Iddi simba akiona cha moto

Pdidy

JF-Expert Member
Nov 22, 2007
50,956
22,150
Iddi Simba akiona cha moto UDSM

lC.gif
Mwandishi Wetu​
Oktoba 7, 2009
rC.jpg

bul2.gif
Adai wapo waliodumaa akili serikalini
WAZIRI wa Serikali ya Rais mstaafu, Benjamini Mkapa, Iddi Simba, amebanwa mbele ya wasomi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), baada ya kuwashambulia kwa hoja, viongozi wasomi serikalini aliodai wameambukizwa udumavu wa akili.
Baada ya kutoa kauli hiyo na kung’ang’ania mtazamo wake huo, Iddi Simba aliandamwa na makombora ya shutuma kiasi cha kulazimika kuwaomba radhi Watanzania kwa kitendo chake cha kushiriki kupitishia sheria mbovu ya madini alipokuwa mbunge.
simba_1.jpg


Iddi Simba
Simba, ambaye kwa wakati huo alikuwa Mbunge wa Ilala, alikiri kushiriki kupitisha sheria hiyo ambayo kwa mujibu wa maelezo yake ni mbovu na inafaa kufutwa, kwa upande mwingine alionekana kuungwa mkono na wasomi wa chuo hicho, sambamba na kupata changamoto kutoka kwa washiriki wengine.
Tukio hilo lilijitokeza juzi katika mkutano wa 17 wa hali ya kisiasa nchini, uliofanyika kwa siku mbili chini ya maandalizi na uratibu wa Mpango wa Utafiti wa Elimu ya Demokrasia Tanzania (REDET), Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ambako mada kadhaa ziliwasilishwa, ikiwamo ya Iddi Simba iliyohusu Sekta Binafsi, Utawala na Maendeleo.
Katika kuonyesha kuwa alikuwa amejiandaa kutoa maneno yanayoweza kuwaudhi baadhi ya viongozi lakini pengine yenye kuungwa mkono na baadhi ya wananchi, kabla ya kuwasilisha mada yake Simba alianza kwa kuomba radhi kwa atakaowakera.
“Napenda nianze kwa kuuliza, kwa nini watu bado masikini pamoja na neema zote tulizopewa na Mungu nchini na huku wageni wakifaidika na raslimali hizo, tena kwa kusaidiwa na viongozi? Pili, kwa nini wasomi kwa muda mrefu waliogopa kuingia kwenye siasa?
“Kuna watalaamu wamenieleza asilimia 51 ya watoto wenye umri chini ya miaka mitano nchini wamedumaa akili na asilimia 53 ya wenye udumavu wa akili wamevuka umri wa miaka mitano. Kwa bahati mbaya, hatuna shule za kutenganisha wenye udumavu wa akili na wasio na tatizo hilo. Kwa hiyo wote wanasoma pamoja. Katika hali ya kawaida, si kawaida kwa wasio na udumavu wa akili kuwaambukiza kitabia wenye udumavu wa akili,”
“Ilivyo ni wenye udumavu wa akili huambukiza kitabia wasio na udumavu huo. Sasa nimesema asilimia 53 ni watu wazima lakini wenye udumavu wa akili, wamesoma pamoja na wengine, hao hao wamo serikalini ni viongozi. Yaani hiyo asilimia 53 inajumuisha viongozi wadumavu wa akili, ambao pia wameambukiza wenzao na hasa wasomi waliomo kwenye uongozi kwa sasa ..ni dhana ya mtapanyo,” alisema Iddi Simba akionekana kuvutia wasomi waliokuwa katika utulivu mkubwa wakimsikiliza kwenye ukumbi wa Nkrumah, Jumatatu wiki hii.
“Kwa hiyo utaona viongozi wasio na udumavu wa akili wamekutana na wenye udumavu wa akili, badala ya kusaidia Taifa nao wameambukizwa udumavu wengine ni wasomi wakubwa,” alisema Simba.
Alisema kwa sasa sekta ya uchumi kwa kiasi kikubwa inadhibitiwa na wageni kutoka nje ya nchi na wazawa wamegeuka kuwa watazamaji wa tamthilia ya kiuchumi katika nchi yao, wakiwa wamefungiwa milango ya kiuchumi na kwamba umbile la sekta binafsi nchini limeundwa na wananchi wengi masikini licha ya ‘ngonjera’ za viongozi kuwa sekta binafsi ndiyo ‘injini’ ya uchumi.
“Wakati nchi inafuata kwa vitendo kanuni za uchumi wa kibepari, bado fikra za taifa zipo kwenye ujamaa. Kwa maneno mengine kwa kusaidiwa au kuongozwa na viongozi tunaimba kijamaa, lakini tunacheza kibebari,” alisema Simba na kuweka bayana kuwa kwa sasa kuna mgongano mkubwa wa maslahi baina ya viongozi na sekta binafsi, kwa kuwa sehemu kubwa ya viongozi ni wafanyabiashara.
Alisema licha ya umuhimu wake kwa taifa, sehemu kubwa ya wadau wa sekta binafsi wamekuwa wakiendesha shughuli zao kwa teknolojia za karne ya 16, enzi za Yesu Kristo, ambapo kilimo kwa mfano, kilikuwa kwa jembe la kukokotwa na wanyama.
“Asilimia 10 tu ya walioko katika sekta binafsi ndiyo wanaotumia teknolojia za kisasa katika kuendesha shughuli zao na hata hivyo ukichunguza zaidi utabaini kuwa wengi wao ni wageni na hali hii haiwashtui baadhi ya viongozi,” alisema.
Hata hivyo, baadhi ya wachangiaji wa mada hiyo waliinuka na kuhoji kuwa naye alikuwa sehemu ya viongozi wa serikalini na hasa Serikali ya Awamu ya Tatu ambayo katika kipindi hicho, uwekezaji katika sekta ya madini ulishika kasi na kutetewa kwa nguvu na Rais aliyepita, Benjamin Mkapa. Wengine wakihoji alikuwa wapi wakati yote hayo yakitokea.
Akitoa majibu, Simba alionyesha kung’ang’ania msimamo wake wa kuwapo kwa viongozi waliodumaa akili serikalini ambao wamekwishawaambukiza udumavu huo wasomi ambao ni viongozi wenzao lakini akionyesha kukiri kutokuwa makini wakati wa kupitisha sheria ya madini, ambayo kwa sasa imependekezwa na tume ya Jaji Mark Bomani ifutwe, na mchakato wa kufanya hivyo unaendelea, ingawa pia haijulikani utakwisha lini.
“Niombe radhi kwa Watanzania, nimeulizwa nilikuwa wapi wakati huo. Nilikuwa bungeni, nikiwa mbunge, naomba radhi Watanzania kwa kushiriki kupitisha sheria ya madini ambayo ki ukweli ni mbovu na inastahili kabisa kufutwa. Nadhani na hata sehemu kubwa ya wabunge tuliokuwa nao wakati ule wanakubali ni sheria mbovu na ifutwe,” alisema.
Hata hivyo, alionyesha kutofurahia mtindo wa kuwasilisha miswada ya mabadiliko ya sheria mbalimbali nchini kwa Lugha ya Kiingereza, isiyofahamika kwa ufasaha kwa baadhi ya wabunge na hivyo kupunguza ufanisi wa wabunge katika kuelewa. Kwa upande mwingine, hakuwa tayari kujibu swali aliloulizwa kuwa ni kwa nini wakati anajiuzulu uwaziri wa Viwanda, Biashara na Masoko, hakutaja sababu halisi za kufanya hivyo na badala yake wakati akijiuzulu alisema amewajibika tu, si yeye mwenye makosa.
Katika Serikali ya Awamu ya Nne, Waziri Simba alijiuzulu kutokana na kashfa ya sukari, na alifanya hivyo si kwa shinikizo la Rais Mkapa bali kutoka kwa wadau mbalimbali nchini hali iliyomlazimu Mkapa kukubali kwa shingo upande kujiuzulu kwa waziri wake huyo na kwamba katika hali isiyokuwa ya kawaida, licha ya kuwasilisha barua ya kujiuzulu, Mkapa alimtaka awasilishe nchi kwenye mkutano wa kimataifa uliohusu masuala ya biashara duniani.
Mbali na Simba, watoa mada wengine akiwamo Profesa Samuel Mushi walionekana kuwa mwiba kwa wawakilishi na watu wengine wanaounga mkono Chama Cha Mapinduzi walioshiriki mkutano huo, hasa pale alipozungumzia uhusiano namna uhusiano kati ya utawala na sekta binafsi ulivyogeuzwa na kuwa uhusiano wa kifisadi.
“Katika Awamu ya Tatu ya Rais Mkapa, yalijitokeza mahusiano kati ya utawala na sekta binafsi ambayo sasa yanaitwa mahusiano ya kifisadi, yaani mahusiano yaliyowawezesha viongozi na watumishi wa serikali kujipatia vipato vitonakavyo na rushwa kwa kuwatumia wafanyabiashara kama mawakala,” alisema na kuthibitisha kauli yake kwa mifano ya kashfa za wizi wa bilioni 133 kwenye Akaunti ya Malipo ya Nje (EPA) kwenye Benki Kuu ya Tanzania (BoT), ununuzi wa ndege ya Rais pamoja na rada ya kijeshi.
“Ushirikiano huu wa kifisadi umeiharibu kabisa ile dhana chanya kwamba sekta binafsi sasa ndiyo injini ya ukuaji wa uchumi. Imegeuka dhana hasi masikioni mwa wananchi kwa sababu wameona sekta hii inatumiwa kuinyonya nchi, hasa kwa wale wanaoficha fedha za ufisadi nje ya nchi.
Akasema watu wanajiuliza na kunukuu; “Ubia wa serikali na sekta binafsi (PPP) utaleta faida gani kwa nchi kama una chembechembe za kifisadi? Na kutaja njia nyingine hasi ya uhusiano kati ya utawala na sekta binafsi kipindi hiki cha soko huria ni ile ya viongozi na watumishi wa serikali kupenda kuanzisha biashara wakiwa bado kazini.
“Jambo hili lina madhara kadhaa, kwanza, mtaji wanaupata kifisadi kwa kutumia ofisi zao za dola. Pili, utendaji wao wa kazi za umma unafifia kwa sababu mawazo yao na muda mwingi wa kazi unatumika katika utendaji wa shughuli binafsi. Jambo hili tunaliita usiasishaji wa biashara yaani sekta binafsi kutumiwa kwa malengo na madhumuni ya kujiimarisha katika siasa na uongozi wa dola. Kwa hiyo kama dola imebiasharishwa (kwa kubinafsishwa), sekta binafsi imesiasishwa kwa kupewa malengo ya kisiasa,” alisema huku naye akionekana kuwavutia wasikilizaji wengi.
Hata hivyo, Mjumbe wa Halmashauri Kuu (NEC) ya CCM, Ramadhani Madabida, aliyekuwapo kwenye mkutano huo alisimama na kumpinga akisema akihoji; “Ni serikali gani mbovu inayopeleka watuhumiwa wa ufisadi mahakamani, tena wenye ushawishi mkubwa kwa jamii?
Madabida ambaye ni Mjumbe wa NEC Taifa akiwakilisha Mkoa wa Dar es Salaam alisema ni vizuri kutofautisha makosa ya watu binafsi ambao ni wanachama wa CCM na makosa ya CCM kama taasisi na kuonya akisema; “Ninyi watu wenye influence (ushawishi) katika jamii msiwe mnatoa statement (matamko) yenye kupotosha, semeni ukweli.”
Kwa upande wake, Mbunge wa Mbeya Mjini-CCM, Benson Mpesya alisema kuna ajali fulani ya kiakili imetokea katika vichwa vya viongozi, akisema miaka kadhaa nyuma, nchi za Korea Kusini, Vietnam zilikuwa na uchumi sawa na Tanzania, lakini leo ziko mbali kiuchumi.
“Niwaeleze jambo ninyi viongozi na wasomi. Hakuna mkulima aliyetoka kijijini na kuja mjini kuuza nyumba za serikali na wala hakuna mwanakijiji aliyekuja kuua, kuuza na kubinafsisha mashirika ya umma. Wasomi msikwepe wajibu wenu ni lazima muwe think tank (chemchem ya fikra) kwa taifa na kwa niaba ya wananchi wanyonge,” alisema Mpesya, ambaye pia yumo katika orodha ya wabunge waliojipambanua kuwa mstari wa mbele katika vita dhidi ya ufisadi nchini.
REDET kwa miaka kadhaa sasa imekuwa ikijihusisha na shughuli mbalimbali za kitaifa zikiwamo za kuendesha makongamano ya kitaifa kuhusu masuala ya siasa na mwelekeo wa nchi, na wakati mwingine kufanya tafiti mbalimbali, zikihusu utendaji wa viongozi mbele ya umma.
 
Hakika nabii hawezi sifiwa kwao. Idi Simba ni mtu mahiri sana hususan katika masuala ya uchumi. Ni mtu anehishimika Duniani kote okea akiwa IMF.

Ni mtu mkweli sana na yupo straight ukilinganisha na wanasiasa wengi hususan wa huko Tanzania.

Yeye kwa kulinda Hishma yake alieza kujiuzuru madarakani kwa kashfa ndogo tu ya sukari ndani ya utawala wa kifisadi wa Ben Mkapa. Jambo ambalo ni nadra sana kwa Watanzania kulifanya mpaka leo Mwinyi kujiuzuru hataki kwa makosa yaliyofanywa na wizara yake anayoiongoza ya kuuwa raia kule mbagala kutokana na uzembe wa kuhifandhi mabomu vibaya.

Ni mtu aliyeweka bayana Uzawa kwanza ndio wamiliki uchumi sera inayopigwa na wengi lakini huo ndio ukweli.

Nakumbuka mara moja nilikutana nae hapa Qatar alikuja kwenye mkutano alinieleza bayana kuwa Tanganyika wakti inapata uhuru wake 1961 alikuwa uchumi wake sawa na malaysia, singapore. lakini mara tu tulipopata uhuru Nyerere alikataa ushauri wa yeye alioutoa hasa kutokana na kupinga mpango mzima wa Kutaifisha mali za watu na kuzigeuza za Serikali.

Ilikuwa 1965 yeye akiwa mchumi alipinga hilo kwa sababu kuu mbili
1. Hiyo ilikuwa dhulma ambayo Mola hapendi na wananchi wasingeweza kuendeleza mali ile kwani hawakua na wataalamu wakutosha kuendeleza mali zile

2. Alisema nchi yoyote duniani inaongozwa na sekta binafsi. Kwani serikali inakusanya kodi kutoka katika sekta binafsi na kuzitumia katika kuendeleza nchi.

Kwa kupingana na Nyerere basi alifukuzwa nchini kabla hata Azimio la Arusha.

nakuheshimu Idi Simba kama mtaalamu mahili wa Uchimi na kusema Ukweli na kuwa wasomi wa tanzania Akili zao ........
 
Back
Top Bottom