Mzee Mwanakijiji
Platinum Member
- Mar 10, 2006
- 33,483
- 40,011
The most recent attack took place on October 21, 2011 in Mbizi Village, Kahama District, Shinyanga Region of Tanzania. A 15-year-old girl with albinism by the name of Kulwa was attacked just after midnight at her home by three masked men. They hacked off her arm above the elbow and the horrified and helpless parents saw them fleeing with the arm wrapped in one of the assailant's coat. Kulwa was treated at Kahama District Hospital and was terrified to return home
Na. M. M. Mwanakijiji
TUNAWEZA kukaa chini na kukubali mapendekezo ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, juu ya vita dhidi ya mauaji ya maalbino au kuyakataa; tunaweza kukubali kuwa waganga wote wa kienyeji wafutiwe leseni zao kwa kudhaniwa kuhusika na uhalifu au kukataa; tunaweza tukakubali waziri mkuu aseme maneno ya kichochezi na yenye kuhatarisha amani nchini au kumpinga. Yote yamo ndani ya uamuzi wetu na ndani ya uwezo wetu.
Natamani kuandika kwa kirefu juu ya kauli zinazodaiwa kutolewa na Waziri Mkuu juu ya wale wanaoshukiwa kufanya mauaji ya maalbino kama zilivyonukuliwa na vyombo mbalimbali vya habari.
Sitafanya hivyo hapa lakini nataka nipinge tu kuwa kuhalalisha mauaji ya watu wengine kwa vile wanatuhumiwa kuua watu wengine, hakutatui tatizo la mauaji bali kunalithibitisha.
Hata hivyo nimeandika mawazo yangu kwa kina kwenye kijarida ninachotoka mtandaoni cha "Cheche za Fikra" na kuelezea kwa kina kwanini naamini kauli hizo za waziri mkuu ni za makosa, za hatari na ni lazima aidha zifutwe, zikanushwe au ziwekwe katika lugha ambayo inakubalika kisheria.
Haziwezi kupuuzwa au kuachwa zisimame kama zilivyo. Niandikie kupata nakala ya kijarida hicho kwa barua pepe bure.
Hata hivyo hapa nataka kusema tu kuwa kuja na sera ya ‘jino kwa jino' na kufuta leseni za waganga wa kienyeji wote nchini hakuwezi kamwe kuondoa mauaji ya maalbino, kwani msingi wake umekosewa tangu awali.
Watawala wetu wanataka watu waamini kuwa kinachochea mauaji ya maalbino ni imani za kishirikina.
Wanataka watu waamini kuwa ni ushirikina unaosababisha ndugu zetu maalbino kuuawa.
Nimeshaandika juu ya mauaji ya maalbino kwa kina huko nyuma, hata hivyo naamini serikali na vyombo vya usalama vinalikabili suala hili kwa makosa, kwani vinaoongozwa na tatizo ambalo si kichocheo cha mauaji haya.
Sisemi kwamba imani za kishirikina hazitumiki katika mauaji haya bali kuwa kiini hasa na kichocheo hasa siyo wacheza ndumba na wapiga ramli.
Kuweka mkazo katika hayo ni kujaribu kutwanga maji kinuni. Hakuhusiani na tatizo lililopo. Mpaka tutambue chanzo cha mauaji haya ndipo kwa hakika tutaweza kupambana nayo na ninaamini mapendekezoo nitakayoyatoa (kinyume na yaliyotolewa na Waziri Mkuu) yanaweza kabisa kukabiliana na tatizo hili.
Nitawakumbusha kitu hapa; ni jinsi gani aliyekuwa mtawala wa Iraq aliweza kusalitiwa maficho yake?
Je, watoto wake Uday na Qusay walisalitiwa kwa misingi gani? Je, ni kitu gani kinaweza kumfanya mtu amsaliti ndugu yake wa damu? Ndugu zangu jibu ni fedha!
Mauaji ya maalbino yameanza na kukolezwa kwa sababu ya tamaa za fedha (utajiri wa haraka haraka). Sasa hili limewahi kusemwa huko nyuma ingawa limesemwa katika maudhui ya matokeo ya imani hizi za kishirikina (kwamba mtu anaenda kwa mganga ili kupata utajiri wa haraka haraka).
Naamini kilichokosewa kwa muda mrefu katika miaka hii miwili ni kuingiza fedha katika vita hii. Niliwahi kuandika huko nyuma haja ya kuanzisha fungu maalumu la kuzawadia watakaowasaliti wenye kutafuta viungo vya maalbino.
Hadi hivi sasa kinachopimwa na wauaji hawa ni kipi kina faida zaidi kuliko kipi kinatisha zaidi.
Kwa wauaji hawa wazo kuwa wanaweza kupata utajiri wa haraka haraka wakifanya mauaji haya inapita kwa kiasi kikubwa kulinganisha na adhabu ya wao kukamatwa au tishio la wao wenyewe kuuawa. (rudia tena fungu hili).
Hivyo njia ya kwanza na kubwa zaidi ya kupambana na mauaji haya ni kuleta fedha kwenye mapambano haya. Je, serikali inaweza kutafuta kiasi cha shilingi milioni 200 au zaidi kuzawadia watakaofichua wanaotafuta viungo vya maalbino? (angalia nimesema wanaotafuta, sikusema wanaoua).
Wale wanaotafuta viungo vya maalbino ndio wenye tamaa ya utajiri wa haraka haraka na kutoka kwao wanatafuta wauaji. Kwa maneno mengine, wenye kudhania watatajirika kwa haraka si wauaji bali wenye kutaka viungo hivyo, ambao ninaamini ni wafanyabishara! Wauaji hawa ni watu wanaolipwa na sitashangaa wanalipwa vizuri mno kiasi cha kuweza kuingia nyumba ya mtu na kumkatakata vipande.
Njia pekee ya kuwanasa hawa ni kuhakikisha kuna dau kubwa zaidi pembeni.
Maana yake nini? Maana yake ni kwamba ukiweka fedha kwenye mapambano haya unalazimisha mtu kupima kipi bora.
Je, aende kuua mtu kwa sh milioni 10 wakati endapo akienda kuwatonya polisi na vyombo vya sheria na akaweza kumnatisha huyo mfanyabiashara na mtego ukapangwa na huyo mtu akatiwa mbaroni yeye ananyanyuka na sh milioni 15 ya halali, lipi alichague? Sasa hivi tunawataka watu hawa wasalitiane kwa sababu ya ‘uzalendo' tu.
Hilo halitoshi, kama kweli tunataka kukomesha mauaji haya hatuna budi kuweka fedha pia kwenye mapambano haya. Maneno ya vitisho hayatoshi na kelele za majukwaani hazitoshi. Kutoa matamko ya kulaani hakutoshi.
Kama tunataka kukomesha mauaji haya ni lazima tulipe gharama yake, naam! Hata gharama ya fedha.
Hili linanileta kwenye uamuzi wa kufuta leseni za waganga wote wa kienyeji. Najua serikali imechukua uamuzi huo kwa nia njema. Hata hivyo naamini imefanya kwa kukurupuka na kwa kuongozwa na hisia.
Kwamba, waganga wa kienyeji wote wanahusika kwa namna moja au nyingine na mauaji ya maalbino. Tatizo la hatua hii kwanza imepotoka kwa sababu haiwezekani waganga wote wa kienyeji kuhusika na mauaji ya maalbino. Na pili, haiwezekani kudhaniwa kuwa wote wanajuana na wamekula njama.
Kufuta leseni hizi, serikali na vyombo vya usalama vinakiri kuwa vimeshindwa kupenyeza (infiltrate) kazi hii. Hili halinishangazi kwani yaliyotokea kwenye sekta ya fedha na wizi mkubwa usingeweza kutokea endapo vyombo vyetu vingeweza kupenya humo na kuwa na watu wao.
Nilipofuatilia katika vyanzo vyangu jibu lilikuwa ni hilo hilo.
Chanzo kimoja cha kuaminika sana kimedokeza kuwa tatizo la TISS (Usalama wa Taifa) ni kuwa hakuna fungu la mitaani au limepunguzwa mno.
Kwa mujibu wa chanzo hicho, fungu hilo la mitaani ndiyo ambalo linatumiwa na vyombo vingi vya usalama kukusanya habari za kijasusi kutoka mitaani.
Kwa kufuta leseni hizi zote serikali inakiri ya kwamba wameshindwa kupenyeza waganga wao wa kienyeji, wameshindwa kuwanunua na kuwaweka kwenye malipo yao waganga hao, na zaidi ya yote wameshindwa kupata wafanyabiashara ambao wangeweza kujipitisha kama wanatafuta wauaji.
Kwa maneno mengine, serikali inathibitisha kile ambacho nimekiandika kwa kirefu mwaka jana.
Usalama wetu wa Taifa unahitaji msaada wa haraka. Bila kuwa tayari kulipa watu katika kukusanya habari, hatuwezi kuzuia vitendo kama hivi. Hivyo jibu bado linarudi kwenye fedha. Sasa tufanye nini?
Naamini serikali inataka kweli kukomesha mauaji ya maalbino. Njia walizozichagua hadi sasa za kauli kali, vitisho, n.k havitoshi kuzuia mauaji haya.
Kunahitajika hatua za makusudi kupambana na uhalifu huu kwa njia za kisheria na si nje ya sheria. Tukikubali kufanya jambo lolote nje ya sheria kwa sababu ya kukerwa, kuchoshwa, kukasirishwa na ‘plight' ya maalbino, hatutendi haki kwa sheria zetu, na kwa hakika tutafungulia utawala wa mwituni ambapo vitendo vya kisasi vitatawala. Mimi suluhisho langu linarudi kwenye pesa na liko hivi:
a. Serikali itenge kiasi kisichopungua sh bilioni moja! Ndiyo nimesema bilioni moja kwa sababu naamini kabisa thamani ya maisha ya ndugu zetu waliouawa inazidi sana kiasi hicho kwa mara nyingi mno kiasi kwamba hakikadiriki.
b. Hivyo kutenga sh bilioni moja ni kidogo tu, kiasi tunachoweza kufanya sisi kama taifa tukizingatia kuwa serikali hiyo hiyo ililala wakati kina Kagoda wanachota sh bilioni 40! Kusema ukweli hata wakitenga sh bilioni 40 hizo kwa ajili ya kupambana na mauaji ya maalbino, binafsi sina tatizo hata chembe kwa kadiri ya kwamba wao na watoto wao hawawi kwenye mkono wa kuzipokea!
c. Kiasi hicho kitengwe katika mafungu mbalimbali kama zawadi na motisha kwa mtu yeyote yule ambaye (1) atafanikisha kukamatwa kwa mtu yeyote anayetafuta viungo vya maalbino, (2) mtu yeyote ambaye anajua mipango ya kumtafuta albino, (3) mganga yeyote ambaye amefuatwa na watu wanaotafuta viungo vya albino.
d. Serikali itenge namba maalumu za simu katika mikoa yote ambapo mtu mwenye taarifa za njama, mipango, au utafutaji wa albino au viungo vya albino ataweza kupiga simu na kutoa taarifa hiyo bila yeye kulazimishwa kujitambulisha.
e. Mtu huyo atapewa neno/alama ya siri ambayo ni utambulisho wake na utamsaidia kupata zawadi pindi habari alizozitoa zikifanyiwa kazi na kusababisha kukamatwa na hatimaye kutiwa hatiani kwa watuhumiwa. Katika kufanya hili iwe wazi kabisa kuwa kuchezea namba hizo kwa kumsingizia "baba mkwe" au "shemeji" na mambo haya ili kumkomoa, kutasababisha adhabu kali kwa mhusika.
f. Ili kuweza kufanikisha (b) naamini msaada wa utaalamu wa PCCB katika kunasa wala rushwa unahitajika. Naamini, PCCB wana utaalamu na ujuzi mkubwa wa kunasa watu kwa mitego hii.
Polisi hadi hivi sasa wamekuwa ni aibu kwa kweli. Kikosi kilichoundwa cha Usalama wa Taifa na wenzao kiongezewe utaalamu wa PCCB.
g. Kwa vile sasa leseni za waganga zimefutwa, serikali ifanye hima kuwaandikisha waganga wa Tanzania bila kuweka ugumu usio wa lazima wa tiba za jadi. Kipimo ambacho kinasemwa kuwa ati hadi dawa zao ziwe zimethibitishwa hospitali ni kipimo kisicho sawa kwani kinaondoa kabisa maana ya tiba za jadi. Imani kwenye tiba za jadi siyo suala la Waafrika tu na tusijione duni kuwa tunazo tiba hizo. Tiba za jadi ziko Ulaya, Marekani, Uchina, na karibu sehemu zote duniani tena Wazungu wao hadi wanajitangaza kwenye ma TV yao. Lakini zaidi ifanye haraka kwa sababu wakichelewa waganga wa nchi jirani wataziba pengo hilo la Tanzania na wauaji wataanza kwenda kwa waganga wa nchi jirani na kuanza kupewa maelekezo hayo. Tutabakia tunashangaa "mbona tumefutia leseni waganga wote lakini bado mauaji yanaendelea"?
h. Katika kuandikisha upya waganga hawa, msisitizo pia uwepo katika kutengeneza mtandao wa kiinteligensia miongoni mwa waganga hawa. Ninaamini kuwa kutokana na kuaminika kwao na nguvu zao katika sehemu mbalimbali waganga hawa wanaweza kutumika siyo katika kukusanya habari za mauaji ya maalbino tu bali pia kuwa kinga ya uhalifu mwingine ambao unapitia kwenye mikono hii ya wataalamu wa jadi.
i. Serikali iongeze fungu la mitaani (street fund) kwa Polisi na TISS ili liweze kutumika kukusanya habari za mitaani kama ilivyokuwa wakati ule wa vita baridi. Kama serikali isingekuwa bahili katika hili nina uhakika ya Richmond yasingefika hapa, ya EPA yasingefika hapa na haya ya maalbino yasingefika hapa. Serikali ingekuwa na watu inaowalipa kutoa habari ambazo ni muhimu kwa usalama siyo za umbea tu. Hofu yangu ni kuwa vyombo vyetu vyaweza kutumika kukusanya habari za wanasiasa na mambo yao kuliko zile za usalama wa nchi. Sitoshangaa kuna mtu yuko serikalini anajiuliza hivi "x,y" ni nani na kama ana mpango wa kugombea ubunge badala ya kukusanya habari za kijasusi kuhusu maalbino! Serikali ikiwa tayari kulipa, itapata habari zozote zile kwani fedha mara zote ni msaliti.
Haya ni mambo machache ambayo naamini yanawezekana kama kweli tunataka kupambana na mauaji haya ya maalbino. Tutaweza kuyakomesha tu kwa kuingiza fedha katikati siyo kwa vitisho vya "jino kwa jino" kwani ukishafanya vitisho hivyo unachofanya ni kuwaambia wauaji waanze kutumia silaha kali zaidi. Matokeo yake Tanzania haitakuwa tofauti sana na Baghdad au Kabul.
Tusikubali hata kidogo kwamba wakati wa matatizo ya kitaifa basi tunaweka pembeni sheria zetu. Tukikubali kuwa kiongozi yeyote wa nchi anaweza kutoa maelekezo ya kuvunja sheria na akaendelea na wadhifa wake bila kukosolewa tutakuwa tumekubali kuleta utawala wa kiimla nchini. Katika kupambana na mauaji ya albino, sisi kama taifa tusikubali kuruhusu mauaji mengine kwa kisingizio cha "kuchoshwa". Tukikubali kuwa wananchi wajichukulie sheria mikononi mwao, tutakuwa tumekubali utawala wa ubabe ambapo wale wanyonge katika jamii, wale dhaifu katika jamii, wale maskini katika jamii ndiyo tutawakuta wakitiwa viberiti kwa kisingio cha kutekeleza maagizo ya mkuu!
Hilo tunalikataa hata kama limesemwa kwa nia njema ya kuuleta ufalme wa Mungu duniani. Sheria zetu lazima zifuatwe wakati wote. Tunakataa kama vile Rais mpya wa Marekani Barack Obama alivyokataa "uchaguzi kuwa ni wa uongo kati ya usalama wetu na tunu zetu tunazozishikilia". Uchaguzi wa aidha kufuata sheria zetu hadi nukta ya mwisho au kufanya mambo kwa sababu ya hisia zilizoumizwa ni uchaguzi tunaoukataa.
Tumetaka kujenga taifa la demokrasia, basi gharama ya kwanza na kubwa zaidi ya utawala wa aina hiyo ni gharama ya kufuata sheria. Tukielekeza macho yetu pembeni, ni bora tujitangaze kuwa ni ufalme wa kiimla wa kundi la watu wachache.