Diwani achanganyikiwa akiwa ukumbini

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
268
WAKATI Chama Cha Mapinduzi (CCM) kikishinda nafasi ya uenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma, Diwani wa Viti Maalumu wa chama hicho Hamisa Mtulla ameshindwa kuapishwa wala kupiga kura baada ya kukumbwa na fadhaa (kuchanganyikiwa) licha ya kuwemo ukumbini.

Licha ya jitihada kubwa iliyofanywa na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma, Dominick Kweka, Mkuu wa Wilaya ya Kigoma, John Mongela na Hakimu Mkazi wa Mkoa wa Kigoma, Emanuel Mrangu, hazikufanikiwa kufanikisha kiapo hicho.

Mwandishi wa habari hizi alishuhudia viongozi hao wakimchukua diwani huyo na kwenda naye Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji kwa ajili ya kumsaidia ili aweze kuapa, lakini haikusaidia.

Kushindwa kuapishwa kwa diwani huyo kunatokana kushindwa kuzungumza na hata alipokuwa akisemeshwa na viongozi hao, alikuwa akizungumza maneno ambayo hayakuwa yakieleweka.

Baada ya kushindikana jambo hilo, alirudishwa katika ukumbi wa mikutano ambako uchaguzi
ulikuwa ukiendelea na licha ya kuwepo ukumbini, hakuwa akijua au kuwa na ufahamu wa kilichokuwa kikiendelea.

Sambamba na diwani huyo wa CCM kutopiga kura, pia Diwani wa Viti Maalumu kwa tiketi ya Chadema, Sauda Matete naye alishindwa kushiriki kwenye uchaguzi huo baada ya kupatwa na kile kinachodaiwa kuchanganyikiwa akili na hivyo kushindwa kufika kabisa kwenye uchaguzi huo.

Katika uchaguzi huo, Diwani wa Kata ya Mkigo, Hamisi Betese wa CCM alitwaa nafasi ya uenyekiti kwa kupata kura 18 dhidi ya kura 16 za Ally Kisala ambaye ni Diwani wa Kata ya Mwandiga kwa Chadema.

Nafasi ya Makamu Mwenyekiti wa halmashauri ilichukuliwa na Diwani wa Kata ya Ilagala, Hamisi Mkwavi aliyepata 18 dhidi ya kura 16 za mpinzani Kumbo Fidelis wa NCCR – Mageuzi.

Akizungumzia matokeo hayo, Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (Chadema), alisema wanakubaliana na matokeo hayo na kwamba hata kama wameshindwa, lakini wameshindwa kwa heshima kutokana na kuweza kulinda kura zao zote.
 
Back
Top Bottom