Mengi: Mafisadi wanatumia fedha kuchafua amani

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,789
288,013
Date::12/20/2008
Mengi: Mafisadi wanatumia fedha kuchafua amani

ASEMA AMEMSAMEHE MASHA

Na Peter Edson
Mwananchi

MWENYEKITI Mtendaji wa IPP, Reginald Mengi amesema mafisadi wanatumia fedha zao kuchafua hali ya amani nchini na kueneza uvumi kuwa nchi haitawaliki kwa sababu ya vita dhidi ya ufisadi. Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Mengi alisema kuwa mafisadi ni waongo wakubwa kwa sababu wanajua kuwa wananchi, wakiongozwa na vyombo vya habari na serikali ya awamu ya nne, wamejizatiti katika vita hivyo.

Mengi ametoa kauli hiyo wakati serikali imeshawafikisha watuhumiwa 21 wa kesi ya wizi wa fedha kwenye Akaunti ya Malimbikizo ya Madeni ya Nje (EPA), huku ikiwapandisha kizimbani mawaziri wawili wa serikali ya awamu ya tatu, Basil Mramba na Daniel Yona kwa tuhuma za kutumia vibaya ofisi, pamoja na Katibu Mkuu mstaafu wa Wizara ya Fedha na Uchumi, Gray Mgonja.

Mengi anachukulia hatua hizo kama nia ya dhati ya serikali ya awamu ya nne ya kupambana na kero ya ufisadi pamoja na kuimarika kwa uhuru wa vyombo vya habari. Mfanyabiashara huyo alisema, ujasiri wa vyombo vya habari katika vita dhidi ya ufisadi umetokana na dhamira kubwa ya Rais Jakaya Kikwete ya kutaka kutokomeza ufisadi nchini na katu nia hiyo ya mafisadi haitafanikiwa.

"Wapo wanaosema kwamba ni unafiki mtupu kuwapiga vita viongozi wanaohusishwa na ufisadi kwa njia moja ama nyingine na kumpongeza Kikwete kwa jitihada zake za kupambana na mafisadi, huu ni unafiki mkubwa," alisema Mengi, ambaye hivi karibuni aliwahi kusema kuwa ametishiwa maisha kutokana na kuwa mstari wa mbele katika vita dhidi ya ufisadi.

Mengi alisema sehemu kubwa ya watu hawa pia hudiriki kusema kuwa kupiga vita ufisadi kunaifanya nchi isitawalike, jambo ambalo alisema ni uzushi mtupu na kwamba ni mawazo mgando yanayotaka kupoteza kasi ya mapambano dhidi ya mafisadi. Alisema ni vema mafisadi wakaelewa kuwa ufisadi ndiyo unaifanya nchi isitawalike na kwamba kuandika habari kuhusu mafisadi hakuwezi kuifanya nchi isiweze kutawalika.

Mengi, ambaye alionekana kutoa kauli kali, alisema ufisadi unapoandikwa unawafanya watu wengine waweze kujisafisha na kubadili nia zao mbaya za kutaka kutumia rasilimali za nchi kwa manufaa yao binafsi.

"Watu wanaoeneza hali hii ni waongo na wanatakiwa kuogopwa sana kwani wengi wao hutumia fedha za ufisadi kuchafua amani ya nchi jambo linalowapa shida viongozi wa juu kutawala nchi," alisema.

Mengi alisema viongozi wanaokumbatia mafisadi wao pia ni sehemu ya mafisadi, kwani ukweli unabaki kuwa fisadi hapendi mambo yake kufichuliwa, hivyo ni vema viongozi wanaotumiwa na baadhi ya mafisadi wakaacha kutoa kauli zinazoashiria kupinga juhudi za Rais Kikwete za kupambana na mafisadi.

Ni vema mafisadi wakaelewa kuwa juhudi zao zenye nia mbaya kamwe hazitaweza kuvunja nguvu na dhamira ya vyombo vya habari, umma na nia ya Rais Kikwete ya kutokomeza kabisa ufisadi nchini Tanzania. "Hatuwezi kuvipongeza vyombo vya habari pekee kwa kazi nzuri ya kupiga vita ufisadi bila kumpongeza Rais Kikwete," alisema Mengi.

Alisema ufike wakati watu wakaelewa kuwa uhuru waliopewa waandishi wa habari na Rais Kikwete ndiyo matunda yanayoonekana hivi sasa, hivyo anayestahili kupongezwa kwanza ni rais na kisha vyombo vya habari na watu wengine. Wakati huohuo, Mengi alisema amefunga rasmi mjadala wa mgogoro baina yake na Waziri wa Mambo ya Ndani, Lawrence Masha kwani suala hilo halina masilahi yoyote kwa taifa.

Alisema mgogoro huo umelenga kabisa katika hisia za mtu binafsi, hivyo haoni sababu ya kuendelea kulumbana na mtu ambaye hajui alitendalo.

"Sipendi tena kuongelea masuala haya, pia kutoka rohoni mwangu natamka kuwa nimemsamehe waziri kijana aliyekuwa anapanga njama za kunifilisi, lakini pia kumsamehe Waziri Masha kwa kuwa wote hawajui walitendalo," alisema Mengi.

Mengi alisema kitendo cha yeye kupewa vitisho na Waziri Masha huku akimtaka kupeleka ushahidi wa mambo ya kufilisiwa kwa muda wa siku saba ni changamoto ambazo amekuwa akikutana nazo kila siku hivyo hazimpi shida. "Maneno ya Mungu yanasema, msamehe mtu yeyote ambaye hajui atendalo, mimi ni nani hadi nishindwe kusamehe?" alihoji Mengi.


Alisema mijadala ambayo haina masilahi kwa taifa bali inalenga kuchochea vitendo vya uvunjifu wa amani ni vema ikawekwa kando ili kuruhusu mambo yenye masilahi kwa taifa kujadiliwa.

Siku za hivi karibuni Waziri Masha pamoja na mwenyekiti huyo wa IPP walishindwa kuelewana kutokana kauli ya Mengi aliyoitoa kupitia vyombo vya habari kuwa kuna waziri kijana anapanga njama za kumfilisi mali zake kwa kumbambikizia kodi kubwa ambayo itamshinda kulipa.
 
Naona huu mjadala haujaisha ila Mengi ametaka kumwonyesha jeuri kwamba yeye Masha sio lolote on hii statement

``Mengi alisema kitendo cha yeye kupewa vitisho na Waziri Masha huku akimtaka kupeleka ushahidi wa mambo ya kufilisiwa kwa muda wa siku saba ni changamoto ambazo amekuwa akikutana nazo kila siku hivyo hazimpi shida`´.

Hivyo tusubiri jeuri ya Waziri kama anao uwezo wa kutimiza sheria ama kukubali msamaha wa Mengi.

Ikumbukwe Mengi hajakanusha kwamba taarifa yake ilikuwa ya uongo bali walipanga huo mpango na aliyetoa vitisho wote amewasamehe maana HAWAJUI WATENDALO
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom