Na Andrew Mushi
MAKALA haya ni mwendelezo wa makala ya wiki iliyopita. Wiki jana nilijaribu kuonyesha kila mmoja wetu alivyo na nafasi kubwa ya kuwa chachu ya maendeleo. Ujumbe muhimu niliojaribu kuujengea hoja ni kuwa, katika sehemu mbali mbali tunamoishi, kuabudu au kufanyia kazi au biashara, kuna mianya na nafasi nyingi zinajitokeza na tukiamua kufungua macho yetu na kuthubutu kuzitumia , basi, mara tutaona mambo yanaanza kujipa. Nikajaribu kutoa mifano michache ya watu waliofanya vitu ambavyo jamii ilifaidi na kustawi kwa vile tu waliamua kujaribu.
Leo nitajaribu kuongelea nafasi tulio nayo tunapojumuika katika makundi mbali tunayoyaanzisha au tumeanzisha. Lakini, kabla sijasonga mbele niseme kwa nini nimesema hivi. Mara nyingi nimesika watu wakisema nitagombea ubunge na mara chache wanasema watagombea udiwani ili waende bungeni wakapige kelele ili maendeleo yaje.
Ni jambo la kusikitisha kuwa tumefikia pahala kuona ili serikali ifanye kitu au maendeleo yaje, ni lazima kupiga kelele. Nafikiri kama jamii huo ni udhaifu.
Inatakiwa tuelekeze muda mwingi na nguvu zaidi kupangilia mipango thabiti na inayofanana na mahitaji na matatizo yetu, na sio kupigiziana kelele.
Nimesoma katika barua pepe mtandaoni pale Mtanzania mmoja anaposema ameona jimboni kwake kuna matatizo makubwa sana ya usafiri na anajiandaa kugombea ubunge mwakani ili akawakomboe wananchi wa jimboni kwake. Ila nimecheka pale Mtanzania mwingine alipomjibu; Wewe kama unataka ubunge, usihangaike kuandaa sera wala habari za madaraja maana hazikupeleki popote.
Mtanzania huyo anamshauri mwenzake aandae pilau, kanga, t-shirts na kofia. Hapo ubunge utakuwa wake, ila eti aanze mapema maana mbunge aliyeko sasa kaanza maandalizi toka Krismas ya mwaka jana.
Mara nyingi tumeshuhudia watu waliojiunga katka makundi mbalimbali na kufanikiwa kuleta mabadiliko makubwa ndani ya jamii. Kikubwa hawakupitia milango ya siasa. Ili nisiongelee mambo ya kusadikika nitatumia mifano hai.
Mpaka kufikia miaka 15 iliyopita, tatizo la usawa wa kijinsia lilikuwa kubwa sana nchini mwetu. Wanawake walikuwa wana nafasi duni sana. Hali ilikuwa mbaya zaidi pale serikali ilipoanza kutekeleza mpango wa kurekebisha uchumi kwa kufuata masharti waliyoopewa na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), na Benki ya Dunia (WB) kunako mwishoni mwa miaka ya 1980. Kwa kifupi, kina mama waliteseka sana na walikuwa na hali duni maana huduma kama elimu, afya, maji na nyinginezo vilipopewa bajeti ndogo, wao ndio walikuwa waathirika wakuu
Mwaka 1994 Wakajitokeza Watanzania 12 (wanawake 10 na kina baba 2) wakasema hatuwezi kuacha hali iendelee kuwa mbaya. Wakajiunga wakaanzisha kikundi kilichojiita Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP). Wakasema wanataka kufanya kitu kimoja kitakacholeta mabadiliko makubwa ya kijamii. Wakachagua suala la Upangaji wa Bajeti kwa kuzingatia mahitaji ya makundi mbali mbali ya kijamii.
Walichomaanisha ni kuwa serikali imezoea kupanga bajeti bila kuzingatia makundi mbalimbali ya kijamii kama vile, kina mama, watoto, walemavu, wazee na vikongwe. Sana sana bajeti inazingatia mahitaji ya kina baba wenye nguvu ambao wakati huo huo hawana mahitaji mengi na majukumu mengi. Kama unabisha niambie kwa nini kila kikicha vilabu vya pombe vinaota kama uyoga na havikosi wateja, ni kina kina nani hao? Jibu unalo!
Waliona huu ni mlango nzuri wa kuingilia ili kujenga hoja yao na serikali na jamii ikawasikiliza. Wakaweka mikakati yao. Wakaona pa kuanzia ni wizara ya fedha maana wao ndio wanapanga bajeti. Hapa ndio jikoni eti! Hawakukimbilia kuanza na kila wizara au kuinyooshea mkono serikali. Unajua siku zote ili jambo lifanikiwe ni vizuri kuwa na mikakati mizuri na ambayo haiwezi kushindwa kirahisi.
Taratibu wakaanza kujenga urafiki na mahusiano na watendaji wa wizara ya fedha . Mara ya kwanza wizara ya fedha walipoona hawa kina mama, maana ndio walikuwa wengi na kina baba wachache wanaongelea upangaji bajeti kwa kwa macho ya kijinsia wakawashangaa, kwanza wao sio wataalamu wa bajeti wala fedha, na zaidi wala sio wachumi.
TGNP hawakukata tama, wakaaza kuwaeleza wanamaanisha nini wanaposema kuna uwezekano wa kupanga bajeti kwa kuzingatia mahitaji ya makundi mbalimbali . Kwa vile walikuwa wanajua wanachokisema na pia kuwaonyesha kwa mifano ni jinsi gani unaweza kuwa na bajeti ya kijinsia serikali ilianza kuwasikiliza.
Walipopewa mwanya wakautumia vizuri na baadhi ya maafisa wa bajeti wakaonyesha mwitikio chanya. Taratibu bajeti kuu ikaanza kuwa na mwelekeo wa kijinsia. Wizara nyingi tu zikaanza taratibu kuingiza masuala ya kijinsia katika mipango yao. Na kwa mikakati mizuri waliokuwa nayo na mbinu, wakapewa nafasi hata ya kuwapatia mafunzo watendaji serikalini jinsi ya kupanga bajeti na mipango yote ya maendeleo kwa kuzingatia jinsia.
Baada ya kuona wameanza kusikilizwa na serikali wakawa wanapanua wigo taratibu. Wakawa wanaenda bungeni Dodoma kuwaelimisha wabunge juu ya hoja yao. Pia wakaanza kuwaingizia hii hoja makundi mengine yanayotetea haki za kijamii. Wakaenda mbali zaidi kwa kushawishi uanzishwaji wa mitandao ya kijinsia katika baadhi ya wilaya hapa nchini. Kwa kifupi kila TGNP walichokifanya wamekuwa na mafanikio mazuri sana. Ila kumbuka bango walilolibeba ni bajeti ya kijinsia, basi, hawakubeba kila kitu!
Kwa wafuatiliaji wa mambo ya maendeleo Tanzania, leo hii kila utakapoenda utasikia watu wanasema jamani tuzingatie jinsia. Kwa kiasi kikubwa ni makundi kama TGNP na wengineo kama TAMWA, WLAC, TAWLA n.k waliopenyeza na kuzengea haya mambo ya jinsia yakawa ajenda ya taifa. Leo kwa kulinganisha na nchi nyingi duniani, Tanzania ni nchi inayojitahidi kupanga mipango yake kwa kuzingatia jinsia. Japo hatujafika lakini dhamira ya dhati toka kwa wanaume na wanawake wa nchi ipo.
Nataka nirudi kwako ndugu msomaji. Nasema badala ya wote kutaka kukimbilia katika siasa, ambako muda mwingi unatumika katika malumbano , tunaweza tukajiunga katika vikundi pale tunaapoona kuna jambo linatukera mtaani kwetu, kijijini kwetu, wilayani kwetu. Tunaweza tukaanza kuliwekea mikakati ya kulitatua. Sisemi mkimbilie kuanzisha NGOs, maana NGOs nyingi tu hazifanyi chochote mpaka wapate hela ya wafadhili. Hii nchi haiwezi kujengwa na hela zaa wafadhili.
Sio vizuri kuanza kwa kupiga kelele. Kama ni suala la elimu, mazingira, ajira, afya, usalama mnaweza kuwa na mikakati mizuri sana, na ikaleta mabadiliko makubwa sana. Najua unaweza kusema mipango mingi inakwamishwa na mafisadi waliojichimbia kila mahali, ni kweli, lakini pia hawa mafisadi papa na nyangumi walipata nafasi ya kuota mizizi kwa sababu tulikuwa tumelala usingizi mzito wakati wao wanafanya mipango ya kutuangamiza. Ila tukijipanga vizuri na kujiwekea mikakati mizuri, hakuna cha mapapa wala nyangumi watakaotukwamisha, tutafanikiwa tu!
amushi1@yahoo.com
Andrew Mushi anasomea shahada ya PhD katika masuala ya Uchumi na Utawala
CHANZO: kwanzajamii.com
MAKALA haya ni mwendelezo wa makala ya wiki iliyopita. Wiki jana nilijaribu kuonyesha kila mmoja wetu alivyo na nafasi kubwa ya kuwa chachu ya maendeleo. Ujumbe muhimu niliojaribu kuujengea hoja ni kuwa, katika sehemu mbali mbali tunamoishi, kuabudu au kufanyia kazi au biashara, kuna mianya na nafasi nyingi zinajitokeza na tukiamua kufungua macho yetu na kuthubutu kuzitumia , basi, mara tutaona mambo yanaanza kujipa. Nikajaribu kutoa mifano michache ya watu waliofanya vitu ambavyo jamii ilifaidi na kustawi kwa vile tu waliamua kujaribu.
Leo nitajaribu kuongelea nafasi tulio nayo tunapojumuika katika makundi mbali tunayoyaanzisha au tumeanzisha. Lakini, kabla sijasonga mbele niseme kwa nini nimesema hivi. Mara nyingi nimesika watu wakisema nitagombea ubunge na mara chache wanasema watagombea udiwani ili waende bungeni wakapige kelele ili maendeleo yaje.
Ni jambo la kusikitisha kuwa tumefikia pahala kuona ili serikali ifanye kitu au maendeleo yaje, ni lazima kupiga kelele. Nafikiri kama jamii huo ni udhaifu.
Inatakiwa tuelekeze muda mwingi na nguvu zaidi kupangilia mipango thabiti na inayofanana na mahitaji na matatizo yetu, na sio kupigiziana kelele.
Nimesoma katika barua pepe mtandaoni pale Mtanzania mmoja anaposema ameona jimboni kwake kuna matatizo makubwa sana ya usafiri na anajiandaa kugombea ubunge mwakani ili akawakomboe wananchi wa jimboni kwake. Ila nimecheka pale Mtanzania mwingine alipomjibu; Wewe kama unataka ubunge, usihangaike kuandaa sera wala habari za madaraja maana hazikupeleki popote.
Mtanzania huyo anamshauri mwenzake aandae pilau, kanga, t-shirts na kofia. Hapo ubunge utakuwa wake, ila eti aanze mapema maana mbunge aliyeko sasa kaanza maandalizi toka Krismas ya mwaka jana.
Mara nyingi tumeshuhudia watu waliojiunga katka makundi mbalimbali na kufanikiwa kuleta mabadiliko makubwa ndani ya jamii. Kikubwa hawakupitia milango ya siasa. Ili nisiongelee mambo ya kusadikika nitatumia mifano hai.
Mpaka kufikia miaka 15 iliyopita, tatizo la usawa wa kijinsia lilikuwa kubwa sana nchini mwetu. Wanawake walikuwa wana nafasi duni sana. Hali ilikuwa mbaya zaidi pale serikali ilipoanza kutekeleza mpango wa kurekebisha uchumi kwa kufuata masharti waliyoopewa na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), na Benki ya Dunia (WB) kunako mwishoni mwa miaka ya 1980. Kwa kifupi, kina mama waliteseka sana na walikuwa na hali duni maana huduma kama elimu, afya, maji na nyinginezo vilipopewa bajeti ndogo, wao ndio walikuwa waathirika wakuu
Mwaka 1994 Wakajitokeza Watanzania 12 (wanawake 10 na kina baba 2) wakasema hatuwezi kuacha hali iendelee kuwa mbaya. Wakajiunga wakaanzisha kikundi kilichojiita Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP). Wakasema wanataka kufanya kitu kimoja kitakacholeta mabadiliko makubwa ya kijamii. Wakachagua suala la Upangaji wa Bajeti kwa kuzingatia mahitaji ya makundi mbali mbali ya kijamii.
Walichomaanisha ni kuwa serikali imezoea kupanga bajeti bila kuzingatia makundi mbalimbali ya kijamii kama vile, kina mama, watoto, walemavu, wazee na vikongwe. Sana sana bajeti inazingatia mahitaji ya kina baba wenye nguvu ambao wakati huo huo hawana mahitaji mengi na majukumu mengi. Kama unabisha niambie kwa nini kila kikicha vilabu vya pombe vinaota kama uyoga na havikosi wateja, ni kina kina nani hao? Jibu unalo!
Waliona huu ni mlango nzuri wa kuingilia ili kujenga hoja yao na serikali na jamii ikawasikiliza. Wakaweka mikakati yao. Wakaona pa kuanzia ni wizara ya fedha maana wao ndio wanapanga bajeti. Hapa ndio jikoni eti! Hawakukimbilia kuanza na kila wizara au kuinyooshea mkono serikali. Unajua siku zote ili jambo lifanikiwe ni vizuri kuwa na mikakati mizuri na ambayo haiwezi kushindwa kirahisi.
Taratibu wakaanza kujenga urafiki na mahusiano na watendaji wa wizara ya fedha . Mara ya kwanza wizara ya fedha walipoona hawa kina mama, maana ndio walikuwa wengi na kina baba wachache wanaongelea upangaji bajeti kwa kwa macho ya kijinsia wakawashangaa, kwanza wao sio wataalamu wa bajeti wala fedha, na zaidi wala sio wachumi.
TGNP hawakukata tama, wakaaza kuwaeleza wanamaanisha nini wanaposema kuna uwezekano wa kupanga bajeti kwa kuzingatia mahitaji ya makundi mbalimbali . Kwa vile walikuwa wanajua wanachokisema na pia kuwaonyesha kwa mifano ni jinsi gani unaweza kuwa na bajeti ya kijinsia serikali ilianza kuwasikiliza.
Walipopewa mwanya wakautumia vizuri na baadhi ya maafisa wa bajeti wakaonyesha mwitikio chanya. Taratibu bajeti kuu ikaanza kuwa na mwelekeo wa kijinsia. Wizara nyingi tu zikaanza taratibu kuingiza masuala ya kijinsia katika mipango yao. Na kwa mikakati mizuri waliokuwa nayo na mbinu, wakapewa nafasi hata ya kuwapatia mafunzo watendaji serikalini jinsi ya kupanga bajeti na mipango yote ya maendeleo kwa kuzingatia jinsia.
Baada ya kuona wameanza kusikilizwa na serikali wakawa wanapanua wigo taratibu. Wakawa wanaenda bungeni Dodoma kuwaelimisha wabunge juu ya hoja yao. Pia wakaanza kuwaingizia hii hoja makundi mengine yanayotetea haki za kijamii. Wakaenda mbali zaidi kwa kushawishi uanzishwaji wa mitandao ya kijinsia katika baadhi ya wilaya hapa nchini. Kwa kifupi kila TGNP walichokifanya wamekuwa na mafanikio mazuri sana. Ila kumbuka bango walilolibeba ni bajeti ya kijinsia, basi, hawakubeba kila kitu!
Kwa wafuatiliaji wa mambo ya maendeleo Tanzania, leo hii kila utakapoenda utasikia watu wanasema jamani tuzingatie jinsia. Kwa kiasi kikubwa ni makundi kama TGNP na wengineo kama TAMWA, WLAC, TAWLA n.k waliopenyeza na kuzengea haya mambo ya jinsia yakawa ajenda ya taifa. Leo kwa kulinganisha na nchi nyingi duniani, Tanzania ni nchi inayojitahidi kupanga mipango yake kwa kuzingatia jinsia. Japo hatujafika lakini dhamira ya dhati toka kwa wanaume na wanawake wa nchi ipo.
Nataka nirudi kwako ndugu msomaji. Nasema badala ya wote kutaka kukimbilia katika siasa, ambako muda mwingi unatumika katika malumbano , tunaweza tukajiunga katika vikundi pale tunaapoona kuna jambo linatukera mtaani kwetu, kijijini kwetu, wilayani kwetu. Tunaweza tukaanza kuliwekea mikakati ya kulitatua. Sisemi mkimbilie kuanzisha NGOs, maana NGOs nyingi tu hazifanyi chochote mpaka wapate hela ya wafadhili. Hii nchi haiwezi kujengwa na hela zaa wafadhili.
Sio vizuri kuanza kwa kupiga kelele. Kama ni suala la elimu, mazingira, ajira, afya, usalama mnaweza kuwa na mikakati mizuri sana, na ikaleta mabadiliko makubwa sana. Najua unaweza kusema mipango mingi inakwamishwa na mafisadi waliojichimbia kila mahali, ni kweli, lakini pia hawa mafisadi papa na nyangumi walipata nafasi ya kuota mizizi kwa sababu tulikuwa tumelala usingizi mzito wakati wao wanafanya mipango ya kutuangamiza. Ila tukijipanga vizuri na kujiwekea mikakati mizuri, hakuna cha mapapa wala nyangumi watakaotukwamisha, tutafanikiwa tu!
amushi1@yahoo.com
Andrew Mushi anasomea shahada ya PhD katika masuala ya Uchumi na Utawala
CHANZO: kwanzajamii.com