Bila misaada wangepita kuomba kura vipi?

Mzee Mwanakijiji

Platinum Member
Mar 10, 2006
33,476
39,995
Na Lula wa Ndali Mwananzela (Raia Mwema)


NATUMAINI msomaji wewe ni mmoja wa watu wenye uwezo wa kuona, kufikiri, kuchambua mambo na hatimaye kufikia uamuzi baada ya kufanya uchambuzi wa kutosha juu ya jambo fulani.



Naamini kuwa katika kufikia uamuzi huo huongozwi na hisia zako (woga, wivu, tamaa, kisasi, uchungu n.k) bali unaongozwa na uhalisia wa vitu kwa kutumia akili. Si kwamba hisia ni mbaya bali kwa vile hisia ni rahisi kushawishiwa na matukio na mazingira, uwezo wa kiakili kupima mambo ni kinga kubwa zaidi ya kuburuzwa kuliko hisia.



Fikiria mtu anapokuja kwako na kusema anaomba umsaidie kwa sababu mtoto wake ni mgonjwa. Hisia zako zitataka mara moja kutoa msaada lakini akili mara moja itakupa tahadhari kuweza kumpima huyo anayekuomba msaada. Utamuhoji maswali ya kiakili ili kuweza kupekua pekua ili hatimaye ufikie mahali uamue kutoa msaada. Katika kufanya hivyo maswali kama “mtoto yuko wapi”, “anaumwa nini”, “nani anamuangalia sasa hivi” n.k yatakuwa ni muhimu sana. Lakini, kama amekuja na mtoto mkononi, na unaona mtoto kakatwa kisu na anavuja damu, hisia zako zitakubaliana na akili yako mara moja kutoa msaada bila ya kuhoji maswali mengi.



Ndiyo maana ni matumaini yangu kuwa tunapoelekea Uchaguzi Mkuu, Watanzania watavuka kizingiti cha maamuzi ya kihisia na kufanya maamuzi ya kiakili zaidi. Maamuzi ambayo hayatafanywa kwa sababu ya kuwafurahisha watu au kuwaonea watu aibu; maamuzi ambayo yatafanywa yakilenga kujipa uwezo wa kweli kujiletea maendeleo. Maamuzi ambayo yataamua kama misaada inatosha kumfanya mtu achaguliwe.


Kuanzia mwishoni mwa mwaka jana na hasa wakati huu na bila ya shaka miezi inayokuja wale wanaotaka kutuongoza watapita wakijaribu kuwatongoza Watanzania kwa misaada mbalimbali. Viongozi hawa (kama tunaweza kuwaita hivyo) wanajipitisha sasa hivi kwa misaada mbalimbali ambayo ilitetewa na mwenzao mmoja juzi bungeni kuwa ni “haki yao” kutoa misaada kwa vile ni wabunge walioko madarakani. Hebu tuwapime kwa kutumia akili kidogo.


Hivi umewahi kuona ombaomba aliyeacha uombaomba kwa sababu hatimaye amepata vya kutosha kuanzisha maisha yake? Unaweza kumtafuta ombaomba ambaye anaweza kukuonyesha, kwa majivuno, kile alichojenga katika maisha yake kwa kutumia misaada? Unafikiri ni kipi rahisi kwa ombaomba – kupewa msaada au kupewa shamba akalime? Ni lipi jepesi kumpa mtu samaki akale au kumpeleka mtoni na kumfundisha kuvua? Ni wazi kwa mtazamo wa ombaomba kupata msaada wa kutatua tatizo la sasa ni bora zaidi kuliko kuanza kushika jembe kulima ili ajipatie chakula yeye mwenyewe, na ni wazi kwa mwenye njaa ni rahisi kukimbilia samaki aliyevuliwa na wengine kuliko kutumia muda wa yeye kujifunza kuvua.


Lakini Watanzania wakiongozwa na serikali ya CCM wanategemea misaada hadi inaudhi (wengine wanadai inakera). Na wakati huu wa kampeni wagombea na wale wenye kutaka kugombea nafasi mbalimbali watapita na kujipitishapitisha kama kina dada poa kwenye miji na vijiji vyetu kila mmoja akiwa mkarimu na mwema; watapita wakija na masanduku ya misaada mbalimbali, misaada ambayo wameihalalisha kuwa sisi wananchi tunaihitaji.
Kwa vile ni rahisi zaidi kupokea misaada kuliko kupewa njia ya kujikwamua, wapo watu kati yetu ambao wanasubiri misaada na hufanya hima kukinga mikono kupokea misaada hiyo bila ya kujiuliza maswali. Hawa ndio wanawawezesha viongozi kuthubutu kuja na gia ya misaada.



Fikra hizi za kutegemea misaada na kukumbatia misaada zimeletwa nchini na CCM hii ya kina Benjamin Mkapa na Jakaya Kikwete. Wamelidekeza Taifa kiasi cha kuwaharibu Watanzania. Watanzania leo hawawezi kufikiria kujiletea maendeleo bila “misaada” na hakuna mtu anayeweza kuja kutaka kugombea bila ya kutoa ahadi za misaada, na wapo ambao wameishiwa hoja kabisa isipokuwa hoja ya misaada.



Nakumbuka mmoja katika kutafuta kura kwa wananchi aliwaahidi kuwa eti akichaguliwa atawaletea maendeleo kwa sababu anafahamiana na wafadhili mbalimbali wa nje ya nchi. Wapo wengine ambao nao kutokana na “connections” zao huko majuu wanakuja na ahadi za mema kwa sababu wanaweza kuleta vitu mbalimbali kama misaada.


Kinachosikitisha ni kuwa Watanzania kama makinda ya ndege tunduni tumefungua vinywa vyetu na kupokea bila kuuliza; iwe ni funza, mchwa, vipepeo au nyasi tu! Tunapokea na kushangilia bila kuhoji na kuwahoji.



Matokeo yake ya kwanza ni kuwa wagombea wamekwishakujua gia ya kuingia nayo ni misaada. Hata mimi leo nikitaka kugombea jimbo lolote kikundi cha watu wenye fikra fupi watakuja na kuuliza “umelifanyia nini jimbo” wakimaanisha “mbona hatujawahi kuona misaada yako”?



Nikijenga hoja kuwa sijatoa msaada kwa sababu hamuhitaji kusaidiwa mnahitaji kuongozwa kujiletea maendeleo wataniangalia kwa kebehi huku wakikimbilia kwa mgombea mbeba misaada! Tumedekezwa na tukadekeka!


Ninachosema ni kuwa kama tunakubali misaada ya kiudhalilishaji na kudekezana ati kwa sababu “kwanini tukatae” tujue kabisa tunauza dhamira na haki zetu. Mtu ambaye anafuata kampeni ya mgombea kwa sababu ya misaada ni mtu ambaye amepoteza uzalendo na ni tegemezi kifikra. Kama wananchi kwenye majimbo mbalimbali watawapima wagombea wa mwaka huu kwa kuangalia nani anapita na misaada mikubwa na mingi basi Taifa lina matatizo si katika uongozi tu bali zaidi kwa wale wanaoongozwa. Nina mapendekezo matatu.


Watanzania walio huru kifikra wakatae misaada ya kizugaji inayopitishwa sasa majimboni. Kukataa kwenyewe wala si kugumu. Mgombea akija na misaada yake anatakiwa kuulizwa:
Kwanini unaleta misaada hii sasa?



Bila ya misaada yako unataka tukuchague kwa nini na utafanya nini kutuongoza kujitegemea na kwa vipi?



Tuzingatie vile vile kuwa fikra hizi za uombaomba wa kudumu zipo ndani ya Serikali; zinaundwa na zinakolezwa na Serikali. Fikiria majibu ya juzi bungeni Serikali ikimjibu Paul Kimiti (Sumbawanga Mjini) juu ya kuendelea kutoa jimboni kwake kwake misaada mbalimbali. Serikali imekubali kuwa jambo hili halina tatizo.



Kinachonishangaza ni kwanini waulizie suala la kutoa misaada badala ya kuongoza shughuli za kujitegemea? Hivi kama wabunge walioko sasa wakifanya mambo ya kujitegemea kusaidia kujenga shule (si kutoa fedha tu bali kuwapo wenyewe na nyundo), kuongoza katika usafi katika maeneo yao, n.k kuna mtu atawalalamikia? Kwanini walilie kutoa misaada; jibu jepesi ni kuwa ndiyo gia pekee waliyonayo ya kuombea kura tena vinginevyo wangekuwa na rekodi ya kutuambia miaka minne iliyopita wamefanya nini na hayo yangetosha kuwafanya wananchi wawakubali tena; tatizo ni kuwa hawana cha kuonyesha sasa, wamebakia na misaada!


Mkiridhika au kutoridhika na majibu ya maswali hayo mawili (na mengine mnayoweza kujitungia) mnamuambia arudi na misaada yake alikoitoa na aiweke akiba hadi akichaguliwa ndiyo ailete tena (kama kweli ana lengo la kuwasaidia) na kama kweli alikuwa na lengo la kuwasaidia wananchi basi ailete misaada hiyo baada ya uchaguzi. Ninawahakikishia mtawachuja wagombea nyinyi wenyewe kabla ya vyama vyao maana wataingia kwa gia gani nyingine ukiondoa misaada ya kuwafanya wananchi mazobo?
Pendekezo la pili ni kuwa kwa vile Rais Kikwete amedai kuwa anataka uchaguzi huu uwe safi na rushwa zisitumike basi la kwanza ni kuzuia misaada yote ya mtu binafsi mwenye kutaka kutoa kwa jimbo analotaka kugombea. Si kuipiga marufuku bali kutoa maelekezo mepesi kuwa misaada yoyote ambayo si sehemu ya utendaji wa Serikali itasitishwa hadi baada ya Uchaguzi Mkuu na kama kweli kuna mtu anataka kutoa msaada basi msaada huo uende nje ya jimbo lake! Nawahakikishia misaada yote itatoweka ghafla na mara moja uwanja utakuwa huru zaidi kwa wagombea mbalimbali kushindana kwa hoja, si kwa wingi wa msaada.



Pendekezo la mwisho ni kuwa kwa vile inaonekana wabunge wengi wanataka kutoa “misaada” kwenye majimbo yao ili wasaidie wananchi wao basi watoe misaada hiyo kupitia taasisi za kutoa misaada! Kwa mfano, waziri mmoja alipewa misaada ya kuwapelekea wananchi wa jimbo lake huko Kilosa, misaada ambayo ilitolewa na Uchina. Misaada hiyo alipewa Rais Kikwete naye akampa Mustafa Mkulo aiwasilishe kwenye jimbo lake na hivyo kumpigia debe kijanja – kumbuka Rais angeweza kutoa misaada hiyo kwa Ofisi ya Waziri Mkuu na kuwaacha wao waamue jinsi ya kuifikisha kule au angeweza kutoa kwa Chama cha Msalaba Mwekundu ambacho Serikali yake haijakisaidia kukipa uwezo (angalau sijui kama imefanya hivyo kwenye mafuriko ya hivi karibuni).



Vinginevyo, nina uhakika mapendekezo yote matatu hayawezi kukubalika kwa CCM, au kwa Rais Kikwete, kwa Yusuf Makamba na msululu wa wengineo, kwani wakikubali wataingilia gia gani ili waombe uongozi?
 
Na Lula wa Ndali Mwananzela (Raia Mwema) Fikra hizi za kutegemea misaada na kukumbatia misaada zimeletwa nchini na CCM hii ya kina Benjamin Mkapa na Jakaya Kikwete. Wamelidekeza Taifa kiasi cha kuwaharibu Watanzania. Watanzania leo hawawezi kufikiria kujiletea maendeleo bila “misaada” na hakuna mtu anayeweza kuja kutaka kugombea bila ya kutoa ahadi za misaada, na wapo ambao wameishiwa hoja kabisa isipokuwa hoja ya misaada.

Mzee Mwanakijiji, unakumbuka enzi za Mwalimu, baada ya vita vya Kagera, Mwalimu akatangaza miezi 18 ya kujifunga mikanda. Benki ya Dunia ikapendekeza tufute elimu bure na kulipia afya ili watupe misaada/mikopo, Mwalimu alikataa kutunza pride ya utaifa lakini na chamoto tulikipata.Hoja ya WB kama Mtanzania anasoma bire, anatibiwa bure, anajitafutia tuu cha kujaza tumbo, atafute cha ziada ili iweje?. Hapa ndio mwanzo wa yote. Watanzania tumebweteka mpaka tumekua kama tumelogwa.Sio CCM ya Mkapa na Kikwete ndio imeleta utegemezi wa misaada, bali ni mageti yaliyofunguliwa na Mzee wa Rukhsa, tukabinafsisha kila kitu tukawapa wageni na sisi kutegemea kila kitu kitatoka kwa Ankal.
Watanzania walio huru kifikra wakatae misaada ya kizugaji inayopitishwa sasa majimboni. Kukataa kwenyewe wala si kugumu. Mgombea akija na misaada yake anatakiwa kuulizwa Kwanini unaleta misaada hii sasa?

Hawa Watanzania walio huru kifikra ni asilimia 10% tuu ya Watanzania, zilitakiwa zifanyike juhudi za dhati kuwapatia uhuru wa kifikra hawa asilimia 90% kabla ya hata zoezi la uandikishaji halijaanza ili wajiandikishe na kuutumia uhuru wao wa fikra kuamua wanachotaka.Kwa mawazo yangu muda uliobakia ni mchache sana, its a bit too little too late!.Sasa ni kusubiri tuu kuthibitisha na kuendelea kuswagwa kwa miaka 5 mingine!.
 
Inauma sana hasa unapoona wale wanaozaniwa kuwa wameelimika ndio vinara wa kulilemaza taifa kwa kumfanya kila raia Matonya anaehitaji misaada. Hatujachelewa bado kungali kuna mda wa kuweza kufanya kitu fulani. Wanaharakati mko wapi? Vyama vya upinzani mko wapi? Acheni kulundikana Dar kukwepa kuwajibika majimboni moja kwa moja. Wawelimisheni raia kuhusu haki zao zilizogeuzwa kuwa fadhila na hawa madhefuli wasio na hata haya ya uso. Maombi yetu kwa Mungu ni haya kwamba atutie nguvu na kutufanya wepesi kuweza kusimama na kushikamana pamoja hata tutakapomwondoa huyu shetani(ccm) wa kujitakia aliyegandamana nasi kama ngozi ya mwili.
 
Pasco ni kweli.. yaani kama kuna kitu kinanitisha kuhusu Tanzania ni hii mentality ya kutegemea misaada; kilele cha haya kilitokea pale Yanga walipojigaraza (karibu bila nguo) kumbembeleza Manji arudi kuwadhamini!! Mimi nakuambia kama ukitaka kujua how deep this mentality is curved deep in our collective psyche itokee watu waanze kukampeni kupinga misaada ya kigeni.. watu hadi watatetemeka kwa kubembeleza..
 
Pasco ni kweli.. yaani kama kuna kitu kinanitisha kuhusu Tanzania ni hii mentality ya kutegemea misaada; kilele cha haya kilitokea pale Yanga walipojigaraza (karibu bila nguo) kumbembeleza Manji arudi kuwadhamini!! Mimi nakuambia kama ukitaka kujua how deep this mentality is curved deep in our collective psyche itokee watu waanze kukampeni kupinga misaada ya kigeni.. watu hadi watatetemeka kwa kubembeleza..
Hahaaaa, ina maana Yanga walimuonea wivu Mzee Matonya?

Je walitumia COPY RIGHT ya Mzee au walim-copy tu?

Inabidi Matonya iwe Trade Mark, labda Watanzania wataanza kuogopa gharama za kumuiga Mzee Matonya.

anthony_matonya.jpg
 
Mzee Mwanakijiji,

Umaskini ndio unawafanya watu wawe omba omba.

Ni sawa na wewe wakati ule unawabembeleza wale Wamisionari wakusaidie kukupeleka USA. Au ndio sasa umesahau?

Ukishiba ni rahisi sana kuwakashifu wenye njaa.
 
Hawa Watanzania walio huru kifikra ni asilimia 10% tuu ya Watanzania, zilitakiwa zifanyike juhudi za dhati kuwapatia uhuru wa kifikra hawa asilimia 90%.

If that is true, very true...then mchawi wetu yuko hapa hapa!! na hao wezi na majangili wa nchi watakuwa wanalijua fika ndo mana hawana hata chembe ya wasiwasi!!
 
Umaskini ndio unawafanya watu wawe omba omba.

umaskini haumsababishi mtu kuwa ombaomba moja kwa moja....wapo watu wametoka familia maskini sana na walisoma shule za vijijini kwa adha kali na wakafanikiwa...wangeomba omba ingekuwa matokeo tofauti. Bado nafikiri kuwa alosema asilimia tisini hatuna uhuru wa fikra kagusa poit kubwa sana. Bila uhuru wa fikra huwezi kujua hata unatarajia nini, huwezi hata kujitambua binafsi!! na uhuru wa fikra unapatkana kupitia elimu...na ieleweke kuwa mara nyingi elimu sio klujua physics au law...ni kujua kuitumia!!
 
If that is true, very true...then mchawi wetu yuko hapa hapa!! na hao wezi na majangili wa nchi watakuwa wanalijua fika ndo mana hawana hata chembe ya wasiwasi!!

Hao asilimia 10 ndio hao wezi na mafisadi. Nchi zote zilizoendelea, zilifanya hivyo kwa kuwatumia wasomi wake wachache kufanya mambo ya maana kwa faida ya nchi.

Sisi wasomi wetu si ndio hao akina Zitto hata bila aibu anatangazia umma anaenda Germany kufanya check-up? Ingekuwa nchi nyingine kwa kutamka hilo angelikuwa amejimaliza kisiasa.

Heri hao wananchi wakinge mikono na kuwakamua wanasiasa maana hawana mwokozi wa kuwasaidia. Opportunities zote zinazibwa na hao hao wasomi na marafiki zao mafisadi. Ukienda shule za kata inabidi uwe genius ili kupata division one ya point 17, vinginevyo wewe ni four tu.
 
jamani elimu ya uraia ndo mkombozi wa kundi kubwa linaloamini kwenye misaada,tuungane kuikomboa TAZANIA,tusiishie kwenye forum kama hizi tu,mi nadhani its high time sasa kusimama kila mtu katika zamu yake.Watanzania wengi wamekuwa brain washed katika swala zima la kujitegemea,wanaaini zaidi katika misaada na kwamba serikali ifanye kila kitu,kundi hili ndo wapiga kura wakubwa wasipokuwa empowered ni ngumu kumn'goa mdudu ccm,tuanze sasa lest empower majirani zetu.........tuwaempower na mambo mbali mbali kifikra,njia za uchumi na taarifa sahii,tukifaulu hapa akili za kila mmoja zitakuwa sawa,atakosekana mjinga wa kupiga kura kwa misaada!!!!
 
Pasco ni kweli.. yaani kama kuna kitu kinanitisha kuhusu Tanzania ni hii mentality ya kutegemea misaada; kilele cha haya kilitokea pale Yanga walipojigaraza (karibu bila nguo) kumbembeleza Manji arudi kuwadhamini!! Mimi nakuambia kama ukitaka kujua how deep this mentality is curved deep in our collective psyche itokee watu waanze kukampeni kupinga misaada ya kigeni.. watu hadi watatetemeka kwa kubembeleza..
Mzee Mwanakijiji, nadhani baadhi ya hawa wanatusaidia, hilo tayari wanalijua, watahakikisha hatuendelei ili wazidi kupose kama watu wa msaada na kukitumia kigezo cha kutoa misaada kama bakora ya kutuchapia, pale watakapohisi tunataka kuamka.

Hii mentality is deeper than whatyou think, hata wengi wa hawa waheshimiwa wetu mle mjengoni, hawana any strategic plans za maendeleo ya watu wao kujiendeleza wenyewe from within ndipo juhudi za serikali na wafadhili kuchangia kusukuma mbele that driving force, wengi ni ma ombaomba tuu, tofauti na Matonya, wao wanaomba kwa vimemo na kuloby lakini kote ni kuomba kule kule kwa imani kuwa bila msaada, hakuna kitakachofanyika.

Hata sasa, tunajiandaa kwa uchaguzi wetu Mkuu, bakuli lilishapita siku nying na limeshashehezwa na fungu la wafadhili na kukabidhiwa UNDP kwele mpango uoitwa Election 2010 Project. Yaani hata uchaguzi wetu wenyewe, ni lazima senti zitoke kwa Ankal!?. sitashangaa kama tenda ya kuchapisha makaratasi pia lazima itapewa kampuni ya Ankal, kama ilivyo miradi yote inayofadhiliwa na WB, computers lazima ziwe Dell!.
 
umaskini haumsababishi mtu kuwa ombaomba moja kwa moja....wapo watu wametoka familia maskini sana na walisoma shule za vijijini kwa adha kali na wakafanikiwa...wangeomba omba ingekuwa matokeo tofauti. Bado nafikiri kuwa alosema asilimia tisini hatuna uhuru wa fikra kagusa poit kubwa sana. Bila uhuru wa fikra huwezi kujua hata unatarajia nini, huwezi hata kujitambua binafsi!! na uhuru wa fikra unapatkana kupitia elimu...na ieleweke kuwa mara nyingi elimu sio klujua physics au law...ni kujua kuitumia!!
Umasikini mbaya kuliko wote ni umasikini wa fikra na ndio maana tunahitaji zaidi ukombozi wa fikra kuliko ukombozi mwingine wowote. Mwalimu alikuwa masikini wa mali, lakini tajiri wa fikra.
 
Mzee Mwanakijiji,

Umaskini ndio unawafanya watu wawe omba omba.

Ni sawa na wewe wakati ule unawabembeleza wale Wamisionari wakusaidie kukupeleka USA. Au ndio sasa umesahau?

Ukishiba ni rahisi sana kuwakashifu wenye njaa.
Umaskini si wa kipato bali wa mawazo. Huu umaskini ndiyo umaskini mkubwa zaidi.
Hebu fikiria unakuwa na "vogue" halafu unalisimamisha pale IFM unawaona warembo wazuri na unajua kabisa kuwa hata kwao baiskeli hakuna halafu unawaambia pandeni niwape lift wanakuambia nani amekwambia anashida ya kupanda mkebe wako. Utajisikiaje? Bila shaka utaweza kabisa ukastaajabu na baadaye ukajua kumbe hata gari hilo lako ambalo ndilo uliloona ni kila kitu kumbe halina maana yoyote katika jamii na jamii wala haithamini. Ikifikia hapo ambapo tutaacha kumhusudu au kumheshimu mtu kwa sababu ya mali alizonazo (physical riches) tutapiga hatua kubwa kwani utu wetu utarudi. Utu wetu ni muhimu na wa thamani sana kuliko fedha na dhahabu!!!
 
Umasikini mbaya kuliko wote ni umasikini wa fikra na ndio maana tunahitaji zaidi ukombozi wa fikra kuliko ukombozi mwingine wowote. Mwalimu alikuwa masikini wa mali, lakini tajiri wa fikra.

Unajua wao wenyewe hao maskini wana fikra potofu kuwa "Mkono mtupu haulambwi"
Ukiwa na fikra zako timilifu ukamwambia maskini usimchague huyo kwa sababu ni mwizi huko huyo huyo mwizi anampatia maskini angalau pombe, kofia na flana hata thamani ya 5000 haifiki atakuona wewe unampotosha. Naamini watanzania wengi ni maskini wa akili na mali ndicho kinacho tupeleka hapa tulipo.
 
Unajua wao wenyewe hao maskini wana fikra potofu kuwa "Mkono mtupu haulambwi"
Ukiwa na fikra zako timilifu ukamwambia maskini usimchague huyo kwa sababu ni mwizi huko huyo huyo mwizi anampatia maskini angalau pombe, kofia na flana hata thamani ya 5000 haifiki atakuona wewe unampotosha. Naamini watanzania wengi ni maskini wa akili na mali ndicho kinacho tupeleka hapa tulipo.
Hili nalo neno!!!!!
 
Back
Top Bottom