nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
• ADAI AMECHOSHWA NA KUNYANYASWA WAPIGA KURA WAKE
na Mustapha Kapalata, Nzega
MBUNGE wa jimbo la Nzega Dk. Hamis Andrea Kigwangalla (CCM), ametishia kujiuzulu ubunge endapo serikali ya chama chake itashindwa kutenda haki kwa wananchi wake.
Mbunge huyo alitoa tishio hilo juzi mara baada ya kufikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi wilaya ya Nzega, akikabiliwa na tuhuma za makosa sita, likiwemo la kuvamia Kituo cha Polisi cha wilaya ya Nzega.
Kigwangalla, akiwa na watuhumiwa wenzake watatu, alisema kama suala lake halitafanyiwa uchunguzi na kupata suluhu pamoja na kuangalia haki kwa pande mbili za walalamikaji, atafanya maamuzi mazito.
Alisema hawezi kuendelea kuwa mbunge huku akishuhudia wananchi wake wakinyanyaswa na kunyimwa haki zao na serikali iliyo madarakani kwani mgogoro huo unajulikana hadi ngazi ya juu.
"Kama serikali isipoingilia na kutenda haki kwa wananchi wa Isunga, Ngwanda, Mwabangu na kwa mbunge wao na watu wengine ambao wameshtakiwa bila utaratibu, mimi naweza kuchukua hatua kali zaidi na hata kujivua ubunge kwa sababu siamini katika dhana ya kufanya kazi ya kuwawakilisha wananchi ya kufanya kazi katika mazingira ya dhuruma, unyanyasaji na ukandamizaji usio na maana.
"Bahati nzuri mimi ni mbunge wa CCM na kama Serikali ya CCM ni sikivu, basi leo isikie kilio changu na ifanye maamuzi. Yaliyonikuta na yaliyonitokea ni mazito na siwezi kuvumilia. Mimi kama mimi, nitaamua kujitoa ubunge na pengine kutokugombea nafasi yoyote ile ya uongozi ndani ya chama," alisema Dk. Kigwangalla.
Mbali ya kutishia kujivua ubunge, mbunge huyo pia alifikia hatua ya kusema kwamba yuko tayari kufa kutetea haki ya wananchi wake dhidi ya manyanyaso ya serikali ya CCM.
Wengine wanaoshtakiwa na mbunge huyo ni Mrisho Hamis, Mathew Dotto na Mwanja Mwandu ambao wote kwa pamoja wanadaiwa kuhamasisha wanakijiji wa Mwabangu kuvamia kituo cha polisi kupinga manyanyaso dhidi ya wachimbaji wadogo wa madini.