BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,789
- 288,023
Date::7/25/2009
Dk Hoseah aonywa, Karamagi, Msabaha bado wachunguzwa
Na Kizitto Noya, Dodoma
Mwananchi
Dk Hoseah aonywa, Karamagi, Msabaha bado wachunguzwa
Na Kizitto Noya, Dodoma
Mwananchi
SERIKALI imempa onyo Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (Takukuru), Dk Edward Hoseah kwa kutokuwa makini katika utendaji wake wa kazi wakati anachunguza mkataba tata kati ya kampuni ya Richmond na Tanesco.
Hata hivyo, serikali imesema mamlaka yake (Hoseah) ya nidhamu imeona hana hatia kijinai kwani sheria ya Takukuru wakati huo, ilikuwa na mapungufu katika kubaini viashiria vya rushwa kwenye mchakato wa zabuni.
Akiwasilisha bungeni taarifa ya utekelezaji wa maazimio ya Bunge kuhusu sakata hilo, Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Adam Malima alisema Dk Hoseah alipaswa kujiridhisha kama kweli kampuni ya Richmond Development Company (LLC) ilisajiliwa nchini au la kabla hajatoa taarifa yake kwa umma.
"Ingawa sheria ilikuwa na mapungufu, mamlaka yake ya nidhamu imebaini kuwa wakati wa kupitia taarifa ya uchunguzi iliyofanywa na wataalamu wake wa Takukuru na kabla hajaitoa kwa umma, alipaswa kujiridhisha kwamba kweli kampuni ya Richmond Development Company (LLC) ilikuwa imeandikishwa hapa nchini au hapana.
"Hivyo mamlaka iliamua apewe onyo kwa kutokuwa makini katika uchambuzi wa taarifa zinazowasilishwa kwake na wataalamu wake, ili kuleta usimamizi wenye tija ndani ya Takukuru."
Lakini serikali imesema bado haina majibu ya maazimio namba nane na 14 ya Bunge yaliyoitaka iwawajibishe viongozi wenye dhamana ya kisiasa waliokuwa mawaziri Dk Ibrahim Msabaha na Nazir Karamagi kwa kuwa uchunguzi dhidi yao haujakamilika.
"…Hadi sasa suala hilo halijafikia tamati kwa kuwa linashughulikiwa zaidi na Takukuru na ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka," alisema Malima.
Mbali na Dk Hoseah watumishi wengine wa umma waliohusika na mkataba huo wamesafishwa kuwa hawakutenda kosa lolote la jinai.
Miongoni mwa watumishi hao ni Mwanasheria Mkuu wa serikali, Johnson Mwanyika ambaye amesafishwa kwamba hakuna ushahidi unaodhihirisha kuwa hawakutumia utaalamu na uzoefu wake kuishauri vizuri serikali katika mchakato mzima wa upatikanaji wa zabuni hiyo.
"Kwa mantiki hiyo, Mamlaka zao za nidhamu zimeridhika na utetezi uliotolewa na watumishi hao na kuwaondolea mashtaka. Hata hivyo watumishi hao wamekumbushwa kuhusu umuhimu wa kuwa makini na thabiti zaidi katika utekelezaji wa majukumu wanayopewa na serikali," ilisema.
Mwanyika ambaye mamlaka yake ya nidhamu ni Rais, taarifa hiyo ilisema, hakuwa na kosa lolote katika mchakato mzima wa kuipa kampuni ya Richmond zabuni ya kuzalisha umeme.
"…Kwa maelezo tuliyonayo, hakuna kosa lolote la kisheria au kinidhamu ambalo alilifanya katika nafasi yake kama mwanasheria mkuu wa serikali katika mchakato mzima ulioipa ushindi kampuni ya Richmond Development Company LLC Development Company kisheria au kinidhamu," ilisema.
Hata hivyo, Malima alisema kwa kuwa kuna shauri mahakamani dhidi ya wamiliki na wawakilishi wa Richmond, iwapo mtumishi yeyote wa umma atatajwa na watuhumiwa hao kwamba alihusika katika makosa ya jinai, serikali haitasita kumfikisha mahakamani.
Alisema serikali imetekeleza Azimio namba 11 lililoitaka ifanyie marekebisho ya sheria ya maadili ya viongozi wa umma kwa kuunda kikundi kazi ambacho tayari kimefanya utafiti na kupitia upya sheria hiyo ya mwaka 1995 kubaini mapungufu yake.
Serikali pia imetekeleza azimo la 12 lililoitaka ijiepushe na matumizi ya mawakala katika manunuzi ya umma kwa kukamilisha utaratibu mpya wa manunuzi ya umma chini ya usimamizi wa Mamlaka ya Manunuzi ya Umma (PPRA).
Katika hatua nyingine serikali imetekeleza Azimio namba 13 lililoitaka isizihusishe Kamati za Bunge kupitia mikataba mikubwa ya kibiashara na ya muda mrefu kwa kuunda timu ya wataalamu ambao wanaandaa utaratibu mwafaka kwa kufanya utafiti katika mabunge ya nchi za Jumuiya za Madola.
Katika kutekeleza maazimio namba 18 na 20, serikali iliunda kamati maalumu ya vyombo vya dola kushughulikia uchunguzi na upelelezi na kumfikisha mahakamani mmoja wa wawakilishi wa Richmond LLC, Naeem Adam Gire.
Hii ni mara ya nne kwa serikali kutoa taarifa inayohusu suala la Richmond, taarifa ya kwanza iliwasilishwa Aprili 25 mwaka 2008, ya pili Agosti 28 mwaka jana na taarifa ya tatu Februari 11 mwaka huu.