Kila mtu asome hii

Taifa_Kwanza

JF-Expert Member
Sep 3, 2010
443
86
amka2.gif

WAKATI Rais Jakaya Kikwete alipoomba kura ili awe rais wa awamu ya nne mwaka 2005, alibuni kaulimbiu ya ”Maisha Bora Kwa Kila Mtanzania” akiahidi kutimiza ahadi zake kwa ”Ari mpya, Nguvu mpya na Kasi mpya.” Akachaguliwa kwa zaidi ya silimia 80 ya kura zilizopigwa huku CCM kikija na tambo za ’ushindi wa kishindo’.
Ili kuhakikisha malengo yake yanatekelezwa kwa ’Ari, Nguvu na Kasi mpya’ kama alivyoahidi, akawaandalia watendaji wa serikali yake (wakuu wa wilaya, mikoa, makatibu wakuu, mawaziri na manaibu wao), semina ’elekezi’ kwenye hoteli ya kitalii ya Ngurdoto mkoani Arusha.
Alipochaguliwa kipindi cha pili mwaka 2010 kwa kura kiduchu tena baada ya kukokotolewa (si kuchakachuliwa kama isemwavyo), akaiendeleza kaulimbiu yake ya awali, lakini mara hii akisema atatekeleza kwa ’Ari zaidi, Nguvu zaidi na Kasi zaidi’.
Akaandaa tena semina ’elekezi’ mjini Dodoma kwa kuwakutanisha watendaji wakuu wa serikali. Ahadi ya ’ari, nguvu na kasi mpya - zaidi’ ikawapa wananchi matumaini mapya - zaidi.
Maisha bora kwa kila Mtanzania: Je! watu wa kawaida, yaani kina ’pangu-pakavu’ wana maisha bora waliyoahidiwa na Kikwete mwaka 2005 kwa ’ari, nguvu na kasi mpya’ na sasa ’ari zaidi, nguvu zaidi na kasi zaidi? Au wanadharaulika zaidi, wanateseka zaidi na kunyang’anywa zaidi rasilimali za nchi yao?
Alipochukua madaraka kutoka kwa mtangulizi wake, Benjamin William Mkapa, thamani ya dola moja ya Marekani ilikuwa sawa na shilingi 1,042/30 za Tanzania na bei za vyakula na bidhaa nyingine zilikuwa chini kuliko ilivyo sasa’ tena kwa mbali.
Thamani ya dola moja ya Marekani mwaka 2010 ilikuwa sawa na shilingi 1,335 za Tanzania na mwaka huu dola moja ya Marekani inanunuliwa kwa shilingi 1,500 na ushei, ikiuzwa kwa takriban shilingi 1,600 za Tanzania. Bado shilingi yetu inaendelea kushuka thamani kwa kutokuwa na uwezo wa kuuza bidhaa nyingi n-nje.
Hii inasababishwa na viwanda kutozalisha kama itakiwavyo kwa ukosefu wa umeme wa uhakika. Mwaka 2003, miaka miwili kabla Kikwete hajakabidhiwa madaraka, dola moja ya Marekani ilikuwa sawa na shilingi 973 za Tanzania.
Jirani zetu, Rwanda, waliopigana vita vya kimbari kwa miaka kadhaa, wana uchumi ulioimarika kuliko sisi. Unapotembelea Rwanda, hukosi kuona usitawi, maendeleo na mabadiliko makubwa yaliyofanywa kwa miaka michache. Tanzania tumebakiwa na itikadi za kisiasa, ubadhirifu uliotopea, wizi na kaulimbiu za hadaa.
Kilimo kwanza: Sekta inayoongoza kwa ajira ya watu wengi Tanzania ni kilimo. Sekta hii ilikua kwa asilimia nne mwaka 2008 lakini mchango wake kwenye pato la taifa ulishuka kutoka asilimia 27 mwaka 2004 mpaka asilimia 24 mwaka 2008.
Sasa serikali imekuja na kaulimbiu ya ”Kilimo Kwanza” kabla ya kuwaandaa na kuwaelimisha wakulima, hasa wale wa jembe la mkono.
Badala yake imekurupuka kama mtu aliyeshikwa na jinamizi (ndoto ya matukio ya kutisha yanayomsibu mtu) na kuja na mpango usiokuwa na mwanga kwa wakulima wadogo. Haiwezekani kukurupuka na kaulimbiu ya ”Kilimo Kwanza” bighairi/minghairi ya kutoa elimu kwa wakulima wadogo; jinsi ya kuandaa mashamba, mbegu bora za mazao yanayofaa na namna ya kuyapumzisha mashamba yao yaliyochoka. Badala yake serikali imezuka na ’Power Tiller,’ matrekta yasiyoweza kupenya ardhi ngumu.
Tangu enzi za ukoloni na baadaye Mwalimu Nyerere, wataalamu wetu wa kilimo na mifugo waliwatembelea wakulima na wafugaji vijijini. Leo, baada ya miaka nenda-rudi ya uhuru, tunategemea wataalamu kutoka n-nje kuja kutufundisha kilimo na ufugaji bora. Twaachiwa mashamba na mifugo ya mfano lakini twashindwa kuyaendeleza!
Yako wapi mashamba makubwa yaliyokuwa yakizalisha ngano, kahawa na maharage katika mikoa ya Arusha na Kilimanjaro; mkonge katika mikoa ya Tanga, Morogoro na Kilimanjaro; na maua ya pareto mkoani Iringa? Ile mikoa mitano (Iringa, Mbeya, Morogoro, Rukwa na Ruvuma) iliyopewa jina la ”Big Five” kwa uzalishaji wa mazao ya chakula, bado inastahiki kuwa na sifa hiyo? Serikali inafanya nini kurekebisha hali hiyo?
Shamba la mpunga la Mbarali amepewa mwekezaji M-burushi kutoka n-nje na kusababisha akaliane mguu-kausha na wananchi. Eneo hilo sasa limekuwa bomu linalosubiri kulipuka lakini serikali bado imelala usingizi wa pono!
Matokeo ya mchango mdogo wa kilimo katika pato la taifa yamesababisha uwezo mdogo wa kupata chakula cha kutosha, kusomesha watoto, ukosefu wa huduma za afya na mwishowe afya za wakulima kudorora na nguvukazi ya nchi kupotea. Ni kwa jinsi gani mkulima wa jembe la mkono, machinga anayeshinda juani kutwa, kibarua na mtu asiye na ajira atashawishika kukubali kuwa kuna ”maisha bora kwa kila Mtanzania?”
Kutokana na tatizo kubwa la umeme nchini hivi sasa, uzalishaji umeshuka na kufanya Tanzania ikose bidhaa nyingi za kuuza nchi za n-nje. Kwa hiyo ni vigumu sarafu yetu kuhitajika katika masoko ya fedha (low currency demand) na hii husababisha kushuka kwa thamani ya sarafu yetu. Maana yake ni kwamba kama nchi haiuzi bidhaa nyingi n-nje, soko la ndani huwa kubwa, hivyo kutokuwa na ziada ya kuuza n-nje.
Kwa hiyo Tanzania inaagiza bidhaa nyingi zaidi kutoka n-nje ili kukidhi mahitaji ya ndani. Kwa sababu hiyo, nchi kama China inatumia mwanya huo kuingiza kwa wingi bidhaa feki nasi tunazipapatikia kama wehu! Sasa Tanzania imegeuzwa jalala la nchi zenye maendeleo makubwa ya viwanda, kuingiza bidhaa duni zinazotengenezwa na wajasiriamali wao.
Dawa na vyakula vilivyokwisha muda wa matumizi huingizwa nchini kwa wingi na hivyo kuongeza kasi ya vifo vya wananchi.
Hebu fikiri hata sigara zinazodhuru afya na kupunguza uhai wa wavutaji, zinaendelea kuingizwa na kutengenezwa kwa wingi nchini. Tunaambiwa asilimia 32 ya wagonjwa wa saratari walio katika Taasisi ya Saratani ya Ocean Road jijini Dar es Salaam walikuwa wavutaji wa tumbaku. Serikali haishtuki!
Hapo hapo serikali inajidanganya kuwa zao la tumbaku linaiingizia pato la shilingi bilioni 50 lakini serikali hiyohiyo hutumia shilingi bilioni 30 mpaka 40 kwa mwaka kwa matibabu ya wagonjwa wa saratani! Huku ni kufilisika kifikra, ni ujuha au wendawazimu?
Kwa upande mwingine, uagizaji mkubwa wa bidhaa za n-nje huifanya Tanzania ihitaji zaidi sarafu ya kigeni (dola ya Marekani) ili kuagiza bidhaa. Hali hii huleta msukumo mwingi wa sarafu yetu kwenye soko la fedha (high currency supply) ambayo husababisha kushuka thamani ya sarafu yetu. Kama hali ni hii, ”maisha bora kwa kila Mtanzania” ni ilani ya kisiasa zaidi; na kiini macho kwa wananchi.
Elimu bora: Hapa serikali imetupiga ’changa la macho.’ Elimu bora i’wapi? Wanafunzi kufanya mitihani wakiwa wamekaa chini kama wanaokula pilau kwenye shughuli za mazishi? Ajitokeze (kwenye safu hii) kiongozi yeyote wa serikali anayemsomesha mwanawe kwenye shule yoyote (msingi au sekondari) ya kata.
Thubutu! Shule zinakosa madawati na vitabu vya kiada lakini viongozi wananunuliwa magari ya anasa ya kuanzia shilingi milioni 60 mpaka 200 kwa mtu mmoja wakati dawati moja la shule ni shilingi elfu 40 tu!
Viongozi na wachumi wetu wanajichumia wenyewe tu.
Wanafunzi wa vyuo vikuu hupigwa mabomu ya machozi na kurushiwa maji ya ’washawasha’ wanapoandamana kudai mikopo ya masomo. Wanafunzi na wahadhiri wao hutishwa kujiingiza kwenye siasa ingawa CCM kilikuwa na matawi, yangalipo na kinaendelea kuyafungua vyuoni. Wapinzani wakifanya hivyo ni haramu. Eti wanafunzi wasishabikie siasa! Mkuki wa nguruwe kwa mwanadamu mchungu eh?
Hukereka mno nionapo viongozi wetu wakishangilia pale kampuni na baadhi ya balozi za nchi za n-nje zikitoa misaada ya madawati kwa shule mbalimbali. Ni fedheha iliyoje kwa serikali! Hivi kweli serikali imeshindwa kumaliza tatizo la madawati katika shule zetu?
Ule mpango wa kuchangia madawati uliishia wapi? Au wajanja walitafuna fedha kama zilivyotafunwa zile za mabasi ya wanafunzi wa shule na hapana aliyechukuliwa hatua zozote? Mbona Kikwete alisimamia michango ya uchaguzi zikapatikana mabilioni? Kama aliweza kwa uchaguzi, kwa nini asifanye sasa ili kupata fedha za kununua madawati ya watoto wa shule?
Ajira milioni moja unusu: Wahenga walisema: ”Ajuaye misonoe (mikoromo yake) ni alalaye naye.” Wananchi wanafahamu vizuri sana ghiliba (udanganyifu wenye nia ya kujinufaisha) za viongozi wa CCM. Kwa hiyo wasidhani wanaweza kuwadanganya watu wote kwa wakati wote – hasha!
Ajira tulizoahidiwa zimeota mbawa. Tunachoona ni wingi wa mikokoteni na maguta (baiskeli za magurudumu matatu) huku vijana wakitokwa jasho na kukoswakoswa na magari. Twawaona wamachinga waliozagaa kila barabara wakiuza bidhaa zinazopendezesha macho lakini feki kutoka China na nguo kuukuu zikiwamo chupi, sidiria na soksi zilizotandazwa sehemu za waendao kwa miguu. Ndiyo ajira milioni moja unusu alizoahidi Kikwete!? Ari zaidi, nguvu zaidi na kasi zaidi: Tunaona jinsi uchumi wa nchi unavyowafaidisha watu wachache wanaoshirikiana na wawekezaji wa n-nje kwa ’ari, nguvu na kasi zaidi’ huku wananchi wapatao milioni 40 wakiendelea kuwa masikini kwa ’kasi zaidi!’ Twasikia namna wanyama wetu wanavyohamishiwa falme za kiarabu na kusafirishwa kupitia uwanja wa ndege wa kimataifa wa Kilimanjaro kwa kasi zaidi! Twaona jinsi wananchi walio maeneo ya migodi wanavyopigwa na kuuawa kwa nguvu zaidi wanapotetea maliasili zao! Hii ndiyo ’ari mpya-zaidi, nguvu mpya-zaidi na kasi mpya-zaidi’ ya kuhujumu rasilimali za nchi kwa ’ari zaidi, nguvu zaidi na kasi mpya-zaidi!’ Ewe Mwenyezi Mungu uliye mwingi wa rehema, wazindue watawala wetu waliotia pamba masikioni. Tujalie amani na upendo – AMINA.

Source: Tanzania Daima
marobarnabas@yahoo.com 0784/0715 33 40 96 na 0756 85 53 14
 
Kwa kweli hayo yaliyoelezwa hapo juu ni ukweli mtupu, kwa maneno mengine huwa tunasema serikali imeshindwa kazi kutokana na ukweli kwamba badala ya kupiga hatua mbele tumekuwa tukirudi nyuma kila kukicha utadhani nchi yetu pamoja na viongozi walilaaniwa na Mwenyezi Mungu.Mambo yamekuwa shaghalabaghala kutokana na ukweli kwamba hatuna viongozi ambao wana uzalendo na nchi yao na matokeo yake ni wananchi kukosa uzalendo pia na hivyo kushusha kiwango cha kujituma kwenye maswala yote muhimu ya kimaendeleo.Mwalimu Nyerere alikuwa kiongozi mzalendo namba moja nchi hii, lakini wale wote waliokuja baada ya yeye kuachia madaraka wamekuwa wakitafuna "NATIONAL CAKE" na washkaji zao huku wazazi wasio na uwezo wakiambiwa wachangie MADAWATI kwa ajili ya vijana wao wanapokwenda kujiunga na shule za Sekondari.Kama vile haitoshi hayo madawati huwa hayaana maana kwa kuwa hata walimu inakuwa ni tatizo cause Serikali inashindwa hata kutekeleza wajibu wake wa kuajiri waalimu bora, hapa mzazi anakuwa demoralized.Ni lazima tufike mahali tufahamu kwamba huu si wakati wa kushabikia siasa na kauli mbiu ambazo kimsingi hutufanya tuonekane wapumbavu mbele ya nchi nyingine jirani, tunahitaji kukataa kauli za ulaghai kwa nguvu zote na kuangalia ni mwelekeo gani tunapaswa kuwa nao baada ya miaka 50 ya UHURU wa Tanganyika.KAULIMBIU NA MANENO MATUPU YA NGUVU MPYA, ARI MPYA NA KASI MPYA havina maana kama tutendelea kuishi katika ufukara huu mkubwa ndani ya nchi yenye rasilimali nyingi karibu kuliko zote AFRIKA.
 
This is another piece of art! Hiyo ilikuwa aina ya sanaa itakayomsaidia kuingia
madarakani na kweli kafanikiwa.
 
Kuhusu vikao huyu bwana Kikwete nimeambiwa kesho (j/nne) atakuwa na kikao hapa DODOMA (sijajua kinahusu nini), na viongozi wote wa vyama vya siasa kutoka mikoa yote ya Tanzania wamealikwa (fikiria gharama ambayo serikali itaingia kwa kufanya huu usanii). Inakera sana!!
Kuhusu kufungua matawi ya vyama vya siasa nje ya vyuo ni dhambi kwa vyama vya upinzani tu ila kwa CCM ni jambo jema sana tena walivyo wahuni wanafanyia kazi zao ndani ya maeneo ya vyuo.. Waliwatumiwa viongozi wa chuo kuniadhibu pale niliporatibu ufunguzi wa tawi la chadema nje ya chuo cha CBE Dodoma. uhuni mtupu.!!
Leo asubuhu bungeni naibu waziri wa nishati Malima anasema hata mashine zote zinazo zalisha umeme nchi hii zikifanya kazi bado kutakuwa na upungufu wa Megawatz 260. Na Malima kaongezea kwa kusea mahitaji ya umeme nchi hii yanaongezeka kwa 13% kwa mwaka.

Yani ni hatari tupu.
 
Back
Top Bottom