RC anaposhangilia Lema kubwagwa mahakamani inamaanisha nini?

sulphadoxine

JF-Expert Member
Nov 1, 2010
2,257
645
WAKATI fulani wakuu wa mikoa na wilaya walihudhuria mafunzo maalum ya siku kumi mjini Dodoma ambapo Waziri Mkuu, Mizengo Pinda aliwaasa kutokujihusisha na ushabiki wa kivyama hasa kipindi hiki cha mfumo wa vyama vingi. Badala yake, Pinda aliwataka wawe huru bila kuegemea upande wowote wa chama cha siasa huku wakitekeleza tu kwa ufanisi mkubwa sera za chama tawala.


Waziri Mkuu alisema: “Ninawaonya msitumbukie katika siasa na wala msijaribu kabisa. Huko kuna vyama vingi vitumikieni vyote ingawa kwa sehemu kubwa mtatekeleza ilani ya Chama Cha Mapinduzi, hivyo simameni kidete ndugu zangu.”


Katika mafunzo hayo, Pinda aliwasihi wakuu hao wa mikoa na wilaya kutokukaa tu ofisini badala ya kuwafuata wananchi na kutambua na kisha kushughulikia kero zao. Pia aliwataka kutumia fursa za kiuchumi zilizopo mikoani ili zitumike kumsaidia mwananchi kuondokana na umasikini.

Kimsingi, huo ndio ulipaswa kuwa wajibu wa wakuu wa mikoa na wilaya huko waendako; kuwatumikia wananchi bila kujali itikadi zao za kivyama, kidini na kikabila lakini ukweli umekuwa tofauti kama makala hii itakavyojaribu kueleza.

Gazeti moja linalotoka kila siku hapa nchini limeandika hivi majuzi kwamba Mkuu wa Mkoa wa Arusha (RC), Magesa Mulongo, alivunja ukimya akaeleza namna alivyofurahishwa na maamuzi ya Mahakama Kuu ya kumvua ubunge aliyekuwa mbunge wa jimbo la arusha mjini, Godbless Lema.

Gazeti hilo, toleo Na. 2724 la Mei 18, katika ukurasa wa tatu, linaandika: “Mkuu wa Arusha, Magesa Mulongo, ameonesha furaha yake ya kuenguliwa kwa mbunge wa Arusha Mjini, Gobles Lema kulikofanywa na Mahakama Kuu Kanda ya Arusha akidai kuwa kumesaidia kudumisha amani katika mkoa huo.”

Gazeti hilo likazidi kuandika: “Akizungumza mara baada ya kuwaapisha wakuu wapya wa wilaya sita katika hafla fupi iliyohudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali, Mulongo alisema kwa sasa Mji wa Arusha umetulia na alimpongeza Jaji Gabriel Rwakibarila ambaye alitoa hukumu iliyomnyang’anya ubunge Lema.”
Kama ni kweli matamshi hayo yametoka kwenye kinywa cha kiongozi huyo wa serikali kulingana na taarifa hiyo, basi hii ni hatari kabisa kwa nchi iliyoridhia utawala wa demorasia na siasa za vyama vingi kwani kwa kufanya hivyo kiongozi huyo wa serikali atakuwa anawagawa watu anaowatawala kwa mujibu wa itikadi za vyama vyao. Kadhalika haendani kabisa na wosia wa Pinda.
 
Kimantiki, mtawala huyu anajitia kwenye wakati mgumu hasa ikizingatiwa kuwa Lema alichaguliwa na wakazi wa jiji hilo analoliongoza na hivyo alipaswa kuheshimu matakwa ya wananchi.

Mkuu huyo wa mkoa haipongezi mahakama labda kwa vile anadhani imefanya kazi yake vizuri, bali kwa sababu hatua ya kumfungia Lema imeleta utulivu Arusha! Nimekuwa ninajiuliza kwamba ni utulivu gani huo anaousema Mulongo ambao sasa upo na wakati Lema akiwa bado ana ubunge wake haukuwepo? Je, ni ule kwamba mkuu wa mkoa ama wilaya ambaye jimbo lake linaongozwa na upinzani kwa upande wa ubunge anaonekana kama hakukisaidia chama chao CCM na hivyo ana hatihati ya kuendelea na ulaji huo?

Kwa lugha nyingine mkuu huyu wa mkoa anawaambia wana-Arusha kwamba ni watu ajabu kwa sababu walichagua mtu ambaye anahatarisha amani ya jiji lake!

Badala ya kumuona Lema kama kikwazo cha amani na maendeleo ya jiji hilo yeye kama mkuu wa mkoa alipaswa kuangalia umasikini wa wakazi wa Arusha na matatizo chungu nzima yanayowakabili ikiwa ni pamoja na ukali wa maisha unaowafanya wakazi hao kuishi kwa gharama za kitalii wakati wao ni watanzania, ubovu wa barabara na miundombinu ya jiji hilo la kitalii na hizi ndizo sababu za wananchi wa mkoa wake kumpenda Lema kwa sababu waliona ana uwezo wa kuzipunguza pengine.

Sitaki kuwazungumzia wakazi wa Arusha mjini kuhusu mtazamo wao kwa kauli kama hizo ambazo kama ni kweli basi ni kejeli mbaya wala sitaki kumtahadharisha mkuu huyo wa mkoa kuhusu namna anavyohatarisha mahusiano yake na wafuasi wa Lema ambao ni wengi bali najiuliza tu ikiwa mbunge huyo wa zamani atarejea madarakani siku moja, mahusiano yake na mkuu huyo wa serikali katika mkoa wake yatakuwaje hasa kwa kuzingatia kuwa Lema amekata rufaa?

Labda mtu anaweza kujiuliza kwani Lema ana mahusiano gani na jamii ya watu wa Arusha mjini hata kauli kama hiyo izue mshangao wangu? Ni wazi kwamba ukishabikia kuanguka kwa Lema unashangilia kuanguka kwa chama chake pia, Chadema.

Shutuma za namna hii kwa mwakilishi wa rais kama Mulongo zingepaswa zielekezwe kwa wale wanaopitisha pembe za ndovu kwenda nje ya nchi, wanaosafirisha wanyama nje bila kufuata utaratibu, wanaoingia mikataba mibovu na kuitia hasara serikali, na wale wote waliohusika na uchakachuaji wa kura za kumpata meya wa jiji hilo na kusababisha hata watu kumwaga damu!

Kuna na mambo mengi tu ya kushughulikiwa na RC Mulongo ikiwa ni pamoja na kutatua matatizo ya migogoro na ugomvi wa ardhi kati ya wananchi na wawekezaji, maslahi duni kwa wafanyakazi wa mashamba ya maua na viwandani, mauaji na wizi wa kutumia silaha ikizingatiwa kuwa jiji la Arusha ndilo lango la utalii kwa wageni wengi wanaokuja kutalii Tanzania na inaitwa pia Geneva ya Afrika. Hivyo utulivu, amani na usalama kwa wakazi wa Arusha ni muhimu sana na hayo niliyotaja hapo yanapochafuka bila kushughulikiwa vizuri na yeye Mulongo akisaidiana na viongozi wengine akiwemo mbunge ndio yanaweza kuharibu amani kuliko anavyofikiri.


Kama ni kweli mkuu huyo wa mkoa alisikika akisema hayo kwa mujibu wa gazeti hilo basi hili linashahadilia mawazo ya watu wengi ambao siku zote wamekuwa wakiwalalamikia wakuu hawa wa mikoa na wilaya wanaoteuliwa na Rais kuwa hawashughulikii matatizo ya wananchi zaidi ya kulinda maslahi ya aliyewateua na yale ya chama tawala. Kama ushabiki wa Lema kuanguka ungelisemwa na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, wengi tusingeshangaa sana lakini hapa unasemwa na kiongozi tunayeaminishwa kwamba ni wa serikali na hayo aliyasema akiwaapisha watuhumiwa wenziye katika mtazamo huu, wakuu wapya wa wilaya! Kwa lugha nyingine alikuwa akiwalisha makada wenzake msimamo kuhusu upinzani!

Sasa hata mimi nalazimika kuamini kwamba hawa jamaa waliosababisha nchi igawike vipande vingi vidogo vidogo vya mikoa na wilaya kwa kisingizio cha kuwaletea wananchi huduma karibu, ni geresha tu, sio kweli bali ukweli ni kulipana fadhili kwa makada wa chama wapiganaji wa kambi za chama tawala na wastaafu wa majeshi yetu ndio maana wanalinda maslahi ya chama zaidi kuliko yale ya umma.

Ikumbukwe kwamba, hivi karibuni mkuu wa mkoa wa Dodoma, Dk. Rehema Nchimbi, naye alikurupuka akipiga marufuku mikutano na maandamano kufanyika katika mkoa huo wakati wa vikao vya bunge na hakuna ubishi kuwa alikuwa akivilenga vyama vya upinzani kwa kisingizio cha tamko la Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa.

Kuna ukweli kwamba jamaa hawa pia huwekwa kiti moto kwenye vikao vya juu vya chama tawala vya mikoa, kama vile kamati ya siasa ambako kwa wadhifa wa wakuu wa mikoa huingia kama wajumbe, halimashauri ya CCM ya mkoa na mkutano mkuu wa mkoa wa chama ambako huwa chini ya wenyeviti wa chama wa mikoa, na huko inasemekana huwa wanahojiwa kuhusu wanavyokisaidia chama kushamiri na kama utendaji ni mbovu hutolewa hata nje ya kikao na kujadiliwa!

Hayo na mengine mengi yanadhihirisha wazi kabisa kuwa vyeo vya jamaa zetu hawa ni vya picha na mtazamo wa kichama zaidi kuliko kama tulivyokuwa tukiaminishwa kuwa ni watendaji wa serikali kwa asilimia mia moja. Ndio maana hatuwezi kushangaa kama ni kweli mkuu wa mkoa kutoa matamshi ya kushabikia mitazamo ya kichama badala ya kutatua matatizo ya wananchi.

Hii pia ni sababu ya msingi kwa umma sasa kuanza kuhoji mantiki na maslahi ya kuwepo kwa vyeo hivi vya kichama visivyo na tija kwa umma wakati kuna makatibu tawala wa mikoa na wilaya na wakurugenzi. Kimsingi hawa jamaa (wakuu wa mikoa na wilaya) wanawabebesha mzigo walipa kodi wa nchi hii bila sababu yoyote. Kweli tunahitaji kuwa na mkuu wa mkoa anayeshangilia upinzani kupoteza jimbo wakati mshahara wake unatokana na wananchi wote wakiwemo hao hao mashabiki wa upinzani

Kitendo hicho kama ni kweli hakina tofauti na refa wa mchezo wa mpira wa miguu ambaye anapaswa kutokuwa na ushabiki kwa upande wowote wa timu zinazocheza, lakini huyu anaamua kushangilia pale timu moja inaposhindwa huku akithubutu kwa uwazi kabisa kumbeba na kumpongeza mfugaji wa goli mbele ya timu pinzani. Huyo refa kweli ataaminiwa tena kwa lolote na wale wa timu pinzani?

Nafikiri moja ya masuala ya msingi kabisa wakati huu wa kipindi hiki cha mchakato wa kupata katiba mpya, wakati tukitembelewa na tume ya kukusanya maoni basi tulitazame hili kwa umakini sana kwani vyeo hivi havina maslahi kwa umma wa watanzania wote na inadhirisha kuwa ni vya kibaguzi.

Mungu ibariki Tanzania.
 
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magesa Mulongo.jpg

Mkuu wa mkoa wa Arusha Magesa Mulongo.
 
kwa hawa wakuu wa mikoa ni wasaidizi wa rais ndio ila wanaposhindwa kudhibiti hisia zao na kujua hisia za wananchi ndio hapo wanapogeuka vituko mfano mmoja ni huyu na anaweza kuongea chochote kwa sababu kwani wananchi wamemchagua ,jibu ni hapana.kwa kuonyesha hisia zako wananchi wanatafsiri ya kuwa umetimiza wajibu wako aidha wa kumfurahisha mkuu wako wako wa kazi au kumuudhi
 
Back
Top Bottom