Mei Mosi 2018: Rais Magufuli atapandisha Mishahara miradi mikubwa ya Serikali ikikamilika, Mwaka jana alinukuliwa Vibaya

Roving Journalist

JF Roving Journalist
Apr 18, 2017
2,812
11,989
SHIRIKISHO la vyama huru vya wafanyakazi Tanzania (TUCTA) ambao ni waandaaji wa sherehe za wafanyakazi kitaifa (MEI MOSI), wamesema sherehe za Mei Mosi mwaka huu zitakazofanyika kitaifa mkoani Iringa kwenye uwanja wa Samora.

Mgeni rasmi katika sherehe hizo atakuwa Rais John Magufuli.

Tukutane hapa kwa updates zaidi.

Matarajio ya wafanyakazi.

1. Toka aingie madarakani hajawai kupandisha mishahara wafanyakazi.

2. Alipunguza 1% ya kodi iliyojificha na hajawai kuwa na impact kwa watumishi

3. Katika ukanda wa afrika mashariki na kusini mwa jangwa la sahara ndio mfanyakazi anakatwa kodi kubwa kuliko mtu yoyote.

4. Hajaajiri katika awamu yake kama ilivyokuwa kwa awamu zilizo pita. Na tukumbuke bajeti inayopitishwa bungeni hakuna kipengere cha ajira mpya na bajeti karibia zote zimepunguzw kwa 10-40%. Hivyo hakuna bajeti ya waajiriwa wapya.

6. Ajira za walimu ni changa la macho kwa sababu bajeti ya sasa imeongezwa kwa 5% tuuu, kwa lile la kusema serikali hii inaboresha elimu ni ndoto za mhana.

7. Bajeti kubwa kuliko zote ni usafiri yaani kuknunua ndege hata afya imekatwa kwa 20% sijajua hao wanaotakiwa kupanda ndege na treni sio watanzania au maana wagonjwa watapanda treni kwenda india kutibiwa? Au ndege zinafika india?

=====



UPDATES: 10:15hrs

=> Sasa kinachoendelea ni maandamano kupita mbele ya mgeni rasmi.

=> Kauli mbiu katika sherehe hizi ni "Kuunganishwa kwa mifuko ya hifadhi ya jamii kulenge kuboresha mafao ya wafanyakazi". Na wanaandamanaji walio wengi wanapita mbele ya mgeni rasmi na mabango yaliyoandikwa hilo neno.
Mey7.jpg
may9.jpg

Mei1.jpg

=> Baada ya watu kupita kwa maandamano, sasa ni maandamano ya Magari ya wafanyakazi. Gari lililopita la kwanza ni gari la wafanyakazi wa bunge, TANESCO, Hospital ya rufaa Iringa, NMB, Posta, TRA nk. Magari yote yamepita yakitoa ujumbe kile wanachokifanya.

10:30HRS

Sasa unaimbwa wimbo wa taifa baada ya hapo utaimbwa wimbo wa wafanyakazi (Solidarity Forever)

Mei3.jpg

=> Sasa Unaimbwa wimbo kutoka kwaya ya JKT Mafinga.

10:50HRS

Kinachoendelea ni utambulisho wa Viongozi waliohudhulia wa Serikali na vyama vya Wafanyakazi unaofanywa na Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (TUCTA) Dk Yahaya Msigwa.

Huku kwa Upande wa Serikali mkuu wa Mkoa wa Iringa Amina Juma anatambulisha Viongozi wa Serikali, anawapa nafasi viongozi wa dini kusalimia

=> Mhashamu Tarcisius Ngalalekumtwa amepewa nafasi ya kusalimia. Katika salamu zake amewasimimamisha watu wote na kuwaombea

Sasa ni Kiongozi wa KKKT Dkt Owdenburg Mdegela, anashukuru wote waliokuja na kuwatakia baraka kwa kusema uwepo wa rais ni baraka tosha.

=> Abubakar Chalamila Shekh Mkuu wa Mkoa wa Iringa pia anatoa neno. Anasema kazi ya viongozi wa dini kwenye sehemu kama hizi huwa ni Dua tu, anatoa dunia na kushukuru. Anachomekea kwa kusema "Inapotajwa Tanzania ni Nchi ya Amani basi Iringa ni Kisiwa cha Amani, Karibu sana Iringa"

=> Mkuu wa Mkoa wa Iringa anaendelea kwa utambulisho wa Wabunge, Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi na Wakuu wa Mikoa wa Jirani walioalikwa. anasema Wapo Mabalozi wa Kenya, Burundi na Mozambique. Anamaliza kwa kuwakaribisha wageni wote

=> Anatoa salamu za chama cha waajiri. Mwakilishi wa ATE Ndugu Senyimbo ndo anatoa salamu.

=> Anapongeza TUCTA kwa kuendelea kutoa ushirikiano kwa waajiri. Anashukuru rais kwa kubali kushiriki siku ya leo.

=> Anasema Kuna maisha baada ya kustaafu, tunategemea mafao mazuri kutoka mifuko ya wafanyakazi. Waajiri tunawataka wafanyakazi kutekeleza kazi wa uadilifu ns bidii na kujiepusha na rushwa. Tunalojukumu la kushirikiana na serikali ili kuleta maandamano.

=> Waajiri tunavutiwa na kazi nzuri inayofanywa na Serikali ya kwako kama ujenzi wa miundo mbinu ni fursa nzuri sana kwa maendeleo. Jitahada za kuboresha sekta ya anga.

=> Chama cha waajiri tanzania tunaamini ili kufikia malengo, sharti kuzingatia mgawanyo sawa wa raslimali zetu. Tunatambua jitihada zako katika kuwatambua watu wenye ulemavu kwani umeteua Walemavu katika Serikali yako.

=> Tnatoa wito kwa wahitimu kuja kujifunza kwa Vitendo, nawapongeza waajiri wanatoa nafasi

=> Waajiri tuna changamoto, Mrundikano wa kodi na tozo mbalimbali, hii inapelekea baadhi ya waajiri kupunguza wafanyakazi. Tunaomba tupunguziwe Mrundikano wa kodi na tozo.

=> Tunapendekeza marekebisho sheria za kazi ambazo zinadumaza kuongeza tija za ushindano na kulemaza wafanyakazi.

=> Muwakilishi kutoka shirika la kazi dunia ILO Wilton Chibebe anatoa salamu. Anasema ILO itaendelea kulinda na kuhakikisha Serikali inalinda na kupata mafao na maslahi yanayotambulika na shirika la ILO.

11:35HRS

=> Waziri wa Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu Jenista Joakim Mhagama amekaribishwa. na anatambulisha viongozi wa Kitaifa wapate cha kusema kidogo. Anaanza kwa kumuita Spika Ndugai asalimie watu wa Iringa.

=> Spika Ndugai anasema Wafanyakazi wote wanakusubiri wewe rais. Mwaka jana kule Moshi uliahidi kuunganisha mfuko na lilipokuja bungeni tukalifanyia kazi na wewe ukaribaliki. Sisi bunge tutazidi kuzitama sheria zote kandamizi. Ombi letu kama wabunge ni mfanye kazi kwa bidii na Tija.

=> Waziri Mkuu Majaliwa anasema; Kama Spika alivyosema, Wafanyakazi wanakusubiri wewe. Mimi nmetembelea kwenye taasisi tofauti. nakiri kazi zinakwenda vizuri na wanafanya kazi kweli kweli, kama nlivyoonesha shukrani zangu kwa wafanyakazi, naomba Wafanyakazi waendelee kufanya kazi.

=> Mhagama anamkaribisha Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga kutoa salamu kwa niaba ya Wageni wote.

=> Mahiga anasema Sisi wanairinga tunayofuraha kuwa mwenyeji kwako wewe rais na kuwa Mwenyeji kwa watu wote. Leo uwanja wa Samora umefurika, mara ya mwisho ilikuwa mwezi wa nane 2015 ilipokuja hapa kwenye kampeni ya kuwa rais wetu. Najua ulipata shida kidogo kupata wadhamini hapa mjini. kura 25 za wadhamini hapa mjini zilikosekana hadi ukaenda nje ya mji, tunakuomba radhi kwa hilo kosa.

=> Ulipokuwa hapa ulitoa ahadi na umezitimiza. ulisema Iringa ilitakuwa Makao makuu ya Utalii na hilo tumelifanya. Umeshachukua maamuzi kwamba Uwanja wa Nduli utalekebishwa.

=> Ulishachukua maamuzi kwamba barabara ya Iringa kwenda Ruaha itakuwa kiwango cha Lami. Mimi nmekua nikikushauri kuhusu Maendeleo ya Iringa na Umenisikiliza. Mjini barabara zimetengenezwa kwa Bil 6.4. Shule Kongwe zote zimekarabatiwa, miradi ya maji ni mabilioni, Kabla ya kuja hapa umefungua barabara kuu ya Afrika ya kati na afrika ya mashariki. Barabara hii inapita katikati ya Mkoa wa Iringa na Ulisema iwe mkombozi kwa watu wa Iringa.

=> Mhagama anamkaribisha Chifu Mkwawa Mrithi wa Chifu wa eneo hili akiwa amesindikizwa na Mzee Malangalila.
Mei 4.jpg

=> Chifu anasema sina Mengi ya kusema zaidi ya kukaribisha rais wetu rais John na Mafuli na Majaliwa. Asante. Amemaliza.

=> Mzee Malangalila ansema, tunatoa uchifu kutokana na ndoa, hatufuati baba ana wake wanne, hii ndo sababu tumempa uchifu mtoto.

=> Waziri Mhagama anasema; Nakushukuru rais kwa kukubali mwaliako wetu, tunatambua unayo majuku Mengi, lakini umeona umuhimu wa Sherehe hizi kuwa muhimu zaidi. Utaata nafasi ya kuwaeleza wafanyakazi hawa mipango mbalimbali ya Serikali.

=> Nitumie muda mfupi kukuhakikishia kwamba mimi na Wenzangu tumekuwa tukikutana viongozi wa vyama vya wafanyakazi mara nyingi ikiwemo kuhudhuria makongamano. Katika vikao hivyo tumejifunza kwamba Ushirikiano kati ya vyama vya wafanyakazi na Serikali ni jambo Lisiloepukika. Mimi na wenzangu tutaendelea kutoa Ushirikiano kwa vyama vya wafanyakazi.

=> Ulipotuagiza tutekelezi ombi la vyama vya wafanyakazi la kuunganisha Mifuko ya vyama vya wafanyakazi, tumefanikiwa kitu ambacho watu wengine wameshindwa. Tumeendelea kuunda mabalaza ya wafanyakazi na kusimamia sheria ya hifadhi ya jamii kwa wafanyakazi.

=> Tumeendelea kulidhia mikataba mbalimbali itakayotuwezesha kusimamia masrahi ya wafanyakazi.

=> Mwaka 2001 Tuliunda hii TUCTA ambayo inaendelea hadi leo. Hii inaonesha serikali inathamini vyama vya wafanyakazi. TUCTA inahitaji wanachama wapya, na hilo unalijua na umeanza kulifanyia kazi kwa kuwapatia wanachama wengi

=>Kupitia miradi mikubwa ya kitaifa ambayo vitatoa maelfu ya ajira, hiyo itaongeza wanachama wa vyama vya wafanyakazi, tunakushukuru sana.

=> Serikali tutaendelea kufanya kazi na nyie kwa kuzingatia sera na taratibu tulizojiwekea. Kama nlivyosema, Mimi ni kama Yohana Mbatizaji, nachukua nafasi hii kuwashukuru na mwenyezi Mungu aibariki siku yetu na aifanikishe siku yetu ya leo. Asante

12:10 HRS

Kwaya ya wafanyakazi (Walimu) wanatoa Burudani

12:20HRS

=> Katibu mkuu wa TUCTA Dk. Yahaya Msigwa amekaribishwa.

Dk. Yahaya: Rais umekuwa ukisema kwamba maendeleo hayana itikadi. Na sisi tunasema masirahi ya wafanyakazi hayana itikadi.

=> Katibu mkuu wa TUCTA: Mgeni rasmi, tulifarijika na kujiona wa thamani uliosema Mfanyakazi ndio injini ya maendeleo katika taifa lolote.

=> Katika Sherehe za Mwaka jana uliongea mengi na ukatoa ahadi kama ifuatavyo;

Wafanyakazi nawahakikishia wafanyakazi tunaanza ukurasa mpya sababu serikali imeamua kwenda mbele na serikali ya awamu ya tano ipo pamoja na wafanyakazi.

=> Bila kudhalau wala kupuuza maoni yenu, Ulisema ulitaka usafishe kwanza kabla hujapandisha mishahara ya wafanyakazi ili tusiwafaidishe wasio sitahili , nawaahidi wafanyazi kuanzia bajeti ijayo ntaongeza mishahara kutoka kiwango kilichokaa kwa muda mrefu, ulisema utarejesha promotion za watumishi wa umma ikiwemo kupandisha madaraja, kuboresha mafao, mfumko wa bei na kuanzisha bima ya afya, utaendelea kuridhia mikataba ya kimataifa, Yoyote atakayehamisha asihame bila kupewa hela ya kuhamishwa, kwenye ofisi yangu kuna malalamiko watu wanahamishwa hawawalipwi. Uisema ukitoka hapa utakutana na mawaziri kufanya mikakati ya kuweka maslahi ya wafanyakazi.

=> Ahadi hizi zlileta muamko kwa wafanyakazi. tunajua yapo kadhaa yametekelezwa na mengine hayajatekelezwa. Tunaomba Mgeni rasmi useme neno ili roho za wafanyazi ziweze kupona. tunaomba majibu ya ahadi za mwaka jana.

=> Ulizungumza swala la ucheleweshaji wa mafao, tunaomba mifuko hii ya hifadhi ya jamii isimamiwe na Wizara moja tu

=> Punguzo la kodi lilitolewa mwaka jana kwa wafanyakazi wa kima cha chini tu. mfanyakazi anakatwa 30% hadi 40% hii ni mateso makubwa kwa mfanyakazi kwani hajaongezewa mshahara kwa muda mrefu. Kodi kubwa inachukuliwa kwenye kodi ya mfanyakazi, tunaomba kipungue.

=> Tunaomba Serikali ipitie kima cha chini cha mshahara. Kima cha chini tunaomba kisipungue laki saba na hamsini elfu bila kulipishwa kodi ndo yanakidhi. hiki ndo kitamtosha baba mama na watoto kujikimu. Tuna matarajio makubwa kwako juu ya hili neno juu ya maisha yao. Wewe ni mtu usio penda matabaka.

Kuna taasisi baada ya kuondoa waajiriwa wa darasa la saba zimeteteleka kwa kukosa mbadala ikiwemo TANESCO na Mashirika ya reli wamekosa kupata watu wa kushika nafasi zile. Tunaomba warudishwe waliokuwepo

1300HRS

=>Rais wa shirikisho la vyama vya wafanyakazi (TUCTA) Tumaini Nyamhokya anasema;

=> Baada ya Salamu anamkaribisha Mgeni rasmi, kwa kusema ni jambo la faraja na heshima kwa TUCTA. Nawashukuru Viongozi wa Serikali waliomabatana nawe.

=> kufikiria namna ya kuboresha masirahi ya wafanyakazi, wanasubiri kusikia neno kutoka kwako

=> Nashukuru serikali yako kwa kuwarejesha watumishi wa darasa la saba walioajiriwa Kabla ya Mei 2004. Tunaomba uendelee kuangalia uwezekano wa kuwarejesha na wengine pia. Asante.

13:06HRS

66F767A2-9C94-4E25-AACD-896F4790F99E.jpeg

Rais Magufuli anaongea:
Mei5.jpg

=> Anaanza na Salaamu kwa wote waliohudhuria mabibi na mabwana.

=> Nlitegemea kwakuwa kuna machifu hapa hii mvua ingekua imeacha kunyesha. Naona kweli imeacha kweli kuna amchifu walioiva.

=> Nawashukuru TUCTA kwa kunialika kwenye sikukuu hizi. Natuminia fursa hii kuungana na waliotangulia kutoa pole kwa misiba ya viongozi vyama vya wafanyakazi na wafanyakazi waliotangulia

=> Hii ni mara ya Kwanza kuja Iringa tangu nichaguliwe kuwa rais, nawashukuru kwa kunichagua. Wanairinga sina cha kuwalipa zaidi ya kusema tutashirikiana.

=> 1978 na 1979 nlijiunga na shule ya serikali ya Mkwawa, ukinambia kihesa makanyagio na kila sehemu napafahamu. Najua namna ya kunywa ulanzi na komoni. Asanteni sana kwa kunitunza wana Iringa. Katika maisha yangu siwezi kuwasahau wanairinga.

=> Leo ni siku ya wafanyakazi, napenda kutumia fursa hi kuwapongeza wafanyazi kwa mchango wenu mkubwa kwa mchango wenu wa kuletea nchi yetu maendeleo. Hingereni sana

=> Serikali ya awamu ya tano itaendelea kushughulikia kero zenu na kuberesha masirahi yenu

=>TUCTA imesema haitakuwa tayari kuwatetea wafanyakazi mabazazi yaani wazembe wafitini walevi mafisaidi nk. Nawashukuru. Nidhamu na uwajibikaji ni jambo mihumu.

=> Mtumishi akiwa mvivu na mzembe anakuwa ni mnyonyaji.

=> TUCTA wameomba kero za wafanyazi zishugulikiwe. Hoja zenu zote ni sahihi na serikali inazikubali na itazifanyia kazi.

=> Leo nmeona bango la Walimu linasema wao wanaendelea kuhama bila kulipa pesa. Waziri mkuu anomba ulisimamie hilo. hatuwezi kuwa tunatoa maagizo halafu mtu mwingine aendelee kufanya hivyo.

Tulishatoa maagizo mtu asihamishwe bila kulipwa. Naagiza tena viongozi ndani ya Serikali Wasihamishwe watu bila kulipa hela za uhamisho. NI matumaini yangu sitarudia tena kulizungumzia hili katika maisha yangu

=> Serikali ya awamu ya tano imefanya mambo mengi;

1. Tumefanikiwa kudhibiti mfumko wa bei sasa ni 3.9. hii imekuwa njia nzuri ya kumsaidia mfanyakazi. Tutahakikisha bidhaa muhimu zinapatikana maeneo yote

2. Tunatoa elimu bila malipo kwa mwezi Bil23.8 kila mwezi miaka miwili tumetoa bil 714

3 tumelipa madeni ya mifuko ya jamii. Madeni ya mafao yalifika trilioni 1.6 n tumelipa trilioni 1.4

4. Tumelipa Wazabuni

=> Tunalipa Bil 900 madeni ya nje tunaendela kulipa na kwa miaka miliwi tumelipa zaidi ya trilioni 2.

=> Mishahara tunalipa Bil 564.501 baada ya kutoa wafanyakazi hewa, zamani tulikuwa tunalipa bil 777

=> Tunatekeleza miradi mbalimbali ya Miundombinu kama SGR, Ujenzi wa meli ununuzi wa ndege, ujenzi wa Umeme, ujenzi wa mradi wa Stigler's Gorge.

=> Tumeongeza Mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu, tunajenga bandari ya mtwara, miradi ya maji, ukarabati wa reli, ujenzi wa rada. Kuna miradi mingi inaendelea.

=> Tumebadili taswira ya utumishi wa umma. Watumishi hewa na wenye vyeti feki. Tumeweza kubaki na watumishi wenye sifa

=> Tumeajiri watumishi wapya zaidi ya 18 elfu.

=> Serikali itaendelea kuajiri na kutekeleza promotion za wafanyakazi.

=> Sekta binafsi na zile za umma tumepata Ongezeko la ajira Milioni moja na laki nane na ishirini na sita elfu mia saba arobaini na tatu

=> Viwanda 3,306 vimejengwa Pwani kuna viwanda vipya 80

=>Tumeshalipa malimbikizo kwa watu hamsini na mbili elfu mia nane hamsini na mbili yenye thamani ya Bilioni themanini na sita na miatatu ishirini na tatu

=> Yoyote mwenye madai halali atalipwa haki yake

=> Ukijenga reli utabeba mizingo Mingi na kupata pesa. Ninaamini ukipeleka pesa hospital bil 266 afya zitaimarika.

=> Mradi wa Stigler's Gorge kwa trilion 3 ni muhimu kwani umeme 2100 vutaendesha viwanda vyetu.

=> Watoto wetu Mil 1 hadi Mil 2 wameandikishwa kusoma bure, kwangu mimi ninaliona ni zuri kuliko hizi bil 23 kila mwezi kujiongezea kwenye mishahara.

=> Kwangu mimi naona hizi hela ni bora kuziweka kwenye miradi kuliko kujiongezea mishahara. Mkitaka hii miradi yote tulioianzisha tuifute ife ili tujipandishie mishahara mimi sina tatizo hata tukijilipa milioni mbili mbili. Kupanga ni kuchagua.

=> Tukitekeleza na kukamilisha hii miradi yote mikubwa kwa ukamilifu, haitachukua muda mrefu mishahara yetu bila kuiongeza na hii si lazima mei mosi.

=> Kwa hizi nyuso za furaha mnazonionesha leo, ningekuwa na hela kwenye chungu zimebaki pale leo ningetamka tu. Lakini nikitamka ntazitoa wapi? Nina mpango wa kuajiri wafanyakazi 52 elfu, ntawalipa nini? Dhamira yangu inanituma kwamba kusubiri ni kitu kizuri. Hebu tujenge miundo mbinu na kuajiri hawa 52,000/.

=> Kwa hali ya sasa ni lazima niwaeleze ukweli. Tutaendelea kulipa viporo vya madeni hadi viishe.
May8.jpg

=>Mwaka huu nitaongeza nyongeza ya mshahara ya kila mwaka kama kawaida.

=> Kutakuwa na mifuko miwili ya hifadhi ya jamii. Mmoja wa watumishi wa umma na mwimgine kwa watumishi binafsi.

=> Hii italahisisha kulipa mafao. Mifuko ilikuwa inashindana wenyewe kwa wenyewe.

=> Katika kipindi hiki deni la tril 1.4 tumelipa katika mifuko ya pensheni. Watenda Kaeni ili mifuko hii miwili ianze kufanya kazi.

=> Kuhusu haya Maswala ya masirahi ya wafanayakazi kimsingi yanategemea kiwango cha kipato. Ndama hunyonya kiwango cha maziwa aliyonayo Mama yake.

=> Nimeteua Majaji ambao watapunguza kesi kwenye mahakama ya kazi.

=> Sijasema kila mfanyakazi awe amemaliza kidato cha nne bali kila mtu afanye kazi sehemu inayoendana na elimu yake.

=> Hatupati watalii wengi kwasababu tulikuwa hatuna usafiri wa anga. tumeanza kulifanyia kazi.

=> Mkakati wa kutangaza Vivutio kama Ruaha, Kitulo maua ndwele, Kalambo ya Pili afrika Karenga na Isimili nk yanaendelea.

=> Tumeamua kununua ndege saba na tatu zimeshawasili na nyingine nne zinawasili hapo baadae mwaka huu zikiwemo ndege kubwa mbili. Hii itaimalisha utalii.

=> Mumeshauri kuimalisha sekta ya Elimu. Swala la elimu ni agenda ya serikali ya awamu ya tano. Hili tumeshaanza kulifanyia kazi. Kwenye elimu tumesambaza vifaa vya maabara na kuajiri walimu na tumefunga vyuo visivyo na sifa.

=> Tumepanga kupeleka umeme kwenye vijiji vyote 176 kwenye Mkoa huu. Tumekamilisha hospitali ya Iringa Manispaa, Tutafanyia kazi eneo la Hospitali linaloingiliana na Magereza. Hii Hospitali ni Muhimu sana kwa watu wanaotoka Cairo hadi Afrika kusini wataitumia sana

=> Ntaenda kuweka jiwe la Msingi hospita ya Kiroro.

=> Tumetenga pesa za kujenga barabara kutoka Iringa hadi Msembe Kilometa 104

=> Kwenye Mkoa huu hamlipishwi kodi ya mazao chini ya tani moja, wakina mama machinga tunawatengeneza vitambulisho ili msisumbuliwe.

=> Nawahakikishia wafanyakazi wote serikali yenu inawathamini wala siwezi nikawashahu. Najua mnayoyafanya ayanleta tija. Naomba muamini leo. Msigwa ananichomekea eti Moshi nliahidi. Mini Moshi Sikuahidi ila leo ndo ninaweza kuahidi.

=> Naomba niahidi na mniquote kweli kweli "Kama miradi hii itamalizika vizuri, kama tukiajiri watu elfu hamsini nambilia kuwalipa vizuri, kipindi changu cha urais hakitaisha kabla ya kupandisha mishahara ya wafanayakazi". Kupandisha kwangu hakutakuwa kwa elfu kumi bali kutakuwa kuapndisha kweli kweli. Naomba muiamini Serikali yenu.

=> Nachotaka kuwambia ndugu zangu, nawapenda wafanyakazi. Nlitamani mwaka huu kupandisha, lakini baada ya kuona hizi changamoto tulizonazo nikaona tuzimalize kwanza na kucontrol bei ya bidhaa. Naomba mnielewe ndugu zangu wafanyakazi

=> Nyuso za upendo mlizonionyesha leo zimenigusa sana. Nyinyi ni watoto wa wakulima na wafugaji, nimewafutia tozo zaidi ya 87, ni jambo zuri sana.

=> Nawashukuru vyama vyote vya wafanyakazi kwa maandalizi Mazuri. Nawashukuru sana Wanairinga. Na juzi nlipokelewa na WanaCCM nikajua CCM haijafa Iringa kulikuwa na uongozi mbaya tu. Leo Tungepiga kura hata kama ni Mahiga leo angeshinda Vizuri sana. Wanairinga hawakujua huyu ni wa Muhimu. Mlipomkataa mimi nikamchukua akawa mbunge na Waziri. Anafanya kazi nzuri sana.

=> Siwezi kuisahau iringa, nakumbuka tulikuwa tunaenda pale stand kwa Mbata kusikiliza disco na mengine mengi. Sijui kama bado upo.

=> Mkoa wa Iringa umeshika nafasi ya Pili kwa ugonjwa wa Ukimwi inayoongoza ni Njombe 11%, Iringa maambukizi ni 11.2% katika watu 100 watu 12.2 ni Wagonjwa.

=> Zamani wanairinga walikuwa wanasema "Ukiona nimenyamasa ngusa tu sambi sako mwenyewe|". Sasa hivi ukiangusha ujue kuna ukimwi.

=> Nawashukuru Wana Iringa, Sijawahi kupata makaribisho makubwa namna hii hapa Iringa. Nina deni kubwa, na naomba Mawaziri wanikumbushe katika madeni ya iringa ili niyamalize haraka. Sitawaangusha.

+> Wafanyakazi nawashukuru tena. Tanzania ina changamoto nyingi. tuirinde amani yetu tuuulinde mshikamano wetu. Tusibaguane kwa vyama vyetu, Ndo Mbunge Msigwa kaenda kukaa katikatika ya Wanaccm ili anukie vizuri.

=> Najua baada ya hapa kila mtu ataenda kuongea anayoyajua yeye, ila nawaomba waandishi wa habari waje niwape haya nliyoyasema na kuzungumza ili wasije wakapotosha.

Kuna mama amejitokeza akilia, anasema anaitwa Salima Koli anasemea alishambuliwa mwaka jana na kuuliwa kiumbe chake tumboni na kuharibiwa kizazi. "Mimi hapa nina familia na nina watoto. Nalalamika Mahakama haijanitendea haki. Nilishambuliwa na kijana mmoja. Nmekosa haki ya Kisheria".

=> Rais amemuagiza RPC na mkuu wa Mkoa kwenda kwa mama Kuchukua jina lake na kumsikiliza kisha watampa mrejesho. rais amesema "Yule aliyempiga hata kama alishinda mahakamani, mkamateni mwende kumshitaki tena. Mchunguzeni huyo mama pia kama Kizazi chake kimetolewa". Nawashukuru sana.

1422HRS
8.jpg

Rais Magufuli amemaliza hotuba

=====

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli amesema Serikali ya Awamu ya Tano imefanikiwa kuzalisha ajira 1,826,743 katika kipindi kifupi cha miaka miwili na nusu iliyopita.

Mhe. Rais Magufuli amesema hayo tarehe 01 Mei, 2018 katika sherehe za maadhimisho ya sikukuu ya wafanyakazi (Mei Mosi) zilizofanyika kitaifa katika uwanja wa CCM Samora Mjini Iringa na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa, Mke wa Rais Mhe. Janeth Magufuli, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Job Yastino Ndugai, Naibu Spika Mhe. Dkt. Tulia Ackson, Mawaziri, Makatibu Wakuu, viongozi wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama, Wabunge, Viongozi wa dini na viongozi wa siasa.

Mhe. Rais Magufuli amefafanua kuwa kati ya ajira zilizozalishwa, wafanyakazi 18,101 ni watumishi wa umma wapya walioajiriwa kupitia kada mbalimbali, sekta binafsi imetoa ajira mpya 582,073 na ajira nyingine zimezalishwa kupitia miradi mbalimbali ikiwemo ujenzi wa barabara na madaraja, umeme, ujenzi wa shule na vyuo, afya, viwanja vya ndege, viwanda, kilimo, mifugo na madini.

Aidha Mhe. Rais Magufuli amesema katika kipindi hicho Serikali imewapandisha vyeo wafanyakazi 88,016 na wengine 25,504 watakaopandishwa ifikapo Julai 2018 na ameahidi kuwa Serikali itaendelea kuajiri watumishi wapya na kuwapandisha vyeo wafanyakazi kadri bajeti itakavyoruhusu.

Kuhusu malimbikizo ya madeni ya wafanyakazi Mhe. Rais Magufuli amesema Serikali imeshawalipa wafanyakazi 52,851 waliokuwa wakidai Shilingi Bilioni 220.627 za madeni ya mishahara na yasiyo ya mishahara yaliyolimbikizwa tangu mwaka 2007 na amewahakikishia watumishi wote wanaodai madeni halali kuwa watalipwa fedha zao.

Aidha, Mhe. Rais Magufuli amesema Serikali imeamua kuelekeza fedha nyingi katika kugharamia miradi mikubwa ya maendeleo na amewataka wafanyakazi kuongeza juhudi na maarifa kazini ili kuongeza ufanisi na uzalishaji mali, na pia ameahidi kuwaongeza mshahara kabla kumaliza kipindi chake cha uongozi.

Mhe. Rais Magufuli amemuagiza Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa kuchukua hatua dhidi ya viongozi wanaowahamisha wafanyakazi pasipo kuwalipa stahili zao na ameonya kuwa hatarajii kusisikia mtumishi mwingine amehamishwa bila kulipwa stahili zake.

Mhe. Rais Magufuli pia amemuagiza Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Jenister Mhagama kuhakikisha mifuko ya hifadhi ya jamii iliyounganishwa kutoka 5 na kubaki 2 ambayo ni Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Sekta Binafsi (NSSF), inaanza kufanya kazi haraka.

Kwa wakazi wa Mkoa wa Iringa Mhe. Rais Magufuli amewahakikishia kuwa Serikali anayoiongoza itaendelea kutekeleza miradi mikubwa ya maendeleo ya mkoa huo ikiwemo kuimarisha miundombinu ya utalii, kujenga barabara na kusambaza umeme katika vijiji 179 vilivyobaki.

Katika taarifa yao iliyowasilishwa na Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) Dkt. Yahya Msigwa, wafanyakazi nchini wamempongeza Mhe. Rais Magufuli kwa juhudi zake zikiwemo kubana matumizi yasiyo ya lazima, kuunganisha mifuko ya hifadhi ya jamii, kupigania rasimali za Taifa, kuondoa watumishi hewa, vita dhidi ya rushwa na dawa za kulevya na ujenzi wa miundombinu, na wamemuahidi kumuunga mkono na hawatawatetea wafanyakazi wazembe, wavivu, watovu wa nidhamu, jeuri na wala rushwa

Gerson Msigwa

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU

Iringa

01 Mei, 2018

=====

HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA,

KWENYE SHEREHE ZA SIKUKUU YA WAFANYAKAZI DUNIANI

IRINGA, TAREHE 1 MEI, 2018



Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu

wa Jamhuri Muungano wa Tanzania;



Mheshimiwa Job Ndugai, Spika wa Jamhuri

ya Muungano wa Tanzania;



Ndugu Tumaini Nyamhokya, Rais wa Shirikisho

la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA);



Mheshimiwa Jenista Mhagama, Waziri wa Nchi,

Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi,

Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu;



Waheshimiwa Mawaziri wengine mliopo;

Mheshimiwa Balozi Mhandisi John Kijazi,

Katibu Mkuu Kiongozi;



Mheshimiwa Amina Masenza, Mkuu wa Mkoa wa Iringa pamoja na Wakuu wa Mikoa mingine

mliopo;



Mheshimiwa Aisha Nyerere, Jaji Mfawidhi wa Divisheni ya Kazi ya Mahakama Kuu;



Ndugu Wellington Chibebe, Mkurugenzi wa Shirika la Kazi Duniani (ILO), Ofisi ya Nchi za Afrika Mashariki;



Ndugu Jayne Nyimbo, Mwenyekiti wa Chama

cha Waajiri Tanzania (ATE);



Waheshimiwa Wabunge na Madiwani mliopo;



Waheshimiwa Mabalozi mliopo;



Ndugu Makatibu Wakuu mliopo;



Waheshimiwa Wakuu wa Wilaya mliopo;





Dkt. Yahya Msigwa, Katibu Mkuu wa Shirikisho

la Vyama vya Wafanyakazi (TUCTA);



Viongozi Wengine wa Vyama vya Wafanyakazi mliopo;



Viongozi Wengine wa Serikali mliopo;



Viongozi wa Vyama vya Siasa na Viongozi wa

Dini mliopo;



Ndugu Wafanyakazi Wenzangu;

Wageni Waalikwa wote;

Ndugu Wana-Iringa, Mabibi na Mabwana:

Kwanza kabisa napenda nitumie fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya njema na kutuwezesha kukutana hapa. Namshukuru pia Mheshimiwa Waziri Mhagama pamoja na Viongozi wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi nchini (TUCTA), wakiongozwa na Rais wake, Bwana Nyamhokya, kwa kunialika tena kushiriki kwenye maadhimisho haya ya Siku ya Wafanyakazi Duniani, au Mei Mosi, ambayo mwaka huu kitaifa yanafanyika hapa Iringa. Nawashukuru sana kwa kunialika.



Napenda pia kutumia fursa hii kuungana na wazungumzaji walionitangulia katika kutoa pole nyingi za misiba ya viongozi wa vyama vya wafanyakazi iliyotokea tangu tulipoadhimisha sherehe hizi mwaka jana. Vilevile, nawakumbuka wafanyakazi wote waliotutoka katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita. Tuzidi kuwaombea marehemu wote ili Mwenyezi Mungu azipumzishe roho za marehemu mahali pema peponi. Amina.





Ndugu Wafanyakazi na Ndugu Wananchi;

Hii ni mara yangu ya kwanza kuja Iringa tangu nichaguliwe kuwa Rais wa Awamu ya Tano wa nchi yetu. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kuwashukuru wana-Iringa kutoka dini zote, makabila yote na vyama vyote kwa kunichagua kuwa Rais wenu. Nawashukuru sana wana-Iringa. Sina cha kuwalipa. Ninachowaahidi tu ni kwamba, nitashirikiana na viongozi wenzangu wa Serikali pamoja na wengine mliowachagua, wakiwemo Waheshimiwa Wabunge na Madiwani, katika kuhakikisha kuwa yale yote tuliyowaahidi tunayatekeleza. Na bila shaka, mtakubaliana nami kuwa, baadhi ya mambo tuliyoahidi tumeyatekeleza kwa mafanikio makubwa na mengine tunaendelea kuyatekeleza.



Ndugu Wafanyakazi Wenzangu;

Leo ni Mei Mosi. Ni Siku ya Wafanyakazi. Naamini wengi wetu hapa tunafahamu kwa nini kila mwaka dunia inaadhimisha Siku hii. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kuwapongeza wafanyakazi wote nchini kwa kuadhimisha Siku hii muhimu. Aidha, nawapongezeni kwa mchango wenu mkubwa mnaoutoa katika kuiletea maendeleo nchi yetu. Hongereni sana wafanyakazi wa Tanzania.



Kwa hakika, mnafanya kazi kubwa. Mnastahili pongezi nyingi kwa mchango wenu mkubwa katika kuliletea maendeleo Taifa letu. Nitumie fursa hii, hapa mwanzoni kabisa, kuwahakikishia wafanyakazi wote nchini kuwa Serikali ya Awamu ya Tano inatambua mchango wenu na kuuthamini sana. Tunawapenda sana wafanyakazi. Tupo pamoja nanyi. Tutaendelea kushughulikia kero zenu zinazowakabili na kuboresha mazingira yenu ya kazi.



Ndugu Wafanyakazi Wenzangu,

Hivi punde tumetoka kusikia Risala nzuri ya TUCTA iliyosomwa na Katibu wake Mkuu, Bwana Msigwa. Kupitia Risala hiyo, TUCTA imeipongeza Serikali kwa kuchukua hatua mbalimbali za kuiletea maendeleo nchi yetu na halikadhalika kutatua baadhi ya kero za wafanyakazi nchini. Zaidi ya hapo, TUCTA imeeleza kuwa haitakuwa tayari kuwatetea wafanyakazi “mabazazi”, yaani wazembe, wavivu, watovu wa nidhamu, wajeuri, wala rushwa, mafisadi, wenye majungu, wafitini, walevi na wote wenye kufanana na sifa hizo. Nawashukuru sana TUCTA.



Ndugu zangu, nidhamu na uwajibikaji kwa mfanyakazi ni jambo la msingi sana. Kwenye hotuba yake ya Mei Mosi mwaka 1974, Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alisema, naomba nimnukuu “Mkulima asiyefanya juhudi katika shamba lake wakati wa kilimo anapunguza mapato ya nchi. Lakini angalau yeye anapata adhabu yake: hatopokea malipo yoyote, mazao yakikosekana au kuharibika kwa sababu ya uvivu wake. Kwa mfanyakazi ipo tofauti. Yeye hapati adhabu anayoipata mkulima. Yeye anaweza kuharibu kazi lakini mwisho wa mwezi anaendelea kupata mshahara wake kamili kama kawaida”, mwisho wa kunukuu.



Hii maana yake ni kwamba nidhamu katika kazi kwa mtumishi ni kitu cha muhimu na cha lazima. Mtumishi au mfanyakazi akiwa mzembe na mvivu, anakosa kutoa mchango katika maendeleo ya Taifa, lakini zaidi ya hapo, anakuwa mnyonyaji kupitia mshahara anaopokea. Hivyo basi, narudia tena kuwashukuru na kuwapongeza viongozi wa TUCTA kwa kuiunga mkono Serikali katika kusimamia nidhamu na uwajibikaji kwenye watumishi wa umma.



Ndugu Wafanyakazi Wenzangu,

Sambamba na pongezi walizotoa kwa Serikali na ahadi ya kutotetea ubazazi kwa wafanyakazi, Risala ya TUCTA imewasilisha hoja mbalimbali kwa Serikali. Baadhi ya hoja hizo zinahusu kero za wafanyakazi ambazo wameomba Serikali izishughulikie. Hoja nyingine ni mapendekezo yao kwa Serikali yenye lengo la kuiletea nchi yetu maendeleo zaidi. Kwa ujumla, niseme tu kwamba, hoja zenu zote ni sahihi. Serikali inazikubali na tunazipokea kwa ajili ya kuzifanyia kazi, ikiwa ni pamoja na zile zenye kuhusu Mikataba ya Kimataifa, Fomu za Polisi Na 3 (PF3), ushirikishwaji Wafanyakazi, uboreshaji elimu, masuala ya Walemavu, n.k. Kwa bahati nzuri, watendaji wakuu wa Serikali karibu wote wapo hapa. Naamini wamezisikia, watazichukua na kwenda kuzifanyia kazi. Hata hivyo, pamoja na kwamba tunazichukua hoja zenu zote, naomba mniruhusu na mimi nieleze baadhi ya mambo ambayo Serikali imefanya.







Ndugu Wafanyakazi;

Tangu Serikali ya Awamu ya Tano iingie madarakani imefanya mambo mengi yenye manufaa na faida kwa Wafanyakazi. Baadhi ya mambo hayo ni kama ifuatavyo;

(i) Tumefanikiwa kudhibiti mfumko wa bei za bidhaa muhimu nchini. Mathalan, wakati tunaingia madarakani, mwezi Novemba 2015, mfumko wa bei ulikuwa ni wastani wa asilimia 6.6. Tumefanikiwa kuishusha, na hivi sasa, kwa mujibu wa takwimu za mwezi Machi 2018, mfumko wa bei umefikia asilimia 3.9. Hii imekuwa njia nzuri ya kumsaidia mfanyakazi. Kama mnavyofahamu, unaweza kupandisha mshahara, lakini endapo bei za bidhaa zitapanda kiholela, uongezaji wa mishahara unakuwa hauna maana yoyote ile. Kwa sababu hiyo, Serikali itaendelea kufanya jitihada za kudhibiti mfumko wa bei za bidhaa muhimu zisipande kiholela ili kuwapa unafuu wafanyakazi na wananchi kwa ujumla, lakini pia tutahakikisha kuwa bidhaa zote muhimu, kama vile vyakula, mafuta na dawa zinapatikana maeneo yote na tena kwa urahisi zaidi.

(ii) Tunatoa elimu bure, ambapo kila mwezi tunatoa shilingi bilioni 23.8, sawa na shilingi bilioni 285.6 kwa Mwaka. Katika miaka miwili na nusu zimetolewa takriban shilingi bilioni 714. Elimu bila malipo imewanufaisha hadi wafanyakazi kwa vile watoto wenu nao sasa hawalipishwi ada na michango.
(iii) Tumelipa Madeni ya Mifuko ya Hifadhi za Jamii. Serikali ilikuwa ikidaiwa michango ya wafanyakazi, ambapo tangu mwaka 2013 ilikuwa haijalipwa au kulipwa kidogo. Madai yalifikia shilingi Trilioni 1.6. Lakini mpaka sasa tumelipa shilingi trilioni 1.4.

(iv) Tumelipa madeni ya Wazabuni na Wakandarasi kiasi cha shilingi trilioni 2. Kufuatiwa kulipwa kwa madeni hayo, wazabuni wameendelea kutoa huduma kwenye taasisi zetu. Aidha, wakandarasi wameendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo iliyokuwa imekwama; na kukamilika kwa miradi hiyo kumeleta na kutazidi kuleta manufaa kwa wafanyakazi.

(v) Madeni ya Ndani na Nje tunalipa kila mwezi takribani shilingi bilioni 900. Kwa miaka miwili na nusu tumelipa shilingi trilioni 2.7

(vi) Mishahara kila mwezi zinalipwa shilingi bilioni 564.501 baada ya kutoa Watumishi hewa. Awali tulikua tukilipa shilingi bilioni 777. Hii maana yake kwa mwaka tunalipa shilingi trilioni 6.77 na kwa miaka miwili na nusu tumelipa shilingi trilioni 16.935. Na bila shaka, mtakubaliana nami kuwa, siku hizi mishahara inalipwa kwa wakati.

(vii) Tunatekeleza miradi mbalimbali ya miundombinu na kuboresha huduma za jamii, ambapo kukamilika kwake kutaleta manufaa kwa nchi yetu, ikiwa ni pamoja na kwenu wafanyakazi. Miradi hiyo ni ujenzi wa SGR kutoka Dar es Salaam hadi Dodoma unaotarajiwa kugharimu kiasi cha shilingi trilioni 7.06 na hadi sasa tumelipa shilingi trilioni 1.1. Miradi mingine mikubwa ni mradi wa kuzalisha umeme wa Stiglier’s Gorge; ununuzi wa ndege; ujenzi wa barabara na madaraja; miradi ya umeme; viwanja vya ndege; ujenzi wa meli; ujenzi wa miundombinu ya afya na elimu; mikopo elimu ya juu, ambapo mwaka huu wa fedha tunatumia shilingi bilioni 483; ujenzi wa Bandari kubwa Dar es salaam, Mtwara na Tanga (shilingi trilioni 1.1); miradi ya maji (takriban shilingi bilioni 600); ukarabati wa Reli ya Kati na Reli kutoka Tanga na Arusha; ujenzi wa Rada Dar es salaam, Mwanza, Songwe na Kilimanjaro; kusambaza vifaa vya maabara kwenye shule 1,696, n.k. Aidha, kuna miradi mingine mingi inayoendelea ikiwa ni pamoja na mradi wa Bomba la Mafuta; miradi ya kilimo, uvuvi na ufugaji. Miradi na shughuli zote hizi zinaigharimu Serikali fedha nyingi .



Sambamba na hayo, tangu tumeingia madarakani mwaka 2015, tumepata mafanikio makubwa katika kubadilisha taswira ya Utumishi wa Umma. Tulianza na zoezi la kuhakiki Watumishi wa Umma ili kuhakikisha kwamba Watumishi wa Umma wanakuwa wale wenye sifa stahiki. Tumefanikiwa kuondoa Watumishi hewa 19,708 na watumishi wenye vyeti feki 14,152. Haya ni mafanikio makubwa ambayo yametuwezesha kuokoa mabilioni ya shilingi, lakini pia tumeweza kubaki na watumishi wenye sifa ya kufanya kazi. Mazoezi haya mawili yamekamilika mwezi Oktoba mwaka 2017.



Kukamilisha kwa mazoezi hayo ya uhakiki, yametufanya tuanze kuajiri watumishi wapya. Mpaka sasa tumeajiri watumishi wapya 18,101 (walimu 6,495, watumishi wa afya 3752, watumishi wa Mambo ya Ndani 6164, Mahakama watumishi 200, Mafundi Sanifu wa Maabara 386, na watumishi wengine) na tunatarajia kuajiri watumishi wengine 22,150 kabla ya kumalizika kwa mwaka huu wa fedha. Aidha, tumeweza pia kuwapandisha madaraja (promotion) watumishi 88,016 mpaka hivi sasa. Tunategemea kukamilisha promosheni nyingine 25,504 kabla ya kumalizika kwa Mwaka huu wa Fedha. Hivyo, jumla, tutakuwa tumetoa promosheni 113,520 kabla ya mwezi Julai, mwaka huu 2018. Napenda kuwahakikishia kwamba Serikali itaendelea kuajiri watumishi wapya na kuwapandisha madaraja kadri bajeti inavyoruhusu.



Ndugu Wafanyakazi;

Ndugu Wafanyakazi;

Kama mnavyojua, tofauti na ilivyokuwa zamani, siku hizi Serikali siyo mwajiri mkubwa. Sekta Binafsi ndiyo mwajiri mkubwa. Na katika hili, napenda kuipongeza sekta binafsi ya hapa nchini kwa kuendelea kutoa fursa nyingi za ajira kwa Watanzania. Wakati Serikali ya Awamu ya Tano inaingia madarakani, Sekta Binafsi ilikuwa na watumishi 2,334,969. Katika miaka miwili na nusu iliyopita, ajira hizo zilizoongezeka hadi kufikia 582,073, ambayo ni sawa na ongezeko la asilimia 24.9. Hili ni ongezeko kubwa la ajira.



Aidha, tukijumlisha na ajira za sekta isiyo rasmi, ajira zilizoongezeka zimefikia 1,826,743. Ongezeko hili ni kutokana na miradi mingi inayoendelea kutekelezwa, hususan kwenye miundombinu ya barabara, madaraja, reli, viwanja vya ndege na rada, bandari, miradi ya umeme, ujenzi wa shule na vyuo, miradi ya afya, miradi ya maji, viwanda, miradi ya gesi, pamoja na miradi katika sekta za kilimo, mifugo, uvuvi, madini na utalii, n.k. Haya ni mafanikio ya kujivunia ya Serikali ya Awamu ya Tano.



Tunaendelea kuboresha mazingira ya sekta binafsi ili izidi kustawi nchini na kutoa ajira nyingi kwa Watanzania. Kama mnavyojua, dhamira yetu ya Tanzania ya viwanda inaendelea kushika kasi. Viwanda vingi vimeanzishwa nchini na vinaendelea kuanzishwa. Kwa mujibu wa matokeo ya sensa ya viwanda iliyotolewa mwezi Juni 2017, viwanda vipya 3,306 vimejengwa, vikiwemo viwanda vya kati na vikubwa; na vingine vingi vinaendelea kujengwa. Katika Mkoa wa Pwani pekee, zaidi ya viwanda vikubwa 80 vinaendelea kujengwa hivi sasa. Hivi vyote maana yake ni ajira mpya kwa Watanzania.



Ndugu Wafanyakazi;

Kukamilika kwa mazoezi ya uhakiki pia kumeiwezesha Serikali kuanza kulipa malimbikizo ya madeni ya watumishi. Mpaka hivi sasa, tumeshalipa malimbikizo ya madeni ya mishahara ya watumishi 52,851 yenye thamani ya shilingi bilioni 68.323. Aidha, tumelipa madeni yasiyo ya mishahara yeye thamani ya shilingi bilioni 152.304. Hii imefanya jumla ya madeni yote ya watumishi tuliyolipa kufikia shilingi bilioni 220.627, ambapo mengi yalikuwa hayajalipwa tangu mwaka 2007.



Wizara ya Fedha kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma wanaendelea kuhakiki na kulipa madeni yaliyosalia kila mwezi. Napenda kuwahakikishia Watumishi wa Umma wote kwamba, yeyote mwenye madai halali atalipwa haki yake. Lakini mwenye madai ya uongo, hatolipwa kamwe.



Ndugu Wafanyakazi;

Kama nilivyosema, Serikali imefanya mambo mengi. Tumetoa ajira, tumelipa madeni yote niliyotaja; tunatoa elimu bure; tunatekeleza miradi mikubwa ya Reli, Bandari, Barabara, Maji, Umeme, Afya. Masuala haya yote yanategemea fedha kutoka mfuko mmoja tu. Sio rahisi kufanya mambo hayo yote, na pia kuweza kupandisha mishahara. Msema kweli ni mpenzi wa Mungu. Ni lazima tuchague. Na mimi kwa mtazamano wangu, nilidhani tuanze kwanza kutekeleza miradi hii mikubwa ya maendeleo ambayo itakapomalizika itatupatia fedha nyingi za kuweza kuongeza mishahara na kufanya mambo mengine ya maendeleo.



Kwa mfano, mimi naamini, tukijenga reli na ikianza kufanya kazi ya kubeba mizigo kwenda nchi za Burundi, Rwanda na pia kuhudumia nchi za DRC na Uganda, itatupatia fedha nyingi za kuweza kupandisha mishahara. Vivyo hivyo, tuktekeleza miradi ya barabara na umeme, tutapata fedha nyingi za kuweza kuongeza mishahara. Tukiongeza bajeti ya afya, wananchi watakuwa na afya njema na hivyo kuweza kushiriki kwenye shughuli mbalimbali za maendeleo. Kwangu mimi naona mambo hayo ni ya msingi zaidi kwa sasa kuliko kupeleka fedha mahali kwingine.



Nchi yetu imeazimia kujenga uchumi wa viwanda, lakini umeme tulionao ni takriban Megawati 1,500. Hivyo, kwangu mimi naona kutekeleza Mradi wa Umeme wa Stiglier’s Gorge utakaogharimu takriban shilingi trilioni 3 kuzalisha Megawati 2,100 ni muhimu zaidi kwa sasa kuliko kupeleka fedha hizo mahali kwingine. Kwangu mimi naona ni busara kutoa fedha za kujenga barabara za kuunganisha Mkoa wa Iringa na mikoa mingine pamoja na kujenga Uwanja wa Ndege wa Nduli ili utuletee watalii wengi, hususan katika kipindi hiki ambacho tumeamua kuifanya Iringa kuwa kitovu cha utalii kwenye Ukanda huu wa Kusini, kuliko fedha hizo kuzipeleka mahali kwingine. Kwangu mimi naona ni jambo jema kutoa fedha takriban shilingi bilioni 23.8 kwa mwezi kugharamia elimu bure ili watoto wengi wa maskini wapate elimu, kuliko kutumia fedha hizo kulipana mishahara. Kwangu mimi pia naona ni vizuri kutoa shilingi bilioni 483 kuwakopesha watoto wa maskini ili waweze kwenda kwenye Vyuo Vikuu, kuliko kutumia fedha hizo kujiongezea mishahara. Kupanga ni kuchagua.



Lakini, mbali na miradi hiyo ya maendeleo, nawaomba wafanyakazi mkumbuke kuwa, kwenye nchi yetu wapo pia wakulima, wafugaji na wavuvi, ambao nao wanahitaji maisha yaliyo bora. Hivyo, wakati tunajifikiria sisi, na wao pia tuwafikirie.



Pamoja na ukweli huo, matumaini bado yapo. Napenda nitumie fursa hii kuwahakikishia Wafanyakazi kuwa, baada ya kukamilisha mazoezi ya kuhakiki na kuanza kuajiri watumishi wapya, jambo kubwa ambalo sasa ni kipaumbele changu kwa watumishi wa umma ni kuboresha mishahara na maslahi mengine ya wafanyakazi. Nafarijika sana kwamba sasa tumeanza kukaa kwenye mstari, nidhamu imerejea, uadilifu unazidi kujengeka, mnafanya kazi kwa uzalendo na weledi, isipokuwa wachache ambao tutazidi kuwachukulia hatua stahiki. Tunaendelea kukamilisha ulipaji wa madeni ya watumishi. Lakini mwaka huu pia tutaendelea kutoa nyongeza ya mwaka ya mishahara (Annual increment). Naomba mniamini.



Ni bahati mbaya tu Katibu Mkuu wa TUCTA amenichomekea kuwa kwenye Sherehe za Mei Mosi mwaka jana niliahidi kupandisha mishahara. Hiyo sio kweli. Mwaka jana sikuahidi kupandisha mishahara. Na hotuba yangu ipo. Hata hivyo, leo ndio naweza kuahidi. Kama miradi hii itaenda vizuri, kama wafanyakazi mtaendelea kujituma na kuchapaka kazi kama mnavyofanya sasa, na kama Vyama vya Wafanyakazi vitaendelea kutoa ushirikiano wa kutosha kwa Serikali kama sasa, nawaahidi, na naomba mninukuu vizuri kuwa, kabla sijamaliza muhula wangu wa uongozi nitapandisha mshahara. Na nitakapopandisha, itakuwa kiwango kikubwa. Sio shilingi elfu 10. Narudia tena. Naomba wafanyakazi mniamini. Mimi ni mfanyakazi mwenzenu. Nilikuwa Mwalimu. Ninafahamu shida za wafanyakazi na kwa kweli ninawapenda sana wafanyakazi wenzangu. Kama ingekuwa inawezekana hata leo ningepandisha. Hata hivyo hali kwa sasa hairuhusu. Hivyo, narudia tena kuwasihi muwe wavumilivu na kuendelea kuchapa kazi kwa bidii ili tuweze kukuza uchumi wetu na hatimaye tutengeneze maisha bora ya baadaye. Mimi naamini kuwa miradi ya maendeleo tunayoitekeleza itakapokamilika, haitachukua muda mrefu kupandisha mishahara. Hata hivyo, kwa sasa, tutaendelea kuweka mkazo mkubwa katika kudhibiti mfumko wa bei.



Ndugu Wafanyakazi;

Mwaka jana katika risala yenu mliomba zoezi la kuunganisha mifuko likamilike mapema. Napenda kuwafahamisha kwamba zoezi hilo limekamilika baada ya Bunge kupitisha Sheria tarehe 31/01/2018 na mimi kuisaini tarehe 08/02/2018. Kilichobaki sasa ni kuanza kutumika kwa Sheria hiyo ambapo kutakuwa na mifuko miwili. Mfumko mmoja wa Watumishi wa Umma na mwingine kwa ajili ya Sekta Binafsi. Sheria iliyotungwa mbali na kuanzisha Mfuko wa Hifadhi ya Watumishi wa Umma (PSSSF) imefanya marekebisho katika Sheria ya Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (The National Social Security Fund Act) Sura ya 50 ili kuifanya NSSF kuhudumia Watumishi wa Sekta Binafsi wakiwemo Wakulima, Wafugaji, Wavuvi, Wajasiriamali wadogo (machinga na mama lishe).



Uunganishaji wa mifuko hii, unategemewa kurahisisha ulipaji wa mafao, kupunguza gharama za uendeshaji wa mifuko na hivyo kuboresha mafao ya wanachama. Katika kipindi hiki pia, kama nilivyoeleza hapo awali, tumeweza kulipa deni la shilingi trilioni 1.4 ya malimbikizo ya michango ya wanachama kwenye mifuko ya pensheni. Malipo haya yamewezesha wastaafu kuendelea kulipwa mafao yao kama wanavyostahili. Napenda kutumia fursa hii kuziagiza Mamlaka husika kukamilisha kwa haraka taratibu husika ili Mifuko hii ianze kazi mara moja; maana naanza kuona dalili za kuwepo kwa kigugumizi na kusuasua katika kukamilisha taratibu za kuanzisha Mifuko hiyo.



Ndugu Wafanyakazi,

Risala yenu pia imegusia suala la makato ya kodi ya mshahara (Pay As You Earn – PAYE); viwango vya mishahara, hususan ya kima cha chini; na vikao vya Bodi za Kima cha Chini cha Mishahara, Bodi za Mishahara pamoja na Chombo cha Ushauri (Labour Economic and Social Council – LESCO). Kuhusu suala hili, napenda kwanza niseme kuwa masuala haya ya maslahi kimsingi yanategemea pia uwezo wa kifedha wa Serikali. Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere aliwahi kusema ‘A calf can only suck the amount of milk her mother cow produces (yaani, ndama hunyonya kulingana na kiwango cha maziwa aliyonayo mama yake)”.



Lakini, pamoja na ukweli huo, Serikali kwa kile kidogo ilichonacho, imekuwa ikijitahidi sana kuboresha maslahi ya watumishi wake. Mathalan, kuhusu suala la PAYE, mwaka juzi tulipunguza kwa asilimia 2 kodi ya mshahara kutoka asilimia 11 hadi asilimia 9. Hii ilitufanya tufanikiwe kufikia malengo tuliyokubaliana (kati ya Serikali na Vyama vya Wafanyakazi) ya kuwa na kiwango cha tarakimu moja (single digit), miaka miwili kabla ya muda uliotakiwa.









Ndugu Wafanyakazi;

Kuhusu suala la ucheleweshaji wa kesi za Mahakama Kuu Kitengo cha Kazi, kama mlivyosikia hivi karibuni nimeteua Majaji 12 wa Mahakama Kuu. Hivyo basi, ni imani yangu kuwa uteuzi huo utapunguza tatizo lililokuwepo la uhaba wa majaji na hivyo kusaidia kupunguza kero ya ucheleweshaji wa kesi kwenye Mahakama Kuu Kitengo cha kazi.



Kuhusu suala la Watumishi wenye Vyeti vya Darasa la Saba, napenda tu niwakumbushe kuwa uamuzi wa Serikali kuendesha zoezi la ukaguzi wa vyeti ulilenga kulinda hadhi ya elimu nchini lakini pia kuamsha ari ya utendaji kazi kwa watumishi wenye sifa. Ni bahati mbaya tu katika kutekeleza zoezi hilo, yalitokea mapungufu. Lakini bahati nzuri, Serikali iliona mapungufu hayo, na kama mlivyosikia Waziri mwenye dhamana tayari ametoa msimamo wa Serikali Bungeni hivi majuzi. Kilichobaki sasa ni utekelezaji. Lakini, endapo bado mfanyakazi ataona ameonewa, namshauri afuate taratibu. Kama ambavyo nimekuwa nikisema, Serikali hii inawapenda wafanyakazi. Hatutaki kumwonea mfanyakazi yoyote. Hatutaki kuona mfanyakazi akinyanyasika. Na katika hili, napenda kurudia, kwa mara ya mwisho, agizo langu kuhusu kutomwamisha mtumishi kabla ya kumlipa fedha zake. Sitarudia tena kusema hili. Atakiuka agizo hili, hatutasita kumshughulikia. Na naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu kulisimamia hilo.







Ndugu Wafanyakazi Wenzangu,

Kama nilivyosema, mbali na hoja hizo zilizohusu kero za wafanyakazi, Risala ya TUCTA pia imetoa mapendekezo na ushauri mbalimbali kwa Serikali kwa lengo la kuiletea nchi yetu maendeleo. Pendekezo lenu la kwanza linahusu umuhimu wa kutangaza vivutio vya utalii. Risala imeeleza kuwa Tanzania inashika nafasi ya pili kwa vivutio vya utalii duniani baada ya Brazil. Licha ya ukweli huo, idadi ya watalii wanaotembelea nchi yetu ni ndogo. Mmetaja sababu mojawapo yenye kusababisha hali hii kuwa ni kushindwa kwetu kutangaza vivutio vyetu. Hilo ni kweli kabisa. Lakini naomba niongeze sababu nyingine. Hatupati watalii wengi kwa vile, kwa muda mrefu, sekta ya usafiri wa anga nchini ilikuwa hoi bin taabani. Na kama mnavyofahamu, asilimia 70 ya watalii hutumia usafiri wa anga.



Kwa kutambua hilo, tumeanza kuchukua hatua za kutangaza vivutio vyetu mbalimbali na kuimarisha usafiri wa anga. Ninyi wana-Iringa mnafahamu vizuri. Mwezi Februari 2018, Mheshimiwa Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan, alizindua mpango kabambe wa kutangaza vivutio vya Ukanda huu wa Kusini ujulikanao kwa jina la Resilient Natural Resorce for Tourism and Growth (REGROW), ambapo takriban Dola za Marekani milioni 150, ambazo ni sawa na takriban shilingi bilioni 330 zitatumika. Kama mnavyofahamu, Ukanda huu wa Kusini, kama ulivyo Ukanda wa Kaskazini, una vivutio vingi, ikiwemo Hifadhi ya Ruaha yenye kusifika kuwa na tembo wengi, Hifadhi ya Kitulo, au maarufu kama Bustani ya Mungu, ambayo ina maua ndwele ambayo hayapatikani mahali popote duniani, Maporomoko ya Kalambo ambayo ni ya pili Barani Afrika, maeneo ya kihistoria ya Kalenga na Isimila, n.k.



Sambamba na mkakati huo wa kutangaza vivutio, kama nilivyosema awali, tunaimarisha pia usafiri wa anga. Hivi sasa, tunajenga viwanja takriban 11 vya ndege kikiwemo kiwanja cha hapa Iringa, ambacho ujenzi wake utagharimu zaidi ya shilingi bilioni 90. Tumenunua pia ndege mpya 7, tatu tayari zimewasili na zimeanza kufanya kazi, na nyingi nne zinatarajiwa kuwasili baadaye mwaka huu, zikiwemo ndege kubwa mbili aina ya Boieng Dreamliner zenye uwezo wa kubeba watu 264. Tuna matumaini makubwa kuwa kutokana na hatua hizi, watalii wengi watatembelea nchi yetu na mchango wa sekta ya utalii, ambayo hivi sasa inaongoza kwa kuipatia fedha nyingi za kigeni nchi yetu, itazidi kuimarika.



Ndugu Wafanyakazi;

Kwenye Risala yenu pia mmegusia umuhimu wa kuwaelimisha wananchi kuhusu viwanda pamoja na kuwekeza kwenye miundombinu wezeshi. Serikali imekuwa ikijitahidi sana kuwaelimisha wananchi kuhusu umuhimu wa viwanda na aina ya viwanda tunavyovitaka.



Kwa kifupi napenda kusema kuwa viwanda vina faida nyingi, ajira, mapato; n.k. Na kuhusu aina ya viwanda tunavyovilenga ni vile vyenye kuajiri watu wengi; vyenye kutumia malighafi zinazopatikana kwa wingi nchini; vyenye kutumia teknolojia ya kati; na ambavyo bidhaa zake zinahitajika kwa wingi hapa nchini lakini pia zinaweza kuuzwa nje ya nchi. Aina hizi za viwanda ni kama vile vya nguo, bidhaa za ngozi pamoja, usindikaji mazao ya kilimo, n.k. Kwa bahati nzuri, wana- Iringa ni wakulima wazuri wa mazao mbalimbali, hivyo wanayo nafasi kubwa katika kujenga Uchumi wa Viwanda nchini.



Ndugu Wafanyakazi;

Risala yenu pia imetoa ushauri kwa Serikali kuimarisha sekta ya elimu, hususan kuliangalia kwa makini suala la tofauti kubwa kati ya wavulana na wasichana kwenye taasisi za elimu; na halikadhali kusimamia suala la ubora wa elimu inayotolewa. Niseme tu kwamba suala la elimu ni ajenda muhimu ya Serikali ya Awamu ya Tano. Tangu tumeingia madarakani tumechukua hatua mbalimbali za kuboresha na kuimarisha sekta hii nyeti na muhimu kwa maendeleo ya nchi. Hatua hizo tayari nimezieleza hapo awali. Elimu bure, nyongeza kubwa ya bajeti ya mikopo ya wanafunzi wa vyuo vikuu kutoka shilingi bilioni 365 mwaka 2015/2016 hadi kufikia shillingi bilioni 427 Mwaka huu wa Fedha, ujenzi wa miundombinu mbalimbali ya elimu (shuleni, vyuoni na kwenye vyuo vikuu). Haya yote yamewezekana kufuatia uamuzi wa Serikali kuongeza bajeti ya elimu. Mwaka 2016/2017 tulitenga shilingi trilioni 1.36 na Mwaka huu wa Fedha shilingi trilioni 1.4. Hivyo basi, niwaombe wazazi kote nchini, kuwahimiza watoto wao, wa kike na wa kiume, kutumia fursa hiyo iliyotolewa na Serikali.



Kwa upande wa kuboresha elimu yenyewe, Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali. Mathalan, kwenye shule za sekondari tumesambaza vifaa vya maabara kwenye shule takriban 1,696. Tumewaajiri mafundi sanifu wa maabara wapatao 386. Aidha, katika Mwaka huu wa Fedha, mpaka sasa, tumewaajiri walimu takribani 6,500 wa shule za msingi na sekondari, wakiwemo walimu 3,728 wa masomo ya sayansi na hisabati. Kwa upande wa elimu ya juu, bila shaka, mlisikia hatua tuilizochukua za kufungia baadhi ya vyuo kudahili wanafunzi au kutodahili wanafunzi kwenye baadhi ya fani, baada ya kujiridhisha kuwa havina sifa. Tulifanya hivyo ili kuhakikisha tunalinda ubora wa elimu inayotolewa hapa nchini.



Ndugu Wafanyakazi Wenzangu,

Nimezungumza mengi sana. Na leo ni Siku ya Wafanyakazi. Hata hivyo, kama nilivyosema mwanzoni, leo ni mara yangu ya kwanza kufika Iringa tangu niingie madarakani. Kwa sababu hiyo, kabla sijahitimisha hotuba yangu, naomba kwa haraka haraka mniruhusu niseme mambo machache yenye kuhusu Mkoa huu wa Iringa. Tayari nimeeleza kuhusu Uwanja wa Ndege wa Nduli, tumepanga kupeleka umeme kwenye vijiji vyote 179 vya Mkoa huu ambavyo havina umeme kupitia REA Awamu ya Tatu.



Sambamba na hayo, tunaendelea kuboresha huduma za afya. Hivi sasa tunafanya ukarabati wa Hospitali ya Mkoa, na napenda kuwaahidi hata mgogoro wa kiwanja wa Hospitali hiyo, nao tutaushughulikia. Tumekamilisha upanuzi wa Hospitali ya Wilaya ya Iringa Manispaa, na hivi sasa tupo kwenye upanuzi wa Hospitali ya Wilaya ya Halmashauri ya Mafinga. Na kesho naenda kuweka Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Wilaya Kilolo. Tunafanya ukarabati na upanuzi wa vituo vya Idodi (Iringa Vijijini); Kidabaga (Kilolo); Ihongole (Mafinga) na Malangali (Mufindi). Haya yote yamewazekana kutokana na Serikali kuongeza bajeti za Wizara ya Afya. Mwaka wa Fedha 2016/2017 tulitenga shilingi trilioni 1.8 na Mwaka huu wa Fedha (2017/2018) shilingi trilioni 2.2.



Kuhusu maji, nafahamu kuwa kuna Wilaya tatu za Mkoa huu zenye kukabiliwa na shida kubwa ya uhaba wa maji, ambazo ni Kilolo, Ilula na Mafinga. Lakini nafahamu pia kuwa hivi sasa kuna takriban miradi 14 yenye thamani ya shilingi bilioni 18.24 inayotekelezwa kwenye Mkoa huu. Aidha, wadau wa maendeleo wanatekeleza miradi mingine 10 kwa thamani ya shilingi bilioni 3.512. Kwenye barabara, TANROADS ilitengewa kiasi cha shilingi bilioni 17.948 kwa ajili ya kuhudumia barabara zake; na TARURA imetengewa shilingi bilioni 9.657 kwa ajili ya kuhudumia barabara zake. Vilevile, tupo mbioni kuanza ujenzi wa barabara ya lami kutoka Iringa mjini hadi Msembe katika Wilaya hii ya Iringa Vijijini yenye urefu wa kilometa 104, ambayo Mheshimiwa Waziri Mahiga ameilezea vizuri.



Mabibi na Mabwana; nafahamu ninyi wana-Iringa ni wakulima wazuri wa mazao mbalimbali. Mwezi Julai mwaka jana Serikali ilifuta tozo 87 za kilimo ili kuwapunguzia wakulima kero ya utitiri wa kodi. Aidha, tulipiga marufuku utozaji kodi wa mazao yanayosafirishwa kutoka Halmashauri moja kwenda nyingine, ambayo hayazidi tani moja. Ni matumaini yangu kuwa kwenye halmashauri hii hamlipishwi ushuru. Kwa marafiki zangu, Wamachinga na Mama Nitilie, Serikali imeanza kuwarasimisha wajasiliamali wadogo kwa kuwapatia vitambulisho maalum, ambavyo mtavilipia kwa kiasi kidogo. Lengo la kuanzisha vitambulisho hivyo ni kuwawezesha kufanya shughuli zenu bila kubughuziwa lakini pia kuchangia maendelea ya nchi yetu.



Ndugu Wafanyakazi wenzangu;

Napenda kuhitimisha kwa kurudia tena kuwashukuru kwa kunialika. Napenda niwahakikishie wafanyakazi kote nchini kuwa Serikali yenu inawathamini sana. Nawaahidi tutaendelea kuboresha mazingira yenu ya kufanyia pamoja na maslahi yenu, kadri uwezo wa kufanya hivyo utakavyokuwa ukiongezeka. Napenda niwapongeze Chama Cha Wafanyakazi wa Viwanda, Biashara, Taasisi za Fedha, Huduma na Ushauri (TUICO) kwa maandalizi mazuri ya shughuli hii. Nawapongeza pia waandamanaji kwa namna mlivyopendeza. Kwa hakika, shughuli zimefana sana.



Napenda pia kuwashukuru wageni wote waalikwa, wakiwemo Mabalozi, kwa kushiriki kwenye Siku hii muhimu. Mwisho lakini sio kwa umuhimu, napenda kuwashukuru wana-Iringa, mkiongozwa na Mkuu wenu wa Mkoa, Mheshimiwa Amina Masenza, Wakuu wa Wilaya pamoja na wana-CCM kwa mapokezi yenu mazuri. Napenda niwahakikishie kuwa yale yote tuliyoahidi, tutayatekeleza. Niwaombe tu tuendelee kudumisha amani na umoja wetu.



Mwisho kabisa, ni kuhusu suala la UKIMWI. Kwa mujibu wa matokeo ya utafiti uliotajwa na ofisi yetu ya Taifa ya Takwimu inaonesha kuwa Mkoa wa Iringa umeshika nafasi ya pili baada ya Njombe. Hapa maambukizi ni asilimia 11.2 wakati Njombe ni asilimia 11.6. Hii inatisha. Hivyo, nawaomba wana – Iringa kuchukua tahadhari dhidi ya ugonjwa huu hatari. UKIMWI bado ni tishio.





Mungu Wabariki Wafanyakazi wa Tanzania!

Mungu Ibariki Tanzania!

“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”
 
Tukutane hapa kwa updates zaidi.

Matarajio ya wafanyakazi.

1. Toka aingie madarakani hajawai kupandisha mishahara wafanyakazi.

2. Alipunguza 1% ya kodi iliyojificha na hajawai kuwa na impact kwa watumishi

3. Katika ukanda wa afrika mashariki na kusini mwa jangwa la sahara ndio mfanyakazi anakatwa kodi kubwa kuliko mtu yoyote.

4. Hajaajiri katika awamu yake kama ilivyokuwa kwa awamu zilizo pita. Na tukumbuke bajeti inayopitishwa bungeni hakuna kipengere cha ajira mpya na bajeti karibia zote zimepunguzw kwa 10-40%. Hivyo hakuna bajeti ya waajiriwa wapya.

6. Ajira za walimu ni changa la macho kwa sababu bajeti ya sasa imeongezwa kwa 5% tuuu, kwa lile la kusema serikali hii inaboresha elimu ni ndoto za mhana.
7. Bajeti kubwa kuliko zote ni usafiri yaani kuknunua ndege hata afya imekatwa kwa 20% sijajua hao wanaotakiwa kupanda ndege na treni sio watanzania au maana wagonjwa watapanda treni kwenda india kutibiwa? Au ndege zinafika india?

Utamsikia tunajenga sgr na umeme wa maji, siwezi kuongeza mishahara asiyetaka kazi aondoke kuna watu wengi mtaani wanahitaji kuajiriwa
 
Akija hapo mwambie waajiliwa wengi kwenye baadhi ya wilaya hapa nchini hawajalipwa staiki zao km fedha za kujikimu,likizo,kupandishwa madaraja na uhamisho.
 
Leo atapandisha mishahara ya Policcm tu! Wafanyakazi wengine hawajawahi kuwa na maana yoyote kwake!
 
Back
Top Bottom