Shahidi: Batilda alifananishwa na Al Qaeda asipewe kura

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,318
33,125
BurianAR%281%29.jpg

Dk. Batilda Burian


Shahidi wa kwanza wa wadai katika kesi ya kupinga ubunge wa Godbless Lema (Chadema-Arusha Mjini), Mussa Hamis Mkanga, ameieleza mahakama kuwa Dk. Batilda Burian, alifananishwa na Al Qaeda kutokana na uvaaji wake wa kilemba au ushungi kichwani.
Alitoa madai hayo mbele ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya
Sumbawanga, Gabriel Rwakibarila, ambaye anasikiliza kesi iliyofunguliwa na wanachama watatu wa CCM, Happy Kivuyo, Agness Mollel na Mkanga, katika Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, baada ya Jaji aliyekuwa akisikiliza kesi hiyo kujitoa wiki iliyopita.
Shahidi hiyo alikuwa akihojiwa na wakili wa wajibu madai, Method
Kimomogoro, aliyetaka kujua iwapo tafsiri ya kuvaa kilemba au ushungi kichwani inamaanisha mtu anayevaa hivyo ni Al Qaeda.
Awali Mkanga alidai kuwa katika mikutano ya Lema ya kujinadi kugombea ubunge katika uchaguzi mkuu uliopita, alisikika akiwaeleza wapiga kura kuwa, “chungeni sana hawa wavaa vilemba msije mkawachagua Al Qaeda.”
Wakili Kimomogoro alimuuliza shahidi huyo iwapo jina Al Qaeda alilisikia wapi kwa mara ya kwanza, ambapo ajibu kwamba alisikia katika maeneo yote ya misikitini mkoani hapa. Alidai alivyosikia ni kwamba mtu akivaa vilemba au ushungi anatajwa kuwa ni Al Qaeda.
Hata hivyo, alidai hajui maana ya neno hilo ingawa amekuwa akilisikia kwenye maeneo ya misikiti.
Alidai katika mikutano ya kampeni za uchaguzi ya Lema iliyofanyika maeneo ya Sombetini, JR, Kwa Mromboo na Cheka Ung’atwe, alisikika akiwaeleza wapiga kura wachunge sana hao watu waliovaa vilemba vichwani msije mkachagua Al Qaeda.
Wakili Kimomogoro alitaka kujua iwapo anawajua watawa wa Kanisa Katoliki na kama nao wanaitwa Al Qaeda vile vile, na jibu la shahidi likawa endapo watakuwa wanapita kwenye maeneo hayo wataitwa Al Qaeda pia kutokana na uvaaji wao wa vilemba kichwani.
Hata hivyo, Wakili Kimomogoro alimrejesha shahidi kwenye viambatanisho b na c vilivyomo katika hati ya mashtaka yao kwamba havionyeshi maneno ya al Qaeda, suala la malaigwanan kuongozwa na mwanamke na wala suala la Dk. Batilda kuwa ameolewa Zanzibar na kama atachaguliwa atakwenda zake Zanzibar kulea watoto na mumewe na akahoji ameyapata wapi.
Mahojiano kati ya Wakili Kimomogoro na shahidi Mkanga yalikuwa kama ifuatavyo:
Wakili: Viambatanisho vya b na c katika hati ya mashtaka yenu, hakuna maneno Al Qaeda, suala la malaigwanan kuongozwa na mwanamke na suala la Dk. Batilda kuwa ameolewa Zanzibar, wewe umepata wapi?
Shahidi: Rudia swali lako
Wakili: Anarudia
Shahidi: Yapo
Wakili: Anamuonyesha viambatanisho b na c vya hati ya mashtaka
Shahidi: anasoma na kujibu kimsingi alichoeleza kama nilivyosema hapo juu alichoeleza Lema sio cha kweli kinalenga kumchafua na kukashifu jina lake (Batilda).
Wakili: Hayo maneno uliyosoma umeona al Qaeda humu?
Shahidi: Ndiyo maana yeye (Batilda) alisema amedhalilishwa.
Wakili: Sikiliza swali langu, neno al Qaeda limo hapa?
Shahidi: Hapana
Wakili: Pia neno malaigwanan kuongozwa na mwanamke hayapo kwenye haya maneno?
Shahidi: Hayapo
Wakili: Pia Dk. Batilda ameolewa Zanzibar na akichaguliwa atakwenda zake huko, yapo?
Shahidi: Hayapo
Wakili: Hivyo kwa ujumla anayepaswa kulalamika kwamba amedhalilishwa, kukashifiwa ni Dk. Batilda mwenyewe au sivyo?
Shahidi: Hizo habari tulimpelekea sisi za Al Qaeda, kaolewa Zanzibar na suala la malaigwanan kuongozwa na mwanamke.
Aidha, Kimomogoro alitaka kujua kilichomuumiza shahidi huyo hadi kufikia hatua ya kufungua kesi, ambapo alidai kuwa ameifungua kesi hiyo kutokana na udhalilishaji wa kijinsia uliotamkwa na Lema wakati wa kampeni za uchaguzi.
“Kilichonigusa zaidi ni suala la kijinsia kwani katika nchi hii kila mtu ana uhuru wa kuchagua na kuchaguliwa, ambapo Lema alikuwa akiwaeleza wapiga kura wasimchague Dk. Batilda kwani kwa tamaduni za Kimasai na Kichaga mwanamke hawezi kuongoza malaigwanan (wazee wa kimila wa kabila la Kimasai na suala la udini, ” alidai.
Pia alimhoji iwapo waliomba kibali Mahakama Kuu cha kufungua shauri hilo au kutoa tangazo kupitia vyombo vya habari kuwa wanakusudia kufungua kesi dhidi ya Lema.
“Sisi tulimpa kazi hiyo wakili wetu kwani yeye anajua taratibu na
sheria za kimahakama na hatukutoa taarifa kupitia vyombo vya habari,” alisema.
Kimomogoro alitaka kujua iwapo shahidi huyo alirekodi maneno yanayodaiwa kutamkwa na Lema wakati wa kampeni, naye alidai kuwa hakuyarekodi.
Kimomogoro alimhoji shahidi huyo, kama walimjulisha Batilda azma yao ya kufungua kesi au kama aliwatuma kufungua kesi hiyo, naye akasema hawakumjulisha kuwa wanafungua kesi wala hakuwatuma kufungua shauri hilo.
Alimhoji Mkanga kuwa iwapo anafahamu kuwa Chadema iliwasimamisha wagombea watatu wanawake katika nafasi za udiwani kati ya wagombea 19 wa nafasi hiyo, hali hiyo haionyeshi kuwa mgombea Lema hana tabia ya unyanyasaji wa jinsia kama ulivyodai?
Shahidi alidai kuwa hata kama mke wako ni mwanamke unaweza ukamkashifu vile vile.
Kwa upande wake, wakili mwandamizi wa Serikali, Timon Vitalis, anayemwakilisha Mwanasheria Mkuu wa Serikali, alimhoji Mkanga kama ifuatavyo:
Wakili: Mlikutana wapi na lini kujua mnataka kufungua kesi?
Shahidi: Tulikutana nyumbani kwa Dk. Batilda, tulipokwenda kumpa pole baada ya kuanguka katika uchaguzi huo, Novemba 2, 2010.
Wakili: Sasa pale kwa Dk. Batilda mlikuwa wangapi?
Shahidi: Kulikuwa na watu wengi
Wakili: Kama mlikuwa watu wengi uliwezaje kujua hao wenzako wawili tu ndiyo wana wazo kama lako la kutaka kufungua kesi hii?
Shahidi: Baada ya kuzungumza nao, wengine hatukuwashirikisha hivyo suala hili la kesi niliongea na wadai wenzangu tu.
Shahidi Mkanga alitoa ushahidi wake kwa siku mbili mfululuzo baada ya kuongozwa na wakili wake Alute Mughwai na baadaye kufuatiwa na mahojiano kati ya wakili Kimomogoro na baadaye wakili wa serikali mwandamizi, Timon Vitalis.
Kesi hiyo itaendelea tena Jumatatu kwa ushahidi.



CHANZO: NIPASHE
 
Back
Top Bottom