BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,789
- 288,013
`Dili` la Mkapa na Yona latesa vigogo...
2009-01-23 10:12:34
Na Joseph Mwendapole
2009-01-23 10:12:34
Na Joseph Mwendapole
Serikali imeshindwa kuwasilisha ripoti ya mgodi wa Kiwira Coal and Power Ltd, katika Mkutano wa 14 wa Bunge unaotarajiwa kuanza mjini Dodoma wiki ijayo, licha ya Wizara ya Nishati na Madini kusema ripoti hiyo imekamilika na inasubiri kupangiwa ratiba ya kuiwasilisha.
Kwa mujibu wa ratiba ya shughuli za Bunge iliyopatikana jana jijiniDar es Salaam, ripoti ya mgodi huo haijapangwa kama moja ya mambo yatakayojadiliwa katika mkutano huo.
Ratiba ya shughuli hizo inaonyesha moja ya mambo mazito yatakayojadiliwa ni pamoja na utekelezaji wa maazimio ya Bunge kuhusu zabuni ya kuzalisha umeme wa dharura ulioipa kampuni ya Richmond Development Company LLC, ya Hoston Texas, Marekani mwaka 2006.
Ratiba hiyo inaonyesha pia serikali italieleza Bunge kuhusu utendaji kazi usioridhisha wa kampuni ya kupakia na kupakua makontena bandarini TICTS na uuzwaji wa nyumba za serikali.
Katika mkutano huo, serikali inatarajiwa kutoa tamko kuhusu uendeshaji wa Shirika la Ndege Tanzania (ATCL).
Suala lingine muhimu litakalojadiliwa kwenye mkutano huo ni pamoja na utendaji usioridhidisha wa Shirila la Reli Tanzania (TRL) unaofanywa na kampuni ya RITES ya India.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Bunge), Philip Marmo, aliliambia gazeti hili jana kuwa suala la Kiwira aulizwe Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini, William Shellukindo.
Marmo alisema inawezekana kamati hiyo imeamua kulijadili na kulimaliza tatizo hilo ndani ya Kamati kwa kuwa si lazima kila hoja ijadiliwe ndani ya Bunge.
Alipotafutwa kuzungumzia suala hilo, Shellukindo alikuwa amezima simu yake wakati simu ya Spika wa Bunge, Samuel Sitta, ilikuwa ikiita na baadaye ikazima kabisa.
Juzi Shellukindo aliliambia gazeti hili kuwa taarifa walizopewa na menejimenti ya mgodi huo zinaonyesha kuwa familia ya Rais Mstaafu Benjamin Mkapa na Waziri wa zamani wa Nishati na Madini, Daniel Yona ni sehemu ya umiliki wa mgodi huo.
Aliwaeleza waandishi wa habari kuwa Kampuni ya Tan Power Resources Ltd ambayo ilianzishwa mwaka 2005 ndiyo iliuziwa mgodi huo na serikali.
Alisema kampuni hiyo ni muunganiko wa makampuni manne yaliyoungana kwa lengo la kuuziwa mgodi huo na kuongeza kuwa makampuni hayo yana wamiliki tofauti.
Aliyataja makampuni hayo kuwa Fosnlid ambayo wamiliki wake ni Nick Mkapa, Fostar Mkapa (wanaodaiwa kuwa ni watoto wa Mkapa) na B. Mahembe wakati Kampuni ya Devconsult Ltd wamiliki wake ni D. Yona na Danny Yonna Jr.
Kampuni nyingine ni Choice Industries inayomilikiwa na Joe Mbuna na Goodyeer Francis; Universal Technologies inayomilikiwa na Wilfred Malekea na Evan Mapundi.
Mgodi huo wenye thamani ya Sh. bilioni 4 ulinunuliwa kwa Sh. milioni 700, lakini zilizotolewa zilikuwa Sh. milioni 70 tu.
Wanasiasa mbalimbali wamekuwa wakishinikiza Mkapa afikishwe mahakamani kutokana na kutumia madaraka vibaya alipokuwa Ikulu.
Akizungumza na Nipashe jana, Dk. Wililbrod Slaa, alisema hakuna sababu ya kutomfikisha mahakamani Mkapa kwani ameshabainika kuwa alijiuzia mgodi huo kinyume cha taratibu.
Alisema habari kwamba ili kumfikisha Mkapa mahakamani kunahitajika aondolewe kinga si za kweli kwani Katiba haisemi hivyo.
``Nimesoma Katiba yote hakuna sehemu ambayo tunatakiwa kumwondolea kinga Mkapa, anayehitaji kuondolewa kinga ni Rais aliyeko madarakani tu, lakini kwa Mkapa Katiba haisemi hivyo kwa hiyo tusipoteze muda tumpeleke mahakamani akajibu tuhuma dhidi yake,`` alisema.
Aidha, alisema Katiba inasema ili Rais aliyeko madarakani aondolewe kinga ya kutokushtakiwa inahitajika theluthi mbili ya kura za wabunge wote, lakini haisemi hivyo kwa Rais aliyemaliza muda wake.
Alisema Mkapa alipewa dhamana ya kulinda rasilimali za Watanzania, lakini kinyume chake aliamua kufanya biashara akiwa madarakani.
``Hapa hakuna namna ambayo Mkapa atajinusuru, akamatwe yeye na Yona wahojiwe namna walivyojiuzia mgodi wa Kiwira na hatua za kisheria zichukuliwe,`` alisema.
SOURCE: Nipashe