Mzee Mwanakijiji
Platinum Member
- Mar 10, 2006
- 33,476
- 39,995
Na Lula wa Ndali Mwananzela (Raia Mwema)
NATUMAINI msomaji wewe ni mmoja wa watu wenye uwezo wa kuona, kufikiri, kuchambua mambo na hatimaye kufikia uamuzi baada ya kufanya uchambuzi wa kutosha juu ya jambo fulani.
Naamini kuwa katika kufikia uamuzi huo huongozwi na hisia zako (woga, wivu, tamaa, kisasi, uchungu n.k) bali unaongozwa na uhalisia wa vitu kwa kutumia akili. Si kwamba hisia ni mbaya bali kwa vile hisia ni rahisi kushawishiwa na matukio na mazingira, uwezo wa kiakili kupima mambo ni kinga kubwa zaidi ya kuburuzwa kuliko hisia.
Fikiria mtu anapokuja kwako na kusema anaomba umsaidie kwa sababu mtoto wake ni mgonjwa. Hisia zako zitataka mara moja kutoa msaada lakini akili mara moja itakupa tahadhari kuweza kumpima huyo anayekuomba msaada. Utamuhoji maswali ya kiakili ili kuweza kupekua pekua ili hatimaye ufikie mahali uamue kutoa msaada. Katika kufanya hivyo maswali kama mtoto yuko wapi, anaumwa nini, nani anamuangalia sasa hivi n.k yatakuwa ni muhimu sana. Lakini, kama amekuja na mtoto mkononi, na unaona mtoto kakatwa kisu na anavuja damu, hisia zako zitakubaliana na akili yako mara moja kutoa msaada bila ya kuhoji maswali mengi.
Ndiyo maana ni matumaini yangu kuwa tunapoelekea Uchaguzi Mkuu, Watanzania watavuka kizingiti cha maamuzi ya kihisia na kufanya maamuzi ya kiakili zaidi. Maamuzi ambayo hayatafanywa kwa sababu ya kuwafurahisha watu au kuwaonea watu aibu; maamuzi ambayo yatafanywa yakilenga kujipa uwezo wa kweli kujiletea maendeleo. Maamuzi ambayo yataamua kama misaada inatosha kumfanya mtu achaguliwe.
Kuanzia mwishoni mwa mwaka jana na hasa wakati huu na bila ya shaka miezi inayokuja wale wanaotaka kutuongoza watapita wakijaribu kuwatongoza Watanzania kwa misaada mbalimbali. Viongozi hawa (kama tunaweza kuwaita hivyo) wanajipitisha sasa hivi kwa misaada mbalimbali ambayo ilitetewa na mwenzao mmoja juzi bungeni kuwa ni haki yao kutoa misaada kwa vile ni wabunge walioko madarakani. Hebu tuwapime kwa kutumia akili kidogo.
Hivi umewahi kuona ombaomba aliyeacha uombaomba kwa sababu hatimaye amepata vya kutosha kuanzisha maisha yake? Unaweza kumtafuta ombaomba ambaye anaweza kukuonyesha, kwa majivuno, kile alichojenga katika maisha yake kwa kutumia misaada? Unafikiri ni kipi rahisi kwa ombaomba kupewa msaada au kupewa shamba akalime? Ni lipi jepesi kumpa mtu samaki akale au kumpeleka mtoni na kumfundisha kuvua? Ni wazi kwa mtazamo wa ombaomba kupata msaada wa kutatua tatizo la sasa ni bora zaidi kuliko kuanza kushika jembe kulima ili ajipatie chakula yeye mwenyewe, na ni wazi kwa mwenye njaa ni rahisi kukimbilia samaki aliyevuliwa na wengine kuliko kutumia muda wa yeye kujifunza kuvua.
Lakini Watanzania wakiongozwa na serikali ya CCM wanategemea misaada hadi inaudhi (wengine wanadai inakera). Na wakati huu wa kampeni wagombea na wale wenye kutaka kugombea nafasi mbalimbali watapita na kujipitishapitisha kama kina dada poa kwenye miji na vijiji vyetu kila mmoja akiwa mkarimu na mwema; watapita wakija na masanduku ya misaada mbalimbali, misaada ambayo wameihalalisha kuwa sisi wananchi tunaihitaji.
Kwa vile ni rahisi zaidi kupokea misaada kuliko kupewa njia ya kujikwamua, wapo watu kati yetu ambao wanasubiri misaada na hufanya hima kukinga mikono kupokea misaada hiyo bila ya kujiuliza maswali. Hawa ndio wanawawezesha viongozi kuthubutu kuja na gia ya misaada.
Fikra hizi za kutegemea misaada na kukumbatia misaada zimeletwa nchini na CCM hii ya kina Benjamin Mkapa na Jakaya Kikwete. Wamelidekeza Taifa kiasi cha kuwaharibu Watanzania. Watanzania leo hawawezi kufikiria kujiletea maendeleo bila misaada na hakuna mtu anayeweza kuja kutaka kugombea bila ya kutoa ahadi za misaada, na wapo ambao wameishiwa hoja kabisa isipokuwa hoja ya misaada.
Nakumbuka mmoja katika kutafuta kura kwa wananchi aliwaahidi kuwa eti akichaguliwa atawaletea maendeleo kwa sababu anafahamiana na wafadhili mbalimbali wa nje ya nchi. Wapo wengine ambao nao kutokana na connections zao huko majuu wanakuja na ahadi za mema kwa sababu wanaweza kuleta vitu mbalimbali kama misaada.
Kinachosikitisha ni kuwa Watanzania kama makinda ya ndege tunduni tumefungua vinywa vyetu na kupokea bila kuuliza; iwe ni funza, mchwa, vipepeo au nyasi tu! Tunapokea na kushangilia bila kuhoji na kuwahoji.
Matokeo yake ya kwanza ni kuwa wagombea wamekwishakujua gia ya kuingia nayo ni misaada. Hata mimi leo nikitaka kugombea jimbo lolote kikundi cha watu wenye fikra fupi watakuja na kuuliza umelifanyia nini jimbo wakimaanisha mbona hatujawahi kuona misaada yako?
Nikijenga hoja kuwa sijatoa msaada kwa sababu hamuhitaji kusaidiwa mnahitaji kuongozwa kujiletea maendeleo wataniangalia kwa kebehi huku wakikimbilia kwa mgombea mbeba misaada! Tumedekezwa na tukadekeka!
Ninachosema ni kuwa kama tunakubali misaada ya kiudhalilishaji na kudekezana ati kwa sababu kwanini tukatae tujue kabisa tunauza dhamira na haki zetu. Mtu ambaye anafuata kampeni ya mgombea kwa sababu ya misaada ni mtu ambaye amepoteza uzalendo na ni tegemezi kifikra. Kama wananchi kwenye majimbo mbalimbali watawapima wagombea wa mwaka huu kwa kuangalia nani anapita na misaada mikubwa na mingi basi Taifa lina matatizo si katika uongozi tu bali zaidi kwa wale wanaoongozwa. Nina mapendekezo matatu.
Watanzania walio huru kifikra wakatae misaada ya kizugaji inayopitishwa sasa majimboni. Kukataa kwenyewe wala si kugumu. Mgombea akija na misaada yake anatakiwa kuulizwa:
Kwanini unaleta misaada hii sasa?
Bila ya misaada yako unataka tukuchague kwa nini na utafanya nini kutuongoza kujitegemea na kwa vipi?
Tuzingatie vile vile kuwa fikra hizi za uombaomba wa kudumu zipo ndani ya Serikali; zinaundwa na zinakolezwa na Serikali. Fikiria majibu ya juzi bungeni Serikali ikimjibu Paul Kimiti (Sumbawanga Mjini) juu ya kuendelea kutoa jimboni kwake kwake misaada mbalimbali. Serikali imekubali kuwa jambo hili halina tatizo.
Kinachonishangaza ni kwanini waulizie suala la kutoa misaada badala ya kuongoza shughuli za kujitegemea? Hivi kama wabunge walioko sasa wakifanya mambo ya kujitegemea kusaidia kujenga shule (si kutoa fedha tu bali kuwapo wenyewe na nyundo), kuongoza katika usafi katika maeneo yao, n.k kuna mtu atawalalamikia? Kwanini walilie kutoa misaada; jibu jepesi ni kuwa ndiyo gia pekee waliyonayo ya kuombea kura tena vinginevyo wangekuwa na rekodi ya kutuambia miaka minne iliyopita wamefanya nini na hayo yangetosha kuwafanya wananchi wawakubali tena; tatizo ni kuwa hawana cha kuonyesha sasa, wamebakia na misaada!
Mkiridhika au kutoridhika na majibu ya maswali hayo mawili (na mengine mnayoweza kujitungia) mnamuambia arudi na misaada yake alikoitoa na aiweke akiba hadi akichaguliwa ndiyo ailete tena (kama kweli ana lengo la kuwasaidia) na kama kweli alikuwa na lengo la kuwasaidia wananchi basi ailete misaada hiyo baada ya uchaguzi. Ninawahakikishia mtawachuja wagombea nyinyi wenyewe kabla ya vyama vyao maana wataingia kwa gia gani nyingine ukiondoa misaada ya kuwafanya wananchi mazobo?
Pendekezo la pili ni kuwa kwa vile Rais Kikwete amedai kuwa anataka uchaguzi huu uwe safi na rushwa zisitumike basi la kwanza ni kuzuia misaada yote ya mtu binafsi mwenye kutaka kutoa kwa jimbo analotaka kugombea. Si kuipiga marufuku bali kutoa maelekezo mepesi kuwa misaada yoyote ambayo si sehemu ya utendaji wa Serikali itasitishwa hadi baada ya Uchaguzi Mkuu na kama kweli kuna mtu anataka kutoa msaada basi msaada huo uende nje ya jimbo lake! Nawahakikishia misaada yote itatoweka ghafla na mara moja uwanja utakuwa huru zaidi kwa wagombea mbalimbali kushindana kwa hoja, si kwa wingi wa msaada.
Pendekezo la mwisho ni kuwa kwa vile inaonekana wabunge wengi wanataka kutoa misaada kwenye majimbo yao ili wasaidie wananchi wao basi watoe misaada hiyo kupitia taasisi za kutoa misaada! Kwa mfano, waziri mmoja alipewa misaada ya kuwapelekea wananchi wa jimbo lake huko Kilosa, misaada ambayo ilitolewa na Uchina. Misaada hiyo alipewa Rais Kikwete naye akampa Mustafa Mkulo aiwasilishe kwenye jimbo lake na hivyo kumpigia debe kijanja kumbuka Rais angeweza kutoa misaada hiyo kwa Ofisi ya Waziri Mkuu na kuwaacha wao waamue jinsi ya kuifikisha kule au angeweza kutoa kwa Chama cha Msalaba Mwekundu ambacho Serikali yake haijakisaidia kukipa uwezo (angalau sijui kama imefanya hivyo kwenye mafuriko ya hivi karibuni).
Vinginevyo, nina uhakika mapendekezo yote matatu hayawezi kukubalika kwa CCM, au kwa Rais Kikwete, kwa Yusuf Makamba na msululu wa wengineo, kwani wakikubali wataingilia gia gani ili waombe uongozi?
NATUMAINI msomaji wewe ni mmoja wa watu wenye uwezo wa kuona, kufikiri, kuchambua mambo na hatimaye kufikia uamuzi baada ya kufanya uchambuzi wa kutosha juu ya jambo fulani.
Naamini kuwa katika kufikia uamuzi huo huongozwi na hisia zako (woga, wivu, tamaa, kisasi, uchungu n.k) bali unaongozwa na uhalisia wa vitu kwa kutumia akili. Si kwamba hisia ni mbaya bali kwa vile hisia ni rahisi kushawishiwa na matukio na mazingira, uwezo wa kiakili kupima mambo ni kinga kubwa zaidi ya kuburuzwa kuliko hisia.
Fikiria mtu anapokuja kwako na kusema anaomba umsaidie kwa sababu mtoto wake ni mgonjwa. Hisia zako zitataka mara moja kutoa msaada lakini akili mara moja itakupa tahadhari kuweza kumpima huyo anayekuomba msaada. Utamuhoji maswali ya kiakili ili kuweza kupekua pekua ili hatimaye ufikie mahali uamue kutoa msaada. Katika kufanya hivyo maswali kama mtoto yuko wapi, anaumwa nini, nani anamuangalia sasa hivi n.k yatakuwa ni muhimu sana. Lakini, kama amekuja na mtoto mkononi, na unaona mtoto kakatwa kisu na anavuja damu, hisia zako zitakubaliana na akili yako mara moja kutoa msaada bila ya kuhoji maswali mengi.
Ndiyo maana ni matumaini yangu kuwa tunapoelekea Uchaguzi Mkuu, Watanzania watavuka kizingiti cha maamuzi ya kihisia na kufanya maamuzi ya kiakili zaidi. Maamuzi ambayo hayatafanywa kwa sababu ya kuwafurahisha watu au kuwaonea watu aibu; maamuzi ambayo yatafanywa yakilenga kujipa uwezo wa kweli kujiletea maendeleo. Maamuzi ambayo yataamua kama misaada inatosha kumfanya mtu achaguliwe.
Kuanzia mwishoni mwa mwaka jana na hasa wakati huu na bila ya shaka miezi inayokuja wale wanaotaka kutuongoza watapita wakijaribu kuwatongoza Watanzania kwa misaada mbalimbali. Viongozi hawa (kama tunaweza kuwaita hivyo) wanajipitisha sasa hivi kwa misaada mbalimbali ambayo ilitetewa na mwenzao mmoja juzi bungeni kuwa ni haki yao kutoa misaada kwa vile ni wabunge walioko madarakani. Hebu tuwapime kwa kutumia akili kidogo.
Hivi umewahi kuona ombaomba aliyeacha uombaomba kwa sababu hatimaye amepata vya kutosha kuanzisha maisha yake? Unaweza kumtafuta ombaomba ambaye anaweza kukuonyesha, kwa majivuno, kile alichojenga katika maisha yake kwa kutumia misaada? Unafikiri ni kipi rahisi kwa ombaomba kupewa msaada au kupewa shamba akalime? Ni lipi jepesi kumpa mtu samaki akale au kumpeleka mtoni na kumfundisha kuvua? Ni wazi kwa mtazamo wa ombaomba kupata msaada wa kutatua tatizo la sasa ni bora zaidi kuliko kuanza kushika jembe kulima ili ajipatie chakula yeye mwenyewe, na ni wazi kwa mwenye njaa ni rahisi kukimbilia samaki aliyevuliwa na wengine kuliko kutumia muda wa yeye kujifunza kuvua.
Lakini Watanzania wakiongozwa na serikali ya CCM wanategemea misaada hadi inaudhi (wengine wanadai inakera). Na wakati huu wa kampeni wagombea na wale wenye kutaka kugombea nafasi mbalimbali watapita na kujipitishapitisha kama kina dada poa kwenye miji na vijiji vyetu kila mmoja akiwa mkarimu na mwema; watapita wakija na masanduku ya misaada mbalimbali, misaada ambayo wameihalalisha kuwa sisi wananchi tunaihitaji.
Kwa vile ni rahisi zaidi kupokea misaada kuliko kupewa njia ya kujikwamua, wapo watu kati yetu ambao wanasubiri misaada na hufanya hima kukinga mikono kupokea misaada hiyo bila ya kujiuliza maswali. Hawa ndio wanawawezesha viongozi kuthubutu kuja na gia ya misaada.
Fikra hizi za kutegemea misaada na kukumbatia misaada zimeletwa nchini na CCM hii ya kina Benjamin Mkapa na Jakaya Kikwete. Wamelidekeza Taifa kiasi cha kuwaharibu Watanzania. Watanzania leo hawawezi kufikiria kujiletea maendeleo bila misaada na hakuna mtu anayeweza kuja kutaka kugombea bila ya kutoa ahadi za misaada, na wapo ambao wameishiwa hoja kabisa isipokuwa hoja ya misaada.
Nakumbuka mmoja katika kutafuta kura kwa wananchi aliwaahidi kuwa eti akichaguliwa atawaletea maendeleo kwa sababu anafahamiana na wafadhili mbalimbali wa nje ya nchi. Wapo wengine ambao nao kutokana na connections zao huko majuu wanakuja na ahadi za mema kwa sababu wanaweza kuleta vitu mbalimbali kama misaada.
Kinachosikitisha ni kuwa Watanzania kama makinda ya ndege tunduni tumefungua vinywa vyetu na kupokea bila kuuliza; iwe ni funza, mchwa, vipepeo au nyasi tu! Tunapokea na kushangilia bila kuhoji na kuwahoji.
Matokeo yake ya kwanza ni kuwa wagombea wamekwishakujua gia ya kuingia nayo ni misaada. Hata mimi leo nikitaka kugombea jimbo lolote kikundi cha watu wenye fikra fupi watakuja na kuuliza umelifanyia nini jimbo wakimaanisha mbona hatujawahi kuona misaada yako?
Nikijenga hoja kuwa sijatoa msaada kwa sababu hamuhitaji kusaidiwa mnahitaji kuongozwa kujiletea maendeleo wataniangalia kwa kebehi huku wakikimbilia kwa mgombea mbeba misaada! Tumedekezwa na tukadekeka!
Ninachosema ni kuwa kama tunakubali misaada ya kiudhalilishaji na kudekezana ati kwa sababu kwanini tukatae tujue kabisa tunauza dhamira na haki zetu. Mtu ambaye anafuata kampeni ya mgombea kwa sababu ya misaada ni mtu ambaye amepoteza uzalendo na ni tegemezi kifikra. Kama wananchi kwenye majimbo mbalimbali watawapima wagombea wa mwaka huu kwa kuangalia nani anapita na misaada mikubwa na mingi basi Taifa lina matatizo si katika uongozi tu bali zaidi kwa wale wanaoongozwa. Nina mapendekezo matatu.
Watanzania walio huru kifikra wakatae misaada ya kizugaji inayopitishwa sasa majimboni. Kukataa kwenyewe wala si kugumu. Mgombea akija na misaada yake anatakiwa kuulizwa:
Kwanini unaleta misaada hii sasa?
Bila ya misaada yako unataka tukuchague kwa nini na utafanya nini kutuongoza kujitegemea na kwa vipi?
Tuzingatie vile vile kuwa fikra hizi za uombaomba wa kudumu zipo ndani ya Serikali; zinaundwa na zinakolezwa na Serikali. Fikiria majibu ya juzi bungeni Serikali ikimjibu Paul Kimiti (Sumbawanga Mjini) juu ya kuendelea kutoa jimboni kwake kwake misaada mbalimbali. Serikali imekubali kuwa jambo hili halina tatizo.
Kinachonishangaza ni kwanini waulizie suala la kutoa misaada badala ya kuongoza shughuli za kujitegemea? Hivi kama wabunge walioko sasa wakifanya mambo ya kujitegemea kusaidia kujenga shule (si kutoa fedha tu bali kuwapo wenyewe na nyundo), kuongoza katika usafi katika maeneo yao, n.k kuna mtu atawalalamikia? Kwanini walilie kutoa misaada; jibu jepesi ni kuwa ndiyo gia pekee waliyonayo ya kuombea kura tena vinginevyo wangekuwa na rekodi ya kutuambia miaka minne iliyopita wamefanya nini na hayo yangetosha kuwafanya wananchi wawakubali tena; tatizo ni kuwa hawana cha kuonyesha sasa, wamebakia na misaada!
Mkiridhika au kutoridhika na majibu ya maswali hayo mawili (na mengine mnayoweza kujitungia) mnamuambia arudi na misaada yake alikoitoa na aiweke akiba hadi akichaguliwa ndiyo ailete tena (kama kweli ana lengo la kuwasaidia) na kama kweli alikuwa na lengo la kuwasaidia wananchi basi ailete misaada hiyo baada ya uchaguzi. Ninawahakikishia mtawachuja wagombea nyinyi wenyewe kabla ya vyama vyao maana wataingia kwa gia gani nyingine ukiondoa misaada ya kuwafanya wananchi mazobo?
Pendekezo la pili ni kuwa kwa vile Rais Kikwete amedai kuwa anataka uchaguzi huu uwe safi na rushwa zisitumike basi la kwanza ni kuzuia misaada yote ya mtu binafsi mwenye kutaka kutoa kwa jimbo analotaka kugombea. Si kuipiga marufuku bali kutoa maelekezo mepesi kuwa misaada yoyote ambayo si sehemu ya utendaji wa Serikali itasitishwa hadi baada ya Uchaguzi Mkuu na kama kweli kuna mtu anataka kutoa msaada basi msaada huo uende nje ya jimbo lake! Nawahakikishia misaada yote itatoweka ghafla na mara moja uwanja utakuwa huru zaidi kwa wagombea mbalimbali kushindana kwa hoja, si kwa wingi wa msaada.
Pendekezo la mwisho ni kuwa kwa vile inaonekana wabunge wengi wanataka kutoa misaada kwenye majimbo yao ili wasaidie wananchi wao basi watoe misaada hiyo kupitia taasisi za kutoa misaada! Kwa mfano, waziri mmoja alipewa misaada ya kuwapelekea wananchi wa jimbo lake huko Kilosa, misaada ambayo ilitolewa na Uchina. Misaada hiyo alipewa Rais Kikwete naye akampa Mustafa Mkulo aiwasilishe kwenye jimbo lake na hivyo kumpigia debe kijanja kumbuka Rais angeweza kutoa misaada hiyo kwa Ofisi ya Waziri Mkuu na kuwaacha wao waamue jinsi ya kuifikisha kule au angeweza kutoa kwa Chama cha Msalaba Mwekundu ambacho Serikali yake haijakisaidia kukipa uwezo (angalau sijui kama imefanya hivyo kwenye mafuriko ya hivi karibuni).
Vinginevyo, nina uhakika mapendekezo yote matatu hayawezi kukubalika kwa CCM, au kwa Rais Kikwete, kwa Yusuf Makamba na msululu wa wengineo, kwani wakikubali wataingilia gia gani ili waombe uongozi?