Miaka 50 Ya Uhuru: Tunagombana Mbele Ya Mwana Mfalme!

maggid

JF-Expert Member
Dec 3, 2006
1,084
1,246
Ndugu zangu,

Mama yangu mzazi enzi za usichana wake alisoma Middle School ya pale Mtaa Kichwele ( Sasa uhuru Street). shule hiyo ikaja kujulikana kama ' Uhuru Girls'.

Ni mmoja wa waliobahatika kuimba nyimbo mbili tofauti za taifa; moja ya mkoloni, na nyingine ya Tanganyika Huru.

Ananisimulia walivyokuwa wakijipanga mstari asubuhi na kuimba; " God Save The Queen!' Na baada ya Desemba 9, 1961, katika mstari huo huo, wakaimba kwa furaha na kwa kujivunia; " Mungu Ibariki Afrika".

Ndio, Tanganyika ikazaliwa, na ikawa kweli ' Young Nation'- Taifa Changa. Na Julius na wenzake akina Oscar na Rashid walikuwa vijana kweli. . Wakati ule wa uhuru hakuna mmoja wao aliyeivuka umri wa miaka 42.


Hao walikuwa marafiki watatu. Ndio, Julius Nyerere, Oscar Kambona na Rashid Kawawa. Katika uchanga ule kama taifa, Julius na Oscar wakafarakana. Urafiki ukaisha na Oscar akakimbilia ' Kwa Mama'- London.


Na Julius na Oscar ilikuwa ni kama Gandhi na Nehru kwa India. Nyerere na Kambona walikuwa na uzalendo na utashi wa kuijenga nchi yao waliyozaliwa na waliyoipigania- Tanganyika. Isipokuwa, walitofautiana kwenye njia ya kupita.

Julius alitaka kupita njia ya Ghandi- Village Swaraj. Kwa maana ya kuimarisha vijij vya Ujamaa na kujenga misingi ya Ujamaa na Kujitegemea. Kwamba vijiji vijitegemee kwa chakula. Uzalishaji uwe wa ushirika na mengineyo yenye kutofautiana na njia ya ubepari kama ya Nehru.

Nehru , tofauti na Ghandi, aliamini kuwa maendeleo ya India yangepatikana kwa kuimarisha viwanda na biashara. Kwa kutumia sayansi na teknolojia ya kisasa kwa viwandani. Na ndivyo ilivyokuwa kwa Kambona.


Ndoto ya Julius Nyerere ilikuwa njema kwa Tanganyika na baadae Tanzania. Kwamba Tanzania iwe nchi huru na iondokane na unyonyaji na ukandamizaji. Tukasema, kuwa Tumenyonywa kiasi cha kutosha, tumeonewa kiasi cha kutosha na Tumenyanyaswa kiasi cha kutosha. Kwamba ni unyonge wetu ndio uliotufanya tunyonywe, tuonewe na tunyanyaswe.


Waliotunyonya, kutunyanyasa na kutuonea kwanza ni wakoloni na baadae ni matajiri katika mfumo wa kitabaka.

Kwa bahati mbaya, ndoto ya Nyerere ilikufa pale Nyerere na TANU walipoua mfumo wa vyama vingi na kwa namna fulani, kuasisi mfumo wa ' ubaguzi wa kisiasa' dhambi ambayo bado inatutafuna hadi hii leo. Ni pale waliokuwa na fikra tofauti na zenye kushutumu wakachukuliwa kuwa ni ' maadui wa ndani' . Ni waahini. Akina Bibi Titi Mohammed, Kamazila na wengine. Walionekana maadui badala ya kutazamwa kama WaTanzania wenye mapenzi mema kwa nchi yao waliyozaliwa.


Naam, miaka 50 ya Uhuru na mbele ya Mwana Mfalme, Prince Charles dhambi ya ubaguzi wa kisiasa imepelekea Mwana Mfalme ashuhudie tunavyoshikana mashati na hata viongozi wa kisiasa kusekwa rumande.
Inanikumbusha, ' Kama Ulaya, Kama Afrika'- Mwandishi Shaaban Robert alipata kuandika waraka wa gazetini wenye kichwa hicho cha habari. ( Gazeti Mambo Leo, Juni, 1932).

Shaaban Robert anaandika; " Nina hakika ya kuwa labda baada ya miaka mingi watakaoturithi wataweza kusema Kama Ulaya, Kama Afrika! Bara kubwa maskini lililokuwa katika giza kwa muda mrefu , hata Wazungu walipofika watu walikuwa wakitiana vidole machono mchana, kila mahali palikuwa na soko la biashara ya aibu. Sasa, taa ya ustaarabu yawaka na nuru yake yaangaza'- Shaaban Robert.


Hapana, soko la biashara ya aibu linaendelea. Ndio, ni aibu. Kwamba tunashindwa kuyamaliza mambo yetu kwa mazungumzo ya kistaarabu na zaidi kuweka misingi ya kuondokana na mambo haya ya hovyo hovyo. Katiba Mpya na yenye kukidhi mahitaji ya taifa la kisasa ni moja ya misingi hiyo.

Na hakika, aibu hii inayotupata inatokana na hulka yetu ya kutaka na kung'ang'ania madaraka. Hulka yetu ya kutoamini katika kugawana madaraka. Hulka yetu ya kutaka kutawala na si kuongoza. Hivyo basi, kutotaka kusikia sauti zenye kushutumu. Haya yamo hata kwenye vyama vya siasa.


Ndugu zangu,

Mwana Mfalme katika siku yake ya kwanza ya ziara yake alitembeleaa Karimjee Hall. Huo ndio ukumbi uliokuwa ukitumika kwa shughuli za Kibunge tangu Tanganyika ilipokuwa himaya ya mama yake Mwana Mfalme- Malkia Elizabeth. Ukumbi huo unafanana na ' House Of Commons'. Spika anakaa mbele juu katikati. Baraza la mawaziri na wabunge wa chama tawala wanakaa upande mmoja wa ukumbi na wale wa upinzani wanakaa upande mwingine.

Hapo waheshimiwa watalumbana na hata kuzomeana. Si kwa chuki, bali kwa kutanguliza maslahi ya nchi. Na hicho ndicho kinachoitwa Multi Party Democracy. Na hakuna kitu kinachoitwa Single Party Democracy bali Single Party Dictatorship.


Naam, kesho Mwana Mfalme, Prince Charles anaruka kurudi kwao London. Na akifika atakwenda ' Kwa Mama' – Buckingham Palace. Tunatumaini hatasema, kuwa ; " Even after 50 years of Independece, Tanzania is still a ' Young Nation!'"

Mungu Ibariki Afrika.
Maggid,
Iringa
Jumatano, Nov 9, 2011
MJENGWA - Picha, Habari & Matangazo
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom