Elections 2010 Mramba, Chenge `ruksa’ kugombea ubunge

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,789
288,015
Mramba, Chenge `ruksa’ kugombea ubunge
Imeandikwa na Oscar Mbuza; Tarehe: 4th July 2010 @ 08:40


WAKATI kukiwa na shauku ya kutaka kujua iwapo mawaziri wa zamani, Basil Mramba na Andrew Chenge wanaokabiliwa na kesi mahakamani wataruhusiwa kugombea tena ubunge katika uchaguzi ujao, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imesema wana-CCM hao bado wana sifa ya kugombea ubunge iwapo wana nia hiyo na endapo watapitishwa na CCM.

Mkurugenzi wa NEC, Rajabu Kiravu, amesema,Mramba na Chenge hawajapoteza haki yao ya kikatiba ya kugombea nafasi za ubunge kama inavyodhaniwa na baadhi ya watu.

Chenge aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali na baadaye kuteuliwa kuwa Waziri baada ya kushinda ubunge katika jimbo la Bariadi Magharibi mwaka 2005, anakabiliwa na kesi ya kuendesha gari kwa uzembe na kusababisha mauaji ya watu wawili katika eneo la Masaki, Dar es Salaam.

Mbunge huyo alifikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Kinondoni kwa mara ya kwanza Machi 30, mwaka jana na kusomewa mashitaka yanayomkabili.

Kesi hiyo bado inaendelea katika Mahakama hiyo. Mramba, Mbunge wa Rombo ambaye pia ni mwanasiasa mkongwe na Waziri wa siku nyingi katika Serikali ya Awamu ya Kwanza, Tatu na Nne, anakabiliwa na kesi ya matumizi mabaya ya ofisi ya umma na kuisababishia Serikali hasara ya Sh bilioni 11.7 alipokuwa Waziri wa Fedha.

Kesi hiyo ya Mramba inayowajumuisha pia Waziri wa zamani wa Nishati na Madini, Daniel Yona na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Gray Mgonja ilianza kunguruma kwa mara ya kwanza Novemba 2, mwaka jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi, Kisutu, Dar es Salaam.

Akizungumzia uhalali wa wabunge hao kuruhusiwa kuyatetea majimbo yao kwenye uchaguzi mkuu ujao kama wana nia hiyo, Kiravu alisema wanayo haki ya kikatiba ya kugombea na kuwa wabunge wakishinda uchaguzi hadi pale Mahakama itakapowatia hatiani kwa makosa yanayowakabili. “Hawa ni washitakiwa hawajatiwa hatiani bado.

Sheria ipo wazi na hata Katiba inaeleza wazi sifa za mtu kugombea ubunge sifa ambazo bado wanazo.

Sheria inasema mtu atapoteza sifa ya kugombea uongozi endapo atafungwa jela kwa muda wa miezi sita na kuendelea,” alisema Kiravu.

Alisema kama mara baada ya kugombea na kushinda ubunge, Mahakama itawatia hatiani wanasiasa hao na kuwafunga jela kwa muda unaozidi miezi sita ndio watapoteza sifa ya kuendelea kuwa wabunge.

Mramba na Chenge hawakupatikana kwa simu kuzungumzia suala hilo, lakini duru za kisiasa katika majimbo yao zinasema kwamba, wamekuwa wakijiimarisha kwa ajili ya kuwania kurudi tena madarakani katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika baadaye mwaka huu.

 
Back
Top Bottom