Pdidy
JF-Expert Member
- Nov 22, 2007
- 50,956
- 22,149
Rais Kikwete anahusika Richmond?
PDIDY
KWA wanafalsafa, nilishasema hakuna neno la bahati mbaya. Kila neno hutolewa kwa kukusudia jambo fulani, huwezi kutamka kitu fulani ukasema kuwa ni bahati mbaya, mfano umetukana mtu, ukiulizwa unasema ni bahati mbaya, mbona hakuna bahati mbaya katika kutukana mawe? Au miti? Kwanini ukaja kwa huyu na ukasema hivi wakati huu?
Katika moja ya mambo yanayoonekana kukosa majibu mwaka huu, ni sakata zima la Kampuni ya Kimareani ya kuzalisha umeme wa dharura ya Richmond. Kampuni hii inaonekana kuwaumiza vichwa watawala wetu kwa kukosa majibu ya msingi.
Watanzania wengi wameumiza vichwa kufikiri sana na kila kukicha wanalalamika, suala la Richmond limekuwa moja ya mambo mazito sana nchini kujadiliwa. Limejadiliwa likaonekana kuwa halina rushwa, hii ni kutokana na ripoti ya Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Edward Hoseah, baadaye iliundwa Kamati ya Bunge kuchunguza sakata hili na kukaonekana kuwa kuna ufisadi mkubwa usiomithilika, tena uliofanywa na viongozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Baada ya kamati kufanya kazi yake, kulitolewa mapendekezo mbalimbali ambayo serikali ilipaswa kuyafanyia kazi, mojawapo ilikuwa ni kuwawajibisha wote waliohusika na kashfa hiyo.
Taarifa nyepesi isiyokidhi hata kuwajibu watoto wadogo, ilitolewa na Katibu Mkuu Kiongozi, Philemon Luhanjo kuwahadaa Watanzania. Akasema kuwa wahusika wamepewa onyo na kuwahakikishia Watanzania kuwa hakukuwa na dalili zozote za rushwa katika sakata hili na Rais Jakaya Kikwete hahusiki na Richmond.
Luhanjo anasema: Katika siku za hivi karibuni kumekuwepo na maneno na vijembe ati kuwa kuna mkono wa Rais Jakaya Kikwete katika kutoa tenda ya kuzalisha umeme wa dharura iliyopata Kampuni ya Richmond. Kiini cha maneno hayo ni kauli za baadhi ya wanasiasa zilizopazwa sauti na baadhi ya vyombo vya habari.
Tunapenda kusema, tena kwa msisitizo kuwa, maneno hayo si ya kweli na hayana msingi wowote. Rais hajahusika na uamuzi wa tenda hiyo kupewa kampuni ya Richmond.
Kauli hiyo ilipokelewa na Watanzania, lakini kama ambavyo nimekwishasema huko nyuma, kauli za viongozi wetu kwa sasa kila zinapotolewa tuzipokee kwa umakini mkubwa kama ambavyo kauli nyingi zinazopingana ambazo amekuwa akizitoa rais mwenyewe wala si kupitia kwa watendaji wake.
Ni kutokana na kashfa ya Richmond, IPTL, taifa letu limekuwa likipata mgawo wa umeme kwa sababu tu Shirika la Ugavi wa Umeme (TANESCO) limekuwa likizilipa kampuni hizo pesa nyingi kiasi cha kushindwa hata siku moja kujitegemea.
Baada ya sakata la Richmond kuhamia bungeni na pia suala la ununuzi mitambo ya Dowans ambayo ni kampuni ambayo iliuziwa tenda ya kuzalisha umeme na Richmond, kumetokea mambo kadhaa yanayotufanya tujiulize kuwa, rais wetu anahusika na Richmond?
Kwanza ilitolewa tahadhari kuwa mitambo ile isingenunuliwa taifa lingeingia gizani, hivyo ili kukwepa giza afadhali mitambo ya kifisadi inunuliwe. Hiyo ilikuwa hoja ya Dk. Idris Rashidi.
Hatujui mtendaji huyu wa serikali aliwasiliana vipi na mkuu wake wa nchi au alimshauri vipi, mpaka akawa na ujasiri wa kupendekeza mitambo hiyo haramu inunuliwe hata kama katika kuinunua tulikuwa tunapingana na sheria ya nchi kuhusu manunuzi ya umma.
Nchi yetu kweli imeingia gizani, chanzo cha tatizo kinafahamika, mkuu wa nchi akatoa amri kuwa sasa mitambo ya IPTL iwashwe.
Sentensi kama hiyo ilionekana kuwa ni nafuu ya Watanzania, kuwa wataepushwa na giza hili. Wizara husika zikaamriwa huenda kwa amri ile ile kama iliyotumika wakati wa kuingiza Richmond, na mawaziri husika wakaingia mkenge kudanganya Watanzania.
Oktoba 21, 2009 Rais Kikwete alitoa agizo kuwa mitambo ya IPTL iwashwe. Oktoba 25, 2009 tayari meli yenye shehena ya mafuta iliwasili Dar es Salaam kwa ajili ya kutumika kwenye mitambo ya IPTL. Tufikiri kwa makini na kwa kina bila woga, tena kwa ujasiri wa uzalendo, kweli hakuna mkono wa rais katika giza linaloendelea nchini, au katika hili suala la kukatika umeme?
Tafakari kuwa Rais Kikwete alitoa tangazo kuwa mitambo ya IPTL iwashwe, Oktoba 21, 2009, kisha tukaambiwa na kina William Ngeleja kuwa serikali imeagiza mafuta ya kutumia kwenye mitambo ya IPTL Arabuni. Baada ya siku chini ya sita, tukataarifiwa kuwa mafuta yameletwa na merikebu ya mizigo na yamefika bandari ya Dar es Salaam yakisubiri kupakuliwa ili mitambo hiyo iwashwe. Tena meli zingine inabidi zisogezwe haraka ili kupisha upakuaji wa shehena ya mafuta ya IPTL.
Tujiulize tena, meli toka Arabuni huchukua siku ngapi? Au mafuta yaliagizwa kabla ya Ikulu kuzungumza? Na ilikuwaje mafuta yakaagizwa kabla ya Ikulu kutoa tamko? Ikulu ilipataje kujua kuwa giza litaingia na nchi itatumia mitambo ya IPTL?
Ni wachache sana watakaokubali kuwa giza hili limepangwa, tena kwa ajili ya kutafuta umaarufu wa kisiasa ambao hauna uzalendo hata kidogo, bali ni udhaifu mbaya sana wa uongozi, unaoashiria rushwa mpaka uongozi wa juu wa nchi.
Meli hii ilikimbia kiasi cha kuvunja rekodi ya safari za meli toka Arabuni kuja Tanzania chini ya muda wa siku sita tu! Imewezekanaje? Kama kweli mafuta yalishaagizwa toka Arabuni kabla, kwanini yaliagizwa? Nani aliagiza? Alikuwa anatekeleza agizo lipi? Alijuaje amri ya rais kabla haijatamkwa? Alijuaje kuwa IPTL wangekubali kuwasha mitambo? Alijuaje kuwa IPTL hawana mafuta ya kuwasha mitambo?
Kufuatia ushahidi huu, nimeweza kuona kuwa majibu ya maswali yafuatayo yanaweza kusababisha rais wetu kuhusishwa na kashfa ya giza la nchi yetu.
Je, rais alipanga na wahusika wa TANESCO ili giza liwepo aweze kutoa tamko?
Pili, aliwasiliana na watu wa IPTL kwa ajili ya biashara ya kuleta mafuta kwa spidi kubwa ya ajabu hususani kwa meli kubwa ambazo zimewahi kusafiri toka Mashariki ya Kati hadi Afrika Mashariki?
Kama hayo mawili si ya msingi, tunaomba kujulishwa mafuta hayo yaliagizwa na nani? Lini? Kwa njia gani ya haraka iliyosababisha yakafika hata muda wa wiki haujafika?
Lakini yakiendelea madudu hayo yote, tujue kuwa ni rais wetu aliyewahi kusema kuwa nchi yetu kwa sasa mgawo wa umeme utakuwa historia, baada ya kutoka Marekeni na kuongea na wawekezaji wa Richmond.
Tunaogopa nini kumuwajibisha Rais Kikwete na serikali yake kwa kushindwa kuwaletea wananchi umeme wa uhakika, badala yake wamekuwa wakitufanyia biashara sisi masikini? Si Rais Kikwete ndiye aliyewaahidi Watanzania kuwa sasa mgawo wa umeme utakuwa historia nchini baada ya kuwapo kwa kampuni za kuzalisha umeme wa dharura kupitia kampuni hii ya Richmond?
Tamko nyonge la Ikulu lililotolewa na Luhanjo liliwahi kusema kuwa: Rais alikataa Kampuni ya Richmond isipewe malipo ya awali (down payment) ya USD 10 million na kutaka ukweli kuhusu uaminifu na ukamilifu (integrity) wa kampuni hiyo ujulikane. Rais alikataa maombi yaliyopelekwa kwake na Wizara ya Nishati na Madini ya kumuomba aagize Wizara ya Fedha, iilipe kampuni hiyo fedha hizo.
Rais aliagiza Wizara ya Fedha ibaki na msimamo wake na kuitaka Wizara ya Nishati na Madini pamoja na TANESCO wafanye mambo mawili. Kwanza, wafanye utafiti zaidi kujua undani wa Kampuni ya Richmond, isije kuwa ni kampuni bandia wakapewa fedha wakatokomea nazo na mitambo isipatikane na hukuna namna ya kuipata kampuni wala wahusika wake.
Pili aliagiza wawatake viongozi wa Kampuni ya Richmond kwanza walete mitambo, ikishafika, ndipo walipwe. Maagizo hayo ya rais yalizingatiwa na Kampuni ya Richmond ikapewa sharti hilo. Lakini, ikashindwa kulitekeleza na kuishia kuingia mkataba na Kampuni ya Dowans iliyokuja kuleta hiyo mitambo badala yake.
Hivi baada ya hapo Rais Kikwete alimchukulia nani hatua kwa kuona kuwa aliyoagiza hayakutekelezwa? Baada ya kujua kuwa Richmond haikuweza kazi na kabla haijaingia mkataba na Dowans, yeye kama Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri alipokeaje hilo, huku akijua kuwa Richmond imelipwa pesa huku ikiwa haijafanya kazi? Kwanini alikaa kimya muda wote mpaka sasa? Kama hahusiki awawajibishe waliohusika. Mungu azidi kutubariki, atufunulie akili zetu tuweze kujua tunayofanyiwa.