Nchi za magharibi kuilenga na kutaka kudhoofisha BRI kuna lengo la kuendelea kuzidunisha nchi za dunia ya tatu

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,010
1,034
VCG111437467407.jpg


Wakati pendekezo la “Ukanda Mmoja, Njia moja” (BRI) la China linatimiza miaka 10 tangu kutolewa, kuna mafanikio mengi yameonekana katika kuhimiza urafiki na ushirikiano kati ya China na nchi zinazoshiriki kwenye pendekezo hilo, na hasa kuleta maendeleo kwa nchi zilizopokea miradi chini ya pendekezo hilo. Lakini ni ukweli pia katika kipindi cha miaka 8 au 9 ya uhai wake, pendekezo hili lilianza kushambuliwa vikali na nchi za magharibi, kwa madai kuwa linadhoofisha nguvu ya ushawishi ya nchi za magharibi kwenye nchi za dunia ya tatu, na hasa Afrika.

Mwanzoni wakati China inatangaza kuanzishwa kwa pendekezo la “Ukanda Mmoja, Njia Moja” maarufu kwa kiingereza kama Belt and Road Initiative (BRI), baadhi ya wachambuzi wa nchi za magharibi walijaribu kulikejeli kama ni pendekezo ambalo halitakuwa na utekelezaji halisi. Miaka mitano au sita baada ya ufanisi wa pendekezo hilo kuanza kuonekana, vyombo vya habari vya nchi za magharibi vikazusha maneno “mtego wa madeni”, lengo likiwa ni kujaribu kuzitia hofu nchi zinazopokea uwekezaji kupitia pendekezo hilo.

Tukiangalia undani wa pendekezo hilo, tunaweza kuona kuwa sababu kubwa iliyofanya pendekezo hilo liwe na mvuto kwa nchi nyingi za dunia ya tatu hasa nchi za Afrika, ni kwamba limeweza kutoa majibu ya changamoto kubwa inayozikabili nchi hizo katika kujitafutia maendeleo. Tukichukulia mfano wa sekta ya miundombinu, tunaweza kuona kuwa hili ni eneo lenye changamoto kubwa, ambalo nchi za magharibi na mashirika kama Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) wamekuwa wagumu kutoa fedha, na kama wakitoa fedha kunakuwa na masharti magumu.

Kupitia BRI, nchi za Afrika zimeweza kupata fedha, teknolojia na hata miradi iliyokamilika ya barabara, reli, vituo vya kuzalisha umeme na hata vya mawasiliano ya habari. Miradi mingi ambayo nchi za Afrika zilikuwa na ndoto ya kuitekeleza tangu wakati wa uhuru, imeweza kutekelezwa katika kipindi cha miaka 10 ya BRI. Tunaweza kuchukulia mifano ya Reli ya Addis Ababa-Djibouti, Bandari ya Doraleh ya Djibouti, Reli ya SGR ya Mombasa-Nairobi, Daraja la Maputo- Katembe la Msumbiji, reli ya Lagos-Kano ya Nigeria ni miradi ambayo nchi hizo zilikuwa na ndoto ya kuitekeleza, lakini hazikuwa na uwezo wa kifedha na kiteknolojia, matatizo hayo yalitatuliwa kupitia ushirikiano na China chini ya BRI.

Unafuu wa mikopo kutoka kwa China ikilinganishwa na ile ya nchi za Magharibi, na utekelezaji wa kasi na kwa viwango unaofanywa na makampuni ya China yanayotekeleza miradi, ndio vimefanya BRI kuwa na mvuto kwa nchi za Afrika. Uzuri ni kwamba kujiunga na BRI ni jambo la hiari, nchi yoyote inaweza kujiunga na pendekezo hilo kama inaona inaweza kunufaika.

Ni kweli pia kuwa baadhi ya nchi zimekuwa na changamoto katika kulipa mikopo inayotumika kwenye ujenzi wa miradi ya BRI, na hii inatokana na ugumu kwa kupanga matumizi ya fedha kutokana na ufinyu wa bajeti za baadhi ya nchi. Hiki ndio kinachotajwa na nchi za magharibi kuwa ni mtego wa madeni. Uzuri ni kwamba China imekuwa na unyumbufu wa kila aina kuhakikisha kuwa nchi hizo zinalipa fedha bila kuhatarisha matumizi ya ndani.

Ni wazi kuwa BRI imekuwa na manufaa kwa nchi zinazoshiriki kwenye pendekezo hilo, na ni kweli pia changamoto hazikosekani. Lakini nchi za magharibi kulilenga pendekezo hilo ambalo kwa kiasi kikubwa linaitikia mahitaji ya nchi za Afrika, ni sawa na juhudi za kuhakikisha kuwa nchi za Afrika zinaendelea kuwa duni, na kujaribu kuzuia moja ya vyanzo muhimu vya fedha, teknolojia na hata kuhimiza maendeleo ya nchi za Afrika. Matokeo ya majaribio ya kudhoofisha BRI barani Afrika, sio tu yatazidhuru nchi za Afrika, bali pia hayana manufaa yoyote kwa nchi zenyewe za Magharibi.
 
Back
Top Bottom