Mapokezi ya Taifa Stars yafunika jiji la Dar kwa maelfu ya mashabiki

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,789
288,015
starsdance.jpg

Baadhi ya wachezaji wa Taifa Stars pamoja na mbunge wa Singida, Mohamed Dewji (mwenye miwani) wakisakata dansi mitaani wakati wa mapokezi Jumatatu baada ya kuishinda Sudan jumla ya magoli 5-2 na kufuzu kwenda Ivory Coast kwa mashindano ya CHAN

Date::12/15/2008
Mapokezi ya Taifa Stars yafunika jiji la Dar kwa maelfu ya mashabiki
Jimmy Tara na Dorice Malyaga
Mwananchi

MAELFU ya wakazi wa jijij la Dar es Salaam jana waliacha shughuli zao kwa muda na kulijitokeza kuipokea timu ya soka ya taifa, Taifa Stars ilipokuwa ikirejea kutoka Khartoum, Sudan ilipofanikiwa kufuzu kucheza fainali za Afrika kwa wachezaji wa ndani (CHAN).

Mbali na kufuzu na kuvunja rekodi ya miaka 28 iliyopita, pia Stars imevunja mwiko wa Sudan wa kutofungwa katika uwanja wao wa nyumbani kwa miaka 13 baada ya kuitandika mabao 2-1, lakini pia katika mchezo wa awali uliofanyika katika Uwanja Mkuu wa Tanzania, Stars ilishinda kwa mabao 3-1, hivyo kusonga mbele kwa mabao 5-2.

Stars iliwasili katika Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere saa 3:15 asubuhi ambapo nahodha wao Henry Joseph na msaidizi wake, Nadir Haroub 'Cannavaro' ndio walikuwa wa kwanza kutoka nje wakiwa wameshika bendera ya taifa na kulakiwa na viongozi wa Shirikisho la Soka Tanzania TFF, viongozi wa serikali wakiongozwa na Waziri Mkuu Mizengo Pinda pamoja na mashabiki.

Ilipotimia saa 3:30 msafara wa timu hiyo ulianza safari kuelekea katika Hoteli ya Kilimanjaro Kempinski ilipoandaliwa hafla fupi ya kuwapongeza na ulifika nje ya uzio wa uwanja, mamia ya mashabiki waliojitokeza walilipuka kwa shangwe, lakini msichana mmoja aliyekuwa akiongoza shughuli hiyo pale uwanjani aliamuru msafara huo urudi ndani kwani Waziri Mkuu Pinda alitarajiwa kuwasili kwa ajili ya kuwapongeza wachezaji.

Msafara wa Waziri Mkuu uliingia uwanjani hapo saa 3:50 na aliposhuka kwenye gari alianza kusalimiana na wachezaji na benchi la ufundi na baada ya kutoa pongezi na salamu kutoka kwa Rais Jakaya Kikwete aliahidi kutoa Shilingi Milioni 3 kama zawadi yake binafsi kwao.

Baada ya Waziri Mkuu kuondoka, msafara wa timu uliondoka kupitia Barabara ya Nyerere, Mandela, Uhuru, Mtaa wa Msimbazi, Barabara ya Morogoro, Bibi Titi, Azikiwe mpaka hoteli ya Kilimanjaro Kempinski.


Katika barabara na mitaa yote ulipopita msafara huo, mashabiki lukuki wake kwa waume bila kujali jua kali lililokuwa likiwaka muda wote waliongozana na msafara huo na wengine wakiwa wamejipanga barabarani kwa ajili ya kuwapongeza wachezaji ambao nao walionekana kuwa wenye furaha muda wote.

Kivutio walikuwa Haruna Moshi 'Boban', Athumani Idd 'Chuji', Mrisho Ngassa, Nurdin Bakari, Jerry Tegete, Meshack Abel, Shaaban Dihile, Kelvin Yondani, Uhuru Selemani na Godfrey Bonny kutokana na kuteremka kutoka katika gari la wazi waliloandaliwa na kuanza kucheza muziki uliokuwa ukipigwa kutoka kwenye gari hilo.

Wakazi wa jiji nao waliziacha shughuli zao na kujitokeza kwa wingi kuwalaki mashujaa hao na kusababisha msongamano mkubwa wa magari.

Kocha wa timu hiyo, Mbrazili Marcio Maximo aliwapongeza wachezaji wake kwa kujituma na kupata ushindi huo na kuongeza kuwa sasa soka ya Tanzania inaanza kusimama na kuahidi kuwa wanakwenda Ivory Coast kushindana na si kushiriki.

Kabla ya kuitoa Sudan, Stars iliitoa Kenya kwa mabao 2-1, ikaisambaratisha Uganda mabao 3-1. Sasa, inasubiri fainali za Afrika kwa wachezaji wa ndani (CHAN) zilizopangwa kufanyika Ivory Coast Februari mwakani.

Mara ya mwisho Stars kufuzu kwa fainali za Afrika ilikuwa mwaka 1980 zilizofanyika nchini Nigeria.
 


...inanikumbusha siku ileeeeeeeeee waliposhangilia sana mpaka wakawa wageni rasmi bungeni, 'wakashikishwa' milioni kadhaa, halafu matokeo yalofatia mnh :(...
 
HALAFU TUSEME MAXIMO HATUFAI NA HAJAFANYA LOLOTE......!
LITAKALOFATA NI TEKE LA MUNGU.....! (yaani tutabaki na laana ya kutokuwa na shukrani)
 
HALAFU TUSEME MAXIMO HATUFAI NA HAJAFANYA LOLOTE......!
LITAKALOFATA NI TEKE LA MUNGU.....! (yaani tutabaki na laana ya kutokuwa na shukrani)
Kuna thread ya Maximo .....hebu kaisome kabla ya kulia lia hapa.
 
Ili Taifa stars ikue na isonge mbele zaidi na zaidi tunahitaji Kocha mwingine na sio Maximo.
Maximo inatosha alipo tufikisha tumlete mwalimu mwingine tena aendeleze soka la bongo.
Pongezi za dhati kwa vijana kwa kazi nzuri walio ifanya mapesa mtakayo mwagiwa msitongozee wanawake,wala kuvuta unga nunueni mashamba,viwanja na mjenge nyumba nyingine mjiwekee akiba.Starehe zipo tu kila siku haziwapiti hata siku moja ila vitu vya msingi na mhimu usipo fanya sasa hivi vinapita mwishowe utakuwa mtupu.
 
Sasa Tuandie timu ili tukafanye vizuri tusije kwenda kuwa wasindikizaji
 
Maximo pekeyake hawezi kubadilisha soka la Bongo. Hatuwezi kuwa na timu ya taifa endelevu kama hatutakuwa na Vilabu bora. Wachezaji wanaporudi kwenye timu zao wanapungua ubora! vilabu vibadilishe mfumo wa kuendesha mambo, wawe pia na timu za watoto na makocha bora la sivyo hata aje Morinyo mtamuona hafai. Kwa sasa bado Maximo anatufaa. Ni maoni 2
 
Wabongo ndio tujue maendeleo ni mchakato na muda ni factor muhimu katika maendeleo. Manake wakandiaji wengi sana leo wanapongeza wakati waliponda sana katika mijadala ya nyuma.

Bravo Maximo, bravo Taifa Stars.
 
Tena ikiwezekana Maximo wamwongeze mkataba bse na kerere zote za wabonge bado yuko Tz.
Ona wazungu wa simba na yanga wanavyotimka
 
Back
Top Bottom