Maswali kwa Anne Makinda

Ochu

JF-Expert Member
May 13, 2008
975
47
Maswali kwa Anne Makinda

ban.blank.jpg


Juvenalis Ngowi​
amka2.gif
KIONAMBALI alikwisha kufunga makabrasha yake yanayohusiana na hoja inayokera masikioni mwa wengi. Hii ni hili dude linalooitwa “posho za wabunge”. Kama ni santuri hii sasa imechuja na inatoa kinyaa kuisikiliza kila siku. Lakini kwa aliyoyasema Mama Makinda, wacha tu niendelee kubaki hapa kwenye hili jambo tena leo.
Kwa ambao hawakubahatika kumsikia Spika wa Bunge Mama Anne Makinda, ni kwamba akiwa kwenye mkutano huko jimboni kwake aliibuka alikotokea na hoja ya posho za wabunge. Akasikika akizungumza kwa uchungu na akafikia hatua ya kutuambia eti wapo wabunge wanaotaka kujiuzulu ubunge kwa ajili ya ugumu wa maisha. Mama Makinda Kionambali anakuja kwako leo na maswali ya kutosha.
Mama Makinda wewe unawafahamu Watanzania na unafahamu hali yao kimaisha? Tunazungumzia watanzania katika wingi wao. Mathalani hapo Njombe, unafahamu wastani wa kipato chao kwa mwaka? Unapozungumzia mshahara wa mbunge unazungumzia nini hasa ewe mama yetu? Mama Makinda nimeambiwa umekuwa bungeni tangu mwaka 1995. Ugumu wa maisha ulianza kuuona lini wewe? Kwa maoni yako ni kazi gani ambayo ukifanya hapa Tanzania ugumu wa maisha haupo? Mama Makinda yajibu haya maswali tafadhali.
Lakini pia umetuambia karibu nusu ya wabunge wanataka kuachia ngazi kwa sababu ya ugumu wa maisha, unaweza kutupatia walau majina kumi (10) tu ya wabunge wanaolilia kuachia ubunge?
Mama yangu hiki ni kipindi cha toba kwa Wakristo na ninakufahamu wewe kama Mkristo hivyo uko kwenye toba. Tuambie kweli kutoka katika uvungu wa moyo wako, ni akina nani hao walikuja kukuambia wanatamani wasingekuwa wabunge?
Uliwajibu nini ewe spika wa kwanza mwanamama ambaye chama kilisema hii ni zamu ya kina mama kuongoza Bunge lakini wakikwepa kuangalia Mahakama na “Exucutive”? Tupashe mama, hao wabunge ambao wana huzuni sana kuwa wabunge hadi wanafikiria kwamba njia pekee ya kuwarudishia unafuu wa maisha ni kukimbia Bunge?
Mama yangu, si unajua ndani ya chama chenu kuna watu wamenuna kwa vile tu kuna pendekezo kwamba ubunge wa viti maalum uwe na kikomo? Au wale wa viti maalumu wao machungu ya maisha hayajawakaba?
Walhahi mama umetoa mpya. Utatusaidia sana kama ukiweza kujibu haya maswali yetu tena kwa uadilifu. Eti ulisema mshahara wa mbunge ni kiasi gani mama? Unafahamu kuhusu mshahara wa mwalimu, hakimu, karani, polisi, mwanajeshi, mesenja, bawabu na mwingine yeyote unayejua kaajiriwa?
Mama hebu twende taratibu kidogo. Hivi ili kuwa mbunge unatakiwa kuwa na taaluma gani au elimu kiwango gani? Kama sikosei nadhani kujua kusoma na kuandika ni kiwango pekee kinachohitajika kisheria ili kuwa mbunge. Tunafahamu wapo wabunge madokta, maprofesa na taja taaluma yoyote unayoitaka. Nini kiliwawasha wakatoka walikotoka kwenda ubunge? Walikuwa wanakwenda kuwakilisha wananchi au kupalilia matumbo yao?
Eti mama hao waliokuambiwa wanataka kususa ubunge walikuambia wataenda kufanya shughuli gani wakiacha ubunge? Na eti walidanganywa na nani hadi wakaacha maisha mazuri wakaenda kwenye maisha hohehahe ya kibunge? Na nnini kimewafunga kwenye huo ubunge? Kwani ubunge ni kama ndoa ya kikatoliki tunakoambiwa ni hadi kifo kiwatenganishe? Duh! Mama tujibu maswali yetu tafadhali.
Na mshahara ulioutaja mama mbona haukujumlisha na marupurupu mengine? Vipi posho ya mafuta ya gari? Vipi mshahara wa dereva? Unaelezea vipi posho ya mbunge anapokuwa nje ya jimbo? Na kama kazi ya ubunge inawafanya wattu wawe malofa ni kipi kinawatuma wengi wao wagawe takrima ili kuipata? Mama unataka kuniambia hakuna watu wamefurumishwa wakitoa rushwa? Wapo walionaswa na vitenge, zimu na pesa taslimu wakati wa chaguzi za ndani za vyama. Hukusikia lolote? Watafute Takukuru wakupe data kabla ya kujibu hili swali. Hapana, nakuheshimu mama Makinda lakini kwenye hili naomba tutofautiane. Tuambie kama umesema kweli.
Nimesikia eti unalalamika kwamba hata wenzenu wa hapo Kenya tu wanawazidi. Tatizo liko wapi? Mama ulishatafiti kidogo tu kujua Tanzania ni nchi ya ngapi kupokea misaada? Kama tunapewa hadi misaada ya vyandarua mama yangu bado kweli unatarajia eti wabunge wa nchi hizi mbili walipwe sawa? Pato la taifa la Kenya ni kiasi gani ewe mama yangu spika? Tuambie tafadhali, utegemezi wa bajeti ya Kenya na Tanzania ni upi mkubwa?
Mama unajaribu kulinganisha vicheko kwenye harusi na kwenye matanga? Mbona hivyo ndivyo sivyo?
Tujibu mama ili tujue kama kauli yako tuifanyie kazi, Mama yangu rais Kikwete anasema anazunguka huku na huko kuhemea vibaba ili tusife njaa. Ulishamwona au kumsikia Rais Kibaki akihemea vibaba na yeye pia? Hivi una habari kwamba kwenye bajeti ya kawaida ya matumizi hapo Kenya hawategemei ufadhili?
Mama kwa nini unalinaganisha visivyolingana? Hebu tuanze sasa kuhakikisha kila kinachofanyika Kenya kinafanyika pia hapa. Madaktari wa Tanzania walipwe mshahara unaolingana na madaktari wa Kenya. Walimu wa Tanzania walipwe mshahara unaolingana na walimu wa Kenya. Lakini sisi si ni nchi mbili tofautti zenye taratibu tofauti? Ndio maana wale hawakuwahi kuwa na Azimio la Arusha.
Wametumia rasilimali zao vizuri kuliko sisi. Tunataka vipi tufanane nao? Tujibu mama. Hapana, ulifika mbali mno.
Mama Makinda unafahamu kipato cha wananchi uliokuwa ukiongea nao? Unafahamu katika kundi hilo wapo watu ambao ahwajawahi kukamata shilingi laki moja kwa mkupuo mmoja? Unapowaambia mshahara wa mbunge ni mdogo unataka watu wapate kizunguzungu. Sijui kama unanipata kwenye hili. Hapana mama, ulichokifanya nakifananisha na mtu anayelalamika hana viatu vipya kwa rafiki yake aliyekatwa mguu! Naam, ni kama kulalamika hujui kucheza kwaito wakati unayemlalamikia ni mlemavu wa miguu. Loh! Nakumbuka maneno ya Samwel Sitta wakati fulani akikuambia usikurupuke. Ingawa aliomba radhi maneno yale tayari alishayatamka!
Nasikia au walau nimeambiwa umesema hutagombea tena ubunge mwaka 2015. Mama na wewe unakimbia kwa ajili ya ugumu wa maisha? Tangu 1975 ndio umegundua sasa kwamba unastahili kupumzika? Lakini mama kwani kazi ya mbunge ni ipi? Kupokea mshahara mnono? Kwani bunge ni mgodi wa vito ambaye anayeingia humo huchukua hadi kushiba? Ninyi si ni wawakilishi wa watu hivyo lazima mtoke kati ya watu na mfanane kwa kiwango kikubwa na mnaowawakilisha?
Nilishakusikia wewe na waziri mkuu kwa nyakati tofauti mkisema wabunge wanawasaidia kifedha wapiga kura wao. Hiyo ndiyo kazi ya mbunge? Kusaidia kusafirisha msiba? Kugawa vijisenti ambavyo haviwezi kumshibisha mtu hata kwa wiki moja?
Kwani ubunge ni mfuko wa hisani kusaidia wapiga kura? Au ubunge ni biashara ambayo mtu amewekeza hivyo anatarajia faida?
Naomba uwaambie wanaotaka kutoka watoke haraka. Wapo walioko tayari kuufanya ubunge bure. Unafahamu kwamba Mwalimu Nyerere mara kadhaa alikuwa akipunguza mshahara wake? Bado mwajidai nanyi ni wafuasi wake? Kweli ukistaajabu ya Musa lazima uyaone ya Firauni. Ukinijibu nitashukuru mama. Kazi njema.


h.sep3.gif

0784 265072 juvengowi@yahoo.com
 
Back
Top Bottom