BARD AI
JF-Expert Member
- Jul 24, 2018
- 3,377
- 8,121
Kesi hiyo inamkabili Muharami Sultan aliyekuwa Kocha wa Makipa wa Simba SC na wenzake watano waliokamatwa kwa tuhuma za kusafirisha Dawa za Kulevya aina ya Heroin Kilo 34.89.
Washtakiwa wote akiwemo Mmiliki wa Kituo cha Cambiasso Sport Academy kilichopo Tuangoma, walifikishwa Mahakamani kwa mara ya kwanza Novemba 21, 2022.
============
Serikali imesema inasubiri vielelezo kutoka taasisi nyingine ya masuala ya mtandao ili kesi ya kusafirisha dawa za kulevya aina ya Heroine kilo 34.89 inayomkabili aliyekuwa kocha wa makipa wa timu ya Simba Sport Club, Muharami Sultan (40) na wenzake watano, iweze kuendelea na hatua nyingine.
Pamoja na kusubiri vielelezo hivyo, tayari wameshachukua maelezo ya mtuhimiwa mwingine ambaye watamuunganisha katika kesi hiyo, baada ya vielelezo hivyo kuwasilishwa mamlaka husika.
Sultani na wenzake, wanakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi namba 71/2022 yenye mashtaka mawili ya kusafirisha dawa za kulevya aina ya heroine zenye uzito wa kilo 34.89.
Leo, Alhamisi Julai 6, 2023 Wakili wa Serikali, Erick Kamala, ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, wakati shauri hilo lilipoitwa kwa ajili ya kutajwa.
Kamala amedai mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Mary Mrio kuwa, upelelezi wa kesi hiyo haujakamilika na kwamba amepewa taarifa kuwa kuna vielelezo waliomba kutoka taasisi nyingine ya masuala la mtandao, hivyo wanasubiria wapewe ili waweze kuendelea na hatua nyingine ikiwemo ya kuwapeleka mahakamani watuhumiwa wapya.
“Shauri limeitwa kwa ajili ya kutajwa, upelelezi bado unaendelea, nimepewa taarifa kuwa kuna vielelezo viliombwa kutoka katika taasisi nyingine masuala ya mtandao tofauti na hii ya kwetu ili kukamilisha upelelezi wa kesi hii ili iweze kuendelea na hatua nyingine,” amedai Kamala.
“Pia tayari mtuhumiwa ambaye anatarajia kuongezwa katika kesi hii, ameshachukuliwa maelezo yake, hivyo kutokana na hali hii tunaomba mahakama ipange terehe nyingine kwa ajili ya kutajwa,” amedai Kamala.
Kamala baada ya kueleza hayo, Hakimu Mrio aliahirisha kesi huyo hadi Julai 20, 2023 itakapotajwa na washtakiwa wapo rumande kutokana na kesi inayowakabili haina dhamana kwa mujibu wa sheria.
Juni 22, 2023 Serikali ilidai kuwa inatarajia kuwafikishwa mahakamani hapo watuhumiwa wengine ambao wamekamatwa na Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) ili waje wasomewe mashtaka yao na kisha kuunganishwa katika kesi hiyo.
Hata hivyo, kesi hiyo imesikilizwa kwa njia ya video, huku washtakiwa wakionekana kwenye video kupitia luninga iliyowekwa katika ukumbi wa mikutano wa Mahakama ya Kisutu.
Kwa mara ya kwanza, washtakiwa walifikishwa mahakamani hapo Novemba 21, 2022 wakikabiliwa na mashtaka mawili ya kusafirisha dawa za kulevya.
Mbali na Sultani, washtakiwa wengine ni mmiliki wa kituo cha Cambiasso Sport Academy kilichopo Tuangoma, Kambi Zubery Seif; Said Matwiko mkazi Magole; Maulid Mzungu maarufu mbonde (54), mkazi wa Kisemvule; John John maarufu ‘Chipanda’ (40) mkazi wa Kitunda na Sarah Joseph.
Katika kesi ya msingi, washtakiwa wanadaiwa Oktoba 27,2022 eneo la Kivule jijini Dar es Salaam kwa pamoja walisafirisha dawa za kulevya aina ya heroine zenye uzito wa kilo 27.10.
Pia, Novemba 4, 2022 maeneo ya Kamegele Wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani washtakiwa kwa pamoja walisafirisha dawa za kulevya aina ya heroine zenye uzito wa kilo 7.79.
MWANANCHI
Pia soma: