HABARI ndiyo hiyo! Mabingwa wa Ligi Kuu ya soka Tanzania Bara, Yanga imemsajili kiungo wa zamani wa Simba, Athuman Idd Chuji kwa ajili ya kuitumikia timu hiyo katika mzunguko wa pili wa ligi hiyo na michuano ya kimataifa, imefahamika.
Habari za kuaminika kutoka ndani ya klabu ya Yanga, zinasema kwamba, Chuji alimwaga wino wa kuichezea timu hiyo kwa miaka miwili baada ya kukamilisha mazungumzo na viongozi wa kamati ya usajili.
Ni kweli Chuji tumemsainisha mkataba wa miaka miwili, baada ya kukamilika kwa mazungumzo, hivyo Chuji ni mmoja kati ya wachezaji watakaovaa uzi wa kijani na njano katika mzunguko wa pili wa Ligi Kuu Bara na michuano ya kimataifa, alisema kiongozi mmoja wa Yanga ambaye hakupenda kutajwa jina lake.
Hata hivyo, huenda klabu hiyo ikaingia tena katika mgogoro wa kumgombea kiungo huyo na mahasimu wao, Simba, ambao mwaka huu ilimsainisha mkataba wa miaka miwili kabla ya kumpeleka kwa mkopo Villa Squad.
Hali ya kuuzwa kwa mkopo Villa Squad, haikumridhisha Chuji, ambaye aligoma na kudai yuko radhi kuuza karanga kuliko kwenda kuichezea timu hiyo inayosuasua kwenye ligi hiyo.
Kama hiyo haitoshi, Chuji alitishia kuchukua sheria kwa Wekundu wa Msimbazi, ambako kupitia kwa mwanasheria wake, alitishia kusimamisha ligi iwapo asingerejeshwa Simba, lakini Simba walibaki na msimamo wa kutokubali kumtumia kiungo huyo, sambamba kudai wameishavunja naye mkataba.
Nalo Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) baada ya msigano huo, liliendelea kusisitiza kuwa Chuji ni mali ya Simba, kwa kuwa aliingia nao mkataba wa miaka miwili, pia kuwa na leseni na ndiyo maana akapata nafasi ya kuichezea katika michuano ya klabu bingwa Afrika Mashariki na Kati Kombe la Kagame.
Chuji aliwahi kuichezea Simba akitokea timu ya Polisi Dodoma, kabla ya baadaye kutimkiaYanga katika uhamisho uliozua mzozo mkubwa baina ya watani hao wa jadi.
JamiiForums uses cookies to help personalise content, tailor your experience and to keep you logged in if you register.
By continuing to use this site, you are consenting to our use of cookies.