Bwana mmoja na mkewe waliishi miaka mingi bila kupata mtoto. Walifanya kila waliloweza, hospitalini, waganga, washauri, lakini bila mafanikio. Hatimaye baada ya kushauriwa na mtu wao wa karibu kwamba waende kanisani kuombewa, wakaenda. Wakamkuta padri na kumweleza shida yao. Padri akawaambia wana bahati sana kwani siku mbili zijazo anatarajia kwenda Roma kwa baba Mtakatifu, akasema akifika huko atawawashia mshumaa wa baraka na kwamba utakapowaka nao watapata mtoto. Kisha akafanya sala na wakaachana. Padri alikwenda Roma na alikaa huko miaka mitano akiwa masomoni. Baada ya miaka hiyo akarudi hapa Tanzania. Yule bwana aliposikia padri amerudi alikwenda haraka kumwona. Padri alifurahi sana kumwona yule bwana na mara moja akamuuliza hali ya familia yake. Jamaa akamwambia padri kwamba hicho ndio kilichompeleka pale. Akamwambia "padri mwaka ule ulipoondoka, mke wangu alizaa mapacha wawili, mwaka uliofuata alizaa mapacha watatu, mwaka uliopita aliza mapacha wanne, na sasa ni mjamzito! Tafadhali padri NENDA UKAUZIME MSHUMAA!"