Njowepo
JF-Expert Member
- Feb 26, 2008
- 9,710
- 2,226
FemAct yabeba wanafunzi elimu juu 60,000 kupiga kura
Na Restuta James
14th October 2010
Mtandao wa mashirika yasiyo ya kiserikali nchini (FemAct) na mashirika mengine ya kiraia, yameandaa mkakati mahususi kuwawezesha wanafunzi 60,000 wa vyuo vya elimu ya juu nchini kupigakura ambao utatanguliwa na maandamano ya amani wiki ijayo.
Wanaharakati hao wameazimia kuishinikiza serikali kufungua vyuo hivyo kabla ya Oktoba 31, mwaka huu na kwamba mkakati huo utatanguliwa na maandamano ya amani yatakayofanyika Ijumaa wiki ijayo hadi ofisi za Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), jijini Dar es Salaam.
Wanaharakati hao waliweka azimio hilo jijini Dar es Salaam jana wakati wa mdahalo uliolenga kuangalia mchakato wa Uchaguzi Mkuu na mwenendo wa kampeni, mdahalo uliofanyika makao makuu ya Ofisi za Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP).
Mwezeshaji wa mdahalo huo ambaye pia ni mwanaharakati mashuhuri nchini, Gema Akilimali, alisema timu ya wanaharakati wa FemAct na wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu, wataandaa tamko la azimio hilo ambalo watalisoma kesho kwa waandishi wa habari.
Alisema pamoja na mambo mengine, tamko hilo litaipa serikali siku tatu za kutangaza hatma ya wanafunzi hao 60,000 kama Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, alivyoahidi bungeni kwamba serikali ingeweka utaratibu wa kuwawezesha kupigakura.
Kama serikali haitasikia japokuwa hatuamini hivyo, tutatafuta namna ya kuwaleta wanafunzi hao vyuoni ili washiriki uchaguzi kama haki yao ya msingi, alisema mwanaharakati mmoja.
Tunajua hakuna kinachoshindikana kwa serikali kwani itapata wapi fedha siku tano baada ya uchaguzi mkuu hadi wafungue vyuo Novemba 5? tunajua pesa zipo tunaiomba serikali isivunje Katiba kwa kuwanyima wanafunzi hawa haki yao ya kupigakura, alisema Katibu Mtendaji wa Agenda Participation2000, Moses Kulaba. Kulaba ambaye alichambua ahadi za wagombea na ilani za vyama, alisema wanaharakati wamekuwa wakifuatilia kwa karibu ahadi pamoja na ilani za vyama, lakini wamebaini kwamba hazilengi kumkomboa mwananchi wa kawaida.
Alisema badala yake wanasiasa hususani wagombea wa urais wamekuwa wakitoa ahadi kubwa na nyingi ambazo wanaona hazitatekelezeka.
Alisema wanasiasa nao wamepoteza mwelekeo wanapopanda majukwaani wanaishia kurushiana maneno na wapinzani wao badala ya kuzungumzia matatizo ya wananchi pamoja na yale yaliyoko kwenye ilani zao.
Tunafuatilia kwa makini sana ahadi za kila mgombea, wakati mwingine tunajiuliza hivi hata hii ameahidi ataweza kuitekeleza?alihoji na kuongeza:
Lakini kikubwa kinachojitokeza kwenye kampeni ni mipasho kwa mgombea huyu kueleza sifa mbaya za mwenzake, wananchi hatuna nafasi ya kuuliza maswali.
Kulaba alisema wanaharakati wanashangaa kuona kwamba wagombea wanaacha kunadi sera zao na badala yake wanaishia kupashana. Haya ya kupashana sisi hatutaki kuyasikia tunahitaji kujua tutatokaje hapa tulipo, alisema.
Alisema kampeni za vyama kama Chama Cha Mapinduzi (CCM), Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na Chama Cha Wananchi (CUF), zinaeleza kuboresha huduma za jamii kama elimu na afya, lakini hazielezi kwa kina namna ambavyo suala hilo litatekelezwa.
Mwenyekiti wa Bodi ya TGNP, Mary Rusimbi, alisema mwenendo wa kampeni pamoja na ilani za vyama, hazionyeshi chama ambacho kinaonyesha kufumua mfumo mbovu uliolifikisha taifa katika umasikini uliopo na namna ya kuubadilisha ili kuleta mabadiliko.
Alisema wanaharakati wanaona kwamba kama mfumo uliopo hautabadilishwa, miaka mitano ijayo kutakuwa na ongezeko kubwa la matabaka kati ya masikini na matajiri, wasomi matajiri na masikini wasiosoma.
Lazima kwanza tuondoe mifumo ya kitabaka, tumesikia mgombea mmoja atajenga hospitali zaidi, lakini kama mfumo wa afya utakuwa hivi ulivyo nani ataweza kutibiwa huko, kama hali ikiwa hivi matabaka yataendelea kuongezeka, alisema.
Rais na Mwenyekiti wa Taarifa kwa Umma kutoka Chama cha Haki za Binadamu cha Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam, Mhapa Peter, ambaye alifuatana na Makamu wa Rais wa Serikali ya wanafunzi wa chuo hicho, Materu Jacqueline, alilaani msimamo wa serikali na kuitaka kusitisha msimamo huo.
Ni kwa vipi tofauti ya siku tano yaani Oktoba 31 hadi Novemba 5, itaathiri mfumo wa fedha wa serikali na kushindwa kabisa kutoa fedha ili wanafunzi wapate haki yao ya kikatiba?
Tunaiomba serikali itoe utaratibu ulioahidiwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, bungeni kwamba sisi tungepiga kura, alisema.
Baadhi ya walemavu waliokuwepo kwenye mdahalo huo, walisema mfumo wa uchaguzi wa mwaka huu umeyabagua makundi maalum kama walemavu.
Hata hivyo, Waziri Mkuu, Pinda na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Jumanne Maghembe kwa nyakati tofauti, wamekaririwa wakisema kwamba serikali haitaweza kubadilisha uamuzi wake wa kufungua vyuo vikuu kabla ya Novemba.
Profesa Maghembe alikaririwa akisema kwamba vyuo vya elimu ya juu sio taasisi zinazoendesha siasa, bali ni maeneo yanayotumika kufundisha watalaamu wa kada mbalimbali.
Pia Nec juzi ilipigilia msumari wa mwisho kwa kusema kwamba wanafunzi hao wana hiari ya kwenda wenyewe vituo walivyojiandikisha kupigakura kwa sababu hakuna uwezekano wa kubadili daftari la wapigakura kwa kuwa lilikwisha kufungwa.
CHANZO: NIPASHE