa wa UWT wanashindwa kuizuia vitu sensitive kama hivyo visitokee, hivi ni kweli unatuambia una taasisi makini kama UWT na wahuni wanakwenda reserve bank (BOT), kuchota mabilioni wao hawana action yoyote ya maana,
Lakini mwisho wa siku unakuja kukuta hiyo taasisi (UWT) imemezwa na siasa na inafanya maamuzi ya wanasiasa kwa usalama wa wanasiasa na wala sio TAifa

NA NDIO KISA CHA KUMTUMIA SHEIKH KUTOA MSG ZA KIFO KWA WAPINZANI WA JK, KWA MASLAHI YA WANASIASA NA SIO TAIFA
 
Back
Top Bottom